jueves, 1 de septiembre de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 22 YA MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI YA 22 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 4:6-15
Zab/Kit: 145:17-18, 19-20, 21
Injili: Lk 6:1-5
Nukuu
Basi baadhi ya Mafarisayo wakawaambia, Mbona mnafanya lisilo halali siku ya sabato?” Lk 6:2 

Yesu akawajibu akawaambia, Hamkulisoma hata hilo alilolifanya Daudi, alipokuwa na njaa, yeye na wale aliokuwa nao?” Lk 6:3 

 “Akawaambia, Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato,” Lk 6:5 

 “Maana nadhani ya kuwa Mungu ametutoa sisi mitume mwisho, kama watu waliohukumiwa wauawe; kwa sababu tumekuwa tamasha kwa dunia; kwa malaika na wanadamu,” 1Kor 4:9

Sisi tu wapumbavu kwa ajili ya Kristo, lakini ninyi ni wenye akili katika Kristo; sisi tu dhaifu, lakini ninyi mna nguvu; ninyi mna utukufu, lakini sisi hatupati heshima,” 1Kor 4:10 

TAFAKARI:Sisi tu wapumbavu kwa ajili ya Kristo. Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato.”

Wapendwa wana wa Mungu, Kristo ni kielelezo cha yote yale tuyafanyayo ili tuurithi ufalme wa Mbingini tulioandaliwa na kuutamani. Kristo ndiye dira na mpango mzima wa Mungu kwa wokovu wetu. Na hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana,” Gal 4.4-5. Leo Yesu anataka Wayahudi, Wewe, na Mimi tuelewe kwamba yale yote tuyafanyayo yaendane na thamani ya upendo wa Mungu kwetu, na Yeye, yaani, Kristo ndiye msingi wa vyote.

 Yesu hapingi kuzishika sheria na kuzihemu, bali anachokipinga ni tabia ile ya kuzishika sheria hizo pasipo ufahamu wake na umaana wake. Sheria hizo wazishikazo Mafarisayo na waandishi badala ya kuwafanya watu wawe karibu na Mungu, zilizidi kuwatenganisha watu na Mungu. Ndiyo maana Wayahudi walikuwa wepesi sana kuona katazo la sheria na adhabu yake, kuliko elekezo la sheria katika ukamilifu. Basi baadhi ya Mafarisayo wakawaambia, Mbona mnafanya lisilo halali siku ya sabato?” Lk 6:2. Kwa kuziamsha dhamiri zao zilizolala, Yesu anawaonyesha mkanganyika wa sheria hizo wanazozishika bila ufahamu na umaana wake. Yesu akawajibu akawaambia, Hamkulisoma hata hilo alilolifanya Daudi, alipokuwa na njaa, yeye na wale aliokuwa nao?” Lk 6:3. Mfano huu ni moja tu ya mapungufu ya sheria zile walizokuwa wakizishika ambazo kwa uhakika haikuwa torati kama alivyowaachia Musa, bali tafarisi yake, yaani, Talmud. 

Tendo walilofanya wanafunzi wa Yesu, yaani, ‘siku ya sabato kupita katika mashamba, na kuvunja masuke na kuyala, wakiyapukusa-pukusa mikononi mwao, 1Kor 4:1, tendo hilo halikuwa tofauti na kile alichofanya Daudi, yaani, kuingia katika nyumba ya Mungu, akaitwaa mikate ile ya Wonyesho, akaila akawapa na hao wenziwe, ambayo si halali kuila ila kwa makuhani peke yao, Lk 6:4.  Sheria hizi na hasa tafasiri ile ya torati, Talmud, zilikuwa na mapungufu makubwa. Ni ukweli wa Mungu uliopotoshwa ili kukidhi mahitaji yao binafsi.

Kristo akiwa msingi wa maisha yetu na sababu ya yale yote tuyafanyayo, tutakuwa huru kweli kweli tukijua ni nani tunayemtumikia. Hivyo Yesu anawaambia Wayahudi “Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato,” Lk 6:5. Kristo ndiye mizania ya kweli kuhusu Mungu tunayemwamini na kumwabudu. Kristo ndiye anayejua siri ya ufalme wa Mungu. Ndugu yangu, Kristo ndiye njia, kweli na uzima, Yoh 14:6. Akiupigilia msumari wa mwisho, Yesu anasema, “hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka; nami nitamfufua siku ya mwisho,” Yoh 6:44. Kristo ndiye itimisho, Siku ya Bwana, na Bwana wa siku ya Bwana, yaani, Sabato.

Mtume Paulo na wenzake, walizama ndani kabisa katika fumbo hili la Kristo, yaani, kielelezo hai na itimisho la yote. Na ndivyo Paulo anavyowataka jumuiya ile ya Korintho wamuona Kristo kupitia maisha yao. Basi ndugu, mambo hayo nimeyafanya kuwa mfano wa mimi na Apolo kwa ajili yenu, ili kwamba kwa mfano wetu mpate kujifunza kutokupita yale yaliyoandikwa; ili mmoja wenu asijivune kwa ajili ya huyu, kinyume cha mwenziwe,” 1Kor 4:6. Kila mbatizwa na mfuasi wa Kristo, ni Kristo mwingine pale alipo. Maisha ya Mkristo lazima yaakisi maisha ya Kristo. Akiyaona maisha yake kama Mtume, Paulo anasema, maana nadhani ya kuwa Mungu ametutoa sisi mitume mwisho, kama watu waliohukumiwa wauawe; kwa sababu tumekuwa tamasha kwa dunia; kwa malaika na wanadamu,” 1Kor 4:9.

Ndani na katika Kristo, Mtume Paulo hayaogopi mateso kwa ajili ya Kristo. Mtume Paulo na wenzake hawahuzuniki wala kudhihakiwa kwa ajili ya Kristo. Na wala hawaoni aibu kuitwa wapumbavu kwa ajili ya Kristo. Nasi wafuasi wake Kristo hatuoni haya kudhihakiwa kwa ajili ya Kristo Yesu. Hivyo Mtume Paulo anaiambia jumuiya ile ya Wakristo wa Korintho kwamba, Sisi tu wapumbavu kwa ajili ya Kristo, lakini ninyi ni wenye akili katika Kristo; sisi tu dhaifu, lakini ninyi mna nguvu; ninyi mna utukufu, lakini sisi hatupati heshima,” 1Kor 4:10. Huu ni mtazama chanya wa Mkristo ambaye Kristo Yesu ni kielelezo na hitimisho la yote katika maisha yake.

 Je, waisikia kiu ya Kristo katika maisha yako? Kristo Yesu hubaki kuwa kiu yako kama Kristo Yesu ataendelea kuwa kielelezo na hitimisho la yote katika maisha yako. Katika kweli hii Mtume Paulo anasema, hata saa hii ya sasa, tuna njaa na kiu, tu uchi, twapigwa ngumi, tena hatuna makao,” 1Kor 4:11. Mkristo mwenye mwono huu chanya katika maisha yake amtazamapo Kristo, mara zote ukabiliana na uovu kwa wema. Na “kisha twataabika tukifanya kazi kwa mikono yetu wenyewe. Tukitukanwa twabariki, tukiudhiwa twastahimili,” 1Kor 4:12. Hali na mazingira haya ambapo Kristo huwa kila kitu kwetu, utujengea furaha ya ndani katika mateso.

Na ndivyo ilivyo kwamba, tukisingiziwa twasihi; tumefanywa kama takataka za dunia, na tama ya vitu vyote hata sasa,” 1Kor 4:13. Hii ni furaha tuipatayao katika mateso tuwapo ndani na katika Kristo Yesu. Na mwenye kuifahamu siri hii huwa baba wa wengi ambaye atawazaa wengi katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili. Mtume Paulo ni mfano halisi aliyeifahamu siri hii. Naye anasema, Kwa kuwa ijapokuwa mna waalimu kumi elfu katika Kristo, walakini hamna baba wengi. Maana mimi ndimi niliyewazaa katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili,” 1Kor 4:15. Je, wapenda kuwa mmoja katika siri hii?  Kama jibu ni NDIYO, basi anza leo kuwa na mwono chanya juu ya Kristo Yesu, na kuwa tayari kuuvaa unyenyekevu kama Kristo alivyo.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Tukitukanwa twabariki, tukiudhiwa twastahimili,” 1Kor 4:12b


Tusali:-Ee Yesu, kwako na kwako tu, tujalie furaha ya kweli. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario