JUMAMOSI WIKI YA 26 YA MWAKA-C
Somo:
Ayu 42:1-3, 5-6, 12-16
Zab/Kit: 119:66, 71, 75, 91, 125, 130
Injili: Lk 10:17-24
Nukuu:
“Najua ya kuwa waweza
kufanya mambo yote, Na ya kuwa makusudi yako hayawezi kuzuilika,” Ayu 42:2
“Nilikuwa nimesikia habari zako, kwa kusikia
kwa masikio; Bali sasa jicho langu linakuona,” Ayu 42:5
“Tazama, nimewapa amri ya kukanyaga nyoka na
nge, na nguvu zote za yule adui, wala hakuna kitu kitakachowadhuru,” Lk 10:19
“Lakini, msifurahi kwa
vile pepo wanavyowatii; bali furahini kwa sababu majina yenu yameandikwa
mbinguni,” Lk 10:20
TAFAKARI:
“Furahini kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.”
Wapendwa wana wa Mungu,
Wanafunzi wa Yesu wale sabini,
wanarudi katika utume wao na kustajabia mambo makuu ya Mungu aliowatendea.
Uhusiano wetu mzuri na Mungu ni chanzo kikubwa sana cha furaha yetu ya kweli.
Lakini Yesu anawaambia wasiwe na furaha tu kwa sababu walimwona shetani
akianguka kutoka mbinguni kama umeme, bali ndani yao Mungu aweza kufanya mambo
makubwa zaidi ya hayo. “Tazama, nimewapa amri ya kukanyaga nyoka na n’nge, na nguvu zote za
yule adui, wala hakuna kitu kitakachowadhuru,” Lk 10:19. Huu ndio msingi wa furaha ya kweli kwa wale wote
wenye hofu ya Mungu. Mahusiano mazuri na Mungu, hutujengea uwezo mkubwa sana wa
kupambana na uovu.
Mara
tuyaonapo haya makuu yakifanyika ndani mwetu tusibweteke. Dunia hii tunapoishi
pamoja na uzuri wake na mambo yake, siyo mahali petu pa kudumu. Hapa ni mahali
tu pa maandalizi ya umilele. Ni jukumu la kila mmoja wetu kupafanya hapa
duniani kuwa sehemu nzuri zaidi ya kuishi huku tukijua siyo sehemu ya mwisho na
ya umilele. Maandalizi mazuri ya hapa duniani ndiyo jibu la uhakika wa maisha
hayo ya umilele. Hivyo furaha yetu kwa yote tutakayoyapata hapa duniani itupe
taswira halisi ya maisha baada ya haya. Kuhusu ukweli huu Yesu anawaonya
wanafunzi wake nasi pia kwa kusema, “Lakini, msifurahi kwa vile pepo wanavyowatii; bali furahini
kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni,” Lk 10:20. Furaha yetu isiwe tu ya
leo na kesho, bali furahi hii ipewe kibali na Mungu Baba wa Mbinguni. Tufurahi
na Mungu milele mbinguni.
Wapendwa wana wa Mungu, ufahamu wa siri na ukweli huu, Mungu anautoa kwa wanyenyekevu wake wa moyo.
Wanyenyekevu wa moyo hufunuliwa siri za Mungu kwa sababu wapo tayari kusikia,
kufanya, na kuishi kadiri ya mpango wa Mungu. Hivyo Yesu anamshukuru Mungu kwa
niaba ya wanyenyekevu wote wa Moyo na kusema, “Nakushukuru, Baba, Bwana wa
mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya umewaficha wenye hekima na akili; umewafunulia
watoto wachanga; Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyokupendeza,” Lk 10:21b. Ni
uchanga wetu kama watoto tupo tayari kujifunza, kusikiliza, kufanya, na kuishi
kadiri ya matakwa ya Mungu.
Mara baada ya kuzama katika fumbo zima la maisha yake, na
kugundua furaha na usalama wake upo kwa Mungu, na hasa pale alipojisalimisha
kwake, Ayubu anayaona makusudi ya Mungu katika maisha yake. Naye anamwambia
Mungu, “Najua
ya kuwa waweza kufanya mambo yote, Na ya kuwa makusudi yako hayawezi
kuzuilika,” Ayu 42:2. Mungu hujua mipango ya kila mmoja wetu kwa sababu kama
Baba utuwazia yaliyo mema siku zote, Yer 29:11. Ayubu anaona udogo wake katika
upendo huu wa Mungu ulio wa ajabu.
Ayubu kwa upande mwingine
anatukumbusha kuweka lawama mbali mara tupatwapo na majanga katika maisha.
Swali la kujiuliza katika hali hiyo ya sintofahamu ni hili; Je, Mungu anataka
kunifundisha nini kwa hili lililonitokea? Naye Ayubu anaihoji nafsi yake na kusema, “ni nani huyu
afichaye mashauri bila maarifa? Kwa maana, nimesema maneno nisiyoyafahamu,
Mambo ya ajabu ya kunishinda mimi, nisiyoyajua,” Ayu 42:3. Mungu aliyeonekana
kuwa mbali sana, na wa historia, sana anaonekana kuwa karibu na rafiki wa
ajabu. Kwa kinywa chake Ayubu anakiri kweli hii na kusema, “nilikuwa nimesikia
habari zako, kwa kusikia kwa masikio; Bali sasa jicho langu linakuona,” Ayu
42:5. Kumbe furaha ya kweli ni kujenga urafiki wa karibu na Mungu.
Ukaribu na Mungu
ukukumbusha udogo wako, na mapaswa yako katika kweli na haki. Ukaribu wako na
Mungu ukuongezea hofu ya Mungu ndani yako, na hivyo kuwa mikono salama zaidi.
Na ukaribu wako na Mungu ukunyenyekesha na kuwa tofauti katika, kuona, kuamua,
na kutenda. Na ndivyo ilivyokuwa kwa Ayubu anapojitazama na kuchukua hatu. Ni
kwa “sababu hiyo
najichukia nafsi yangu, na kutubu Katika mavumbi na majivu,” Ayu 42:6. Ukaribu
wako na Mungu ukuongoza katika toba ya kweli na majuto. Unyenyekevu ule
ukupelekeao kuona tofauti, kuamua tofauti, na kutenda tofauti, ni sawa na
kuzaliwa upya na katika nuru ya kweli,
Mungu mwenyewe.
Kuzaliwa upya huku na
kuwa katika nuru ya Mungu kunamrudishia hadhi yake Ayubu ikiwa ni pamoja na
yale aliyoyapoteza hapo mwanzo, Ayu 42:13-15. Hakika mtu yule amtegemeaye Bwana
hatopungukiwa na chochote. Mahangaiko na sintofahamu huwa za muda tu, na unapo
simama imara kiimani katika hali na mazingira haya ya sintofahamu, Mungu ubaki
kuwa mtetezi wako, mwaminifu kwako, na kukuongoza katika njia salama na
kukubariki. “Basi hivyo Bwana akaubarikia huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo
wake; naye alikuwa na kondoo kumi na nne elfu, na ngamia elfu sita, na jozi za
ng'ombe elfu, na punda wake elfu,” Ayu 42:12. Nani kama Mungu?
Ndugu yangu tulio
safiri zote katika tafakari hii, furaha ya kweli siyo kwa haya tunayojibovusha
nayo leo na sasa, bali pale tunapopewa kibali na Mungu na kutuheshabiwa haki.
Ayubu anapata kibali mbele ya Mungu na kuhesabiwa haki kwani Mungu alipendezwa
naye. “Kisha baada ya mambo hayo Ayubu
akaishi miaka mia na arobaini, naye akawaona wanawe, na wana wa wanawe, hata
vizazi vinne,” Ayu 42:16. Mungu upendezwa na kila mmoja wetu tunapokuwa
waaminifu katika Sura na Mfano wake, Mwa 1:27, kwa sababu ni kwa jinsi hiyo
alikuumba, na kwa namna hiyo ataka uwe.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nilikuwa nimesikia habari zako,
kwa kusikia kwa masikio; Bali sasa jicho langu linakuona,” Ayu 42:5
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, tujalie furaha ya ndani kwako na ndani yako. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario