lunes, 26 de septiembre de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI; SIKUKUU YA MALAIKA WAKUU: MIKAELI, GARBIELI, NA RAFAELI


ALHAMISI WIKI YA 26 YA MWAKA-C

Sikukuu ya Malaika wakuu: Mikaeli, Gabrieli na Rafaeli

Somo: Dan 7:9-10, 13-14

Zab: 138:1-2ab, 2cde-3, 4-5

Injili: Yoh 1:47-51

Nukuu:

Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa,” Dan 7:14

Yesu akajibu, akamwambia, Kwa sababu nilikuambia, Nilikuona chini ya mtini, waamini? Utaona mambo makubwa kuliko haya,” Yoh 1:50

Akamwambia, Amin, amin, nawaambia, Mtaziona mbingu zimefunguka na malaika wa Mungu wakikwea na kushuka juu ya Mwana wa Adamu,” Yoh 1:51

TAFAKARI: “Naye atayatenda yote kadiri ya mahitaji yetu. Tumwamini daima.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anasheherekea sikukuu ya Malaika wa Kuu; Mikaeli, Gabrieli, na Rafaeli. Hawa malaika wakuu wanatambulika hivyo kutokana na kazi zao na jumbe zao walizokuwa wakiziwakilisha kwa watu mbalimbali kutoka kwa Mungu. Tafsiri ya majina yao imebeba ujumbe na maana ya kile walicho. Malaika Mkuu Mikaeli, kutoka Kiebrania inamaanisha “Nani ni sawa na Mungu?” Ni malaika alikingaye Taifa la Mungu. Jina hili linamaanisha pia “zawadi kutoka kwa Mungu.” Kazi yake na namna alivyotumika tunaweza rejea sehemu hizi katika Maandika Matakatifu {Dan 10:21; 12:1, Kut 23:20, Yud 9, Ufu 7:12}.

Malaika Mkuu Gabrieli kwa Kiebrania inamaanisha “Bingwa au Mshindi wa Mungu.” Ni mpeleka ujumbe maalum kwa watu kutoka kwa Mungu. Tunaona Malaika huyu Mkuu akimsaidia Nabii Danieli kutafsiri ndoto {Dan 8:16; 9:21}. Gabrieli anapeleka pia ujumbe kwa Zakaria kuhusu kuzaliwa kwa Yohane Mbatizaji {Lk 1:19}. Tunaona vile vile Malaika huyu Gabrieli akimfikishia ujumbe Bikira Maria kuzaliwa kwa Mwokozi wetu Yesu Kristo {Lk 1:26}. Malaika Mkuu Rafaeli, kwa Kiebrania, “Aliyeponywa na Mungu. Vile vie ilimaanisha mlinzi wa geti la hekalu kwenye agano la kale.

Wapendwa wana wa Mungu, tunapotazama kazi za malaika hawa tunaona ni kwa namna gani Mungu amewatumia katika historia nzima wa wokovu wetu. Kanisa pasipo shaka leo linasheherekea kwa kutambua nafasi na kazi zao kwa wokovu wa Mwanadamu. Ni kweli kwamba malaika humzunguka Mungu pale alipo na kuwa tayari kufanya yale atakayo Mungu. Lakini leo kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo, Padre ambaye ni Kristo mwingine, amepewa mamlaka na uwezo wa kumshusha Mungu kwa watu anaowahudumia kupitia Sakramenti ya Ekaristi Takatifu. Hivyo kwa kupitia Mwanaye Yesu Kristo, Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa,” Dan 7:14.

Ndugu zangu katika Kristo, tunapomwamini Kristo na kukaa katika njia, kweli na uzima wake, tunashirikishwa makubwa zaidi ambayo hatukuwahi kuyaona. Yesu anamwambia Nathanaeli ukweli huu, “Kwa sababu nilikuambia, Nilikuona chini ya mtini, waamini? Utaona mambo makubwa kuliko haya,” Yoh 1:50. Kristo akiwa ndiyo Jana yetu, Leo yetu, na Umilele wetu, anayafahamu yote kwa sababu kwa kupita yeye yote yalifanyika, Yoh 1:3. Kwa uwezo huu aliokuwanao Yesu, anawaambia wanafunzi wake na sisi pia kwamba, Amin, amin, nawaambia, Mtaziona mbingu zimefunguka na malaika wa Mungu wakikwea na kushuka juu ya Mwana wa Adamu,” Yoh 1:51. Yatupasa kusadiki yote haya naye Mungu kupitia mwanaye Mpendwa Yesu Kristo atayatenda maishani mwetu kadiri ya mahitaji yetu.

Tumsifu Yesu Kristo!

Akamwambia, Amin, amin, nawaambia, Mtaziona mbingu zimefunguka na malaika wa Mungu wakikwea na kushuka juu ya Mwana wa Adamu,” Yoh 1:51

Tusali:-Ee Yesu Mwema tujalie Imani thabiti. Amina

MALAIKA WAKUU WA MUNGU MTUOMBEE. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario