ALHAMISI WIKI YA 26 YA MWAKA-C
Sikukuu ya Malaika wakuu: Mikaeli,
Gabrieli na Rafaeli
Somo: Dan 7:9-10, 13-14
Zab: 138:1-2ab, 2cde-3, 4-5
Injili: Yoh 1:47-51
Nukuu:
“Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa
kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka
ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza
kuangamizwa,” Dan 7:14
“Yesu akajibu, akamwambia, Kwa sababu nilikuambia, Nilikuona
chini ya mtini, waamini? Utaona mambo makubwa kuliko haya,” Yoh 1:50
“Akamwambia, Amin, amin, nawaambia, Mtaziona mbingu zimefunguka na
malaika wa Mungu wakikwea na kushuka juu ya Mwana wa Adamu,” Yoh 1:51
TAFAKARI: “Naye atayatenda
yote kadiri ya mahitaji yetu. Tumwamini daima.”
Wapendwa
wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anasheherekea sikukuu ya Malaika wa Kuu;
Mikaeli, Gabrieli, na Rafaeli. Hawa malaika wakuu wanatambulika hivyo kutokana
na kazi zao na jumbe zao walizokuwa wakiziwakilisha kwa watu mbalimbali kutoka
kwa Mungu. Tafsiri ya majina yao imebeba ujumbe na maana ya kile walicho.
Malaika Mkuu Mikaeli, kutoka Kiebrania inamaanisha “Nani ni sawa na Mungu?” Ni
malaika alikingaye Taifa la Mungu. Jina hili linamaanisha pia “zawadi kutoka
kwa Mungu.” Kazi yake na namna alivyotumika tunaweza rejea sehemu hizi katika
Maandika Matakatifu {Dan 10:21; 12:1, Kut 23:20, Yud 9, Ufu 7:12}.
Malaika
Mkuu Gabrieli kwa Kiebrania inamaanisha “Bingwa au Mshindi wa Mungu.” Ni
mpeleka ujumbe maalum kwa watu kutoka kwa Mungu. Tunaona Malaika huyu Mkuu
akimsaidia Nabii Danieli kutafsiri ndoto {Dan 8:16; 9:21}. Gabrieli anapeleka
pia ujumbe kwa Zakaria kuhusu kuzaliwa kwa Yohane Mbatizaji {Lk 1:19}. Tunaona
vile vile Malaika huyu Gabrieli akimfikishia ujumbe Bikira Maria kuzaliwa kwa
Mwokozi wetu Yesu Kristo {Lk 1:26}. Malaika Mkuu Rafaeli, kwa Kiebrania,
“Aliyeponywa na Mungu. Vile vie ilimaanisha mlinzi wa geti la hekalu kwenye
agano la kale.
Wapendwa
wana wa Mungu, tunapotazama kazi za malaika hawa tunaona ni kwa namna gani
Mungu amewatumia katika historia nzima wa wokovu wetu. Kanisa pasipo shaka leo
linasheherekea kwa kutambua nafasi na kazi zao kwa wokovu wa Mwanadamu. Ni
kweli kwamba malaika humzunguka Mungu pale alipo na kuwa tayari kufanya yale
atakayo Mungu. Lakini leo kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo, Padre ambaye ni
Kristo mwingine, amepewa mamlaka na uwezo wa kumshusha Mungu kwa watu
anaowahudumia kupitia Sakramenti ya Ekaristi Takatifu. Hivyo kwa kupitia
Mwanaye Yesu Kristo, “Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa
kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka
ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza
kuangamizwa,” Dan 7:14.
Ndugu zangu katika Kristo, tunapomwamini Kristo na kukaa
katika njia, kweli na uzima wake, tunashirikishwa makubwa zaidi ambayo
hatukuwahi kuyaona. Yesu anamwambia Nathanaeli ukweli huu, “Kwa sababu nilikuambia, Nilikuona chini ya mtini, waamini?
Utaona mambo makubwa kuliko haya,” Yoh 1:50. Kristo akiwa ndiyo Jana yetu, Leo
yetu, na Umilele wetu, anayafahamu yote kwa sababu kwa kupita yeye yote
yalifanyika, Yoh 1:3. Kwa uwezo huu aliokuwanao Yesu, anawaambia wanafunzi wake
na sisi pia kwamba, “Amin, amin, nawaambia, Mtaziona mbingu zimefunguka na malaika wa
Mungu wakikwea na kushuka juu ya Mwana wa Adamu,” Yoh 1:51. Yatupasa kusadiki
yote haya naye Mungu kupitia mwanaye Mpendwa Yesu Kristo atayatenda maishani
mwetu kadiri ya mahitaji yetu.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Akamwambia, Amin, amin, nawaambia, Mtaziona mbingu zimefunguka
na malaika wa Mungu wakikwea na kushuka juu ya Mwana wa Adamu,” Yoh 1:51
Tusali:-Ee Yesu Mwema tujalie
Imani thabiti. Amina
MALAIKA WAKUU WA
MUNGU MTUOMBEE. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario