IJUMAA
WIKI YA 22 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 4:1-5
Zab/Kit: 37:3-4, 5-6, 27-28, 39-40
Injili: Lk 5:33-39
Nukuu
“Mtu
na atuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri za Mungu,”
1Kor 4:1
“Hapo
tena inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu,” 1Kor
4:2
“Nao wakamwambia, Wanafunzi wa Yohana hufunga mara nyingi,
na kuomba dua; na kadhalika wanafunzi wa Mafarisayo; lakini wanafunzi wako hula
na kunywa!” Lk 5:33
“Lakini
Yesu akawaambia, Je! Mwaweza kuwafanya wafunge walioalikwa arusini, akiwapo
bwana arusi pamoja nao?” Lk 5:34
“Lakini
siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi, ndipo watakapofunga siku zile,” Lk
5:35
“Lakini divai mpya sharti kutiwa katika viriba vipya,” Lk
5:38
“Wala
hakuna anywaye divai ya kale akatamani divai mpya; kwa kuwa asema, Ile ya kale
ndiyo iliyo njema,” Lk 5:39
TAFAKARI: “Mtu
na atuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri za Mungu.”
Wapendwa katika Kristo,
Yesu anapotoa mfano wa vazi kuukuu na jipya, na kwa upande mwingine divai ya
zamani na kiriba kipya anataka kutufundisha jambo hili; “kwanza kabisa lazima
tujue sababu na malengo ya maisha yetu hapa duniani.” Hatupo hapa duniani kwa
bahati mbaya hata kidogo. Tupo katika ulimwengu huu kadiri ya mpango wa Mungu
ambao ni dhahiri na mathubuti. Hivyo lolote lile lililo jema mbele ya Mungu
huwiishwa na kufanya upya. Katika Injili ya leo tunaona watu wakimletea Yesu
malalamiko juu ya kufunga na kuomba.
Kufunga kwetu na kuomba kwetu uifaidia kwanza
kabisa roho zetu na wenzetu. Tunawajibu huo kiimani, na yatupasa kuutekeleza
pasipo shaka. Ndiyo maana Yesu anawauliza watesi wake swali hili: “Je! Mwaweza kuwafanya wafunge walioalikwa arusini,
akiwapo bwana arusi pamoja nao?” Lk 5:34. Maisha yapaswa kusherehekewa kwa
sababu ni mali na zawadi ya Mungu.
Hivyo
basi, upya wetu kiimani hutoshelezwa na upya tuupokeao kwa Yesu tunaposhiriki
Masakramenti yake tukiwa katika hali ya usafi. Hivyo “divai mpya sharti kutiwa katika
viriba vipya,” Lk 5:38. Ndani na katika Kristo kiimani hujengeka kwa matendo
madogo madogo yanayompendeza Mungu. “Wala
hakuna anywaye divai ya kale akatamani divai mpya; kwa kuwa asema, Ile ya kale
ndiyo iliyo njema,” Lk 5:39. Ndugu yangu ukiona vinaelea ujue vimeundwa. Je,
tufanye nini ili enende katika Kristo na ndani ya Kristo?
Kama
tunajua kwamba hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna
afaye kwa nafsi yake, Rum 14:7, maisha yetu bila Kristo yatakuwa na walakini
mkubwa. “Mtu
na atuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri za Mungu,”
1Kor 4:1. Kama tu watumishi wa Kristo na mawakili wa siri za Mungu, maisha yako
hapa duniani na kadiri ya wito wako ni dhamana kubwa kwa sababu
yeshathaminishwa kwa damu ya Yesu pale Msalabani. “Nanyi mfahamu kwamba
mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka
katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya
thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo,”
1Pet 1:18-19. Je, watambua thamani ya maisha yako kama mfuasi wa Kristo?
Wapendwa wana wa Mungu,
thamani ya Ukristo wako itategemea sana na mamna unavyo mwakilisha Kristo kama
wakili wake katika kweli na uaminifu. Ukristo wako usibaki katika jina tu, bali
imani ya kweli ndani yako, na Kristo akiwa ndiye kielelezo chako katika yote. Na “hapo
tena inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu,” 1Kor
4:2. Ni kuwa mwaminifu katika kuifuata njia yake, yaani, kuubeba msalaba wako kwa
uaminifu bila kumsaliti Kristo. Ni kuiishi kweli kadiri ya mafundisho yake
Kristo, na zaidi amri ile ya upendo.
Ukipenda kama
alivyopenda Kristo utafanya yote yampendezaye Mungu. Na mwisho ni kuuishi uzima
wa kweli kwa kushiriki Masakramenti katika hali ya usafi wa moyo, na hasa
Sakramenti ya Ekaristi Takatifu. Hali hii ya usafi wa moyo ndiyo impelekeayo
Mtume Paulo kusema kwamba, “Lakini, kwangu
mimi, si kitu kabisa nihukumiwe na ninyi, wala kwa hukumu ya kibinadamu, wala
sijihukumu hata nafsi yangu,” 1Kor 4:3. Mara zote tuongozwe na dhamiri safi na
yenye hofu ya Mungu. “Maana
sijui sababu ya kujishitaki nafsi yangu, lakini sihesabiwi haki kwa ajili hiyo;
ila anihukumuye mimi ni Bwana,” 1Kor 4:4.
Kuujua wajibu wako na
kuutimiza kadiri ya takwa lake na kwa upendo ndiko kutakapo kuhesabia haki. “Basi
ninyi msihukumu neno kabla ya wakati wake, hata ajapo Bwana; ambaye
atayamulikisha yaliyositirika ya giza, na kuyadhihirisha mashauri ya mioyo;
ndipo kila mtu atakapoipata sifa yake kwa Mungu,” 1Kor 4:5. Ndugu yangu,
usichoke kutimiza wajibu wako kwa upendo. Hakuna aliyefilisika kwa kupenda na
kutoa kwa upendo.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Lakini
divai mpya sharti kutiwa katika viriba vipya,” Lk 5:38
Tusali:-Ee
Yesu, tujalie neema ya kutimiza wajibu wetu kwa upendo. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario