miércoles, 14 de septiembre de 2016

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 24 YA MWAKA-C

IJUMAA WIKI YA 24 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 15:12-20
Zab/Kit: 17:1, 6-7, 8, 15
Injili: Lk 8:1-3
Nukuu
Basi, ikiwa Kristo anahubiriwa ya kwamba amefufuka katika wafu, mbona baadhi yenu husema kwamba hakuna kiyama ya wafu?” 1Kor 15:12

 “tena kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubiri kwetu ni bure na imani yenu ni bure,” 1Kor 15:14

 “Lakini sasa Kristo amefufuka katika wafu, limbuko lao waliolala,” 1Kor 15:20 

 “na wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba,” Lk 8:2 

na Yoana mkewe Kuza, wakili wake Herode, na Susana, na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao,” Lk 8:3 

TAFAKARI:Na kama Kristo hakufufuka, imani yenu ni bure.”

Wapendwa wana wa Mungu, katika ulimwengu huu wa vitu na ‘ponda mali kifo chaja,’ unajaribu kwa namna yoyote ile kuondoa uwepo wa Mungu, na kumwinua mwanadamu kama hatma ya kila kitu. Kwa nini uwepo wa Mungu ni tatizo katika ulimwengu huu wa vitu na ponda mali kifo chaja? Uwepo wa Mungu unasema kuhusu hatma ya mwanadamu ikiwa ni maisha baada ya kifo. Uwepo wa Mungu unasema na kuzisuta dhamiri zetu kuhusu; kweli, haki, upendo na huruma. Hizi ni tabia na hali ya Mungu. Binadamu katika ulimwengu wa vitu na starehe zake, ni aheri aishi bila uwepo wa Mungu kwani unamwogofya kuhusu kiyama na hukumu yake.

Mtume Paulo katika somo letu la leo anauweka bayana mpango mzima wa historia yetu ya wokovu na kile kitakacho jiri siku ya mwisho. Ukweli ni kwamba, “ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana,” Gal 4.4-5. Hivyo Kristo kama kielelezo chetu ndiye pia hitimisho letu na hakimu yetu.

Mateso na kifo chake Kristo yanasema zaidi kuhusu ukombozi (wokovu wa mwanadamu), na maisha ya umilele, yaani, ufufuko baada ya mateso na kifo cha Kristo- mtu yule mwenye haki. Katika mtazamo huu, mateso hayatenganishwi na ukombozi, na wala ukombozi hautenganishwi na ufufuko. Kwa maneno mengine, palipo na utukufu palitanguliwa na msalaba, na palipo na msalaba panatupeleka katika utukufu. Hali na mazingira haya ya Mateso, Msalaba, Wokovu, Ufufuko, na Utukufu yanasema sana kuhusu Yesu Kristo. Na mazingira hayo na hali hizo, zinasema sana kuhusu kiyama ya wafu.

Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, kupoteza muda wako na nguvu zako kupinga uwepo wa Mungu na kiyama ya wafu ni sawa na kutwanga maji katika kinu. Kama wabisha nipe hakikisho la wewe kwamba hauzeeki na hutokufa. Ukweli ni huu ambao wengi hatupendi kuusikia; “hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna afaye kwa nafsi yake,” Rum 14:7. Ni katika uelewa huu kwamba Mtume Paulo anauliza swali hili, Basi, ikiwa Kristo anahubiriwa ya kwamba amefufuka katika wafu, mbona baadhi yenu husema kwamba hakuna kiyama ya wafu?” 1Kor 15:12. Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo wasema sana juu ya upya wa maisha, na hesabu ya maisha hayo ya upyaisho siku ya mwisho-kiyama.

Wapendwa wana wa Mungu, yapo mambo mengi naweza kuwa na mashaka nayo, ila hili sina shaka nalo hata kidogo. Ukitazama wale wote walikuwa na hofu ya Mungu, na kwa namna moja au nyingine walianzisha mifumo ya maisha na kuwaongoza watu katika imani fulani, waliishi na mwisho wa siku walikufa. Ukweli huu ni pamoja na Kristo mwenyewe. Kristo alizaliwa kama Mungu na Mwanadamu  katika asili hizo mbili; na kwa namna ya pekee, aliishi na kuhisi uchungu na mateso kama wanadamu wengine ingawa hakutenda dhambi, 1Pet 2:21-22, na mwisho alikufa. Lakini jambo la pekee ni hili, alikaa kaburini siku ya kwanza, ya pili, na ya tatu alifufuka. Wengine, yaani, waazilishi wa mifumo ya maisha na hofu ya Mungu kiimani, tangu walipolala hadi leo hawajaamka. Hawa wanasubiri kuamshwa na Kristo siku ya mwisho.

Hivyo kwa kufufuka kwake Yesu Kristo kiyama ya wafu ipo. Tunatumaini kwamba nasi siku moja tutafufuliwa kutoka wafu kwa sababau kielelezo chetu, yaani, Yesu Kristo, kesha yashinda mauti, Ebr 2:9. Hivyo ni kiroja kufikiri kwamba, kama hakuna kiyama ya wafu, Kristo naye hakufufuka,” 1Kor 15:13. Kweli juu ya Kristo haituambii hivyo. Kristo kafufuka, na kiyama ipo. Hivyo ndugu yangu, mamlaka fundishi ya Kanisa yanapata uzito wake kwa sababu Kristo anayetangazwa na kuhubiriwa kesha fufuka. Ni katika mantiki hiyo kwamba, kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubiri kwetu ni bure na imani yenu ni bure,” 1Kor 15:14. Na lingekuwa jambo hili ni la kizushi tu (Ufufuko wa Kristo), basi lisingeweza kudumu kwa miaka hiyo yote zaidi ya 2000. Mungu bado anafanya kazi na watu wake kila siku. Ndugu yangu,Kristo amefufuka katika wafu, limbuko lao waliolala,” 1Kor 15:20. Na ndani na katika Kristo wote watahuishwa. 

Wapendwa wana wa Mungu, Injili ya leo inatufundisha jambo la muhimu sana kuhusu maisha yetu ya kiroho na mali tulizonazo. Jambo la muhimu siyo tu kusikia juu ya kule unakokwenda au unako tarajia kwenda, bali kujua njia itakayo kufikisha kule unapokwenda ua tarajia kwenda. Ukweli ni kwamba, waliokwisha kupata neema, baraka, na uponyaji ni wale tu waliojinyenyekesha kwa Kristo mwanakondoo wa Mungu, na kumtumikia kwa mali zao. Hawa ni wale walioifahamu njia ya kuwafikisha kule ilipo furaha yao ya ndani na ya kweli.

Hawa ndio wale wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao,” Lk 8:2a, 3b. Je, ndugu yangu, una uhusiano wa namna gani kati ya maisha yako ya kiroho na mali ulizokuwa nazo?

Tumsifu Yesu Kristo!

Lakini sasa Kristo amefufuka katika wafu, limbuko lao waliolala,” 1Kor 15:20


Tusali:- Ee Yesu, tuongoze katika njia iliyo sahihi kila siku ya maisha yetu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario