JUMATATU
WIKI YA 23 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 5:1-8
Zab/Kit: 5:5-6, 7, 12
Injili: Lk 6:6-11
Nukuu
“Yakini
habari imeenea ya kuwa kwenu kuna zinaa, na zinaa ya namna isiyokuwako hata
katika Mataifa, kwamba mtu awe na mke wa babaye,” 1Kor 5:1
“Nanyi
mwajivuna, wala hamkusikitika, ili kwamba aondolewe miongoni mwenu huyo
aliyetenda jambo hilo,” 1Kor 5:2
“Kwa maana Pasaka wetu amekwisha kutolewa kuwa
sadaka, yaani, Kristo; basi na
tuifanye karamu, si kwa chachu ya kale, wala kwa chachu ya uovu na ubaya, bali
kwa yasiyochachika, ndio weupe wa moyo na kweli,” 1Kor 5:7b-8
“Lakini
yeye akayatambua mawazo yao, akamwambia yule mwenye mkono uliopooza, Ondoka,
simama katikati; akaondoka akasimama,” Lk 6:8
“Ndipo
Yesu akawaambia, Nawauliza ninyi, Je! Ni halali siku ya sabato kutenda mema, au
kutenda mabaya; kuponya roho au kuangamiza?” Lk 6:9
“Wakajawa na
uchungu, wakashauriana wao kwa wao wamtendeje Yesu,” Lk 6:11
TAFAKARI: “Nanyi
mwajivuna, wala hamkusikitika.”
Wapendwa wana wa Mungu, kutokuwa na hofu ya Mungu ndani mwa mtu
umuondolea aibu na woga wa kutenda yale yasiyo mpendeza Mungu. Mtu wa mtindo
huo ujazwa ujasiri kwa yasiyo dhaniwa kufanywa kwa akili ya kawaida. Hali na
mazingira haya yanaikuta jumuiya ya Korintho, hasa kwa swala la mahusiano ya
kimapenzi katika familia. Hii ni zinaa mbaya sana! Naye Mtume Paulo anasema, “Yakini habari imeenea
ya kuwa kwenu kuna zinaa, na zinaa ya namna isiyokuwako hata katika Mataifa,
kwamba mtu awe na mke wa babaye,” 1Kor 5:1. Pamoja na hali hiyo mbaya
kimaadili, jambo hilo haliwaogofi jumuiya ya Korintho. Badala yake wanajisifia
na kujipongeza. “Nanyi mwajivuna, wala hamkusikitika, ili kwamba
aondolewe miongoni mwenu huyo aliyetenda jambo hilo,” 1Kor 5:2. Jamii inayofurahia uovu anguko lake ni kubwa
sana.
Yaliyotokea Korintho nyakati hizo za
Mtume Paulo si mageni tuitazamapo jamii yetu leo. Zipo kesi nyingi tu za
mahusiano ya kimapenzi kati ya familia
na hata ndugu wa damu. Jambo hili linakuwa baya sana pale hali hiyo
inapochukuliwa kama jambo la kawaida licha ya kufanywa kwa usiri mkubwa. Hata
hivyo uzito wa jambo hili haupo tu kwa swala la mahusiano ya karibu na ya
kimapenzi kwa ndugu wa karibu na wa damu, bali uzito huu upo pale ambapo jamii
ufurahia uovu na hata kuubariki kuendelee.
Leo kwa sababu zetu binafsi na maslahi
binafsi, tunakosa nguvu ya kimaadili kukemea uovu kwa vile tu mtenda uovu huo
yu upande wetu. Ni swahiba wetu, nk. Mwono huu na kiwango hiki cha uelewa ni
anguko kubwa la jamii. Na hivi ndivyo asemavyo Mtume Paulo, “Kwa maana kweli,
nisipokuwapo kwa mwili, lakini nikiwapo kwa roho, mimi mwenyewe nimekwisha
kumhukumu yeye aliyetenda jambo hilo, kana kwamba nikiwapo,” 1Kor 5:3. Jamii
inapokosa ule uthabiti wa kusema, kuonya, na kukosoa katika maana ya kujenga,
kesho ya jamii hiyo inakabiliwa na giza nene sana. Uhalalishaji wa uovu ni njia
na sababu mojawapo ya kuiua dhamiri hai ndani ya mtu. Hali hii siyo ya kufumbia macho hata kidogo!
Kwa ushauri wake Paulo
anasema, lazima “kumtolea Shetani mtu huyo, ili mwili uadhibiwe,
ili na roho iokolewe katika siku ya Bwana Yesu,” 1Kor 5:5. Maana yake ni
kwamba, uovu ni uovu tu, hatuwezi kuuhalalisha kwa jambo au namna yoyote lile.
Tatizo kubwa hapa ni woga na unafiki wa kusema lililo kweli hasa pale jambo
hilo, yaani, uovu linapofanywa au kutendwa na kwenye nguvu na katili, au
mamlaka fulani.
Na mara zote swali
kubwa hubaki kuwa hili, ‘ni nani atakaye mfunga paka kengele?’ Badala yake
wengi kwa unafiki tunabaki kusifia hali hiyo na wakati mwingine kujisifu
wenyewe tukifikiri kwamba kwa kufanya hivyo
tutabaki salama. “Kujisifu kwenu si
kuzuri. Hamjui kwamba chachu kidogo hulichachusha donge zima?” 1Kor 5:6. Mambo
makubwa na yakushangaza machoni mwa watu leo yalianza kidogo kidogo na watu
kukaa kimya bila kuchukua hatua yoyote ile ya kukemea kwa sababu ya hofu, woga,
na unafiki.
Salama yetu ipo katika
kweli na haki. Na usalama upo pale tutakapo kuwa tayari kuona ukweli wa jambo
kama lilivyo, na siyo kama tulivyo. “Basi, jisafisheni, mkatoe ile chachu ya kale,
mpate kuwa donge jipya, kama vile mlivyo hamkutiwa chachu,” 1Kor 5:7. Chachu
hiyo ya kuona jambo kama lilivyo ipo ndani ya kila mmoja wetu. Na hii ndiyo
dhamiri hai ndani ya mtu. Tusiisaliti dhamiri hii kwa urafiki upofu au kujionea
huruma na kutaka watu watuonee huruma. “Kwa maana Pasaka wetu amekwisha
kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo; basi
na tuifanye karamu, si kwa chachu ya kale, wala kwa chachu ya uovu na ubaya,
bali kwa yasiyochachika, ndio weupe wa moyo na kweli,” 1Kor 5:7b-8. Kristo kwa
Mkristo ndiyo kielelezo halisi ya kupambana na uovu.
Mkristo mwenye kufumbia
macho uovu ajue kwamba haishi maisha ya ufufuko. Mkristo mwenye kuishi maisha
ya ufufuko uyatafuta yaliyo juu kule Kristo aliko. “Basi mkiwa mmefufuliwa
pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa
Mungu. Yafikirini yaliyo juu,
siyo yaliyo katika nchi,” Kol 3:1-2. Na mwenye
kuridhia na kuushabikia uovu, hata kama anaishi hana uhai ndani yake.
Kristo anatutaka tuwe
na uhai, na tena tuwe nao tele. Kristo Yesu ndiye Njia, kweli, na Uzima wetu,
Yoh 14:6. Kristo akiwa ndiye Mchungaji mwema wa kondoo zake, anajitofautisha na
mwivi mwenye nia ya kuiba na kuwachinja kondoo. Katika hili Yesu anasema, “Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu;
mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele. Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake
kwa ajili ya kondoo,” Yoh 10.10-11. Ni kwa namna hiyo ya uchungaji mwema, na akiwa katika sinagogi
akifundisha siku ya sabato, Yesu anakutana na mtu aliyepooza mkono, Lk 6:6.
Huyu ni kondoo wake na mwenye kuhitaji uponyaji. Kwa upande wa pili, Mafarisayo
walioishikilia sheria ya sabato hasa kutokufanya kazi, wanamtega Yesu waone
atakachofanya ili wawe na sababu ya kumtia hatiani, Lk 6:7. Watu hawa hawana
nia ya kuutokomeza uovu, bali kuuridhia na kuushabikia uovu kwa manufaa yao
binafsi.
Pamoja na hali na
mazingira hayo Yesu anasimamia mafundisho sahihi juu ya Upendo wa Mungu, na
kuuvunja ukimya ule wa uovu. Na ndivyo alivyo yatambua “
mawazo yao, akamwambia yule mwenye mkono uliopooza, Ondoka, simama katikati;
akaondoka akasimama,” Lk 6:8. Huu ndio ujasiri wa Mkristo hai na mwenye kuiona
kweli, kuisema kweli, na kuisimamia kweli. Na baada ya kuiona kweli, kuisema
kweli, na kuisimamia kweli, “ndipo Yesu
akawaambia, Nawauliza ninyi, Je! Ni halali siku ya sabato kutenda mema, au
kutenda mabaya; kuponya roho au kuangamiza?” Lk 6:9. Swali hili la Yesu limebeba mafundisho ya kweli
kuhusu huruma na upendo wa Mungu.
Lengo la Yesu hapa ni kuziamsha kama
siyo kuzifufua dhamiri zao zilizokuwa zimekufa. Aulizalo Yesu kwa Mafarisayo
anakuuliza wewe na mimi pia. Na mwisho katika kuisimamia kweli kisawa sawa,
Yesu “akawakazia
macho wote pande zote, akamwambia yule mtu, Nyosha mkono wako. Akaunyosha;
mkono wake ukawa mzima tena,” Lk 6:10. Na hili ndilo
anguko lao wale wauridhiao na kuushabikia uovu, “wakajawa
na uchungu, wakashauriana wao kwa wao wamtendeje Yesu,” Lk 6:11. Mwisho wa
chuki ni aibu!
Tumsifu Yesu Kristo!
“Je! Ni halali siku ya sabato
kutenda mema, au kutenda mabaya; kuponya roho au kuangamiza?” Lk 6:9
Tusali:-Ee Yesu, tufanye vyombo vyako vya haki,
kweli, Upendo na Amani. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario