sábado, 10 de septiembre de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 24 YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 24 YA MWAKA-C
Somo I: Kut 32:7-11, 13-14
Zab/Kit: 51:1-2, 10-11, 15, 17 (K) Lk 15:18
Somo II: 1Tim 1:12-17
Injili: Lk 15:1-32
Nukuu
Tena Bwana akamwambia Musa, Mimi nimewaona watu hawa, na tazama, ni watu wenye shingo ngumu basi sasa niache, ili hasira zangu ziwake juu yao, niwaangamize, nami nitakufanya wewe uwe taifa kuu,” Kut 32:9-10

“Na Bwana akaughairi ule uovu aliosema ya kwamba atawatenda watu wake,” Kut 32:14

Nami namshukuru Kristo Yesu Bwana wetu, aliyenitia nguvu kwa sababu aliniona kuwa mwaminifu, akaniweka katika utumishi wake; ingawa hapo kwanza nalikuwa mtukanaji, mwenye kuudhi watu, mwenye jeuri, lakini nalipata rehema kwa kuwa nalitenda hivyo kwa ujinga, na kwa kutokuwa na imani,” 1 Tim 1:12-13

Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi,” 1Tim 1:15

 “Mafarisayo na waandishi wakanung'unika, wakisema, Mtu huyu huwakaribisha wenye dhambi, tena hula nao,” Lk 15:2

Ni nani kwenu, mwenye kondoo mia, akipotewa na mmojawapo, asiyewaacha wale tisini na kenda nyikani, aende akamtafute yule aliyepotea hata amwone?” Lk 15:4

Nawaambia, Vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda ambao hawana haja ya kutubu,” Lk 15:7 

 “Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena; nifanye kama mmoja wa watumishi wako,” Lk 15:18-19

 “mleteni ndama yule aliyenona mkamchinje; nasi tule na kufurahi; kwa kuwa huyu mwanangu alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana. Wakaanza kushangilia,” Lk 15:23-24 

 “Akamwambia, Mwanangu, wewe u pamoja nami sikuzote, na vyote nilivyo navyo ni vyako,” Lk 15:31 

TAFAKARI: “Neema, Upendo na Huruma ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zako.”

Wapendwa wana wa Mungu, Leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 24 ya mwaka “C” wa Kanisa. Kwa namna ya pekee, masomo yetu yote ya leo yanakutafakarisha wewe na mimi kuiona ‘Neema, Upendo, na Huruma ya Mungu ambayo ni kubwa kuliko dhambi zetu. Na zaidi ya wazo kuu hilo la leo, masomo yetu haya ya leo yanahusisha ‘Neema, Upendo, na Huruma hiyo ya Mungu, Uzima na Utukufu ndani na katika Yesu Kristo.

Somo la kwanza Mungu anaonyesha huruma kwa watu wake kupitia Mtumishi wake Musa. Musa akiwa mlimani kupokea amri za Mungu, waliobaki chini wakisubiri maelekezo hayo ya Mungu, wanajifanyia mambo yao kwa kujichongea sanamu zoa kama utambulisho wa Mungu wao wa kutengeneza. Tendo hili lilikuwa chukizo kubwa kwa Mungu. Kwa hasiri hii Mungu anataka kuliangamiza taifa lote la Israeli kwa kutokuwa na subira. Bwana akamwambia Musa, “Mimi nimewaona watu hawa, na tazama, ni watu wenye shingo ngumu. Basi sasa niache, ili hasira zangu ziwake juu yao, niwaangamize,” Kut 32:9-10.

Kutokana na hasiri hii ya Mungu, Musa analiombea taifa lake, kwa kumkumbusha Mungu ahadi zake alizozitoa na kuzifanya na Ibrahimu, Isaka na Israeli. Kwa huruma yake Mungu, anaghairi hasira yake. “Na Bwana akaughairi ule uovu aliosema ya kwamba atawatenda watu wake,” Kut 32:14. Mungu wetu ni Huruma na mara zote yupo tayari kuhurumia na kutusamehe tunapoyakiri makosa yetu na kumrudia. Unapodondoka katika ubinadamu wako usisahau njia ya kumrudia Muumba wako, yaani, kufanya toba ya kweli na majuto ya dhambi zako.

Sakramenti ya Upatanisho/Kitubio ndiyo mlango sahihi wa kupita baada ya kuvurugwa na dhambi, na ndicho kisima sahihi na andaliwa cha kukoga na kujitakasa baada ya kuchafuka kwa dhambi. Kwenye Mlango huu na kisima hiki ndipo tunapokutana na Neema, Upendo, na Huruma ya Mungu. Huruma hii ya Mungu iwe pia ndani yangu hasa pale ninapotakiwa kutoa huruma hiyo bila masharti katika kusamehe. Huu ndio mwito wako na wangu ninapomwamini Mungu, na Mwanaye Yesu Kristo.

Wapendwa wana wa Mungu, kama wewe umebatizwa elewa kuwa unaishi ndani ya wokovu aliokupatia Bwana wetu Yesu Kristo kwa kifo chake pale msalabani. Ni jambo la kusikitisha sana kwamba tulio wengi hatuoni thamani ya wokovu huu tuliopewa bure kwa Upendo wa Mungu Baba kupitia Mwanaye Yesu Kristo. Tendo hili kwetu ni heshima kubwa sana, kwani tumenyanyuliwa katika udogo wetu kama vyombo vya udongo, 1Kor 15:49; 2Kor 4:7, na kuinuliwa palipo juu kabisa alipo Kristo na Mungu wetu.

Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, licha ya mastahili haya aliyopewa wanadamu, Mungu hakumuondolea mwanadamu huyu uhuru wake wa kuamua kutenda yaliyo mazuri au mabaya. Uhuru tuliopewa na Mwenyezi Mungu ni changamoto kubwa sana katika kuiishi Imani yetu. Uhuru huu mara nyingi unatutoa katika mstari wa kuyaishi yale yampendezayo Mungu. Ni kwa kupitia uhuru huu pia tunaweza kuziacha njia zetu mbaya na kumrudia Mungu kwa toba na majuto.

Hivyo basi, kila siku ya maisha yangu ninaitwa katika wongofu wa roho yangu. Siyo kuokoka, bali kuongoka kwani wokovu kesha tupatia Kristo. Wokovu ambao ni uwezekano wa kufanywa wana wa Mungu kesha tupatia Kristo mwenyewe kwa sadaka ya mateso na kifo chake pale msalabani. Hivyo yanipasa kuziishi ahadi zangu za ubatizo muda wote wa maisha yangu hapa duniani.

Ndugu yangu, miaka ile mitatu ya mwisho ya Yesu hapa duniani inathibitisha furaha ya Mungu, na hasa kwa yule mwenye kutubu na kuacha njia yake mbaya. Na huu ndio mpango wa Mungu katika historia nzima ya wokovu wa mwanadamu. Naye Mungu anasema, “sikufurahii kufa kwake mtu mwovu; bali aghairi mtu mwovu, na kuiacha njia yake mbaya, akaishi,” Eze 33:11a. Furaha ya Mungu ni kuanza naye upya, na Yeye utuchukulia katika upya wetu bila kuyahesabu yaliyopita. Mungu usamehe yote bila kuhoji historia yako ufanyapo toba ya kweli na majuto ya dhambi zako. Mfano mzuri ni simulizi hili la Mwana Mpotevu kutoka Somo letu la Injili, Lk 15:11-32.

Katika Injili hii ya leo, Yesu anazihoji dhamiri zetu katika kweli na haki, na kusema, Ni nani kwenu, mwenye kondoo mia, akipotewa na mmojawapo, asiyewaacha wale tisini na kenda nyikani, aende akamtafute yule aliyepotea hata amwone?” Lk 15:4. Ujumbe hapa ni kwamba, wewe na mimi kama viongozi na wenye dhamana mbele ya umma, tuwe tayari kukitetea kile kilicho dhaifu kwa sababu furaha ya kweli si usalama tu wa wengi bali sote tuwe salama. Kama kiongozi ni wajibu wangu kwamba wote niliokabidhiwa wafike salama na asipotee hata mmoja. Kiongozi anayekimbilia ukamilifu wa wengi, na kuwapoteza wachache na wakati mwingine bila kujua “kulikoni,” kiongozi huyo ni dhaifu sana. Yesu anasema, “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele,” Yoh 3:16 

Kamwe Mungu hawezi kufurahia tendo hilo la kutomjali mmoja katika hali na mazingira yake kwa sababu hata huyo unayemuona si mkamilifu kwa vigezo vya kibinadamu, ilhali mtu huyu yupo tayari kuiacha njia yake mbaya na kumrudia Mungu, ila wewe kwa kuishikilia sheria, tena mbovu haupo tayari kufikiri nje ya sheria ile, Mungu anakiu naye, Yoh 19.28. Ndugu yangu, tambua kwamba mtu huyo ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, Mwa 1:27. Na kwa sababu hiyo Mungu hachoki kutafuta kile kionekacho dhaifu na kilichopotea. Katika hili Yesu anasema, Vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda ambao hawana haja ya kutubu,” Lk 15:7 

Tunahesabiwa haki si kwa matendo yetu mema tu na ukaribu wetu mbele ya Mungu, bali kwa utayari wetu wa kuona udhaifu ndani yetu na kufanya toba ya kweli na majuto ambayo kwa kutenda dhambi ndiyo sababu kubwa leo ya mwendelezo wa mateso ndani na katika Kristo Yesu.

Wapendwa katika Kristo, leo huruma na msamaha huo tunaupata kupitia Kristo mwenyewe ambaye ndiye  Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli,” Yoh 1:14. Leo pia kwa namna ya pekee huruma na msamaha huo wa dhambi tunaupata kupitia Mama Kanisa kama Sakramenti ya wokovu wetu.

Mamlaka hayo (Kanisa kama Sakramenti ya wokovu) kayatoa Kristo mwenyewe katika Kanisa, na kwa watumishi wake waliohesabiwa haki hiyo na Mama Kanisa kabla ya kupaa kwake Mbinguni. Naye akiisha kusema hayo, akawavuvia, akawaambia, Pokeeni Roho Mtakatifu. Wo wote mtakaowaondolea dhambi, wameondolewa; na wo wote mtakaowafungia dhambi, wamefungiwa,” Yoh 20:22-23. Hivyo ndugu yangu, Mungu Baba kupitia Mwanaye Mpenzi na Kanisa lake, ananialika kupatanishwa naye kila ninapo pumzi yake. Je, ni kwa nini sasa yatupasa kupita kwa Kristo ili niupate huo upatanisho na Mungu?

Wapendwa wana wa Mungu, sehemu ile ya 2Kor 5: 17-21, inatupatia jibu halisi na kamili ‘kwa nini lazima Kristo.’ Ni kwa kupitia Kristo na ndani ya Kristo tunakuwa viumbe vipya na kuanza upya katika safari ya uzima wa milele. Ni kwa sababu hiyo, hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya,” 2Kor 5:17. Na nikupitia Kristo tu ambaye, Yeye asiyejua dhambi (Mungu) alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu katika Yeye,” 2Kor 5:21. Hivyo kwa mantiki hii, hakuna miongoni mwetu awezaye kujihesabia haki pasipo Kristo. Haitawezekana hata kidogo ndungu yangu!

Ni kwa ukweli huo kwamba, ‘siwezi jihesabia haki pasipo Kristo,’ kweli ambao inapingwa vikali na Mafarisayo na Waandishi. Watu hawa walijihesabia haki pasipo haki ya kweli ambayo yatoka kwa Mungu mwenyewe. Yesu anawakemea wazi wazi na kutoa angalizo kwetu kwa kusema, Waandishi na Mafarisayo wameketi katika kiti cha Musa; basi, yo yote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi,” Mt 23:2-3. Kwa mtazamo huu wa Mafarisayo na Waandishi, hawakuona haja ya majuto ya dhambi zao, na hata kufanya toba ya kweli.

Mafarisayo na Waandishi walijiona safi na kamili, na hivyo hawakuhitaji Huruma na Msamaha wa Mungu. Ukaribu wa Yesu na ushiriki wake na wokosefu kwa lengo la kuwatoa katika hali zao duni na udhaifu ulio tokana na dhambi, tendo hili linaonekana kikwazo kwa Mafarisayo na Waandishi. Na hii ndiyo sababu ya manung’uniko yao kwa Yesu, “Mtu huyu huwakaribisha wenye dhambi, tena hula nao,” Lk 15:2. Mfano wa Mwana Mpotevu katika Injili ya leo unajibu manung’uniko hayo ya Mafarisayo na Waandishi. Mfano huu unaweka wazi ukweli huu kwamba, ‘Neema, Upendo, na Huruma ya Mungu ni KUBWA kuliko dhambi za mwanadamu pale mwanadamu huyo afanyapo majuto na toba ya kweli.’

Kwa kujibu manung’uniko waliyokuwa nayo Mafarisayo na Waandishi juu wa ukaribu aliokuwa nao Yesu kwa wadhambi, Injili inahainisha wahusika wakuu watatu; Baba Mzazi, Mwana Mpotevu, na Kaka ya Mwana mpotevu. Wengine ni watumishi au watumwa wa Baba mzazi wa Mwana Mpotevu, na marafiki wa Mwana Mpotevu. Mwana mpotevu, tena aliye mdogo katika familia hii, anafanya kitu ambacho si cha kawaida katika jamii. Kitendo cha kuomba urithi au sehemu ya mali yake kabla ya kifo cha baba yake, kilimaanisha kumtakia mabaya Baba yake. Ni kutokumtambua Baba yake. Ni kumchukulia Baba yake kama marehemu.

Kwa upande wa Baba, na kwa tabia na asili yake, anaonyesha mambo makuu matatu; Ubaba Kamili, Upendo usiyo shaka na mipaka, na Ustahimilivu katika tendo zima la Huruma ya kweli. Hivyo ni kutokana na Upendo huo aliokuwa nao kwa wana na familia yake, anakubali aibu hiyo, na kufanya kadiri ya matakwa ya mwanaye. Baba anampa sehemu ya urithi wake. Hata baada ya siku si nyingi, yule mdogo akakusanya vyote, akasafiri kwenda nchi ya mbali; akatapanya mali zake huko kwa maisha ya uasherati,” Lk 15:13.Yaliyompata kijana huyu wote tunafahamu vizuri simulizi hili.

Ndugu yangu, kutenda makosa ni hali yetu sote wanadamu. Ila tofauti ipo hapa; unapotambua umefanya kosa na kuchukua hatua kwa uliyoyafanya ndiko kunakokurejeshea hadhi na heshima yako tena. Alipozingatia moyoni mwake, alisema, Ni watumishi wangapi wa baba yangu wanaokula chakula na kusaza, na mimi hapa ninakufa kwa njaa,” Lk 15:17. Baada ya kutindikiwa vingi na mambo kwenda ndivyo sivyo, Mwana Mpotevu analiona kosa lake na anakiri kwa matendo na maneno, “Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena; nifanye kama mmoja wa watumishi wako,” Lk 15:18-19. Ndugu yangu, hii ndiyo toba na majuto ya kweli juu ya dhambi. Tunachoangalia si aibu tutakayopata, bali Huruma, Msamaha, na Mastahili tunayotarajia kuyapata kwa Upendo wake Mungu kwa kufanya toba ya kweli.

Mpendwa katika Kristo, ninapodondoka kwa sababu ya dhambi, nisione aibu kuamka na kuomba msamaha kwa Muumba wangu. Yeye Mungu anasema, “mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja, Mwenyezi.” Ufu 1:8. Je, kuna mwingine wa  kumkimbilia zaidi ya Mungu wetu? Mungu aliye Upendo hana mipaka wala masharti ya pekee ninapomrudia. Mungu anasema, “nawapenda wale wanipendao, na wale wanitafutao kwa bidii wataniona,” Mit 8:17.

Upendo wa Baba hauna mfano. Baba huyu anapomwona mtoto wake, hapendi na wala haitaji kujua historia ya yale maovu aliyofanya. Furaha yake ni kumwona kama alivyo na anajua kurudi kwake ni toba ya kweli. Na hivi ndivyo ilivyo kwa Mungu wetu wa Upendo, Huruma, na Neema. Anachofanya Baba katika simulizi hili la Mwana Mpotevu ni kumrudishia stahili na hadhi yake kama mwana na mmoja wa familia yake. Alipomwona tu mwanaye,  baba aliwaambia watumwa wake, Lileteni upesi vazi lililo bora, mkamvike; mtieni na pete kidoleni, na viatu miguuni,” Lk 15:22. Mwana Mpotevu anarudishiwa hadhi na mastahili yake kama mwana familia kama ilivyo na itakavyo kuwa mbele ya Mungu tunapofanya majuto na toba ya kweli. 

Tendo hili la Baba, wapendwa wana wa Mungu, linakuwa sononeko la Kaka ya Mwana Mpotevu. Haoni maana ya furaha hii na sababu ya kuwa hai mdogo wake. Akakasirika, akakataa kuingia ndani. Basi babaye alitoka nje, akamsihi,” Lk 15:28. Ndugu yangu, katika safari ya wokovu, usipende kujitazama mwenyewe. Wokovu ni kwa wote na nifuraha ya Mungu na kwa wote wenye mapenzi mema, yaani, Watakatifu wa Mungu. Tendo la wokovu ni furaha na sherehe kwa wote kwa sababu tunairudia sura yetu halisi, yaani, sura ile na mfano ule wa Mungu tulioumbwa nayo, mwa 1:27. Sura hii ufifishwa na kufubaishwa na hali yetu ya dhambi.

Kwa furaha ya kumuona tena Mwana wake aliyepote, Baba anatoa maelekezo na kusema, Mleteni ndama yule aliyenona mkamchinje; nasi tule na kufurahi; kwa kuwa huyu mwanangu alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana. Wakaanza kushangilia,” Lk 15:23-24. Katika mfano huu, Yesu anawakemea Waisraeli na hasa Mafarisayo na Waandishi ambao wanahuzunika kwa yale ayafanyayo Yesu kuufunua Upendo wa Mungu Baba.

Wapendwa katika Kristo, yatupasa kutiana moyo na kufurahi mwenzetu anapomwongokea Mungu na kuishi maisha ya kumpendeza Mungu. Mara nyingi hatuachi kuwasema vibaya wale wanaojitahidi kuishi njia impendezayo Mungu. Tunawapachika majina mengi, na kuwakatisha tamaa kabisa. Kwa upande wetu, mwenzetu anapojitahidi kuishi vizuri, basi iwe changamoto ya mimi kufanya vizuri. Hivyo basi tulio karibu na mwanga wa Mungu, na kuenenda kadiri ya upendo wa Mungu, tuwe na huruma kwa wote wanaomrudia Muumba wao tukijua kwamba, tu pamoja na Baba na Upendo wake sikuzote, na vyote alivyo navyo ni vyetu sote, Lk 15:31. Hivyo yanipasa kuuvua ubinafsi wangu na niwe na huruma ili nione hitaji ya mwingine, mwili na kiroho.

Ndugu yangu, wakati ndiyo sasa! Kaa na tafakari namna utendavyo. Je, ninafanya kadiri ya mapenzi ya Mungu au najitazama mwenyewe? Urithi wako ni fursa uliyo nayo sasa katika utendaji. Niepuke sononeko la Mwana yule Mkubwa, “Tazama, mimi nimekutumikia miaka mingapi hii, wala sijakosa amri yako wakati wo wote, lakini hujanipa mimi mwana-mbuzi, nifanye furaha na rafiki zangu; lakini, alipokuja huyu mwana wako aliyekula vitu vyako pamoja na makahaba, umemchinjia yeye ndama aliyenona,” Lk 15:29-30. Je, kwa kuwa karibu na Baba ninatumia fursa hiyo vizuri kuonja Huruma na Upendo wake kwangu? Na kama Mwana Mpotevu, Je, baada ya kuishi ovyo kwa muda wote huo, nipo tayari kufanya toba ya kweli na kuiacha njia hiyo?

Basi yanipasa nielewa kwamba nafasi niliyo nayo ni leo na sasa tu. Ni vyema nikachukua hatua sasa na kuutafuta uso wa Bwana. “Mtafuteni Bwana, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya Bwana,” Sef 2:3. Kukengeuka kwangu na kunakonifanya kuwa nje ya Imani yangu kunatokana kwanza kabisa na ujinga wangu, yaani, kutokujua thamani ya Imani yangu, na lengo lake katika safari ile ielekeayo katika uzima wa milele.

Mtume Paulo ni mmoja ya watu walioishi vibaya na baada ya kujitambua, hasa pale alipojeuzwa na Kristo anayasema haya kinabaugaba. Nami namshukuru Kristo Yesu Bwana wetu, aliyenitia nguvu kwa sababu aliniona kuwa mwaminifu, akaniweka katika utumishi wake; ingawa hapo kwanza nalikuwa mtukanaji, mwenye kuudhi watu, mwenye jeuri, lakini nalipata rehema kwa kuwa nalitenda hivyo kwa ujinga, na kwa kutokuwa na imani,” 1 Tim 1:12-13. Kristo akishakutembelea na kukugusa huwezi kubaki katika hali yako ya zamani.

Tendo hili ndilo lijulikanalo kama KUONGOKA. Mt. Augustino ni mfano mwingine wa wale walioacha njia zao mbaya na kuongoka. Tusomapo kitabu chake cha Maungamo tunaona wazi tendo hili la kuongoka. Mt. Augustino anafafanua kwa undani alivyoutafuta ukweli sehemu mbalimbali na kusahau kwamba ukweli huo alikuwa nao ndani yake. Alipoigusa Neema ile ya Wokovu wa Kristo ndani yake yote yalifunuliwa na akawa mpya ndani na katika Kristo.

Ni vyema nikaelewa vizuri njia ya wokovu wangu kwa mimi niliye batizwa na mfuasi wa Kristo. Ni kweli kwamba pasipo Kristo na ndani ya Kristo Wokovu huo kwangu hautawezekana. Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi,” 1Tim 1:15. Hata pamoja na ukweli huo, yote hufanyika kwetu siyo kwa mastahili yetu, bali kwa kuhesabiwa haki na Mungu na kwa kupitia Mwanaye Mpenzi Yesu Kristo. Na kwa ajili hii nalipata rehema, ili katika mimi wa kwanza, Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele,” 1Tim 1:16.

Kuhesabiwa haki na Mungu na kwa kupitia Mwanaye Mpenzi Yesu Kristo, kunaturejesha katika uhasili wa Mungu, yaani; Neema, Upendo, Huruma, Haki, na Msamaha. Naam, Yeye ni Mfalme wa milele, asiyeweza kuona uharibifu, asiyeonekana, Mungu peke yake, na iwe heshima na utukufu milele na milele. Amina,” 1Tim 1:17.

Mama Valensa Misalaba alibahatika kupata watoto watatu, mmoja wa kiume ambaye ndiye wa kwanza, na wawili wakike. Mtoto wake wa kiume-Mathayo, alikuwa na umri wa miaka 7, na hao wa kike wawili, moja alikuwa na miaka mitatu na huyo wa mwisho alikuwa na miezi sita.

Ndoa ya Mama Valensa Misalaba haikuwa na furaha hata kidogo. Kipigo kutoka kwa mme wake kilikuwa kitu cha kawaida na kufikia hasa anapokuwa amelewa. Na ikipita siku mumewe hajalewa ndiyo furaha na amani ingawa katika hali kama hiyo mmewe haachi kuwa mkali na katili katika mazungumzo ya kawaida tu.

Siku mmoja jioni, na baada ya mmewe kuondoka kwenda kulewa pombe za kienyeji, Mama Valensa Misalaba alichukua uamuzi mgumu wa kutoroka na watoto wake kwenda kwa Kaka yake ambaye alikuwa anaishi umbali wa mwendo wa masaa sita hivi kwa bus. Mama Valensa hakuwa na wazazi kwani wote walifariki kipindi yeye akiwa na miaka 11. Mfukoni Mama huyu alikuwa na shilingi 50 TU.

Usafiri wa wakati ule kutoka hapo alipo hadi kufika kwa Kaka yake iligharimu shilingi 250. Hata hivyo kutokana na hali na mazingira yale ya mateso hakuwa na namna nyingine zaidi ya kutoroka. Kwa vile alikuwa anaishi karibu na Barabara kuu ya Mabasi, Singida-Babati, alikuwa na uhakika wa kupata usafiri kuelekea eneo la Babati alipokuwa anaishi Kaka yake.

Kufika tu barabara kuu alipunga mkono na bus moja  lililokuwa linatoka Singida kuelekea Arusha lilisimama. Akaingia ndani ya bus yeye na watoto wake huku Konda wa bus lile akimwambia, “Mama uandae nauli yako mkononi.” Baada ya mwendo wa nusu saa hivi, Konda alimwendea Mama Valensa na kudai nauli. Mama Valensa kabla ya kutoa nauli ile alianza kumwomba radhi Konda yule na kusema, “Kama yangu na mdogo wangu, nina shilingi 50 tu hapa nilipo, na ninajua nauli ni shilingi 250. Nimelazimika kusafiri muda huu kuelekea kwa Kama yangu huko Babati kuepuka kipigo na kifo kutoka kwa mume wangu,” Mama Valensa alikuwa anayasema hayo huku akimwonyesha makovu na majeraha aliyokuwa akiyapata kutoka kwa Mume wake.

Kwa hasira na bila kuwa na chembe ya huruma, Konda alimjibu, “Wewe Mama acha kuuza sura. Hizi hadithi nimezisikia sana huku barabarani. Ninachotaka ni nauli kamili la sivyo unashuka mbugani hapa uliwe na simba.” Jambo la ajabu katika sintofahamu ile kati ya Konda na Mama Valensa, huku watoto wake wakilia kwa hofu ya kushushwa, hakuna mtu yeyote kati ya abiria wale aliyefungua mdogo wake kumsaidia Mama Valensa.

Ndipo kwa hasira Konda alimwamuru Dereva asimamishe bus na Mama Valensa na watoto wake washuke. Walishuka na kutupiwa vitu vyao nje kusiko na utaratibu. Baada ya mwendo wa dakika kama tano hivyo, dereva wa bus lile aliona kwa mbele kundi kubwa la simba wakielekea kule walipotoka. Hakika alijua kitakachotokea hata hivyo akufanya chochote.

Na baada ya kama nusu saa hivi simba wale waliwakaribia, na Mama Valensa alijua kitakachotokea. Alimwambia mwanaye Mathayo apande juu ya Mti ulikuwa karibu, naye na watoto wake wawili wa kike aliwakumbatia kwa kuwafunika kanga. Simba wale mbarara waliokuwa na njaa waliwavamia na kuwachana vipande vipande. Mathayo alipiga yowe kwa nguvu zake zote lakini sauti ile haikusikika popote.

Kulipoanza kupambazuka, Mathayo aliona gari dogo kwa mbali na ndipo alipopiga kelele kupata msaada. Gari lile lilisimama na ndipo Mathayo aliposimulia haya yote. Watu wale na gari lile walikuwa ni maafisa wa wanyama pori.

Ndugu yangu, simulizi hili ambalo lilitokea miaka mingi ya nyuma iliyopita, (miaka ya 90), linanikumbusha wajibu wangu na nafasi niliyo nayo kwa mwitaji yeyote yule. Katika hali na mazingira kama ya Mama Valensa, yanipasa kuvivaa viatu vyake, na kuwa na huruma na upendo. Konda angeyaokoa maisha ya Mama Valensa na binti zake wawili kama angevivaa viatu vya Mama Valensa, yaani, kusikiliza shida na mahangaiko yake. Jamii yetu leo wapo wengi kama Mama Valensa wanao hitaji upendo na huruma kama Mungu anavyotukirimia kila siku bila mipaka.

Tumsifu Yesu Kristo!
Mwanangu, wewe u pamoja nami sikuzote, na vyote nilivyo navyo ni vyako. Tena, kufanya furaha na shangwe ilipasa, kwa kuwa huyu ndugu yako alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana,” Lk 15:31-32


Tusali:-Ee Yesu Mwema, nijalie moyo wa huruma na upendo. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario