JUMANNE
WIKI YA 23 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 6:1-11
Zab/Kit: 149:1-2, 3-4,
5-6a, 9b
Injili: Lk 6:12-19
Nukuu
“Au
hamjui ya kwamba watakatifu watauhukumu ulimwengu? Na ikiwa ulimwengu
utahukumiwa na ninyi, je! Hamstahili kukata hukumu zilizo ndogo?” 1Kor 6:2
“Nasema
hayo nipate kuwatahayarisha. Je! Ndivyo, kwamba kwenu hakuna hata mtu mmoja
mwenye hekima, awezaye kukata maneno ya ndugu zake?” 1Kor 6:5
“Na baadhi yenu
mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini
mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika Roho wa Mungu
wetu,” 1Kor 6:11
“Ikawa
siku zile aliondoka akaenda mlimani ili kuomba, akakesha usiku kucha katika
kumwomba Mungu,” Lk 6:12
“Hata
kulipokuwa mchana aliwaita wanafunzi wake; akachagua kumi na wawili miongoni
mwao, ambao aliwaita Mitume,” Lk 6:13
“Simoni,
aliyemwita jina la pili Petro, na Andrea nduguye, na Yakobo na Yohana, na
Filipo na Bartolomayo, na Mathayo na
Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Simoni aitwaye Zelote, na Yuda wa Yakobo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyekuwa
msaliti,” Lk 6:14-16
TAFAKARI: “Bali mwashitakiana, ndugu kwa ndugu, tena mbele yao
wasioamini.”
Wapendwa wana wa Mungu, “hakuna
mti mzuri uzaao matunda mabaya, wala mti mbaya uzaao matunda mazuri; kwa kuwa kila mti hutambulikana kwa matunda yake; maana,
katika miiba hawachumi tini, wala katika michongoma hawachumi zabibu,” Lk
6:43-44. Maneno haya mazito ya Bwana wetu Yesu Kristo, yanaturudisha katika
hali halisi ya ubinanadamu wetu. Mtakatifu Thomasi wa Akwino katika mafundisho
yake, anasema, “neema hufanya kazi katika uhalisia.” Kwa maana nyingine, kuna
uhusiano wa moja kwa moja kati ya kile mtu alicho na matendo yake. Kwa ufahamu
wa kawaida-‘common sense,’ inatuwia vigumu kuelewa kwa undani kilichopo ndani
ya mtu kwa kile atakacho kuwa au aombacho kuwa na hasa pale kinapo kinzana na
kile atendacho.
Ni vigumu kuamini na kuelewa
mama ambaye anakesha kila siku akiomba neema na baraka za Mungu kuwa mama na
mlezi mzuri ilhali kila apatapo ujauzito-mimba huitoa. Huku ni kucheza na neema
na baraka za Mungu. Tutapigwa na mshangao mkuwa pale tutakapo hukumiwa na wale
wanaoishi kweli hii, yaani, mlandano wa maisha yao na matendo yao. Hawa ndio
wateule na watakatifu wa Mungu. Naye Mtume Paulo katika hili anasema, “Au hamjui ya kwamba watakatifu watauhukumu
ulimwengu? Na ikiwa ulimwengu utahukumiwa na ninyi, je! Hamstahili kukata hukumu
zilizo ndogo?” 1Kor 6:2. Mara nyingi na baadhi ya watu na hasa viongozi wa
kisiasa kwa kutaka huruma ya wanyonge walio wengi, wamelitumia vibaya jina la
Mungu kama kichaka cha kuficha uovu wao na kuwapumbaza wanyonge wanaotaka
kusikia heri za peponi zisizo na kweli katika uhalisia.
Ndugu yangu, fumbua
macho yako na ona vizuri. Si vyema kuruhusu Jina la Mungu kunajisiwa mimbarini
na baadhi ya watu na hasa viongozi wa kisiasa kwa kutafuta umaarufu na kuonewa
huruma na umma wa watu na kufanya eneo hilo kama kichaka cha kuhalalisha uovu
wao. Tunapo ruhusu hali na mazingira kama hayo, tujiandae kwa adhabu ya Mungu.
Mungu hafanyiwi dhihaka hata kidogo. “Nasema
hayo nipate kuwatahayarisha. Je! Ndivyo, kwamba kwenu hakuna hata mtu mmoja
mwenye hekima, awezaye kukata maneno ya ndugu zake?” 1Kor 6:5. Maneno yetu yaendane na matendo yetu.
Na maombi yetu yaakisi maisha yetu na kile tutakacho kuwa. Kinyume chake ni
dhihaka mbele ya Mungu, na maigizo mbele wa wanadamu.
Ni jambo la kushangaza kwa Mkristo na
anayeamini ufufuo siku ya mwisho mwenye kuishi kwa chuki na visasi, na asiye
tayari kusamehe. Na mara nyingine tunaonyesha hali hii hata kwa wale wasio na
imani thabiti. “Bali
mwashitakiana, ndugu kwa ndugu, tena mbele yao wasioamini,” 1Kor 6:6. Hili ni
sikitiko kubwa kwa Kristo aliyekukomboa wewe na mimi pasipo mastahili yako au
yangu. Kwa nini basi tunakoswa huruma? Kwa
nini tunaendeleza sera za chuki na kupandikiza mbegu hiyo hata kwa watoto wetu?
“Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi
ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala
waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala
watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang'anyi,” 1Kor 6:9-10.
Hakika katika haya hakuna mbingu.
Ndugu yangu, unapoendekeza
ubinadamu na ubinafsi wako ni vigumu kumwona Kristo kwa wengine. Kwa matendo
haya ya mwili, yaani, “uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui,
ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda,
ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama
nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo
hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21. Usalama wako na wangu upo kwenye
tunda la roho, yaani, “upendo, furaha,
amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo
hakuna sheria,” Gal 5:22-23. Kiongozi kama kioo cha jamii anayoiongoza hanabudi
kuwa na tunda hili la roho. Kiongozi mwenye kupandikiza mbegu ya chuki na
visazi ajiandae kuvuna tufani la machafuko.
Wapendwa wana wa Mungu,
ikiwa hu hai leo na sasa basi jua kwa Mungu bado hujachelewa hata kwa wingi wa
dhambi zako. Tumia muda wako vizuri leo na sasa ukiyachunguza mapungufu yako,
ile uenende katika njia sahihi ya Mungu. Huruma na neema ya Mungu ni kubwa kuliko
dhambi zako. Ni kwa huruma na neema hiyo ya Mungu, “baadhi
yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini
mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika Roho wa Mungu
wetu,” 1Kor 6:11. Jeuri na kiburi ya nafasi, cheo, na madaraka uliyo nayo ni
kwa muda tu. Ipo siku utagundua kuzungukwa kwako leo kote na watu kulimaanisha
tu nafasi uliyokuwa nayo na wala sio utu
kwako na watu uliokuwa unawaongoza. Majuto ni mjukuu!
Yesu Kristo kama
kiongozi wetu na aliyeishi kile alichokisema, ili kutimiza hazma ya kile
alichokijia, yaani, kumkomboa mwanadamu kutoka utumwa wa dhambi, aliyaweka yote
wazi tangu mwanzo. Iwaya ya yote, Yesu Kristo alikuwa na kauli mbiu kama dira
ya kila mmoja kufuata ili kufika kule alikotaka sote tufike-uzima wa milele.
Kauli mbiu hii ilikuwa hivi; “Wakati umetimia,
na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini Injili,” Mk 1:15. Kwa maana
nyingine, huruma na neema ya Mungu hufanya kazi yake pale tunapoipokea huruma
na neema hiyo kwa kufanya toba ya kweli na majuto ya dhambi.
Na
hata baada ya kutoa kauli mbiu yake hiyo, Yesu alionyesha wazi mpango kazi wake
mwanzoni kabisa kabla ya kufanya chochote. Na mambo yalikuwa hivi; “Akaenda Nazareti, hapo
alipolelewa; na siku ya sabato akaingia katika sinagogi kama ilivyokuwa desturi
yake, akasimama ili asome. Akapewa chuo cha
nabii Isaya, akakifungua chuo, akatafuta mahali palipoandikwa, Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta
kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa
kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:16-19. Mpango
kazi mzima wa Yesu hauna uchochezi wa aina yoyote ile, wala vitisho. Ni habari
njema kweli kweli na iliyojaa matumaini.
Baada ya kutoa mpango
kazi wake, Yesu akiwa Mungu na Mwanadamu, alihitaji watu wa karibu naye ili
kuitenda kazi ile aliyoijia kama tulivyoona hapo mwanzo. Kuwapata watu hawa,
Yesu hakukurupuka, bali aliyaweka yote mikononi mwa Baba yake aliye mtuma. Hivyo,
“Ikawa siku zile aliondoka akaenda mlimani
ili kuomba, akakesha usiku kucha katika kumwomba Mungu,” Lk 6:12. Ni baada ya maombi haya, Yesu anawachagua
wanafunzi wake. Na “hata kulipokuwa
mchana aliwaita wanafunzi wake; akachagua kumi na wawili miongoni mwao, ambao
aliwaita Mitume,” Lk 6:13. Hawa ndio wale Thenashara-Mitume kumi na wawili, Mt
10:2-5, yaani, “Simoni,
aliyemwita jina la pili Petro, na Andrea nduguye, na Yakobo na Yohana, na
Filipo na Bartolomayo, na Mathayo na
Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Simoni aitwaye Zelote, na Yuda wa Yakobo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyekuwa
msaliti,” Lk 6:14-16.
Hawa Thenashara ndio
waliokuwa wasaidizi wake wa karibu katika kutimiza lile alilolijia yaani,
kukuweka wewe na mimi huru kutoka utumwa wa dhambi. Na hawa Thenashara,
“akawapa uwezo na mamlaka juu ya pepo wote na kuponya maradhi,” Lk 9:1.
‘Aliwapa mamlaka’ ikimaanisha uhuru wa kufanya yale yampendezayo Mungu. Katika
kweli hii, Yesu aliruhusu ubunifu katika utendaji kila mmoja kadiri ya karama
zake. Hakika Kristo Yesu ni kiongozi kweli kweli, na mfano kwetu ulio hai.
Tujifunze kwake.
Baada ya kufanikisha mpango huu, ikiwa
ni pamoja na kuweka wazi kauli mbiu yake, mpango kazi wake, na kuwachagua watu
wake wa karibu, yaani, Thenashara, alianza mara moja kazi ile aliyoijia. Hivyo “waliokuja
kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao; na wale
waliosumbuliwa na pepo wachafu; waliponywa. Na makutano yote walikuwa wakitaka
kumgusa, kwa sababu uweza ulikuwa ukimtoka ukiwaponya wote,” Lk 6:17b-19. Yesu
kamwe hakupoteza muda wake kupambana na watesi wake. Kwa maana nyingine, Yesu
hakuwa na muda wa kupoteza kupambana na wapinzani wake; Mafarisayo, Waandishi,
na Wazee, bali aliutumia muda wake wote wa miaka ile mitatu kuhubiri Habari
Njema za Ufalme wa Mbinguni. Matokeo ya kazi yake ni uwepo wa wewe na mimi leo
kama Wakristo na wafuasi wake wenye hofu ya Mungu. Ni wajibu msingi kwa matiki
hiyo kwamba wewe na mimi yatupasa kuwa mawakili wa Kristo pale tulipo.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Ikawa
siku zile aliondoka akaenda mlimani ili kuomba, akakesha usiku kucha katika
kumwomba Mungu,” Lk 6:12
Tusali:-Ee Yesu, tufanye mawakili wako wema
pale tulipo kila mmoja kadiri ya wito na karama zake. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario