ALHAMISI WIKI YA 25 YA MWAKA-C
Somo:
Mhu 1:2-11
Zab/Kit:
90:3-4, 5-6, 12-13, 14, 17bc
Injili:
Lk 9:7-9
Nukuu:
“Na Herode mfalme
akasikia habari za yote yaliyotendeka, akafadhaika kwa sababu watu wengine
walisema ya kwamba Yohana amefufuka katika wafu,” Lk 9:7
“Lakini Herode akasema, Yohana nilimkata
kichwa; basi ni nani huyu ambaye ninasikia mambo haya juu yake? Akataka
kumwona,” Lk 9:9
“Mhubiri asema, Ubatili
mtupu, ubatili mtupu, mambo yote ni ubatili,” Mhu 1:2
“Mtu ana faida gani ya
kazi yake yote aifanyayo chini yajua?” Mhu 1:3
“Kizazi huenda, kizazi
huja; nayo dunia hudumu daima,” Mhu 1:4
TAFAKARI:
“Ubatili.”
Wapenda wana wa Mungu, kadiri ya Mhubiri, anayaona maisha si kitu wala chochote,
bali ni ‘ubatili mtupu, ubatili mtupu, mambo yote ni ubatili,’ Mhu 1:2. Swali
la msingi na la kujiuliza ni hili, nitawezaje kuitamani hiyo kesho kama sioni
maana ya leo? Kama tumeumbwa ili tuishi milele, na Mungu akaona inafaa tuwepo
ulimwenguni hapa, iweje tena niwe na mawazo haya kwamba mtu apata nini kwa kazi
yake yote, na kwa juhudi ya moyo wake alivyojitahidi chini ya jua?’ Mhu 1:3;
2:22.
Ndugu yangu, ni vyema
nikaelewa kwamba vyote vinavyoonekana na visivyoonekana alivyoviumba Mungu kwa
asilimia kubwa vinamlenga huyu mwanadamu aliyepewa heshima ya juu kabisa kwa
kuumbwa kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Ni katika hali na mazingira hayo, “Bwana aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu;
ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa,
aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni Bwana, wala hapana mwingine,” Isa 45:18.
Pamoja na mahangaiko na sintofahamu za maisha, ulimwenguni hapa pana kusudio la
Mungu katika maisha yetu. Hapa ndipo uwanja wa kujua kusudi la kuumbwa kwetu na
kujiandaa katika uzima ule wa milele. Duniani hapa ni pahala pa kujiandaa, na
siyo mwisho wetu.
Ni
kweli kwa wakati twaonekana kupita na dunia kubaki. Hatuna sababu ya kukata
tamaa kwanii huo ndio ukweli kama asemavyo Mhubiri kwamba, “Kizazi
huenda, kizazi huja; nayo dunia hudumu daima,” Mhu 1:4. Hata hivyo kwa muda mfupi tuwapo hapa duniani ni vyema kufahamu vizuri
kusudi la kuumbwa kwetu. Na kusudi la kuumbwa kwetu tungali hapa nduniani ni
kumjua Mungu, kumpenda Mungu, kumtumikia Mungu, na mwisho kurudi kwake
mbinguni.
Ni
kweli kabisa hapa na pale tutakatishwa tamaa, ila isiwe sababu ya kutokuona
kusudi la Mungu katika upana wa uumbaji wake. Ufanyalo zuri leo, kesho laweza
kufutwa kwa hila tu na kutoweka. Ila pamoja na hali hiyo, hatuwezi kufuta wema
wa lililo jema mbele ya macho ya Mungu. Kumbe si vyema kuutazama ulimwengu
mwono asi. Ukiruhusu hali hii, basi elewa ushajifungia mwenyewe katika gereza
fikra zako mwenyewe na kuliruhusu giza litawale maisha yako. Ni kweli isiyotia
shaka kwamba, kwa mwona na mtazama wako kama tokeo la mang’amuzi yako, “mambo
yote yamejaa uchovu usioneneka, jicho halishibi kuona, wala sikio halikinai kusikia,”
Mhu 1:8. Na hata kama huo ndio ukweli kwa kiasi
fulani, jambo hilo linapobaki katika historia yake, huendelea kuwa somo kwa
vizazi na vizazi. “Maana kuna mtu ambaye kazi yake ni kwa hekima,
na kwa maarifa, na kwa ustadi; naye atamwachia mtu asiyeshughulika nayo kuwa
sehemu yake. Hayo tena ni ubatili, nayo ni baa kuu,” Mhu 2:21.
Pamoja na mtizamo huu
wa Mhubiri, maisha ni zaidi ya yale tuyafanyayo leo au kuyamiliki. Jambo la
maana na muhimu ni kuwa huru nje ya yale tuyafanyayo na kuyamiliki. Tusipojibadua
katika haya, maisha hukosa maana na hasa pale yanapotoweka yale tuyafanyayo na
kuyamiliki. Ni swala la wakati kwamba itafika mahali
hatutaweza kufanya chochote. Ukweli ni kwamba, “yaliyokuwako ndiyo
yatakayokuwako; na yaliyotendeka ndiyo yatakayotendeka,” Mhu 1:9ab
Je, katika hali na
mazingira kama hayo ya kutokufanya chochote, utu wetu utatoweka kwa sababu tu
wazee? Utajiri na mali tulizonazo tumemilikishwa kwa muda tu na wakati ukifika
watamilikishwa wengine, nasi tutaondoka kama tulivyokuja bila chochote kwa
sababu, “Nchi
na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, Dunia na wote wakaao ndani yake,” Zab
24:1. Ndugu yangu, tunapojimilikisha yale ambayo kwa asili siyo yetu, mwisho wa
siku huwa ni ubatili na masikitika makubwa. “Kwa
kuwa (Mtu kama huyo) siku zake zote ni masikitiko, na kazi yake ni huzuni;
naam, hata usiku moyoni mwake hamna raha. Hayo nayo ni ubatili,” Mhu 2:23.
Ndugu
yangu, mtu wa kuyapa maana maisha yako ni wewe mwenyewe. Na kama leo unaishi
hapana shaka kwamba leo yako ni tokeo la jana yako, na kesho yako iwe nzuri au
mbaya yategemea sana unachofanya leo na sasa. Kumbe ni vyema nikawa na fanya
kila mara kama siyo kila siku zoezi la dhamiri. Dhamiri njema kama sauti ya
‘Mtoto mchanga na Mtakatifu ndani yetu,’ ukuzwa kwa kufahamishwa yaliyo mema,
mazuri, na yenye kulibeba tumaini la kweli. Huu ni mwaliko kwako na kwangu
kuzitafakari njia zetu kila siku.
Na katika kutafakari njia zako yatupasa kuhoji ukaribu wako
na Mwana wa Mungu. Herode anaingiwa na hofu baada ya kusikia habari za Yesu kwa
sababu alifikiri baada ya kumwangamiza Yohane Mbatizaji kwa kumkata kichwa siku
ya sherehe ya kuzaliwa kwake-Herode, angeendelea kuisahaulisha na kuiridhisha
dhamiri yake mbaya katika uovu. Herode anataka kumwona Yesu si kwa sababu
anataka kuanzisha uhusiano mzuri naye, bali bila shaka kutafuta namna ya
kumwangamiza ili asiwe tishio kwake kama alivyokuwa mtangulizi wake, Yohane
Mbatizaji.
Hivyo Herode anawajibu wale waliomletea habari juu ya Yesu
na kusema, “Yohana nilimkata kichwa; basi ni nani
huyu ambaye ninasikia mambo haya juu yake? Akataka kumwona,” Lk 9:9. Tukitaka
kuwa na amani ya kweli ndani yetu lazima tupatanishwe na Kristo. “Huyu manabii
wote humshuhudia, ya kwamba kwa jina lake kila amwaminiye atapata ondoleo la
dhambi,” Mdo 10:43. Na bila kujisalimisha kwa Kristo Yesu, Bwana na Mwokozi
wetu, yote ndani yetu ubaki kuwa ‘ubatili.’
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Yohana nilimkata kichwa; basi ni
nani huyu ambaye ninasikia mambo haya juu yake? Akataka kumwona,” Lk 9:9
Tusali:-Ee Yesu, tujalie neema ya kuyaona yote kama
uyaonavyo Wewe. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario