domingo, 18 de septiembre de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 25 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 25 YA MWAKA-C
Somo: Mit 21:1-6, 10-13
Zab/Kit: 119:1, 27, 30, 34, 35, 44
Injili: Lk 8:19-21
Nukuu
Moyo wa mfalme huwa katika mkono wa Bwana; Kama mifereji ya maji huugeuza po pote apendapo,” Mit 21:1 

Kila njia ya mtu ni sawa machoni pake mwenyewe; Bali Bwana huipima mioyo,” Mit 21:2 

Kutenda haki na hukumu Humpendeza Bwana kuliko kutoa sadaka,” Mit 21:3 

 “Akaletewa habari akiambiwa, Mama yako na ndugu zako wamesimama nje wakitaka kuonana nawe,” Lk 8:20 

Akawajibu akasema, Mama yangu na ndugu zangu ndio hao walisikiao neno la Mungu na kulifanya,” Lk 8:21 

TAFAKARI:Mama yangu na ndugu zangu ndio hao walisikiao neno la Mungu na kulifanya.”

Wapendwa katika Kristo, hofu ya Mungu licha ya kutuongoza katika kweli, haki na upendo wa dhati, utuunganisha kuwa kitu kimoja katika Kristo. Sote huwa ndugu katika Kristo si kwa njia hii ya kibailojia, bali ufanywa ndugu kiroho na kuvushwa katika mitizamo ya kibinadamu isiyo beba umilele ule tunaoutamani. Hivyo Yesu analisema jambo hii akifafanua maana ya ndugu pale alipoletewa taarifa ya uwepo wa Mama yake na ndugu zake wakimsubiri nje ya Hekalu. Naye anasema, Mama yangu na ndugu zangu ndio hao walisikiao neno la Mungu na kulifanya,” Lk 8:21. Ni kwa hofu ya Mungu tu twaweza lisikia neno la Mungu na kulifanya.

Hivyo Yesu anamaanisha kweli asemavyo, “Mama yangu na ndugu zangu ndio hao walisikiao neno la Mungu na kulifanya,” Lk 8:21. Kwa maneno haya haikumaanisha kwamba Yesu anaukana uhasili wake na familia yake, bali anakwenda zaidi ya mipaka ya kifamilia, koo, kabila na utaifa. Sote kwa kupitia Yesu Kristo, Neno wa Mungu aliyefanyika mwili na kukaa kwetu, tunaunganishwa na upendo wa Mungu. Na tunapolisikia na kulifanya neno hilo la Mungu bila mawaa, baraka na neema huwa matunda yake.

Bila hofu ya Mungu binadamu huweza kufanya matendo maovu yasiyo na mfanano hata na wanyama. Wanyama waweza kuwa mfano kwetu kwa matendo yao. Je, wabisha? Hivi ulishawahi kuona Simba akimuua simba mwenzake hivi hivi tu? Je, ni wangapi wamepoteza maisha yao kwa mkono wa binadamu wenzao? Je, ushaona Nyani akinyonga kichanga chake? Je, ni vichanga vingapi kila dakika vinanyongwa duniani leo? Hakika wanyama wanasomo zuri kwetu la kujifunza pale tunapoikosa hofu ya Mungu.

Kwa upande wa kijamii, kiongozi asiyekuwa na hofu ya Mungu ni hatari sana. Kwa mamlaka yake aweza kufanya lolote, hasa pale anapozungukwa na magoigoi wanaosukumwa na hofu ya woga. Hadhi ya kiongozi yeyote yule ni kuwa na hofu ya Mungu, kusimama katika kweli na haki. Hivyo, Moyo wa mfalme huwa katika mkono wa Bwana; Kama mifereji ya maji huugeuza po pote apendapo,” Mit 21:1. Mfalme au kiongozi yeyote yule mwenye hofu ya Mungu ufikiri papana na kwa undani kabla ya kusema chochote. Kubwatuka hovyo na kunakoleta sintofahamu kati ya wale anaowaongoza siyo dalili za kiongozi mwenye hofu ya Mungu.

Kiongozi au hata mtu mwingine yoyote yule upimwa njia zake kwa kile alicho. Kila njia ya mtu ni sawa machoni pake mwenyewe; Bali Bwana huipima mioyo,” Mit 21:2. Na ndani ya kila mtu ipo nguvu fulani inayoongoza maisha ya mtu huyo. Maisha ya mtu huweza kuongozwa au kusukumwa kwa hatia, sifa, mali, na hata umaarufu fulani. Njia salama ni kusukumwa na hofu ya Mungu. Ni kutenda katika, kweli, upendo haki, na amani. Hivyo, kutenda haki na hukumu Humpendeza Bwana kuliko kutoa sadaka,” Mit 21:3. Sadaka yoyote ile isiyokuwa na uhusiano na Mungu katika kweli, haki, upendo, na amani, ni chukizo kwa Mungu, na igizo kwa mwanadamu.

Hivyo ni vyema kila siku, na hasa pale ambao tuna dhamana mbele za watu kujiepusha na majigambo, kiburi, na sifa pasipo siha. Kwani macho yenye kiburi, na moyo wa kutakabari, Hata ukulima wa waovu, ni dhambi,” Mit 21:4. Kama Mkristo na mwenye kujali na kuwajibika elewa kwamba hu mfano wa Kristo mwenyewe pale ulipo kama Mfalme. Na Ufalme wake Kristo ni Ufalme wa kweli na haki, upendo na huruma, unyenyekevu, na msamaha.

Tunapoishi ufalme huu wa Kristo katika kweli, utuepusha na udanganyifu wa ulimwengu wa vitu na ushindani. Hivyo yapo maonyo ambayo yatupasa kuyaelewa na kuepukana nayo. Kwanza kabisa lazima kujua kwamba, Mawazo ya wenye bidii huuelekea utajiri tu; Bali kila mwenye pupa huuelekea uhitaji,” Mit 21:5. Je, mawezo yako mwisho wa siku ukufikisha pale Kristo alipo?

Jambo la pili ni kuishi katika kweli, na kupata yote ikiwa ni pamoja na mahitaji yako kwa njia ya haki. Kinyume chake ni kwamba, kupata akiba ya mali kwa ulimi wa uongo Ni moshi upeperushwao; ni kutafuta mauti,” Mit 21:6. Je, ni wangapi leo tunaishi katika mauti haya tunapoutafakari utajiri tuliokuwa nao kwa njia ya dhuluma na udhalimu?

Tatu, ni vyema ukajua kwamba leo ikiwa wewe na mimi, upo kama ulivyo kutokana na historia yako, na makuzi yako. Hivyo penye nafsi ya mtu ndipo penye muhimili wake wote. Nafsi ipo kati ya mwili na roho. Nafsi yako ikiegemea mwili, basi kuna uwezekano mkubwa kuangamia, ila nafsi yako ikiegemea roho, hapo kuna uzima wa milele, Gal 5:19-23. Na kwa namna hivyo uovu wa mtu ni pale nafsi yake inapoegemea mwili na kutamani matendo ya mwili. Nafsi ya mtu mbaya hutamani uovu; Jirani yake hapati fadhili machoni pake,” Mit 21:10.

Nne, maisha ni shule pale ulipo. Matokeo ya shule hii ya maisha ni utakatifu wako. Hivyo cheza vizuri kwa kila jambo huku ukilenga umilele wako. Na  Mwenye mzaha aadhibiwapo, mjinga hupata hekima; Na mwenye hekima afundishwapo, hupokea maarifa,” Mit 21:11. Maarifa na ufahamu wako ukujenge kuiona nuru ya Mungu, na nuru hiyo iangaze matendo yako.

Tano, ishi katika haki na kwa kila mmoja pale ulipo, iwe una dhamana juu yao au hauna. Kwa sababu, mwenye haki huitafakari nyumba ya mtu mbaya; Jinsi wabaya waangushwavyo wakaangamia,” Mit 21:12. Palipo na haki pana amani, kwani amani ni tunda la haki. Na mwisho, kuishi katika hofu ya Mungu ni kujifunza kusikiliza zaidi kuliko kuongoa na kujitetea tu pasipo siha yoyote ile. Kwa kuutoa muda wako kusikiliza mahangaiko ya wengine kunakufanya kushiriki pia uchungu na maumivu yao. Hivyo tendo hilo hubadili pia namna ya kutenda kwako. Kinyume chake ni kwamba, azibaye masikio yake asisikie kilio cha maskini, Yeye naye atalia, lakini hatasikiwa,” Mit 21:13. Kusikiliza mahangaiko ya wengine ni moja ya tiba kwa mwenye mahangaiko hayo.

Tumsifu Yesu Kristo!

Kutenda haki na hukumu humpendeza Bwana kuliko kutoa sadaka,” Mit 21:3


Tusali:-Ee Yesu, tujalie neema ya kuvuka mipaka ya familia zetu, koo zetu, kabila zetu na utakifa kwetu, ili uonekane katika wote na katika yote. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario