JUMATATU
WIKI YA 24 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 11:17-26, 33
Zab/Kit: 40:7-8a,
8b-9, 10, 17
Injili: Lk 7:1-10
Nukuu
“Lakini
katika kuagiza haya, siwasifu, ya kwamba mnakusanyika, si kwa faida bali kwa
hasara,” 1Kor 11:17
“Je! Hamna nyumba
za kulia na kunywea? Au mnalidharau kanisa la Mungu, na kuwatahayarisha hao
wasio na kitu? Niwaambieni? Niwasifu? La! Siwasifu kwa ajili ya hayo,” 1Kor
11:22
“Maana kila
mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata
ajapo. Kwa hiyo, ndugu zangu,
mkutanikapo mpate kula, mngojaneni,” 1Kor 11:26, 33
“Kwa maana mimi
nami ni mtu niliyewekwa chini ya mamlaka, mwenye askari chini yangu;
nikimwambia huyu, Nenda, huenda; na huyu, Njoo, huja; na mtumwa wangu, Fanya
hivi, hufanya,” Lk 7:8
“Yesu
aliposikia hayo alimstaajabia, akaugeukia mkutano uliokuwa ukimfuata, akasema,
Nawaambia, hata katika Israeli sijaona imani kubwa namna hii,” Lk 7:9
TAFAKARI: “Ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha
katika Roho Mtakatifu.”
Wapendwa wana wa Mungu, Maandiko Matakatifu yanatupa angalizo na
kusema, “ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha
katika Roho Mtakatifu,” Rum 14:17. Ni wazi jumuiya hii ya Korintho walianza
kupoteza maana halisi la fumbo la ‘Ekaristi Takatifu,’ ingawa fumbo hili kwa
nyakati zile lilijulkana kama ‘Kuumega Mkate Pamoja,’ Lk 24:35, Mdo 2:42.
Mkusanyiko huo wa jumuiya ya kwanza ya Wakristo baada ya kusali na kujadili
yaliyohusu jumuiya yao kimwili na kiroho, na swala zima la uinjilishaji,
walishirikishana chakula cha pamoja ikiwa ni kukumbuka karamu ile ya mwisho ya
Bwana wetu Yesu Kristo na Mitume wake.
Mkate na Divai ambavyo vilibeba fumbo hili Kisakramenti-ishara ya nje
inayoonekana wazi kwa uwepo wa neema isiyoonekana, vielelezo hivi shikika na
onekana, yaani, Mkate na Divai, kila mwanajumuiya aliyekuwa na uwezo alivileta
kutoka nyumbani kwake. Kwa vile siyo kila mmoja kwenye jumuiya alikuwa na uwezo
wa kuandaa hayo, masengenyo na kunyapaliana yalijitokeza. Na ndiyo maana
kusanyiko lao katika mwono huo, Mtume Paulo analiita si kusanyiko lenye faida
bali lenye hasara. “Lakini
katika kuagiza haya, siwasifu, ya kwamba mnakusanyika, si kwa faida bali kwa
hasara,” 1Kor 11:17. Maumbo haya ya Mkate na Divai licha ya kuwa ishara ya
ndani lenye kutupa uzima wa mwili na roho, ilimaanisha pia upendo na umoja wa
wabatizwa wote kama Mwili wa Kristo, nalo ndilo kusudi la kukusanyika kwao kama
KANISA.
Badala yake, Mkusanyiko
ule ulilenga upande mmoja tu, yaani, mwili, na kuelekeza nguvu zote kwa mfalme
tumbo. Na hiki ndicho kisa cha sokomoko lote la kusengenyana, kutengana kwa
masikini na matajiri, na hata kunyapaliana. Naye Mtume Paulo anasema, “Kwanza mkutanikapo kanisani nasikia kuna faraka
kwenu; nami nusu nasadiki; kwa
maana lazima kuwapo na uzushi kwenu, ili waliokubaliwa wawe dhahiri kwenu,”
1Kor 11:18-19. Mwelekeo huu wa kumwabudu mfalme tumbo, wengine kati yao
walipitiliza na kutumia Divai ile kama kileo na kuishia kulewa na kupoteza
maana halisi ya uwepo wa Mkate na Divai kama Mwili na Damu ya Kristo-Sakramenti
ya Ekaristi Takatifu. Kwa mshangao huu, Mtume Paulo anasema, “Basi
mkutanikapo pamoja haiwezekani kula chakula cha Bwana; kwa maana kila mmoja hutangulia kutwaa
chakula chake katika kule kula; hata huyu ana njaa, na huyu amelewa,” 1Kor
11:20-21.
Kwa maana halisi ya Maumbo hayo ya Mkate na
Divai, na uhusiano wake na Kanisa kama nilivyokwisha kusema hapa mwanzo, tendo
lile la kunyapaliana na kukufuru kulikotokana na ulevi, matendo hayo siyo
kusudi la kukusanyika kwako kama Kanisa- Mwili wa Kristo. Kwa maana nyingine,
hapo siyo sehemu ya mambo hayo. Naye Mtume Paulo anazihoji dhamiri zao na
kusema, “Je!
Hamna nyumba za kulia na kunywea? Au mnalidharau Kanisa la Mungu, na
kuwatahayarisha hao wasio na kitu? Niwaambieni? Niwasifu? La! Siwasifu kwa
ajili ya hayo,” 1Kor 11:22. Hakika hakuna cha kujivunia kwa kuyafanya hayo
yenye kupotosha maana halisi ya Mwili na Damu ya Yesu, na uhusiano wake na
Kanisa, wewe na mimi tukiwa ndiyo viungo vyake, 1Kor 12:27
Baada ya kukemea hili,
Mtume Paulo anatoa mafundisho halisi ya Fumbo hili la Mkate na Divai. Naye
Paulo analisema hilo kadiri ya Mapokeo, yaani, kutoka Yesu Mwenyewe na Mitume
wake. “Kwa maana mimi nalipokea kwa Bwana
niliyowapa nanyi, ya kuwa Bwana Yesu usiku ule aliotolewa alitwaa mkate, naye akiisha kushukuru akaumega,
akasema, Huu ndio mwili wangu ulio kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho
wangu,” 1Kor 11:23-24.
Ni ukumbusho katika
maana ya Agano la Pekee alilolifanya Mungu kupitia Mwanaye Yesu Kristo, na
twafanya hivyo kila mara tukikumbuka sadaka ile ya pekee ya Yesu Kristo pale
Msalabani ambayo ndiyo sababu ya wokovu wetu kutoka utumwa wa dhambi. Na ndiyo sababu pia ya mimi na wewe kuwa wana
na warithi wa Ufalme wa Mungu. “Na
vivi hivi baada ya kula akakitwaa kikombe, akisema, Kikombe hiki ni agano jipya
katika damu yangu; fanyeni hivi kila mnywapo, kwa ukumbusho wangu,” 1Kor 11:25.
Na kwa kufanya hivyo kwa moyo mkunyufu na hofu ya Mungu, twaitangaza mauti ya
Bwana hata ajapo. “Maana kila mwulapo mkate
huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata ajapo. Kwa hiyo, ndugu zangu, mkutanikapo
mpate kula, mngojaneni,” 1Kor 11:26, 33
Ndugu yangu tunaye
safiri sote katika tafakri hii, kwa maumbo haya ya Mkate na Divai, Mwili na
Damu ya Yesu, Yesu Kristo ni uzima halisi. Kristo ni uzima halisi tunaposhiriki
Ekaristi Takatifu katika mastahili yake. Yesu anatuambia, “Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona
njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe” Yoh 6:35. Ni katika kula
chakula hiki-mwili na damu yake, Yesu
anahaidi mambo mawili makuu: Moja, ni ufufuko siku ya mwisho. Naye anasema, “Aulaye mwili wangu na
kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho,” Yoh
6:54. Na katika kula chakula hiki-mwili na damu yake, Kristo hukaa ndani yetu.
Naye anasema, “Aulaye mwili wangu na
kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake,” Yoh 6:56.
Hata
hivyo Mtume Paulo anatupa angalizo la chakula hiki cha uzima. Naye anasema, “Basi kila aulaye mkate
huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili, atakuwa amejipatia
hatia ya mwili na damu ya Bwana,” 1Kor 11:27. Yatupasa kuijongea Meza ya Bwana
tukiwa na mastahili ya kufanya hivyo-usafi wa mwili na roho, yaani, pasipo
hatia yoyote. Zaidi ya hapo ni kuikufuru Meza ya Bwana. Je, tuna IMANI hiyo au
tunafanya kama tunavyofanya kwa mazoea tu?
Wapendwa
wana wa Mungu, IMANI ya kweli inayoacha ubinafasi wetu pembeni na kumtanguliza
Mungu, ndiyo anayoisifu Yesu leo katika Injili tuliyoisikia. Imani hii ndiyo
aliyoistahajabia Yesu juu ya akida yule aliyekuwa na mtumwa wake mgonjwa
aliyehitaji uponyaji wa Yesu. Baada ya kupata ombi hili kutoka kwa akida yule,
Yesu anachukua hatua mara moja na akiwa njiani imani ya kweli ya akida yule
inajidhihirisha. “Basi Yesu
akaenda pamoja nao. Hata alipokuwa si mbali na nyumba yake, yule akida alituma
rafiki kwake, akamwambia, Bwana, usijisumbue, maana mimi sistahili wewe uingie
chini ya dari yangu; kwa hiyo
nilijiona sistahili mwenyewe kuja kwako; lakini, sema neno tu, na mtumwa wangu
atapona,” Lk 7:6-7.
Huu ndio uhai halisi wa
Kristo kati yetu, ambao leo upo katika maumbo ya Mkate na Divai, yaani,
Ekaristi Takatifu. Tuwapo mbele ya uwepo huu halisi wa Kristo, ni wakati wa
kushikamana na Kristo, na kuachana na ubinadamu wetu, vionjo vyetu, na
matamanio yake, ikiwa ni pamoja na mamlaka tuliyonayo katika jamii. Katika
kweli hii Akida yule anasema, “Kwa maana
mimi nami ni mtu niliyewekwa chini ya mamlaka, mwenye askari chini yangu;
nikimwambia huyu, Nenda, huenda; na huyu, Njoo, huja; na mtumwa wangu, Fanya
hivi, hufanya,” Lk 7:8. Pamoja na nguvu na mamlaka hizi za kibinadamu Mungu
abaki kuwa Mungu, na Kristo abaki kuwa Kristo, Baba na Mwakozi wetu.
Hapa ndipo Yesu
alipostaajabu; “Yesu aliposikia hayo
alimstaajabia, akaugeukia mkutano uliokuwa ukimfuata, akasema, Nawaambia, hata
katika Israeli sijaona imani kubwa namna hii,” Lk 7:9. Ndugu yangu, mshangaze
Kristo kwa kusimama katika imani iliyo kweli. Iwapo imani ya kweli, Kristo yupo
na hujidhihirisha pasipo mawaa kabisa. Kristo hutenda yote pale tunaposhikamana
naye. Hivi ndivyo ilivyokuwa kwa yule Akida na mtumwa wake mgonjwa kwamba, “Na
wale waliotumwa waliporudi nyumbani, wakamkuta yule mtumwa ni mzima,” Lk 7:10.
Jina la Bwana wetu Yesu Kristo lihimidiwa milele na milele. Amina.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Yesu
aliposikia hayo alimstaajabia, akaugeukia mkutano uliokuwa ukimfuata, akasema,
Nawaambia, hata katika Israeli sijaona imani kubwa namna hii,” Lk 7:9
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, tujalie Imani ya kweli, na mara zote utuepushe na vionjo vyetu.
Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario