miércoles, 7 de septiembre de 2016

TAFAKARI: SIKUKUU YA KUZALIWA MAMA BIKIRA MARIA

SIKUKUU YA KUZALIWA MAMA BIKIRA MARIA
Somo I: Mik 5:1-4a
Zab: 13:6ab, 6c
Injili: Mt 1:1-16, 18-23
Nukuu:
Sasa utajikusanya vikosi vikosi, Ee binti wa vikosi; yeye amemhusuru; watampiga mwamuzi wa Israeli shavuni mwake kwa fimbo,” Mik 5:1

Bali wewe, Bethlehemu Efrata, uliye mdogo kuwa miongoni mwa elfu za Yuda; kutoka kwako wewe atanitokea mmoja atakayekuwa mtawala katika Israeli; ambaye matokeo yake yamekuwa tangu zamani za kale, tangu milele,” Mik 5:2 

 “Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu,” Mt 1:18

Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri,” Mt 1:19

Basi alipokuwa akifikiri hayo, tazama, malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto, akisema, Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu,” Mt 1:20

Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao,” Mt 1:21

 “Tazama, bikira atachukua mimba, Naye atazaa mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi,” Mt 1:23

TAFAKARI: Sasa utajikusanya vikosi vikosi, Ee binti wa vikosi; yeye amemhusuru.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anasheherekea sikukuu ya kuzaliwa kwa Mama Bikira Maria. Bikira Maria alikuwa mwanamke Myahudi aliyeishi kati ya karne ya 1 KK na karne 1BK. Kadiri ya mapoke, wazazi wake walijulikana kama Ana na Yoakimu. Mama Bikira Maria ni mke wa Yosefu, na alimzaa Yesu Kristo kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Kwa sababu hiyo na kwa utakatifu wake anapewa heshima ya pekee katika madhehebu mengi ya Ukristo. Hata hivyo, Maandiko Matakatifu yanawasifu watu mbalimbali kutokana na jinsi walivyomuamini. Mungu na kutenda makuu kwa ajili ya taifa lake.

Abrahamu alimuamini Mungu akawa tayari kumtolea sadaka  mwanae Isaka, tukio lililomfanya apate baraka  ya pekee ya kuwa baba wa waamini. Na mambo yalikuwa hivi, Malaika wa Bwana akamwita Ibrahimu mara ya pili kutoka mbinguni akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema Bwana, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu,” Mwa 22:15-18.

Yosefu, mwana mpenzi wa Yakobo, alikuwa mwaminifu hata akaliokoa taifa lisiangamie kwa njaa  Naye akawaambia ndugu zake, Nanyi kweli mlinikusudia mabaya, bali Mungu aliyakusudia kuwa mema, ili itokee kuokoa taifa kubwa, kama ilivyo leo,” Mwa 50:20

Musa ndiye mkomozi  wa Taifa la Mungu  katika Agano la Kale:  aliongoza Israeli  kutoka utumwani Misri  akalipatia sheria kutoka kwa Mungu katika mlima Sinai. Maandiko ya Agano la Kale yanakiri, Wala hajainuka tena katika Israeli nabii kama Musa, ambaye Bwana alimjua uso kwa uso; katika ishara zote na maajabu yote, ambayo Bwana alimtuma kuyatenda katika nchi ya Misri, kwa Farao, na kwa watumishi wake wote, na kwa nchi yake yote; na katika ule mkono wa nguvu wote, tena katika ule utisho mkuu wote, alioutenda Musa machoni pa Israeli wote,” Kumb 34:10-12.

Waliofuata ni Yoshua, Debora, Gideon, Ruthu, Samweli, wafalme Daudi na Solomoni, manabii Eliya, Isaya, Yeremia, Ezekiel na wengineo. Mwishoni Yesu Kristo  akamsifu Yohane Mbatizaji  akisema, “Basi, wajumbe wa Yohana walipokwisha ondoka, alianza kuwaambia makutano habari za Yohana, Mlitoka kwenda nyikani kutazama nini? Unyasi ukitikiswa na upepo? Lakini mlitoka kwenda kuona nini? Mtu aliyevikwa mavazi mororo? Jueni, watu wenye mavazi ya utukufu, wanaokula raha, wamo katika majumba ya kifalme. Lakini, mlitoka kwenda kuona nini? Nabii? Naam, nawaambia, na aliye zaidi ya nabii. Huyo ndiye aliyeandikiwa haya, Tazama, namtuma mjumbe wangu Mbele ya uso wako, Atakayeitengeneza njia yako mbele yako. Nami nawaambia, Katika wale waliozaliwa na wanawake hakuna aliye mkuu kuliko Yohana; lakini aliye mdogo katika ufalme wa Mungu ni mkuu kuliko yeye,” Lk 7:24-28

Elizabeti, mama wa Yohane, alijiona hastahili kutembelewa na Bikira Maria, Mama wa Yesu, akamuita, Mama wa Mungu. Naye Elizabeti anajiuliza,  “Limenitokeaje neno hili, hata mama wa Bwana wangu anijilie mimi?” Lk 1:43. Bikira Maria si mtu wa ziada katika mpango wa Mungu  bali ni mshiriki mkuu wa ukombozi  wa binadamu. Maria amechangia wokovu kwa kukubali mpango wote wa Mungu aliyetaka amzae Mwanae, amlee na kumfuata kiaminifu hadi msalabani, aliposhiriki kumtoa kama sadaka ya kutuokoa. Msimamo wake ulikuwa mmoja tu: “Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema,” Lk 1:38a. Tukichunguza nafasi yake katika fumbo  hilo, tunaweza kukiri pamoja naye kuwa ni Mwenyezi Mungu  aliyemtendea makuu, Lk 1:49, kwa kuwa, “Hawezi mtu kupokea neno lo lote isipokuwa amepewa kutoka mbinguni,” Yoh 3:27.  Yale yote ambayo Wakristo  wengi wanayasadiki kuhusu Bikira Maria, hakujipatia bali alijaliwa na Mwenyezi Mungu huku akiitikia kwa hiari  fumbo la mpango wake.

Jambo la pili kumfahamu Mama Bikira Maria itatupasa kumwona Mama huyu katika maisha ya Yesu. Yesu, kama mtu yeyote mcha Mungu, aliwaheshimu na kuwatii wazee wake: Akashuka pamoja nao mpaka Nazareti, naye alikuwa akiwatii; na mamaye aliyaweka hayo yote moyoni mwake,” Lk 2:51. Na ishara ya kwanza kwenye maishaya hadhara  ya Yesu iliongozwa na Bikira Maria katika arusi  ya Kana  ya Galilaya,  akisukumwa na huruma  kwa wenye shida: kwa ombi lake Yesu aligeuza maji  kuwa divai, na wanafunzi wake wakamwamini. Yohane alisimulia hivi, “Siku ya tatu palikuwa na arusi huko Kana, mji wa Galilaya; naye mama yake Yesu alikuwapo. Yesu naye alikuwa amealikwa arusini pamoja na wanafunzi wake. Hata divai ilipowatindikia, mamaye Yesu akamwambia, ‘Hawana divai’. Yesu akamwambia, ‘Mama tuna nini mimi nawe? Saa yangu haijawadia’. Mamaye akawaambia watumishi, ‘Lo lote atakalowaambia, fanyeni’. Basi kulikuwako huko mabalasi sita ya mawe, nayo yamewekwa huko kwa desturi ya Wayahudi ya kutawadha, kila moja lapata kadiri ya nzio mbili tatu. Yesu akawaambia, ‘Jalizeni mabalasi maji’. Nao wakayajaliza hata juu. Akawaambia, ‘Sasa tekeni, mkampelekee mkuu wa meza’. Wakapelekea. Naye mkuu wa meza alipoyaonja yale maji yaliyopata kuwa divai, (wala asijue ilikotoka, lakini watumishi walijua, wale walioyateka yale maj), yule mkuu wa meza alimwita bwana arusi, akamwambia, ‘Kila mtu kwanza huandaa divai iliyo njema; hata watu wakiisha kunywa sana ndipo huleta iliyo dhaifu; wewe umeiweka divai iliyo njema hata sasa’. Mwanzo huo wa ishara Yesu aliufanya huko Kana ya Galilaya, akaudhihirisha utukufu wake, nao wanafunzi wake wakamwamini,” Yoh 2:1-12

Bikira Maria anasifiwa kwanza kwa imani yake kuu kabisa, kuliko kwa kumchukua Yesu tumboni tu. Yesu alitaka kuwainua wasikilizaji wake wafuate mambo ya roho kuliko ya mwili. Mtu mmoja akamwambia, Tazama, mama yako na ndugu zako wamesimama nje, wanataka kusema nawe. Akajibu, akamwambia yule aliyempasha habari, Mama yangu ni nani? Na ndugu zangu ni akina nani? Akawanyoshea mkono wanafunzi wake, akasema, Tazama, Mama yangu na ndugu zangu! Kwa maana ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyu ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu,” Mt 12:47-50.

Vilevile, wakati wa utume  wake, alimsikia “mwanamke mmoja katika lile kundi la watu akisema, “Heri tumbo lililokuzaa, na matiti uliyonyonya. Lakini yeye alisema, Afadhali, heri walisikiao neno la Mungu na kulishika,” Lk 11:27-28 

Kwa hiyo wapendwa wana wa Mungu, tunapotafakri fumbo hili la kumwilishwa kwa Neno na kukaa kwetu, tutambue kwamba licha ya udogo wetu, udhaifu wetu, mapungufu yetu,  na unyonge wetu, sasa ni wakati wa kuinuliwa kwetu kutoka katika utumwa wa dhambi na kuwa watu wapya. Mungu anapenda kuanza upya na kila mmoja wetu na kuusimika ufalme wake milele. Nabii Mika nawaambia wana wa Israeli, Bali wewe, Bethlehemu Efrata, uliye mdogo kuwa miongoni mwa elfu za Yuda; kutoka kwako wewe atanitokea mmoja atakayekuwa mtawala katika Israeli; ambaye matokeo yake yamekuwa tangu zamani za kale, tangu milele,” Mik 5:2. Udogo na unyenyekevu huo anauchukuwa Mama Bikira Maria.

Tendo la Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu limewezekana kutokana na “NDIYO” ya Mama Bikira Maria. Na Neno huyo, yaani, Mwanaye Yesu Kristo, ndiye atakayechomolewa kutoka katika Taifa hili la Israeli, atasimama na kulilisha kundi lake kwa nguvu za Bwana. Naye atasimama, na kulisha kundi lake kwa nguvu za Bwana, kwa enzi ya jina la Bwana, Mungu wake; nao watakaa; maana sasa atakuwa mkuu hata miisho ya dunia” Mik 5:4. Utawala wake siyo kwamba utaleta amani tu, bali Yeye mwenyewe ni Amani. Na mtu huyu atakuwa amani yetu,” Mik 5:5.

Wapendwa katika Kristo, utendaji wa Mungu ni wa ajabu sana! Uteuzi wake hauna upendeleo hata kidogo. Ila jambo ambalo lililo wazi ni hili; Mungu hupenda kuwainua wanyonge na hasa wale waliodharauliwa, na wakati huo huo kuwanyenyekesha wale wote wanaojiinua na kujikweza. Historia nzima ya wokovu wetu inaufunua ujumbe huu wa Mungu. Embu watazama watu hawa; Zakaria, Elizabeti, Manoa na Mke wake, Samsoni, Mariamu, na wengine wengi tu, walikuwa watu wa kawaida kabisa na wakati mwingine walidharauliwa kutoka na mtindo wa maisha yao na mitazamo ya nyakati. Ila Mungu hupenda kuvitumia vile vilivyodhaifu na kuvinyeyekeza vile vijikwazavyo.

Ndiyo “Alifanyika mwili, akakaa kwetu:”-hapa ndipo alipochukua hali yetu ya kibinadamu, ikiwa ni pamoja na mazingira yetu isipokuwa hakutenda dhambi. Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake,” 1Pet 2:22. Hata hivyo anakubali kuzaliwa katika hali na mifumo ya kwetu katika asili zetu. Hivi ndivyo ilivyokuwa,   “Kitabu cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu. Yakobo akamzaa Yusufu mumewe Mariamu aliyemzaa YESU aitwaye Kristo,” Mt 1:1, 16. Historia ya familia ya Yesu, Ukoo, Kabila na Taifa, unaufunua mpango mzima wa Mungu katika historia hii ya wokovu wetu.

Wapendwa wana wa Mungu, hakuna hata mmoja wetu aliyechakugua kuzaliwa katika familia hiyo aliyopo. Hii ni pamoja na ukoo wake, kabila lake na Taifa lake. Yote ni mapenzi na mpango wa Mungu. Tusema vipi basi pale tunapowaona baadhi yetu wakizisifia familia zao, koo zao, makabila yao na Mataifa yao? Hivi kweli kuna sababu yoyote ile ya kujisifia? Jibu ni HAPANA! Basi kama ni kujisifu, Yesu  angekuwa wa kwanza kufanya hivyo. Lakini Yesu, ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu,” Flp 2:6-7

Wapendwa katika Kristo, kwa tendo la Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu akichukua hali yetu ya kibinadamu na mazingira yetu, ni heshima kubwa sana kwetu. Pili, Mwokozi huyu anatufundisha unyenyekevu uliotukuka. Nasi tujifunze kwa mwalimu wetu Yesu Kristo kwani kwake kuna  ufahamu wote.

Wapendwa wana wa Mungu, sehemu hii ya Injili tuliyoisoma leo, na hasa, Mt 1:18-19, inatufanya tujiulize swali hili. Kwa nini Yusufu alikusudia kumwacha Mariamu ikiwa walikuwa bado kuoana? Ukweli ni kwamba, mila na desturi za Kiyahudi zilikuwa tofauti na zetu. Mwanaume na mwanamke waliunganishwa pamoja wakati wanapopeana miadi ya kuoana (uchumba), ingawa hawakuruhusiwa kuhusiana kimwlili hadi baada ya harusi. Yusufu alikuwa anapanga kuuvunja uchunba wao rasmi baada ya kugundua kuwa Mariamu ana mimba ili hali hakuwahi kukutana naye kimwili.

Yusufu anataka kulifanya jambo hili kuwa siri ili kumnusuru Mariamu kifo cha aibu ambacho kingempata kama jambo lile lingegundulika katika jamii. Kama Yusufu angetaka kutafuta haki yake, sheria ilisema hivi kuhusu ubikira;  “Mtu akitwaa mke, akamwingilia na kumchukia, kisha akamshitaki mambo ya aibu kumzushia jina baya, akasema, Nimemtwaa mwanamke huyu, nami nilipomkaribia sikuona kwake alama za ubikira; Lakini likiwa ni kweli neno hili, la kutoonekana kwake yule kijana alama za ubikira; na wamtoe nje yule kijana (kike) mlangoni pa nyumba ya baba yake, na waume wa mji wake wampige kwa mawe hata afe; kwa vile alivyofanya upumbavu katika Israeli, kwa kufanya ukahaba katika nyumba ya baba yake; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako,” Kumb 22:13-14, 20-21. Kwa hali aliyokuwa nayo Mariamu si tu tatizo la ubikira, ila alionekana ana mimba.Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu,” Mt 1:18

Kwa vile Yusufu alimpenda sana Mariamu aliona ni vyema kumwondoa katika aibu ile, ili asife kwa kupigwa mawe. Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri,” Mt 1:19. Hapa ndipo tunapoona utu wa Yusufu. Utu huu ndio unaomfanya kuhesabiwa haki na Mungu kama mtu wa haki. Yusufu hakupenda kulihukumu jambo lile asilolijua. Yusufu alimjua vizuri Mariamu ikiwa ni pamoja na malezi aliyopata kutoka kwa wazazi wake. Hata hivyo tukio hili la mimba lilibaki kitendawili kikubwa kwa Yusufu. Kwa upande mwingine hapa tunafundishwa kwamba ukiwa na mashaka na kitu fulani usitende chochote. Jambo au kitu kile kipe kwanza Muda. Kitendo cha Yusufu kutaka kumwacha kwa siri Mariamu ilikuwa kulipa jambo lile muda. Je, ingetokea kwako au kwangu kwa namna yoyote ile ungelipa jambo hili muda?

Swali lingine ambalo linatujia katika habari hii, Mt 1:18 ni hili; Je Mariamu alikuwa na mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, au Yesu alikuwa uzao wa viuno vya Daudi kwa mujibu wa Mdo 2:30?-(“Basi kwa kuwa ni nabii, akijua ya kuwa Mungu amemwapia kwa kiapo, ya kwamba katika uzao wa viuno vyake atamketisha mmoja katika kiti chake cha enzi”). Mariamu alikuwa bikira; Biblia inasema Roho Mtakatifu "alimfunika" Mariamu, si kwa jinsi ya kuhusiana kimwili. Yusufu alikuwa baba pekee wa kisheria aliyemuasili Yesu, hakuwa baba halisi. Lakini Yesu alikuwa mzao halisi wa ukoo wa Daudi kupitia Mariamu, kama orodha ya vizazi yenye kupitia kwa Mariamu ya Lk 3:23-37 inavyoonyesha. Aya nyingine zenye kusema kuwa Yesu ni mtoto (mzao wa ukoo) wa Daudi ni Mat 12:23; 15:22; 20:30; 21:9,15; Marko 10:47-48; 12:35; Luka 10:41; 18:38-39; Yoh 7:42; 2 Tim 2:8; Ufu 5:5; 22:16. Je, Mat 1:23 (Tazama, bikira atachukua mimba, Naye atazaa mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi)  inatafsiri Isa 7:14 (Kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto mwanamume, naye atamwita jina lake Imanueli) kimakosa kwa kutumia jina "bikira?"

Jibu ni hapana. Si tu kwamba neno la Kiebrania lililotumiwa hapa linamaanisha amaa "bikira" ama "msichana", lakini pia tafsri ya Kigiriki ya Agano la Kale (Septuagint) imelitafsiri neno hili kuwa “parthenos,” yaani bikira. Swali lingine ambalo tunaweza kujiuliza ni hili: Kwenye Mat 1:23 na Lk 1:26-35, inawezekanaje Yesu aliyezaliwa na bikra awe mzao wa ukoo wa Daudi? Hapa kuna mambo matatu ya kuzingatia;
1. Yesu hakuwa mtoto halisi wa Yusufu. Kama angekuwa, Yer 29:32 ingekuwa ni unabii wa uongo.
2. Yesu alikuwa mtoto wa Yusufu kisheria. Leo hii, mwanaume anayemuoa mwanamke aliye na mtoto anakuwa baba wa mtoto huyo kisheria, ingawa si baba halisi.
3. Yesu alikuwa mtoto halisi wa Mariamu. Yesu alikuwa wa ukoo wa Daudi kisheria kupitia Yusufu, na Yesu alikwa wa ukoo wa Daudi kuuhalisi kupitia Mariamu. Kadiri ya Mat 1:25, asimjue kamwe hata alipomzaa mwanawe; akamwita jina lake YESU,” Mt 1:25”.  Je Mariamu alikuwa na watoto wengine wowote? Mstari huu hautakuwa na maana yeyote na wenye kupotosha kama Yusufu na Mariamu hawakuwa wamewahi kuwa na uhusiano wa kimwili.

Zaidi ya hapo, Mat 13:55-56; Mak 6:4; Gal 1:19; na Yuda 1 pia zimerekodi kuwa Yesu alikuwa na wadogo wake wa kiume (ndugu). Eusebius, katika kitabu chake kiitwacho Ecclesiastical History (karibu mwaka 360 BK) 2:23 na d 3:20 pia anasema kuwa wadogo wane wa kiume wa Yesu walikuwa Yakobo aliyeitwa mwenye haki), Yose (au Yusufu), Yuda na Simoni.

Moja ya majibu yatolewayo na Kanisa Katoliki ni kuwa Yusufu alikuwa na watoto kupitia ndoa yake ya awali, lakini si kupitia kwa Mariamu. Hata hivyo, hakuna ushahidi toka kwenye historia ya Kanisa kuwa Yusufu aliwahi kuwa na ndoa nyingine kabla ya ile na Mariamu, au mdogo wake yoyote wa kiume hakutokana na Yusufu na Mariamu.

Jibu lingine la Kanisa Katoliki ni kuwa kwenye jamii za Kimediteranian neno "ndugu" linaweza kumaanisha binamu na ndugu/jamaa wa karibu wenye umri unaofanana, na si tu kaka au wadogo wa mtu. Hata hivyo, Ambrose wa Milani alikuwa wazi kuwa Yesu hakuhitaji msaada wowote ili aweze kuwaunganisha watu na Mungu, na Mariamu hakupaswa kusujudiwa (On the Holy Spirit kitabu cha 3 sura ya 11 na.80 mwaka 381 BK). Alisema, "Na mtu yeyote asihamishie jambo hili kwa Bikira Mariamu; Mariamu alikuwa hekalu la Mungu. Na kwa hiyo Yeye (Mungu) pekee ndiye anayepaswa kuabudiwa Yeye afanyaye kazi katika hekalu lake (mwenyewe)."

Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na kuona ukweli huo hatuwezi kupinga kwamba yote hayo yalifanyika chini ya mpango mzima wa Mungu. Mungu hawezi kujikanganya mwenyewe. Hivyo Nabii Yeremia anasema, Tazama siku zinakuja, asema Bwana, nitakapomchipushia Daudi Chipukizi la haki; naye atamiliki mfalme, atatenda kwa hekima, naye atafanya hukumu na haki katika nchi,” Yer 23:5. Huyu ndiye Bwana wa haki na utawala wake ni utawala wa hekima na hukumu zake ni za haki. Ujio wa Masiha ni habari ya wokovu na kuwekwa huru mwili na roho. Katika siku zake Yuda ataokolewa, na Israeli atakaa salama, na jina lake atakaloitwa ni hili, Bwana ni haki yetu,” Yer 23:6. Basi na tuwe watu wa haki, tukitenda yaliyo kweli na haki, na kuhukumu kwa haki. Kuyatimiza hayo, tujifunze unyenyekevu wa Mama Bikira Maria.

Tumsifu Yesu Kristo!

Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao,” Mt 1:21


Tusali:- Ee Yesu, tujalie unyenyekevu na utayari wa kufanya mapenzi yake. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario