jueves, 8 de septiembre de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 23 YA MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI YA 23 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 10:14-22a
Zab/Kit: 116:12-13, 17-18
Injili: Lk 6:43-49
Nukuu
Kwa ajili ya hayo, wapenzi wangu, ikimbieni ibada ya sanamu,” 1Kor 10:14 

Kikombe kile cha baraka tukibarikicho, je! Si ushirika wa damu ya Kristo? Mkate ule tuumegao, si ushirika wa mwili wa Kristo?” 1Kor 10:16

 “Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani,” 1Kor 10:21

Kwa maana hakuna mti mzuri uzaao matunda mabaya, wala mti mbaya uzaao matunda mazuri; kwa kuwa kila mti hutambulikana kwa matunda yake; maana, katika miiba hawachumi tini, wala katika michongoma hawachumi zabibu,” Lk 6:43-44 

TAFAKARI: “Mhenga au Lihoka katika Imani.”

Wapendwa wana wa Mungu, katika Injili ya leo, Yesu anaijenga kwa upana taswira ya kuwa Wahenga, yaani, kutambulika kwa matendo yetu mema. Kama mtu huwa kile alacho, basi kile alicho mtu leo ni tokea la historia yake. Yesu anasema, tu wahenga kwa sababu, kwa kuwa kila mti hutambulikana kwa matunda yake; maana, katika miiba hawachumi tini, wala katika michongoma hawachumi zabibu,” Lk 6:44. Kwa maneno mengine hawezi kutoa usicho kuwa nacho. Na zaidi ya hayo, kwangu mimi na wewe leo wenye ufahamu huu, yanipasa kutenda mema na kuwa mwema kila siku. Hiyo ndiyo njia salama kwa mwili na roho yako katika umilele.

Matokea ya kweli hii ni kwamba, mtu mwema katika hazina njema ya moyo wake hutoa yaliyo mema, na mtu mwovu katika hazina mbovu ya moyo wake hutoa yaliyo maovu; kwa kuwa mtu, kinywa chake hunena yale yaujazayo moyo wake,” Lk 6:45. Mtu mwema ndiye Mhenga, na mtu mwovu ndiye Lihoka.

Ndugu yangu, ni lipi ungependa kuwa au kuacha nyuma baada ya maisha yako hapa duniani? Yesu anatupa uhakika wa kile tutakachokuwa pale tutakapoamua kufuata mafundisho yake. Kila mtu ajaye kwangu, na kuyasikia maneno yangu na kuyatenda, nitawaonyesha mfano wake,” Lk 6:47. Ni kwa kusikia neno lake na kulitenda huwa wahenga mara baada ya maisha yetu hapa duniani.

Lihoka, yaani, roho ovu, katika maana ya ‘evil spirit,’ kwayo hakuna kitu cha kuigwa. Ni roho ya uharibufu, yaani, ‘destructive spirit,’ isiyo pendezwa na jema au wema. Ni roho isiyotulia na isiyo na mwelekeo wa kudumu na wa umilele. Ni sawa na yule aliyesikia ila hakutenda, mfano wake ni mtu aliyejenga nyumba juu ya ardhi pasipokuwa na msingi, mto ukaishukia kwa nguvu, ikaanguka mara; na maangamizi yake nyumba ile yakawa makubwa,” Lk 6:49.

Muhenga ikiwa ni mtu yule mwenye kuacha kitu cha kuigwa, na kielelezo halisi cha wema, Mfano wake ni mtu ajengaye nyumba, na kuchimba chini sana, na kuweka msingi juu ya mwamba; na kulipokuja gharika, mto uliishukia nyumba ile kwa nguvu, usiweze kuitikisa; kwa kuwa imejengwa vizuri,” Lk 6:48. Ndugu yangu, wewe hu mhenga au lihoka? Ichunguze nafsi!

Mhenga kamwe haishi kwa hofu. Muhenga uiishi kweli katika haki. Katika hili, Mtume Paulo anatupa wosia kuikimbia ibada ya sanamu, 1Kor 10:14. Ibada za sanamu ni kutumaini nguvu fulani kutoka kitu ambacho hakina uhai na uhasili wa hicho ukitegemeacho. Ibada ya kisanamu huanza na wewe mwenyewe kwa kujiinua kusiko kweli na kujivika kinyago-‘mask,’ na kupoteza taswira yako ya kweli.

Ibada ya sanamu hubeba pia yale tuyatukuzayo katika maisha yasiyosema chochote au kuthibitisha chochote kuhusu umilele wako, mfano; utajiri wako, umaarufu wako, cheo chako, na nguvu kimamlaka isiyoweza kukuokoa siku ya mwisho. Katika hili Musa anamsifu Mungu na kusema kwa furaha baada ya kuvuka  baharí ya Sham, “nitamwimbia Bwana, kwa maana ametukuka sana; Farasi na mpanda farasi amewatupa baharini,” Kut 15:1. Tumaini letu na Mungu ayafanyaye yote katika yote ndani yetu. Na  “kwa ajili ya hayo, wapenzi wangu, ikimbieni ibada ya sanamu,” 1Kor 10:14. Wakuabudiwa ni Mungu peke yake.

Kristo akiwa ndiye kielelezo chetu na kiunganishi chetu kama daraja kuelekea kwa Baba na Ufalme wake, tunaposhiriki Sakramenti ya Ekaristi, yaani, mwili na damu yake, kamwe tusivunje ushirika pamoja naye, jirani zetu, na Mungu. Mtume Paulo anatuachia changamoto hii: Kikombe kile cha baraka tukibarikicho, je! Si ushirika wa damu ya Kristo? Mkate ule tuumegao, si ushirika wa mwili wa Kristo?” 1Kor 10:16. Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, Kristo akiwa yote katika yote, yaani, Kanisa nasi tu viungo vyake katika mwili huo yaani, Kanisa, tu mfano na fumbo hili la Ekaristi Takatifu. Mtume Paulo alisema fumbo hili kama ifuatavyo, kwa kuwa mkate ni mmoja, sisi tulio wengi tu mwili mmoja; kwa maana sisi sote twapokea sehemu ya ule mkate mmoja,” 1Kor 10:17. Ndugu yangu, wewe na mimi si chochote bila Kristo mwenye kuyaratibisha yote na kuyaunganisha katika umoja na utofauti wake kama Kanisa na Sakrameti ya WOKOVU.

Kweli hii inapojidhihirisha, yaani, Kanisa kama Sakramenti ya Wokovu, na  Kristo kama mwili, nasi kama viungo vyake, sadaka tuzitoazo huwa na maana. Kinyume chake, yaani, kufifishwa kwa kweli hii, sadaka tuzituazo ukosa maana ndani na katika Kristo Yesu, na kumtukuza shetani aliyependa muda wote sifa pasipo siha. Kwa maana hiyo, vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu; nami sipendi ninyi kushirikiana na mashetani. Hamwezi kunywea kikombe cha Bwana na kikombe cha mashetani,” 1Kor 10:20. Michanganyo katika maisha ni saratani mbaya sana kiroho. Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani,” 1Kor 10:21. Ni heri kuwa joto au baridi kiimani kuliko kuwa vuguvugu kiimani.

Tumsifu Yesu Kristo!

Kila mtu ajaye kwangu, na kuyasikia maneno yangu na kuyatenda, nitawaonyesha mfano wake,” Lk 6:47


Tusali:-Ee Yesu, tujalie Imani thabiti. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario