Somo
I: Hab 1:2-3; 2:2-4
Zab/Kit: 95:1-2, 6-7, 8-9
Somo II: 2Tim 1:6-8, 13-14
Injili: Lk 17:5-10
Nukuu
“Ee Bwana, nilie hata
lini, wewe usitake kusikia? Nakulilia kwa sababu ya udhalimu, ila hutaki
kuokoa,” Hab 1:2
“Bwana akanijibu,
akasema, Iandike njozi ukaifanye iwe wazi sana katika vibao, ili aisomaye apate
kuisoma kama maji,” Hab 2:2
“Kwa sababu hiyo
nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono
yangu,” 2Tim 1:6
“Maana Mungu hakutupa
roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi,” 2Tim 1:7
“Ilinde ile amana nzuri
kwa Roho Mtakatifu akaaye ndani yetu,” 2Tim 1:14
“Mitume wakamwambia
Bwana, Tuongezee imani,” Lk 17:5
“Bwana akasema, Kama
mngekuwa na imani kiasi cha chembe ya haradali, mngeuambia mkuyu huu, Ng'oka,
ukapandwe baharini, nao ungewatii,” Lk 17:6
“Vivyo hivyo nanyi,
mtakapokwisha kuyafanya yote mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na
faida; tumefanya tu yaliyotupasa kufanya,” Lk 17:10
TAFAKARI:
“Tuongezee imani Bwana.”
Wapendwa wana wa Mungu
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 27 ya mwaka “C” wa Kanisa. Mama Kanisa
kwa namna ya pekee leo anatutaka tutafakari kwa makini kuhusu IMANI. Imani
ikiwa ni kuamini pasipo shaka yanayoonekana na yasiyoonekana, Ebr 11:1, Imani
thabiti ni suluhu ya mambo mengi tusiyoyajua bado. Imani thabiti utuzamisha
kwenye fumbo zima la maisha. Ukweli ni kwamba ingawa twaishi katika ulimwengu
huu yapo mambo mengi tusiyoyajua licha ya ufahamu wetu kama wanadamu.
Nabii Habakuki
aliyefanya unabii wake katika jamii isiyo amini katika haki na baadaye kuwa
chukizo kwa Mungu, anaona anguko kubwa sana mbele yake. Unabii huu
unafananishwa na kile alichokiona Yesu kutokea juu ya anguko la Yerusalemu na
mwisho wa nyakati, Mt 24. Pamoja na ukweli kwamba Nabii Hakukuki anaona uovu
ndani ya jamii yake, na watesi wao, yaani, mataifa yaliyokuwa yanawazunguka, pona
yao kama taifa kutoka ovu huo ni kusimama katika imani ya kweli na haki.
Kuushinda uovu uliosababishwa kwa kutokutenda haki, Mungu anamjibu na kusema,
“Tazama, roho yake hujivuna, haina unyofu ndani yake; lakini mwenye haki
ataishi kwa imani yake,” Hab 2:4.
Hata pamoja na jibu
hilo la Mungu, kuelewa ukweli huo na kuukubali kwa wezekana tu kwa Imani. Ni
kwa imani tu twaamini ushindi wa mwisho katika uaminifu wetu kwa Mungu. Sehemu
hii ya unabii wa Habakuki twaweza utafasiri katika mwelekeo wa fundisho kadiri
ya vitabu vile vya hekima. Naye Nabii Isaya katika kweli hii anasema, “Nyakati
zako zitakuwa nyakati za kukaa imara; za wokovu tele na hekima na maarifa;
kumcha Bwana ni hazina yake ya akiba,” Isa 33:6. Na katika mwono huo huo na
ulio wa juu zaidi, Mtume Paulo katika fundisho lake la kuhesabiwa haki kwa
Imani, anasema, “Kwa maana haki ya Mungu inadhihirishwa ndani yake, toka imani
hata imani; kama ilivyoandikwa, Mwenye haki ataishi kwa imani. Ni dhahiri ya
kwamba hakuna mtu ahesabiwaye haki mbele za Mungu katika sheria; kwa sababu
Mwenye haki ataishi kwa imani,” Rum 1:17; Gal 3:11. Hapa hakuna mkanganyo au
kupingana kwa kweli hiyo. Uaminifu kwa Mungu ndiyo upekee huo uokoao, na
uaminifu ndio uwezekano wa Imani kwa Mungu.
Mtume Paulo katika
mantiki hii anatutaka tuelewe kwamba wokovu siyo tu swala la imani kwa wakati
ujao, bali ni tendo la imani halisi, na chanzo cha uaminifu endelevu. Undani na
uzito wa fundisho hili la Mtume Paulo ndilo alisemalo kwa Timotheo kwamba,
“Shika kielelezo cha maneno yenye uzima uliyoyasikia kwangu, katika imani na
upendo ulio katika Kristo Yesu. Ilinde ile amana nzuri kwa Roho Mtakatifu
akaaye ndani yetu,” 2Tim 1:13-14
Katika somo letu la
Injili, Mitume wanamwomba Yesu awaongezee Imani, Lk 17:6. Kwa upande mwingine
twaweza kuona tatizo ambalo linawakabili
wafuasi wake Yesu-Wakristo, ikiwa ni pamoja na wewe na mimi kama wabatizwa.
Fundisho la Yesu, yaani, “Kama mngekuwa na imani kiasi cha chembe ya haradali,
mngeuambia mkuyu huu, Ng'oka, ukapandwe baharini, nao ungewatii,” Lk 17:6,
tunaweza lihusisha na habari ile ya uponywaji wa kijana yule aliyekuwa na pepo
mwenye kumtesa sana, na wanafunzi wake Yesu kushindwa kumtoa, Mk 9:18. Baada ya
Yesu kumkemea Baba wa kijana yule kwa kutokuwa na Imani, “Mara babaye yule
kijana akapaza sauti, akasema, Naamini, nisaidie kutokuamini kwangu,” Mk 9:24.
Ndugu yangu, Imani ya
kweli na thabiti hata kama ingekuwa ndogo kiasi gani inatokeo kubwa na la ajabu
katika maisha yetu, (Rej Mt 17:20, 21:21). Neno kuhusu mtumwa, Mt 17:7-10,
linatupatia fundisho la pekee. Yesu mwenyewe akiichukulia hali ya maisha yake
aliyokuwa akiyaishi licha ya ukuu aliokuwa nao-Mungu na Mwanadamu, mtumwa
anatufundisha na kutuonyesha fundisho hususi kuhusu habari njema. Mtumwa hawezi
jiinua na kujipongeza kwa kazi yake, zaidi ya kufanya na kutimiza wajibu wake.
Na hivi ndivyo Mtume Paulo asemavyo, “Maana, ijapokuwa naihubiri Injili, sina
la kujisifia; maana nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili!”
1Kor 9:16. Hakuna la kujisifia, zaidi ya kutimiza kwa uaminifu kile upaswacho
kutimiza.
Fundisho hili ya Yesu
katika Injili ya leo linaenda kinyume kabisa na mwono ule wa mafarisayo
waliojiongezea mapambio kwa kazi zao na kusahau ukweli kwamba siyo kazi katika
kazi ndizo zinazotuhesabia haki, bali ni neema na kwanyo ni zawadi ya Kimungu
kwetu. Kamwe hatuwezi jifananisha na vitu au idadi ya yale tuyatendayo, bali
roho na upendo ule utusukumao kufanya mambo hayo hata kama ni madogo na
macheche sana. Hivyo roho hiyo na upendo huo katika kutenda, na kwa kibali
chake Mungu na kwa kadiri ilivyompendeza twahesabiwa haki. Na hii ndiyo maana
ya maneno haya ya Yesu, kwamba, “Vivyo hivyo nanyi, mtakapokwisha kuyafanya
yote mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu
yaliyotupasa kufanya,” Lk 17:10. Kuna furaha ya kweli tunapojibandua kutoka
vitu na mali, na kutovifanya ndio mwisho wa kila kitu ingawa twavihitaji hapa
na pale.
Kwa maana hiyo, wewe na
mimi kama Wakristo tusipokuwa na Kristo Yesu katika maisha yetu tuna hasara
kubwa sana. Na ukweli ni huu; bila Kristo Yesu huna njia, kweli, na uzima, Yoh
14:6. Na kama huna hivi, je, uzima wa milele unawezekana kwako? Tunapomwamini
Kristo Yesu, Yeye hukaa kati yetu, naye huwa mwanga, kweli, na uzima wenyewe.
Ni kweli hapa na pale tutakutana na magumu fulani katika ufuasi wetu kwake. Ila
bila Kristo ni vigumu kuyabeba hayo na kuyashinda. Pamoja na udhaifu na uduni
wa mwanadamu kama asemavyo Mhaburi, 103:14-15, mtu huyu mara zote na muda
wowote anaitwa na Kristo Yesu.
Mtume Paulo licha ya
kugundua kwamba Timotheo ameitwa na Kristo Yesu katika kuiishi na kuihubiri
Injili, bado kuna mambo hayajakaa sawa. Katika kweli hii anamkumbusha Paulo
anamkumbusha Timotheo na sisi pia, “kuichochee karama ya Mungu, iliyo ndani
yako kwa kuwekewa mikono yangu. Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya
nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi,” 2Tim 1:6-7. Nguvu na neema hii yapaswa
kuonekana kwa Mkristo, na siyo kuwa goigoi.
Mtume Petro katika hili
(kutokuwa na woga na hofu) anasema, “Kwa hiyo ndugu, jitahidini zaidi kufanya
imara kuitwa kwenu na uteule wenu; maana mkitenda hayo hamtajikwaa kamwe,” 2Pet
1:10. Mkristo hana sababu ya kumwogopa mtu au kitu chochote kile, kwa sababu,
“Katika pendo hamna hofu; lakini pendo lililo kamili huitupa nje hofu, kwa
maana hofu ina adhabu; na mwenye hofu hakukamilishwa katika pendo,” 1Yoh 4:18.
Jambo la ajabu leo baadhi yetu Wakristo na tuliopewa dhamana na Mama Kanisa
tumekuwa goigoi hata kusimama tu katika kweli hofu imetupiga.
Je, Yesu anasema nini
kuhusu kumwonea haya mbele za watu katika kweli na haki? Ni vyema tukayakumbuka
vizuri maneno haya ya Yesu, Bwana, na Mwokozi wetu. Naye anasema, “Kila
atakayenionea haya mimi na maneno yangu, Mwana wa Adamu atamwonea haya mtu
huyo, atakapokuja katika utukufu wake na wa Baba na wa malaika watakatifu,” Lk 9:26.
Neno la Mungu ndilo litupalo nguvu na ujasiri. Na Imani na Upendo na nguvu ya
Roho Mtakatifu ndivyo vinavyotuwezesha kuushika ujumbe na mafundisho ya Mungu.
“Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina
langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia,” Yoh 14:26.
Na Roho huyu Mtakatifu
siyo roho mtakavitu, na mwenye kufanya kadiri ya matakwa yako au yangu. “Lakini
yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa
maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena,
na mambo yajayo atawapasha habari yake,” Yoh 16:13. Huyu ndiye Roho Mtakatifu,
na siyo roho mtakavitu. Siyo roho mtakavitu kwa sababu ya tabia yake kwamba;
moja, ni kuongoza katika kweli yote. Pili, hunena kwa shauri lake mwenyewe.
Tatu, huyasikia ayanenayo (kama upendo wa Mungu Baba na Mwana). Na mwisho,
upasha habari yake kwetu.
Kijana Tumaini Ndewenga
alitoka kijiji kilichoaminika sana kwa uchawi. Akiwa mwaka wa pili Chuo Kikuu
Baba yake mzazi alifariki. Kifo
cha Baba yake kilihusishwa na Mzee Change hapo kijijini. Mzee huyu akiisha
kunywa pombe na kulewa huaza kujisifia kuwa yeye ndiye gwiji la uchawi hapa
kijijini.
Akiwa kwenye msiba wa Baba yake, Mzee Change alisikika
kilabuni akisema, “na hako katoto kake kasomi nakapa siku 7 nako katamfuata
Baba yake huko aliko.” Maneno haya yalisambaa kwa haraka sana kijijini hapo
kama moto wa petroli, kwa sababu wasifu wa Mzee Change hakuna asiyeujua. Habari
hii ilipomfikia Tumaini alisema, “mwambieni Mzee Change yeye atakufa siku mbili
kabla ya hizo saba alizonipa kuisha.”
Kijana Tumaini ambaye
hakuwahi kuterereka hata siku moja kuhusu kile alicho amini juu ya uhai kuwa ni
mali na zawadi ya Mungu, habari ile haikumshtusha hata kidogo. Hata hivyo
Tumaini alitaka kutoa somo kwa wanakijiji wenzake. Somo lenyewe lilikuwa hivi;
zikiwa zimebaki siku siku mbili ili neno la Mzee Change kutimia juu ya Tumaini,
Mzee Change akiwa kilabuni anapata pombe muda wa saa moja usiku, Tumaini
alimchukua jogoo na kumnyonyoa angali mzima na kwenda moja kwa moja nyumbani
kwa Mzee Change na kumfunga Jogoo yule kwenye tendego la kitanda.”
Mzee Change kama
kawaida yake alirudi nyumbani akiwa kesha lewa na kujilaza kitandani. Ilipofika
majira ya saa kumi na moja alfajiri, jogoo yule alianza kuwika na sauti
ilisikika ikitoka uvunguni mwa kitanda. Ghafla Mzee Change alishtuka na
kutazama uvunguni. Mara alipomwona jogoo asiyekuwa na manyoya alifungasha kila
kilicho chake na kukimbia kijiji kile akiamini kifuatacho ni kifo kama alivyosema
Tumaini kabla ya siku mbili za mwisho alizotabiri Tumaini kufa yeye atakufa.
Ndugu yangu, simama
katika imani ya kweli!
Tumsifu Yesu Kristo!
“Ilinde ile amana nzuri kwa Roho
Mtakatifu akaaye ndani yetu,” 2Tim 1:14
Tusali:-Ee Yesu Mwema, tuongezee
Imani, ili tuwaze mara zote na kutenda Matakatifu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario