sábado, 17 de septiembre de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 25 YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 25 YA MWAKA-C
Somo I: Amo 8:4-7
Zab/Kit: 113:1-2, 4-6, 7-8, (K) 1, 7
Somo II: 1Tim 2:1-8
Injili: Lk 16:1-13
Nukuu
“Lisikieni hili, ninyi mnaopenda kuwameza wahitaji, na kuwakomesha maskini wa nchi, mkisema, Mwezi mpya utaondoka lini, tupate kuuza nafaka? Na sabato nayo, tupate kuandika ngano? Mkiipunguza efa na kuiongeza shekeli, mkidanganya watu kwa mizani ya udanganyifu; tupate kuwanunua maskini kwa fedha, na wahitaji kwa jozi ya viatu; na kuziuza takataka za ngano,” Amo 8:4-6

Akamwita, akamwambia, Ni habari gani hii ninayosikia juu yako? Toa hesabu ya uwakili wako, kwa kuwa huwezi kuwa wakili tena,” Lk 16:2 
 
Yule wakili akasema moyoni mwake, Nifanyeje? Maana, bwana wangu ananiondolea uwakili. Kulima, siwezi; kuomba, naona haya,” Lk 16:3
 
Hakuna mtumishi awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana, ama atamchukia huyu na kumpenda huyu, ama atashikamana na huyu na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali,” Lk 16:13 
 
Basi, kabla ya mambo yote, nataka dua, na sala, na maombezi, na shukrani, zifanyike kwa ajili ya watu wote,” 1Tim 2:1 

kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka, tuishi maisha ya utulivu na amani, katika utauwa wote na ustahivu,” 1Tim 2:2 

 “Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu,” 1Tim 2:5 
 
TAFAKARI: “Hamwezi kumtumikia Mungu na mali.”
 
Wapendwa wana wa Mungu, maneno haya ya Bwana wetu Yesu Kristo, “Hamwezi kumtumikia Mungu na mali,” kwetu ni mwito wa kuyachunguza maisha yetu vyema. Na kwa maneno hayo ya Yesu, anatoa elekezo sahihi na salama kuhusu maisha yako ya yangu katika umilele, na yenye kibali mbele ya uso wa Mungu licha ya mapungufu na udhaifu wetu. Kama kwayo ni mwito wa kuyachunguza maisha yangu, yanipasa kujua uhusiano wa maisha yangu ya kiroho, nafasi yangu katika jamii, na mali/utajiri nilizo nazo/nilio nao. Na swali ni hili; kati ya hivyo vitatu (maisha ya kiroho, nafasi/cheo, na mali/utajiri), ni kipi/vipi kinasukuma/vinavyosukuma maisha yako? Mali au utajiri na cheo vikiwa ndivyo vinavyoyasukuma maisha yako, ni hatari sana kudondoka katika dhuluma, na hasa kwa masikini na wanyonge.
Na huu ndio ujumbe wa Mungu anaoutoa Nabii Amosi kwa  matajiri na mwenye mamlaka waliokuwa sababu ya dhuluma kwa masikini. Ujumbe huu unawataka waziache njia zao mbaya na kumrudia Mungu. Naye anasema: Lisikieni hili, ninyi mnaopenda kuwameza wahitaji, na kuwakomesha maskini wa nchi, mkisema, Mwezi mpya utaondoka lini, tupate kuuza nafaka? Na sabato nayo, tupate kuandika ngano? Mkiipunguza efa na kuiongeza shekeli, mkidanganya watu kwa mizani ya udanganyifu; tupate kuwanunua maskini kwa fedha, na wahitaji kwa jozi ya viatu; na kuziuza takataka za ngano,” Amo 8:4-6. Leo Nabii Amosi angalikuwa katika jamii yetu angeongelea ugumu wa maisha uliosababishwa na unaosababishwa na watu wachache waliolifisidi taifa letu na wanaoendelea kulifisidi. Hawa ndio wale wajulikanao kwa ‘umaarufu wao’ kama ‘mafisadi.’ Wito ni kuonja moyoni na kughairi uovu kwa sababu waovu na uovu ni chukizo mbele ya uso wa Mungu. “Laana ya Bwana i katika nyumba ya waovu, Bali huibariki maskani ya mwenye haki,” Mit 3:33

Lolote lile lililo ovu halina umilele ndani yake. Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu (Yesu Krito), sadaka hii ya Mwana wa Mungu pale Msalabani, na ufufuko wake, ndicho kikomo cha uovu wote. Hii ndiyo njia aliyoichangu Mungu kuushinda uovu. Na tunaushinda uovu tukiwa ndani na katika Kristo Yesu. Kristo ndiye mizania yetu katika kweli, upendo, haki, na amani.

Wapendwa katika Kristo, Injili ya leo inatupatia hali halisi kuhusu hesabu yetu siku ya mwisho. Yesu analisema jambo hilo akitolea mfano wa Tajiri mmoja na Wakili wake dhalimu. Bila kujua siku wala saa, Wakili huyu dhalimu anatakiwa na Tajiri yake kutoa hesabu ya uwakile wake, baada ya Tajiri yake kupata habari ya kutapanywa kwa mali zake. Ni vyema tukaona kwa undani kidogo msukumo wa maisha unaoongozwa na  mali/utajiri na sifa/cheo, na hatma yake katika maisha ya kiroho.
 
1. Watu wengi wanaongozwa na mali
Watu wa mtindo huu,  tamaa yao ya kupata vitu linakuwa ndilo lengo la maisha yao yote. Kweli hili haijalishi upo wapi na ndani ya mfumo upi wa maisha. Msukumo huu wa kutaka zaidi kila siku una misingi yake katika udanganyifu wa kuwa nikiwa na vingi nitakuwa na furaha zaidi, nitakuwa wa muhimu, na nitakuwa salama; lakini mawazo hayo yote matatu si ya kweli. “Lakini hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu,” 1Tim 6:9. Mali huleta furaha ya "muda mfupi tu." Na sababu kubwa ndugu yangu, vitu havibadiliki, hivyo vinatuchosha na tunataka vipya, vikubwa, na bora zaidi.
 
Kuna imani pia kwamba nitapata mali nyingi nitakuwa wa muhimu. Umuhimu wako na umuhimu unaotegemea ulivyo navyo ndugu yangu ni vitu viwili tofauti. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi,” 1Tim 6:10. Thamani yako haitegemei mali zako, Mungu anasema kitu cha muhimu maishani mwako si vitu! Imani ya watu wengi kuhusu fedha ni kwamba kuwa nazo nyingi kutanipa usalama. Huwezi!
 
Ndugu yangu, utajiri unaweza kupotezwa mara moja kwa sababu zisizozuilika. Usalama halisi unaweza kupatikana katika kile ambacho huwezi kunyang'anywa yaani uhusiano wako na Mungu. Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu,” 1Tim 6:7. Mt. Augustino anatuwasa kutoka kwenye kanuni yake, "kuna furaha kubwa kuwa na vichache kuliko kuwa na vingi." Hata hivyo tatizo hapa ni kipimo cha huo uchache na huo wingi.
 
2. Watu wengi wanaongozwa na kutaka sifa
Ndugu yangu, wakati mwingine watu hawa wanaruhusu matarajio ya wazazi, waume, au wake, watoto, waalimu au rafiki zao kutawala maisha yao. Watu wazima bado wanajaribu kupata sifa kwa wazazi wao ambao hawajafurahi kamwe. Wengine wanasukumwa na vikundi vya marafiki, wanahofu wenzao watawafikiriaje. Kwa bahati mbaya, wale wafuatao kundi au maoni ya mtu binafsi hupotea ndani yake.
 
Ndugu yangu, kwa nini kujifungia katika gereza hili la fikra na maoni? Mtu awaye yote akifundisha elimu nyingine, wala hayakubali maneno yenye uzima ya Bwana wetu Yesu Kristo, wala mafundisho yapatanayo na utauwa, amejivuna,” ITim 6:3-4b. Sifa yetu kubwa ni kulitenda lile alilofundisha Bwana wetu Yesu Kristo kwani ndilo lenye uzima wa milele. Mara nyingi kupenda sana sifa huku na wakati mwingine kunakoendana na matumizi mabaya ya madaraka, huwa kilio kwa wanyonge na ukandamizaji wa haki za watu, hasa wanyonge.
 
Ndugu yangu, sijui funguo zote za mafanikio, lakini funguo moja ya kushindwa ni kujaribu kumpendeza kila mtu. Kutawaliwa na maoni ya watu wengine ni njia wazi ya kukosa makusudi ya Mungu katika maisha yako. Bwana wetu Yesu Kristo anatupa angalizo kwa jambo hili, "hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu, ama atashindana na huyu na kumdharau huyu: hamwezi kumtumikia Mungu na mali." Mt 6:24.
Kuna nguvu nyingi zinazoweza kuongoza maisha yako lakini zote mwisho wake ni mfu: kutotumia vipawa ulivyo navyo, mahangaiko ya moyo, na maisha yasiyo ya utoshelevu. Bali wewe, mtu wa Mungu, uyakimbie mambo hayo; ukafuate haki, utauwa, imani, upendo, saburi, upole,” 1Tim 6:11. Kuishi katika mfumo huu ndiko kutakako kupa amani ya kweli na utulivu wa ndani.
Ndugu yangu, kuishi maisha yanayoongozwa na malengo, ni kutawaliwa, na kuelekezwa na makusudi ya Mungu. Hakuna kitu cha muhimu zaidi kama kujua malengo ya Mungu kwa maisha yako, na hakuna mbadala kwa hilo-siyo mafanikio, utajiri, kujulikana, au anasa. Bila malengo, maisha ni mwendo usio na maana, shughuli bila mwelekeo, na matukio bila sababu. Bila malengo, maisha ni kitu duni, kidogo sana, kisicho na umuhimu wowote.
 
Hivyo, alichokifanya kwa haraka Wakili yule ni kurejesha uhusiano wa haraka na wateja zake ambao ndio hatma ya maisha yake kwa sasa. Katika jambo hili ilimpasa kutoa msamaha wa madeni bila kuhathiri utajiri wa Tajiri yake. Hivyo, Yule bwana akamsifu wakili dhalimu kwa vile alivyotenda kwa busara; kwa kuwa wana wa ulimwengu huu katika kizazi chao wenyewe huwa na busara kuliko wana wa nuru,” Lk 16:8. Kwa kuyasema haya, Yesu anatuacha na swali zito la kujibu. Swali hilo ni hili: Mimi na wewe tunasubiri nini kurejesha uhusiano wetu na Mungu kwa muda na nafasi tuliyonayo sasa tukiwa bado kwenye nuru, yaani, kwa ubatizo wetu na agano letu katika maisha, iwapo Wakili huyu na udhalimu wake aliweza kurejesha uhusiano wake na wateja zake? Wokovu ndiyo sasa.
 
Je, kwa hali na mazingira haya yaliyo jaa uovu na yasiyo rafiki na maisha yako na yangu kiroho tufanye nini? Kama wabatizwa na wafuasi wa Kristo Yesu, na wenye hofu ya Mungu, Mtume Paulo anatupa changamoto ya maisha ya kiroho, na wosia pia. Ni kweli bila Mungu kwa nguvu zetu wenyewe hatutoweza chochote. Ili kitu au jambo hilo lidumu katika hali yake, yatupasa kumshirikisha Mungu katika kila jambo tulifanyalo. Hivyo, kabla ya mambo yote, nataka dua, na sala, na maombezi, na shukrani, zifanyike kwa ajili ya watu wote,” 1Tim 2:1. Hapa tunawaombea wote; yaani wema na waovu katika maana ya kwamba, wema Mungu azidi kuwasimamia katika kila jambo kwa lengo la kuushinda uovu kwa wema, na wale waovu Mungu awabadili tabia na nia zao mbaya.
 
Ni wajibu wetu pia kama Kanisa kwa imani yetu, na wananchi kwa kuzaliwa kwetu na uzalendo wetu kuwaombea viongozi wetu wadumu katika kweli, upendo, haki, na amani kwa wote bila kumbagua yeyote. Tunawaombea haya viongozi wetu kwa sababu wengi kutokana na nafasi walizopewa na umma wa watu wanazitumia vibaya kwa ulevi wao wa madaraka. Ni kwa namna hiyo tunasali na kuwaombea wafalme na wote wenye mamlaka, tuishi maisha ya utulivu na amani, katika utauwa wote na ustahivu,” 1Tim 2:2. Pamoja na kufanya hili ambalo ni wajibu msingi kabisa, na tukiiombea amani nchi yetu,  tusisahau kuwa amani ni tunda la HAKI. Tutende haki kila mmoja kadiri ya wito na nafasi yake katika jamii, na siyo kuihubiri amani bila kutenda haki. Kufanya hivi ni chukizo kwa Mungu, na maigizo kwa mwanadamu.
 
Kuiombea amani nchi yetu, na wakati huo huo kutenda haki kwa mujibu wa sheria na Katiba tuliyo nayo kama sheria Mama, jambo hilo ni zuri, nalo lakubalika mbele za Mungu Mwokozi wetu; ambaye hutaka watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli,” 1Tim 2:3-4. Tusipoongozwa na kweli hii, huko mbele ni giza tupu. Marehemu Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, na Mtumishi wa Mungu, katika uchanga wa Taifa letu miaka ya sitini aliyatamka haya juu ya Uhuru na Maendeleo na kusema, “Tanzania ni ya Watanzania; na, Watanzania ni wote. Mtu mmoja hana haki kusema ‘Mimi ni wote.’ Na hakuna Mtanzania kwenye haki ya kusema ‘najua lililo zuri kwa Tanzania na wengine lazima walifanye.” Tatizo letu kubwa leo kama Taifa ni pale tunapotanguliza “u mimi wetu.”
Tunapofanya hilo (kuendeleza ubinafsi wetu), taswira ya Mungu ndani yetu utoweka, kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu,” 1Tim 2:5. Hata Waswahili wanasema, “kidole kimoja hakivunji chawa.” Na hata pale tunaposimama wenyewe, basi tusimame kwa maslahi mapana ya wote katika kweli na haki kama Kristo Yesu ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote, utakaoshuhudiwa kwa majira yake,” 1Tim 2:6. Na mwisho wa siku historia hubaki kuwa mwalimu mwaminifu kwetu. 

Ajenda binafsi yenye malengo binafsi mwisho wake ni kuumbuka kwa sababu Mungu hachezewi kamari wala kupigiwa bao. Pasipo imani dhabiti na kweli kwa yale yote tuyatendayo, mwisho wa siku tutajulikana kama waigizaji ambao hatukumaanisha tuliyokuwa tunafanya ingawa machoni mwa watu yalivuta hisia kubwa sana na zenye matumaini. Na kwa upande wa Mtume Paulo anasema wazi kwamba ndani na katika Kristo Yesu (mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu), naye-Paulo kwa ajili ya huo naliwekwa niwe mhubiri na mtume, (nasema kweli, sisemi uongo), mwalimu wa Mataifa katika imani na kweli,” 1Tim 2:7. Haya ndiyo maisha yanayoongozwa na malengo. Na katika hili, Mtume Paulo anasema, nataka wanaume wasalishe kila mahali, huku wakiinua mikono iliyotakata pasipo hasira wala majadiliano,” 1Tim 2:8. Tufanye yote tukiwa na tumaini lile KUU kwamba, ‘Kristo Yesu ndiye mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu, na bila Yeye hatuwezi tukafanya lolote lile, liwe dogo au kubwa,’ Yoh 15:5. Amina! 
 
Yohane Masikio au kwa jina la utani na kwa kazi yake, “Galibi Mchuuzi” hujidamka kila siku alhajiri na mapema akiwa na kapu lake lenye bidhaa mbali mbali, kuelekea kituo cha mabasi kufanya biashara. Kwa mfumo huu wa maisha yake, Galibi Mchuuzi kila siku kwake ni biashara, jumatatu hadi jumapili, liwe jua au mvua, baridi au joto. Jambo lingine la ajabu na la pekee, Galibi Mchuuzi hutembea na pesa zake zote, yaani, faida ya kila siku. Pesa hii uificha ndani ya kaputula ambayo juu yake huvaa suruali, mara zote huvalia kibarakashee-kofia ambayo mara nyingi huvaliwa na Ndugu zetu Waislam.
 
Siku moja jumapili mchana akiwa kwenye mizunguko yake ya kusaka hela kwa biashara yake ile ya umajinga, ghafla alijisikia vibaya na hatimaye ilimbidi kujilaza pembezoni mwa barabara. Na kwa bahati nzuri ni muda huo huo Paroko wa eneo lile, Padre Ombeni, alikuwa anarudi kutoka vigangoni kuadhimisha Misa Takatifu.
 
Mara Paroko alisimama na kwenda kujua nini kilichomjiri Galibi Mchuuzi kwani mara kwa mara Paroko upishana naye njiani. “Rafiki kulikoni. Mbona umejilaza hapa?,” Padre Ombeni alimuuliza. Bila kusema chochote, Galibi aliingiza mkono ndani ya suruali yake na kuchomoa burungutu la pesa na ndani ya mfuko mdogo wa plastic kulikuwa na kitambulisho cha ubatizo. Vyote alimkabidhi Padre Ombeni. Na hapa ndipo Paroko alipogundua kuwa Galibi alikuwa Mkristo, na jina lake ni Yohane Masikio, aliyebatizwa Parokiani hapo miaka 37 iliyopita.
Kwa sauti ya mbali, Yohane Masikio aliomba kuungama. Paroko alifanya hilo ikiwa ni pamoja na kumpa mpako wa wagonywa, na Ekarist Takatifu. Baba Paroko akamwinua pamoja na kapu lake kumwingiza kwenye gari na kumwahisha hospitalini ambayo haikuwa mbali na parokia. Baada ya siku tatu, Yohane Masikio alipona kabisa na kuja kutoa shukrani kwa Paroko.
 
Na mambo yalikuwa hivi, “Baba Paroko aksante sana kwa kuyaokoa maisha yangu. Baada ya huduma ile nilijisikia kuinuliwa juu kwa nguvu za ajabu na kuingizwa Kanisani na kundi la watu walikuwa wamevaa nguo nyeupe. Walinipeleka mpaka chini ya Msalaba Mkubwa uliokuwa pembezoni kwa Altari ya Kanisa hilo, na kuniambia, ‘Mtazame huyo unayeendelea kumtesa hadi sasa,’ wakinielekezea kwa Yesu Msalabani. Baada ya hapo sikuwaona tena wale watu, nami ndipo niliposhtuka na kujiona nipo Hospitalini na ufahamu wa kutosha.” Je, kwa hili nifanye nini?
 
Baada ya ukimwa kidogo, Paroko Ombeni alimjibu na kusema, “kamwe usimtese tena Yesu. Njia unayoifuata siyo nzuri, hivyo yachunguze maisha yako ya kiroho, na biashara yako. Mungu bado anakupenda, na ndiye aliyewatuma wale watu waliovalia nguo nyeupe. Hao ni malaika.”
 
 Padre, “naweza kuungama tena?” Yohane Masikio, aliuliza kwa shauku kubwa. “Mwanangu, jisikie huru kupatanishwa na Mungu. Nifuate kwenye sanduku la maungamo,” Paroko Ombeni alisema kwa upole na upendo mkubwa.
Tumsifu Yesu Kristo!
 
Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu,” 1Tim 2:5
 

Tusali:-Ee Yesu na Kimbilio letu, tufanye chombo chako cha haki, upendo na amani, na mwisho tuandae kwa kifo chema. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario