JUMATANO
WIKI YA 23 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 7:25-31
Zab/Kit: 45:11-12, 14, 15, 16, 17
Injili: Lk 6:20-26
Nukuu
“Basi,
naona hili kuwa jema, kwa ajili ya shida iliyopo, kwamba ni vema mtu akae kama
alivyo,” 1Kor 7:26
“Je!
Umefungwa kwa mke? Usitake kufunguliwa. Umefunguliwa? Usitafute mke,” 1Kor 7.27
“Akainua macho
yake akawatazama wanafunzi wake, akasema, Heri ninyi mlio maskini, kwa sababu
ufalme wa Mungu ni wenu,” Lk 6:20
“Heri
ninyi mlio na njaa sasa, kwa sababu mtashiba. Heri ninyi mliao sasa, kwa sababu
mtacheka,” Lk 6:21
“Heri
ninyi watu watakapowachukia, na kuwatenga, na kuwashutumu, na kulitupa nje jina
lenu kama neno ovu, kwa ajili ya Mwana wa Adamu,” Lk 6:22
“Furahiwani
siku ile na kuruka-ruka, kwa kuwa, tazama, thawabu yenu ni kubwa mbinguni,
maana, baba zao waliwatenda manabii vivyo hivyo,” Lk 6:23
TAFAKARI: “Maisha ni kuchagua, na ukishachagua ni kuwajibika ipasavyo.”
Wapendwa wana wa Mungu, hakuna lililo rahisi katika maisha. Kila aina
ya mtindo wa maisha una changamoto zake. Kuwajibika katika maisha kama ipasavyo
ndiko kutakako kuletea nafuu katika maisha hayo. Kwa maneno nyingine unapofanya
uzembe fulani na wakujitakia kwa kile ulichochagua kuishi na ndio wito wako, maisha
hayo lazima yatakuwiya magumu.
Hali hiyo ya uzembe ikupelekayo katika ugumu wa maisha, ni sawa na
kuhesabika kuwa huru kinadharia ila mfungwa kivitendo. Hutoweza kuwa na furaha
katika hali na mazingira kama hayo kimaisha. Mtume Paulo anapojitazama mwenyewe
na mtindo wa maisha-useja, anaona unafuu wake. Unafuu huo unaonekana kwake kwa
sababu kesha ipokea hali hiyo, na kuwajibika ipasavyo. Naye anasema, “basi, naona hili kuwa
jema, kwa ajili ya shida iliyopo, kwamba ni vema mtu akae kama alivyo,” 1Kor
7:26. Maisha ni kuwajibika.
Kama swali chokonezi, Mtume
Paulo anaenda kwenye uhalisia wa kile akisemacho. Naye anauliza, “Je! Umefungwa kwa mke? Usitake kufunguliwa.
Umefunguliwa? Usitafute mke,” 1Kor 7:27. Mwenzi wako wa ndoa hawezi kuwa mzingo
kwako kama ulichagua mwenyewe mfumo huo wa maisha kuwa bila shuruti na ukawa
tayari kuwajibika kwa kile ulichochagua. Ikiwa uliingia katika mfumo huo wa maisha
kwa vionjo na mbwembwe za wakati, jiandae kwa sintofahamu nyingi katika maisha
hayo. “Lakini,
kama ukioa, huna hatia; wala mwanamwali akiolewa, hana hatia; lakini watu kama
hao watakuwa na dhiki katika mwili nami nataka kuwazuilia hayo,” 1Kor 7:28. Dhiki huja pale unapoishi maisha bila malengo.
Maisha yoyote yale uongozwa na lengo.
Hata hivyo, pamoja na mipango mengi mtu aweza kuwa nayo katika maisha, lengo
kuu la maisha ni kuishi milele. Maisha ninayoishi leo na sasa yanisukume katika
ukamilifu wake, yaani, umilele licha ya udhaifu nilio nao hapa na pale. Maisha
ninayoishi yaniandae katika cheo changu halisi, yaani, utakatifu. Bila
utakatifu siwezi kuiona mbingu. “Lakini,
ndugu, nasema hivi, muda ubakio si mwingi; basi tokea sasa wale walio na wake
na wawe kama hawana; na wale
waliao kama hawalii; na wale wafurahio kama hawafurahi; na wale wanunuao, kama
hawana kitu,” 1Kor 7:29-30.
Maisha niliyochagua na
kuwajibika kwayo yasiwe ndiyo mwisho wa kila kitu, bali yawe chachu ya mimi
(kama mtawa na mkleri) au wote wawili (katika Sakramenti ya ndoa) kuufikia
UTAKATIFU. Hivyo mambo yale ya kujibovusha
kwa kupenda mno starehe, anasa na tafrija nijiepushe nayo. Niwe na kiasi kwa
kila kitu. Na hii ndiyo maana ya maneno haya kwamba, “Na
wale wautumiao ulimwengu huu, kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya
ulimwengu huu yanapita,” 1Kor 7:31
Ndugu yangu unayesafiri
nami katika tafakari hii, katika jamii yetu leo wapo watu wengi wanaolia kwa
shida mbalimbali na hawana pa kushika. Maisha kwao kila siku afadhali ya jana. Na
huu ndio ujumbe wa Yesu kwa wanafunzi wake; “Akainua
macho yake akawatazama wanafunzi wake, akasema, Heri ninyi mlio maskini, kwa
sababu ufalme wa Mungu ni wenu,” Lk 6:20.
Hata pamoja na hali hii
wapo wanaosheherekea na kutapanya vitu ovyo bila kuwajali wahitaji na wanyonge. “Lakini, ole wenu ninyi mlio na mali, kwa kuwa
faraja yenu mmekwisha kuipata,” Lk 6:24. Kristo
anatuambia wanaotaabika sasa katika ulimwengu huu watacheka na kufurahi milele.
“Heri ninyi mlio na njaa sasa, kwa sababu
mtashiba. Heri ninyi mliao sasa, kwa sababu mtacheka,” Lk 6:21
Kwa upande wa pili,
wote wanaocheka sasa na kuyafumba macho yao kwa kutokuona shida za wenzao hao
wataomboleza daima. “Ole wenu ninyi ambao
mmeshiba sasa, kwa kuwa mtaona njaa. Ole wenu ninyi mnaocheka sasa, kwa kuwa
mtaomboleza na kulia,” Lk 6:25. Je,
ndugu yangu kwa nini waandaa maombolezo ya kudumu katika umilele wote
unaposhindwa kunyoosha mkono wa heri kwa mwitaji unayeishi naye katika familia
yako, jumuiya yako ya kitawa, jumuiya yako ndogo ya Kikristo, ofisi moja ya
kazi, kigango chako, na hata parokia yako?
Vile vile katika jamii yetu leo wapo wengi
wanaochukiwa bila sababu ya msingi, wanaotengwa kutokana na misimamo yao katika
kweli na haki, wanaoshutumiwa na kunenewa uovu kwa sababu tu wanapenda kumuishi
Kristo na kuwa pembeni ya kundi ovu linalopendwa na wengi. Hawa Kristo anasema
thawabu yao ni kubwa mbinguni. “Heri ninyi
watu watakapowachukia, na kuwatenga, na kuwashutumu, na kulitupa nje jina lenu
kama neno ovu, kwa ajili ya Mwana wa Adamu. Furahiwani
siku ile na kuruka-ruka, kwa kuwa, tazama, thawabu yenu ni kubwa mbinguni,
maana, baba zao waliwatenda manabii vivyo hivyo,” Lk 6:22-23.
Kinyume chake ni wale wanaopenda kuonwa wema na
kusifiwa hata kama hawajafanya chochote. “Ole
wenu ninyi watu wote watakapowasifu, kwa kuwa baba zao waliwatenda manabii wa
uongo mambo kama hayo,” Lk 6:26. Hawa taji lao ni unabii
wa uongo ambalo halina thamani yoyote mbele ya Mungu. Hawa ndio wale wanaopoteza
muda na maisha yao kila siku kuwapendezesha watu na wao wenyewe kutaka
kupendezeshwa. Ni sawa na parachuti lililojaa hewa na kuelea juu kabisa angani
na mara hufikwa na kikomo linapokutana na ncha ndogo sana ya mwiba. Hewa yote
hutoweka na kusinyaa.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Heri
ninyi watu watakapowachukia, na kuwatenga, na kuwashutumu, na kulitupa nje jina
lenu kama neno ovu, kwa ajili ya Mwana wa Adamu,” Lk 6:22
Tusali:-Ee Yesu Mwema, tujalie moyo
wa huruma na upendo kwa wote tunaoishi nao. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario