ALHAMISI
WIKI YA 23 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 8:1b-7, 11-13
Zab/Kit: 139:1-3,
13-14ab, 23-24
Injili: Lk 6:27-38
Nukuu
“Lakini mtu
akimpenda Mungu, huyo amejulikana naye,” 1Kor 8:3
“Na yule aliye
dhaifu aangamizwa kwa ujuzi wako, naye ni ndugu ambaye Kristo alikufa kwa ajili
yake,” 1Kor 8:11
“Hivyo,
mkiwatenda dhambi ndugu zenu na kuitia jeraha dhamiri iliyo dhaifu, mnamtenda
dhambi Kristo,” 1Kor 8:12
“Lakini nawaambia
ninyi mnaosikia, Wapendeni adui zenu, watendeeni mema wale ambao wawachukia
ninyi, wabarikieni wale ambao wawalaani ninyi, waombeeni wale ambao
wawaonea ninyi,” Lk 6:27-28
“Maana mkiwapenda
wale wawapendao ninyi, mwaonyesha fadhili gani? Kwa kuwa hata wenye dhambi
huwapenda wale wawapendao,” Lk 6:32
“Bali wapendeni
adui zenu, tendeni mema, na kukopesha msitumaini kupata malipo, na thawabu yenu
itakuwa nyingi; nanyi mtakuwa wana wa Aliye juu, kwa kuwa yeye ni mwema kwa
wasiomshukuru, na waovu,” Lk 6:35
“Basi,
iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma,” Lk 6:36
TAFAKARI: “Basi,
iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma.”
Wapendwa wana wa Mungu, Upendo wa kweli huvunja
mipaka yote na kuta zote zinazotuzuia kuuona upendo wa Kristo na sadaka yake
pale msalabani. Upendo huu utusukuma kupenda hata pale tunapoumia kama binadamu
kwa kufanya tendo hilo kutokana na yaliyotusibu na yaliyopita na kutufanya kile
tulicho. Upendo huu ujenga tena daraja Imara la kuwapenda hata wale maadui
wetu. Tendo hili la upendo linatukutanisha na Yesu aliyependa hata kuutoa uhai
wake kwa ajili yetu. Kwa tafsiri hii, upendo unakuwa AMRI.
Hivyo Yesu anatuambia
leo neno hili la uzima sisi tusiosikia, “wapendeni adui zenu, watendeeni mema
wale ambao wawachukia ninyi, wabarikieni
wale ambao wawalaani ninyi, waombeeni wale ambao wawaonea ninyi,” Lk 6:27-28.
Tendo hili ndilo linalotofautisha kati ya anayemjua Kristo na aliye mfuasi wake
Kristo, Mpagani na anayeongozwa na hofu ya Mungu, na Mkristo wa kubatizwa na
anayeishi ahadi za ubatizo.
Upendo wa kweli unakupa
mtazamo mpya wa vitu na hasa watu wale wote unaokutakana nao na kuishi nao.
Huruma huwa msukumo wako wa ndani katika kuuona kweli, kuitafakari, na kuitenda
hata kama mazingira ukuwiya vigumu kufanya hivyo. Tendo hili kimtizamo kwa yale
yote unayokutana nayo, ukuweka karibu sana na Mungu. “Basi,
iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma,” Lk 6:36. Huruma hii ufunua
undani wetu ambao huwa kielelezo sahihi cha kuona upendo wa Mungu kwa wenzetu
hasa pale tunapotoa hukumu kwa wenzetu.
Mzaburi anatufikirisha
ukweli huu kwa kusema, “Bwana, kama wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani
angesimama?” Zab 130:3. Ndugu yangu, hapa tunaalikwa kuwa na huruma kama Mungu
alivyo na huruma nasi. Mara tulifanyapo tendo hili ndani na katika Kristo
ambaye ndiye ufunuo ulio kamili wa Mungu, tendo hili huwa baraka na mizania ya
kuhesabiwa haki mbele za Mungu. “Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho
mtakachopimiwa,” Lk 6:38b. Je, walifahamu jambo hili? Mwisho wa maisha yetu
hapa duniani tuwe tayari kwa maswali haya matatu mbele ya Mungu:
1. Ulipenda
vipi katika maisha yako niliyokupa hapa duniani?
2. Umetumiaje
vipaji nilivyokupa?
3. Je,
maisha ya Mwanangu mpendwa Yesu Kristo yalikuwa na maana yoyote kwako?
Wapendwa katika Kristo,
tukiwa tunajiandaa vyema kuyajibu maswali hayo, hatutakoswa na chochote endapo
upendo utakuwa ndiyo namna yetu ya kuona na kutenda. Kwa kuwa “twajua ya kuwa
sisi sote tuna ujuzi. Ujuzi huleta majivuno, bali upendo hujenga,” 1Kor 8:7b. Utambulisho wako na kujulikana kwako kwa Mungu
hakutakuwa kwa njia nyingine zaidi ya ‘kupenda.’ “Lakini
mtu akimpenda Mungu, huyo amejulikana naye,” 1Kor 8:3. Upendo wa kweli
utakuwajibisha katika kweli na haki yale yahusuyo wewe na wengine unaoishi nao.
Na mwenye kuishi katika
kweli na haki, hujua ni nani anayemtumikia na kumwabudu. Kama wafuasi wa
Kristo, tunayemwambudu na kumtumikia ni Mungu wa kweli na aliye hai. Naye Mtume
Paulo anasema, “Basi kwa habari ya kuvila
vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu; twajua ya kuwa sanamu si kitu katika
ulimwengu, na ya kuwa hakuna Mungu ila mmoja tu,” 1Kor 8:4. Leo tunazungukwa na
imani za ajabu na hofu zisizo na kikomo. Mungu tunayemwabudi siyo Mungu wa
vitisho.
Mungu wetu ni huruma, neema na msamaha. “Kwa
maana ijapokuwa wako waitwao miungu, ama mbinguni ama duniani, kama vile
walivyoko miungu mingi na mabwana wengi; lakini
kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake,
nasi tunaishi kwake; yuko na Bwana mmoja Yesu Kristo, ambaye kwake vitu vyote
vimekuwapo, na sisi kwa yeye huyo,” 1Kor 8:5-6. Hakuna sababu ya kujawa na hofu
ukiwa ndani na katika Kristo Yesu.
Ni wazi kwamba siyo
wote wenye kujazwa ufahamu wa kweli kati ya imani na matendo yao. Ni kweli
kwamba, “ujuzi huu haumo ndani ya watu wote;
ila wengine kwa kuizoelea ile sanamu hata sasa hula kana kwamba ni kitu
kilichotolewa sadaka kwa sanamu; na dhamiri zao, kwa kuwa dhaifu, hunajisika,”
1Kor 8:7. Ikiwa mtu ni tokeo la
historia na makuzi yake, ni wazi kabisa imani za walio wengi bado zimesongwa na
mila na desturi zao.
Hatumwendei Mungu kwa
mtindo wa kuuchengesha ukweli kuhusu Yeye. Kumbe kwa wewe ujuaye kweli kuhusu
Kristo yakupasa kuwa chumvi na mwanga pale ulipo. Ukweli ni kwamba, tusipokuwa
mwanga na chumvi pale tulipo, “yule aliye
dhaifu aangamizwa kwa ujuzi wako, naye ni ndugu ambaye Kristo alikufa kwa ajili
yake,” 1Kor 8:11. Kumbuka kuwa mbatizwa yeyote na mwenye kuishi ahadi zake za
ubatizo ni Kristo mwingine pale alipo. “Hivyo, mkiwatenda dhambi ndugu zenu na kuitia
jeraha dhamiri iliyo dhaifu, mnamtenda dhambi Kristo,” 1Kor 8:12.
Usimuhuzunishe Kristo kwa matendo yako ambayo hata kwa kutokuyafanya
hautapungukiwa chochote.
Ni vyema ukawa mfano wa
kuigwa hasa pale unapozungukwa na wale wenye imani changa. Si vyema kuwa
makwazo kwao. Mfano wa hili la makwazo Mtume Paulo anasema, “Kwa
hiyo, chakula kikimkwaza ndugu yangu, hakika sitakula nyama hata milele, nisije
nikamkwaza ndugu yangu,” 1Kor 8:13. Ni vyema nikajizua kufanya yale yawakwazayo
wenye imani changa hata kama kwa kufanya hivyo kwangu ni stahili.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Hivyo,
mkiwatenda dhambi ndugu zenu na kuitia jeraha dhamiri iliyo dhaifu, mnamtenda
dhambi Kristo,” 1Kor 8:12
Tusali:-Ee
Yesu, nifanye chombo cha upendo na imani ya kweli pale nilipo. Amina.
No hay comentarios:
Publicar un comentario