lunes, 26 de septiembre de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 26 YA MWAKA-C


JUMATANO WIKI YA 26 YA MWAKA-C

Somo: Ayu 9:1-12, 14-16

Zab/Kit: 88:10bc-11, 12-13, 14-15

Injili: Lk 9:57-62

Nukuu:

 “Yesu akamwambia, Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake,” Lk 9:58

 “Yesu akamwambia, Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu,” Lk 9:62

“Ndipo Ayubu akajibu, na kusema, Kweli najua kuwa ndivyo hivyo; Lakini mtu huwaje mwenye haki mbele za Mungu?” Ayu 9:1-2

 “Yeye ni mwenye hekima moyoni, na mwenye uwezo katika nguvu; Ni nani aliyejifanya kuwa mgumu juu yake, naye akafanikiwa?” Ayu 9:4

TAFAKARI: “Yeye ni mwenye hekima moyoni, na mwenye uwezo katika nguvu; Ni nani aliyejifanya kuwa mgumu juu yake, naye akafanikiwa?”

Wapendwa wana wa Mungu, kadiri ya Injili ya leo, Yesu anampa angalizo mtu yule aliyekutana naye njiani na kusema yupo tayari kufuatana naye ko kote atakapokwenda. Yesu akamwambia, Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake,” Lk 9:58. Kwa maneno mengine Yesu anatuambia hakuna maslahi yo yote kibinadamu zaidi ya maisha ya umilele kutoka kwake. Kama ni swala la utajiri na kuwa na maisha mazuri siyo kipaumbele cha kwanza katika ufuasi wetu kwake. “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Mt 6:9. Kazi yetu ya kwanza ni kuutafuta ‘kwanza ufalme wa mbinguni’ na mengine yote tutapewa kwa ziada na kadiri ya mahitaji yetu.

Jambo la pili na la muhimu tunalofundishwa leo kuhusu Imani ya kweli na ufuasi usio na mawaa ni ‘utambuzi wa kweli na kujua nafasi ya Mungu katika maisha yako.’ Bila shaka wengi wetu tuna hofu ya kifo. Hata hivyo, kifo kipo pale pale upende au usipende. Na kama umezaliwa basi ipo siku utakufa. Kuzaliwa si lazima, bali kufa ni lazima kama umezaliwa. Kwa hiyo katika mantiki hii ya kifo na uhalisia wake, hatupaswi kukiogopa. Yatupasa kuishinda hofu ya kifo ili uwe tayari kukipokea kifo kama njia pekee ya maisha yale baada ya kifo hapa duniani, kuishi umilele. Hakutakuwa na maisha ya umilele baadaye bila kupita katika fumbo hili la kifo.

Hivyo Yesu anamtoa hofu ndugu yule aliyetoa hoja ya kwenda kwanza kumzika Baba yake ndipo amfuate. Naye Yesu anamwambia, “Waache wafu wawazike wafu wao; bali wewe enenda ukautangaze ufalme wa Mungu,” Lk 9:60. Je, Yesu anatukataza kuwazika wazazi wetu? La hasha! Kufanya hivyo angekuwa anaenda kinyumbe na ile amri ya nne ya Mungu, “waheshimu baba yako na mama yako; siku zako zipate kuwa nyingi katika nchi upewayo na Bwana, Mungu wako,” Kut 20:12. Yesu anachotaka kukuambia wewe na mimi leo ni kwamba, kifo ni ‘kweli isiyopingika na hivyo shughuli zake na mazingira ya yake, isiwe sababu ya kutokupokea ujumbe wake wa uzima wa milele.

Na jambo la tatu na la mwisho tunalofundishwa leo kuhusu Imani na ufuasi thabiti ni ‘kule kuwa na msimamo thabiti wa wito ulio nao na kutunza kile ulichoitiwa.’ Hii ni pamoja na kutokuwa ndumilakuwili au kigeugeu cha kutaka‘kutazama au kurudi nyuma ulikotoka kwa malengo ya kujaribu tena.’Bali lipaswalo ni kujenga uaminifu na utayari wa kutimiza kile ulichoitwa na kukubali bila shuruti kwa sifa na utukufu wake Mungu. Na hicho ulichoitwa na kukubali kwa hiari yako kiwe mwitikio chanya hasa pale linapojitokeza swala ya huduma kwa watu au umma.

Wengi wetu baada ya kubatizwa tumerudi kuishi maisha ya kipagani kabisa. Na wengi katika kundi hili wamekuwa washirikina wa kupindukia na kuongozwa na nguvu za giza ili hali wamejivika visakramenti mwili mzima. Ushirikina ‘ni kuamini nguvu fulani kutoka kitu fulani kisicho na uhusiano kimantiki.’ Katika hili Yesu anatupa angalizo, na kusema, “Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu,” Lk 9:62. Kwa maneno mengine ni heri kuwa baridi au joto, kuliko kuwa vuguvugu katika Imani.

Ayubu ni mfano mzuri na dhahiri wa kusimama katika imani thabiti. Siri kubwa aliyokuwa nayo Ayubu juu ya imani yake ni kutokushikamana na vitu na kujifananisha navyo. Ayubu alijisalimisha kabisa mikono mwa Mungu. Baada ya kuyatafakari maisha yake na uhusiano wake na Mungu, “ndipo Ayubu akajibu, na kusema, Kweli najua kuwa ndivyo hivyo; Lakini mtu huwaje mwenye haki mbele za Mungu?” Ayu 9:1-2. Mungu ndiye haki, na Yeye tu ndiye mwenye kutuhesabia haki. Hivyo mtu “kama akipenda kushindana naye, Hawezi kumjibu neno moja katika elfu,” Ayu 9:3. Katika hali na mazingira kama haya usalama wako upo pale tu utakapo jisalimisha mikononi mwake bila kujibakiza.

Ayubu kwa namna ya pekee pia anagundua kuwa Mungu ndiye kila kitu. Kwake hakuna linalomshinda, na vyote vipo kama vilivyo kwa nguvu zake, Ayu 9:5-12. Mungu huyu aliye hai na wapekee ndiye uiongoza mifumo yote hai (inayoonekana na isiyoonekana) kadiri apendavyo Yeye. Ni kweli pasipo shaka kwamba  “Yeye ni mwenye hekima moyoni, na mwenye uwezo katika nguvu,” Ayu 9:4a. Na vyote avifanyavyo Mungu vina lengo la umilele. Kushindana au kupingana na Mungu kwa ufahamu wako ni kushindwa kabla hata ya kuanza kutekeleza jambo hilo. Hivyo “ni nani aliyejifanya kuwa mgumu juu yake, naye akafanikiwa?” Ayu 9:4b. HAKUNA!

Tumsifu Yesu Kristo!

“Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu,” Lk 9:62

Tusali:-Ee Yesu Mwema, tujalie neema na nguvu na kupita katika majaribu ya Imani. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario