domingo, 31 de julio de 2016

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 18 YA MWAKA-C

JUMATATU WIKI  YA 18 YA MWAKA-C
Somo: Yer 28:1-17
Zab: 119:29, 43, 79, 80, 95, 102
Injili: Mt 14:13-21
Nukuu:
 “Ndipo nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania, mbele ya makuhani, na mbele ya watu wote waliosimama ndani ya nyumba ya Bwana, naam, nabii Yeremia akasema, Amina, Bwana na atende hivi; Bwana ayatimize maneno yako uliyotabiri, kuvirudisha hapa vyombo vya nyumba ya Bwana na watu wote waliofungwa, toka Babeli, hata mahali hapa,” Yer 28:5-6 

 “Kisha nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania, Sikia sasa, Ee Hanania; Bwana hakukutuma; lakini unawatumainisha watu hawa maneno ya uongo,” Yer 28:15 

Basi Bwana asema hivi, Tazama, nakutuma uende zako toka juu ya uso wa nchi; mwaka huu utakufa, kwa sababu umenena maneno ya uasi juu ya Bwana,” Yer 28:16 

Basi nabii Hanania akafa, mwaka uo huo, mwezi wa saba,” Yer 28:17

Naye Yesu aliposikia; hayo, aliondoka huko katika chombo, akaenda mahali pasipo watu, faraghani. Na makutano waliposikia, walimfuata kwa miguu kutoka mijini mwao,” Mt 14:13 

Yesu akatoka, akaona mkutano mkuu, akawahurumia, akawaponya wagonjwa wao,” Mt 14:14

Yesu akawaambia, Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula,” Mt 14:16

TAFAKARI:Nabii atabiriye habari za amani, neno la nabii yule litakapotokea, ndipo nabii yule atakapojulikana, kuwa Bwana amemtuma kweli kweli.”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, si jambo la ajabu leo kusikia na hata kuona mifumuko ya unabii na hata wengine kujipambanua kama manabii. Kuwa nabii siyo kitu cha kujitwalia wala kujinasibu, bali ni kuhesabiwa haki na Mungu mwenyewe tukijua kile usemacho ni ujumbe wa Mungu na umetumwa na Mungu kusema hivyo na siyo kadiri ya ndoto zako, au tafsiri zako zenye malengo binafsi. Kwa maantiki hiyo, Nabii atabiriye habari za amani, neno la nabii yule litakapotokea, ndipo nabii yule atakapojulikana, kuwa Bwana amemtuma kweli kweli,” Yer 28:9. Ni katika mizania hii tunaona nani ni nabii wa kweli kati ya Yeremia na Hanania. Hanania anatoa utabiri wa uongo kwa lengo tu la kumfurahisha mfalme kwa sababu ndicho mfalme atakacho kusikia, Yer 28:1-4.

Akijua unabii ule si wa kweli, Ndipo nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania, mbele ya makuhani, na mbele ya watu wote waliosimama ndani ya nyumba ya Bwana, naam, nabii Yeremia akasema, Amina, Bwana na atende hivi; Bwana ayatimize maneno yako uliyotabiri, kuvirudisha hapa vyombo vya nyumba ya Bwana na watu wote waliofungwa, toka Babeli, hata mahali hapa,” Yer 28:5-6. Kwa kujipambanua na kuwasadikisha watu kwamba asemacho ni kweli kutoka kwa Mungu, nabii Hanania akaitwaa ile nira iliyokuwa juu ya shingo ya Yeremia, akaivunja,” Yer 28:10. Tendo hili la kuivunja nira juu ya shingo la Yeremia lilimaanisha  ndivyo Bwana atakavyoivunja nira ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli, kabla haujatimia muda wa miaka miwili mizima, na kuiondoa shingoni mwa mataifa yote,’ Yer 28:11. Ni mbaya sana kujiinua nafsi yako, na hasa pale utakapo kupata sifa kutoka kwa watu na kujipendekeza kwa wakubwa na kusahau ile kweli. 

Hata hivyo Mungu huwa hamfichi mnafiki. Huyu ndiye Mungu asiye kwenda na mawimbi yetu wanadamu wala matakwa yetu binafsi. Ndipo neno la Bwana likamjia Yeremia, baada ya Hanania, nabii, kuivunja ile nira iliyokuwa juu ya shingo ya Yeremia, kusema,  Enenda ukamwambie Hanania, ukisema, Bwana asema hivi, Umezivunja nira za mti; lakini badala yake utafanya nira za chuma,” Yer 28:12-13. Na nira za chuma ilimaanisha kwamba, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nimetia nira ya chuma juu ya shingo ya mataifa haya yote, ili wamtumikie Nebukadreza, mfalme wa Babeli nao watamtumikia; nami nimempa wanyama wa nchi pia,” Yer 28:14. Kitendo hiki kilimaanisha kwamba, ‘wana wa Israeli hawakutaka kulijua kosa lao lililowafanya kuwa katika hali ile ya utumwa.’

Ingawa Huruma na Neema ya Mungu ipo muda wote na wakati wowote, bila kufanya toba ya kweli na majuto kumrudia Mungu, huruma na neema hiyo ya Mungu itapita tu bila kuguswa nayo. Na wale wote wenye kuupindisha ukweli wa Mungu kama ulivyo hawawezi kubaki salama. Kisha nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania, Sikia sasa, Ee Hanania; Bwana hakukutuma; lakini unawatumainisha watu hawa maneno ya uongo,” Yer 28:15. Hii siyo maana ya kuwa Nabii wa Mungu kama mjumbe wake mwaminifu. Na hivi ndivyo Yeremia alivyo ufikisha unabii wa kweli kwa Hanania;  Basi Bwana asema hivi, Tazama, nakutuma uende zako toka juu ya uso wa nchi; mwaka huu utakufa, kwa sababu umenena maneno ya uasi juu ya Bwana,” Yer 28:16. Na unabii huu ulitimia kwa nabii Hanania kwani alikufa mwaka uo huo, mwezi wa saba,’ Yer 28:17

Kristo Yesu ndiye ukamilifu wa nyakati na unabii wote uliyo kwisha tangulia kabla yake. Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana,” Gal 4:4-5. Na Injili ya leo tunaona hali hiyo ya kuwa wana kwa ukarimu wa Mungu kwa watu wake. Yesu anawaonea huruma wale waliokuwa wanasikiliza neno lake la uzima. Kibinadamu wanafunzi wa Yesu wanatoa ushauri kwa Yesu kuwa watu waachwe waende zao vijini na kutafuta chakula. Yesu anawakumbusha wajibu wao kuwa yawapasa kuwalisha watu hao chakula. Hivyo Yesu anawaambia, Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula,” Mt 14:16. Wapendwa katika Kristo, kwa ubatizo wetu tunashiriki ukuhani wa Kristo, unabii, na ufalme wake. Hivyo kila mbatizwa kadiri ya wito wake anajukumu la kuwapa chakula watu wale aliokabidhiwa. Na zaidi chakula hiki siyo tu hiki cha leo na kesho bali neno la uzima wa milele, ili wamjue Kristo, Mwana wa Mungu kuwa ndiye ‘Njia ya kweli, kweli isiyo shaka, na Uzima wetu,’ Yoh 14:6

Tumsifu Yesu Kristo!

Yesu akawaambia, Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula,” Mt 14:16


Tusali:-Ee Yesu, tuepushe na unabii na manabii wa uongo, na mara zote tubaki katika kweli yako. Amina

viernes, 29 de julio de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 18 YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 18 YA MWAKA-C
Somo I: Mhu 1:2; 2:21-23
Zab: 95:1-2, 6-7, 8-9
Kol 3:1-5, 9-11
 Injili: Lk 12:13-21
Nukuu:
 “Maana kuna mtu ambaye kazi yake ni kwa hekima, na kwa maarifa, na kwa ustadi; naye atamwachia mtu asiyeshughulika nayo kuwa sehemu yake. Hayo tena ni ubatili, nayo ni baa kuu,” Mhu 2:21 

 “Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu,” Kol 3:1 

 “Hapo hapana Myunani wala Myahudi, kutahiriwa wala kutokutahiriwa, mgeni wala mshenzi, mtumwa wala mwungwana, bali Kristo ni yote, na katika yote,” Kol 3:11 

Akamwambia, Mtu wewe, ni nani aliyeniweka mimi kuwa mwamuzi au mgawanyi juu yenu?” Lk 12:14

Akawaambia, Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo,” Lk 12:15

Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu,” Lk 12:20-21

TAFAKARI: “Na jina lake Mataifa watalitumainia. Kristo ni yote, na katika yote.”

Wapendwa wana wa Mungu, Leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 18 ya mwaka “C” wa Kanisa. Tunapoyatazama masomo yetu ya leo tunazamishwa na Mama Kanisa kutafakari na kushirikishana kweli hii, kwamba, “Na jina lake Mataifa watalitumainia. Kristo ni yote, na katika yote.” Somo la kwanza kadiri ya Mhubiri, anayaona maisha si kitu wala chochote, bali ni ‘ubatili mtupu, ubatili mtupu, mambo yote ni ubatili,’ Mhu 1:2. Swali la msingi na la kujiuliza ni hili, nitawezaje kuitamani hiyo kesho kama sioni maana ya leo? Kama tumeumbwa ili tuishi milele, na Mungu akaona inafaa tuwepo ulimwenguni hapa, iweje tena niwe na mawazo haya kwamba mtu apata nini kwa kazi yake yote, na kwa juhudi ya moyo wake alivyojitahidi chini ya jua?’ Mhu 2:22.

Ndugu yangu, ni vyema nikaelewa kwamba vyote vinavyoonekana na visivyoonekana alivyoviumba Mungu kwa asilimia kubwa vinamlenga huyu mwanadamu aliyepewa heshima ya juu kabisa kwa kuumbwa kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Ni katika mantiki hiyo, “Bwana aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni Bwana, wala hapana mwingine,” Isa 45:18. Pamoja na mahangaiko na sintofahamu za maisha, ulimwenguni hapa pana kusudio la Mungu katika maisha yetu. Hapa ndipo uwanja wa kujua kusudi la kuumbwa kwetu na kujiandaa katika uzima ule wa milele. Na kwa kusudi la kuumbwa kwetu, hapa duniani ndipo tutakapo mjua Mungu, mpenda Mungu, mtumikia Mungu, na mwisho kurudi kwake mbinguni.

Ni kweli kabisa hapa na pale tutakatishwa tamaa, ila isiwe sababu ya kutokuona kusudi la Mungu katika upana wa uumbaji wake. Ufanyalo zuri leo, kesho laweza kufutwa kwa hila tu na kutoweka. Ila pamoja na hali hiyo, hatuwezi kufuta wema wa lililo jema mbele ya macho ya Mungu. Na hata jambo hilo linapobaki katika historia yake, huendelea kuwa somo kwa vizazi na vizazi. Maana kuna mtu ambaye kazi yake ni kwa hekima, na kwa maarifa, na kwa ustadi; naye atamwachia mtu asiyeshughulika nayo kuwa sehemu yake. Hayo tena ni ubatili, nayo ni baa kuu,” Mhu 2:21. Pamoja na mtizamo huu wa Mhubiri, maisha ni zaidi ya yale tuyafanyayo leo au kuyamiliki. Jambo la maana na muhimu ni kuwa huru nje ya yale tuyafanyayo na kuyamiliki. Tusipojibadua katika haya, maisha hukosa maana na hasa pale yanapotoweka yale tuyafanyayo na kuyamiliki. Ni swala la wakati kwamba itafika mahali hatutaweza kufanya chochote.

Je, katika hali hiyo ya kutokufanya chochote, utu wetu utatoweka kwa sababu tu wazee? Utajiri na mali tulizonazo tumemilikishwa kwa muda tu na wakati ukifika watamilikishwa wengine, nasi tutaondoka kama tulivyokuja bila chochote kwa sababu,  Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, Dunia na wote wakaao ndani yake,” Zab 24:1. Ndugu yangu, tunapojimilikisha yale ambayo kwa asili siyo yetu, mwisho wa siku huwa ni ubatili na masikitika makubwa.Kwa kuwa siku zake zote ni masikitiko, na kazi yake ni huzuni; naam, hata usiku moyoni mwake hamna raha. Hayo nayo ni ubatili,” Mhu 2:23.

Wapendwa Taifa la Mungu, Injili ya leo, inatutaka tutafakari kwa undani maisha yetu na uhusiano wake na mali. Ndugu moja anamwendea Yesu mbele ya mkutano na kumwamuru amwambie ndugu yake amgawie urithi wao, Lk 12:13. Badala yake, Yesu anamuuliza swali la msingi na la kushangaza. Akamwambia, Mtu wewe, ni nani aliyeniweka mimi kuwa mwamuzi au mgawanyi juu yenu?” Lk 12:14. Swali hili linatutaka kuweka bayana nini maana ya maisha yetu na mahusiano yake na mali. Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, elewa leo kwamba maisha yako ni dhamana hapa duniani, na mali tulizo nazo tumeazimwa tu kwa muda. Mali ni za Mungu.

Wapendwa wana wa Mungu, muda wetu hapa duniani na nguvu zetu, akili, nafsi, mahusiano, na mali zetu zote ni zawadi toka kwa Mungu ambazo ametukabidhi tuvitunze na kuvitumia vizuri. Sisi ni mawakili wa yale Mungu atupayo. Wazo hili la uwakili huanza na utambuzi wa kuwa Mungu ndiye mmiliki wa kila kitu na kila mtu duniani. "Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, dunia na wote wakaao ndani yake." Zab 24:1. Hivyo Yesu anamtahadharisha kijana yule na sisi pia kwa kutuambia kwamba, “Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo,” Lk 12:15. Uzima wako na furaha yako ya kweli haitokani na wingi wa mbali ulizokuwa nazo. Kwa maana nyingine, vitu hivyo kwa kuwa navyo kwa wingi havituhesabii haki mbele za Mungu. Ndugu yangu, kama humwamini yule aliyefufuliwa kutoka wafu yaani, Kristo Yesu, wingi wa utajiri wako ni bure kabisa kwa sababu mali zote ni za Bwana ukiwa na wewe mwenyewe. Mtume Paulo anasema, sisi tunaomwamini yeye aliyemfufua Yesu Bwana wetu katika wafu; ambaye alitolewa kwa ajili ya makosa yetu, na kufufuliwa ili mpate kuhesabiwa haki,” Rum 4:24b-25. Hivyo wingi wa mali zako bila Imani juu ya Kristo mfufuka ni bure.

Hakika "hatumiliki" chochote kwa wakati wetu mfupi wa kuishi duniani. Mungu "hutukopesha" dunia tunapoishi hapa. Ilikuwa mali ya Mungu kabla hujaja, na Mungu anamkopesha mtu mwingine ukifa. Je unabisha? Ndugu, ukweli ni kwamba unaifurahia dunia hii kwa muda mfupi tu. Injili ya leo inatuambia kwamba asiyefahamu ukweli huu ni MPUMBAVU kama mkulima yule tajiri aliyetaka kufurahisha nafsi yake kwa kusema, ‘pumzika basi, ule, unywe, ufurahi,” bila kujua ni nani aliye sababu ya uzima wake. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu,” Lk 12:20-21. Ndugu yangu bado furaha yako ipo kwenye mali?

Mungu alipowaumba Adamu na Hawa, aliwakabidhi uangalizi wa uumbaji wake na akawaweka kuwa wadhamini wa uumbaji wa mali yake. "Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi," Mwa 1:28

Kazi ya kwanza ambayo Mungu aliwapa wanadamu ni kuangalia na kutunza "vitu" vya Mungu duniani. Wajibu huu haujaondolewa kamwe. Ni sehemu ya malengo yetu leo. Kila kitu tunachokifurahia yapasa tukione kama dhamana ambayo Mungu ameiweka mikononi mwetu. "Hapo tena inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu." 1Kor 4:2

Yesu mara kwa mara anaonyesha kuwa maisha ni dhamana na anatoa mfano wa talanta, mfanya biashara alikabidhi watumishi utajiri wake alipo safiri. Aliporudi alitathmini kazi ya kila mtumishi na kumpa ujira sawasawa na kazi yake. Yule tajiri anasema,  "vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya Bwana wako," Mt 25:21.

Ndugu, mwisho wa maisha yako duniani utatathminiwa kulingana na ulivyotumia yale Mungu aliyokukabidhi. Hii inamaana kwamba mambo yote unayofanya, hata yale mambo madogo madogo ya kila siku, yana matokeo ya umilele.

Kama utaona mambo yote kuwa dhamana, Mungu anaahidi zawadi tatu katika maisha ya milele. Kwanza, utapewa "uthibitisho". Atasema, "kazi nzuri! umefanya vyema." Kisha "utapandishwa" daraja na utapewa jukumu kubwa katika umilele: "nitakuweka uwe mwangalizi wa vitu vingi." Na mwisho utakaribishwa katika "karamu." "Njoo ushiriki katika furaha ya Bwana wako.

Watu wengi wanashindwa kufahamu kuwa pesa ni jaribu na dhamana toka kwa Mungu. Mungu anatumia pesa kutufundisha kumtegemea; na kwa watu wengi fedha ni jaribu kuu kupita yote.Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi,” 1Tim 6:10. Mungu anaangalia jinsi tunavyotumia pesa ili kupima jinsi gani tunaaminika. "Basi, kama ninyi hamkuwa waaminifu katika mali ya udhalimu, ni nani atakayewapa amana mali ya kweli?" Lk 16:11. Huu ni ukweli wa muhimu sana. Mungu anasema kuna uhusiano wa moja kwa moja baina ya ninavyotumia pesa zangu na hali yangu ya kiroho. Jinsi ninavyotawala pesa zangu "utajiri wa dunia" ni kigezo cha kiasi gani Mungu anaweza kunikabidhi baraka za kiroho, "utajiri wa kweli".

Hebu jiulize ndugu yangu, Je, namna ninavyotumia fedha zangu yaweza kumzuia Mungu kufanya mambo zaidi maishani mwangu? Je, ninaweza kuaminiwa katika utajiri wa kiroho? Wapo watu wachache katika mazingira na maisha yetu, waliweza kuthibitisha uhusiano wa moja kwa moja baina ya walivyotumia pesa zao na hali ya kiroho ya maisha yao. Pesa au utajiri wao havikuwa kipao mbele katika maisha yao. Watu na maisha yao ya dhiki ilikuwa kero zake na mara zote alijitahidi kutafuta suluhu ya kero hizo za watu. Mtu wa namna hii ndiye tunayeweza kuumpa dhamana ya kusimamia mali ya umma. Alilolisema ndilo alilolifanya. Dhima hii ndiyo iliyompa nguvu ya Kimaadili. Mfano wa mtu huyu ni Baba yetu wa Taifa; Julius Kambarage Nyerere, aliyetutangulia katika haki. Apate rehema kwa Mungu apumzike kwa amani. Sina shaka katika maisha yake. Ipo siku atapewa uangalizi mkubwa zaidi na Mama Kanisa na kuwa Mwombezi wetu-Mtakatifu.

Yesu Kristo anasema, "na yule asiyejua, naye amefanya yastahiliyo mapigo, atapigwa kidogo. Na kila aliyepewa vingi, kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake huyo watataka na zaidi." Lk 16:48. Maisha ni dhamana. Na kadiri Mungu anavyokupa zaidi, ndivyo anakutaka uwajibike zaidi.

Ndugu yangu, pamoja na kuishi leo na sasa na changamoto zake, yanipasa kujua shabaha ya maisha yangu ipo wapi. Kama Mkristo na mfuasi wa Kristo, Kristo ndiye shabaha maisha yangu. ‘Na jina lake Mataifa watalitumainia. Kristo ni yote, na katika yote.’

Kwa nini Kristo ndiye shabaha ya maisha yako kama Mkristo na mfuasi wake? Ndugu yangu, wakati fulani wanafunzi wa Yohana Mbatizaji walimwona Yesu akiwa anabatiza, nao walimwendea Yohana Mbatizaji ili kujua juu ya kile afanyacho Yesu, na nafasi yake katika ufahamu na umaana wake. Yohana akajibu, akasema, Hawezi mtu kupokea neno lo lote isipokuwa amepewa kutoka mbinguni,” Yoh 3:27. Kwa jibu hili la Yohana ilithibitisha Kristo ndiyo njia sahihi na hapana shaka juu yake. Pamoja na ukweli kwamba vyote vilifanyika kwa huyo (NENO-CHRISTO); wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3, kwa kinywa chake Yesu Kristo analithibitisha hili na kusema, hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa na Baba yangu,” Yoh 14:65. Ni ndani na katika Kristo kuna njia, kweli, na uzima. Naye Yesu anasema,Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, nje ya Kristo una nini kilichochako zaidi ya dhambi zako?

Kristo ndiye shabaha ya maisha yako unapotazama fumbo zima la mateso, kifo na ufufuko wa Kristo. Tendo hili la UFUFUKO wa Bwana wetu Yesu Kristo ndiyo fursa ya pekee kwa wale wote wamuaminio Kristo, ambaye ndiye mwisho wa shaka yote. Naye Mtume Petro analisema tukio hili katika undani na upana wake. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 4:12. Ndugu yangu hapo ulipo Kristo yupo? Hapo ulipo usalama upo bila Kristo? Ndugu yangu hata nikipoteza vyote katika ulimwengu huu kama ninaye Kristo ndani ya maisha yangu sitokuwa nimepungukiwa na chochote.

Na hivi ndivyo asemavyo Mtume Paulo hasa kwa wale wanaaminio ufufuo wa Kristo, na upya wa maisha yao ndani na katika Kristo; Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu,” Kol 3:1. Tendo la Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo linatusukuma toka ndani ya mioyo yetu na imani yetu kuyatafuta yaliyo juu kule Kristo aliko. Kwa Mkristo yeyote hapa duniani asipolifanya jambo hili kuwa kielelezo cha maisha yake, basi ajue kwake ufufuko hauna maana ye yote. Mtume Paulo anasema hivi kuhusu ufufuko, “tena kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubiri kwetu ni bure na imani yenu ni bure,” 1Kor 15:14. Ufufuko wa Kristo ndiyo kiini cha Imani yetu.

Ndugu yangu, mambo yaliyo juu aliko Kristo ni yale yote yanayotuongoza huko aliko, yaani ufalme wa mbinguni na umilele wake. Kwa maneno mengine ni kuvaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba,” Kol 3:10. Utu huu upya ni tendo la kupiga vita aina zote za dhambi kwa sababu dhambi ufifisha na kuzorotesha utu wetu wa ndani ambao ni nafsi na roho.

Jambo la pili na lenye maana kabisa katika maisha ya kiroho ni kufikiri muda wote yale yaliyo juu na siyo yaliyo katika nchi. Hapa Mtume Paulo anaongelea sana swala la nafsi ya mtu. Nafsi inapoegemea zaidi katika mwili matokea yake ni anguko kuu na mwisho wa matumaini yote ya kuurithi ufalme wa Mungu. Hapa ndipo binadamu anapoonekana mara zote kufikiri yaliyo katika nchi na yasiyo na umilele. Kuepukana na kadhia hii, Mtume Paulo anatoa angalizo kwa kusema,  Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu; kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu,” Kol 3:5-6. Ghadhabu ya Mungu hapa ni kuukosa ufalme wake na kuangamia milele pasipo kuwa na nuru yake.

 Ndugu yangu, pale nafsi inapoegemea roho, ndipo tunapojazwa tumaini jipya na kufanywa upya siku kwa siku.Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku,” 2Kor 4:16. Kuishi ukweli huu ndani na katika Kristo ni kuchuchumilia cheo chetu halisi, yaani UTAKATIFU WAKO! Cheo hiki kila mmoja wetu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu ndiyo stahili yake, na anaipata kwa kuishi kweli kwa mafundisho ya Kristo, na kutimiza ukweli huo kwa uaminifu. Hivyo hasili zetu katika maana ya mila na desturi zetu, familia zetu, koo zetu, makabila yetu, na utaifa wetu hazina uhalalisho wowote katika cheo hiki kama hatunaye Kristo katika maisha yetu ya kila siku. Ni kwa sababu hii Mtume Paulo anawapa angalizo watu wa nyakati zake, na sisi pia kwa kusema, hapo hapana Myunani wala Myahudi, kutahiriwa wala kutokutahiriwa, mgeni wala mshenzi, mtumwa wala mwungwana, bali Kristo ni yote, na katika yote,” Kol 3:11.

Wapendwa katika Kristo, angalizo la mtindo huo alilotoa Mtume Paulo na lenye kutuweka katika mstari sahihi kuelekea urithi tulioandaliwa na wenye hadhi ya cheo chetu, ndiyo changamoto kubwa kama wafuasi wake Kristo. Na changamoto ya Mkristo ni kupenda hata pale pasipopendeka, ikiwa kipimo cha upendo huo ni kupenda bila kipimo. Kwa kupenda kwa mtindo huu, mimi na wewe tuwe tayari kuyapokea yale aliyoyapokea Kristo Yesu, ila kwa sasa na kwa tumaini kubwa ni kwamba, Kristo kesha yashinda mateso hayo, Kristo kesha ushinda Msalaba.

Ni katika pendo hilo Kristo anapomponya mtu yule aliyepooza mkono, Mt 12:13, Mafarisayo wanafanya shauri la kumwangamiza, Mt 12:14. Ila kwa mbinu hizi hawatafanikiwa kama ulivyokuwa utabiri wa Nabii Isaya, akisema,Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; Mpendwa wangu, moyo wangu uliyependezwa naye; Nitatia roho yangu juu yake, Naye atawatangazia Mataifa hukumu,” Mt 12:17-18. Kumbe usalama wangu na wako upo kwa Kristo mwenyewe, na huu ndio ule  “Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata ailetapo hukumu ikashinda,” Mt 12:20. Naam, Na jina lake Mataifa watalitumainia,” Mt 12:21. Je, bado una mashaka na Kristo Yesu?

Upendo Katete, binti aliyetoka familia masikini sana ya Bwana na Bibi Lazaro Katete, alisoma kwa shinda sana hadi kufikia kiwango cha kuwa Daktari bingwa wa magonjwa ya akina Mama na Watoto. Kuhitimu masomo yake hayo ilikuwa mwanzo mpya wa maisha mapya katika familia yao. Baada ya miezi sita ya kuajiriwa kwake, ulilipuka ugonjwa wa Ebola katika nchi yake na hivyo aliona ni wakati wa kuitumia elimu na utaalamu wake, na kama sadaka katika nchi yake.

Baada ya mwenzi mmoja akiwa anatoa huduma hiyo katika kambi rasmi ya wagonjwa wa Ebola, hali ilibadilika ghafla kwani naye alionekana ana dalili za kuambukizwa ugonjwa huo. Kambi nzima iliingiwa na hofu, si kwa sababu ya ugonjwa ule ambao kwa wakati ule ulikuwa si kitu cha kuepukika, bali waliingiwa hofu kumwana mtu ambaye alikuwa karibu nao na kujitoa bila kujibakiza kuwahudumia hawezi tena kufanya hivyo.

Na baada ya wiki mbili, Upendo Katete alifariki. Hakika lilikuwa pigo kubwa sana kwa jamii ile na hasa wazazi wake na familia yake kwa sababu nuru ile iliyokuwa inang’aa ilizimika ghafla. Familia yake haikupata hata nafasi ya kumwona na hata kumpa heshima ya mwisho kwa kuuaga mwili wake, kutokana na hathari za wao pia kuambukizwa.

Baada ya miaka mitano, na kwa kutambua mchango wake na historia ya maisha yake, jamii yake na msaada kutoka nje ya nchi ile, waliamua kujenga hospitali kubwa sana kwa heshima yake yenye kutoa huduma kwa akina mama na watoto. Kumbe tukio hili linatukumbusha maneno haya ya Yesu,  Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi,” Yoh 12:24. Ndugu yangu, ni wazi leo Upendo Katete hayupo tena katika hali ya kushikika, ila bado na kwa kiasi kikubwa anaendelea kuishi na kutoa hudumu kwa jamii yake kupitia hospitali hii; “Upendo Katete Hospital.”

Tumsifu Yesu Kristo

Hapo hapana Myunani wala Myahudi, kutahiriwa wala kutokutahiriwa, mgeni wala mshenzi, mtumwa wala mwungwana, bali Kristo ni yote, na katika yote,” Kol 3:11


Tusali:-Ee Yesu, maisha yetu yana maana ndani na katika wewe. Tupe ujasiri wa kuyatafuta katika maisha yetu kila siku yale ya juu pale ulipo. Amina

jueves, 28 de julio de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 17 YA MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI  YA 17 YA MWAKA-C
Somo: Yer 26:11-16, 24
Zab: 69:15-16, 30-31, 33-34
Injili: Mt 14:1-12
Nukuu:
Ndipo hapo makuhani, na manabii, wakawaambia wakuu na watu wote, wakisema, Mtu huyu amestahili kufa, kwa sababu ametabiri juu ya mji huu, kama mlivyosikia kwa masikio yenu,” Yer 26:11 

Ndipo Yeremia akawaambia wakuu wote na watu wote, akisema, Bwana ndiye aliyenituma kutabiri juu ya nyumba hii, na juu ya mji huu, maneno hayo yote mliyoyasikia,” Yer 26:12

 “Maana Herode alikuwa amemkamata Yohana, akamfunga, akamtia gerezani, kwa ajili ya Herodia, mke wa Filipo nduguye,” Mt 14:3 

Kwa sababu Yohana alimwambia, Si halali kwako kuwa naye,” Mt 14:4 

 “Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe; akatuma mtu, akamkata kichwa Yohana mle gerezani,” Mt 14:9-10

TAFAKARI: “Kuwa tayari na jiandae kwa kulipa gharama pale utakapo simama katika kweli na haki.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo kwa namna ya pekee tunapotafakari ule ‘utayari wa kulipa gharama pale utakapo simama katika kweli na haki,’ Nabii Yeremia na Yohane Mbatizaji ndiyo dira na kielelezo cha kweli hiyo. Ipo vita kubwa sana kati ya giza na mwanga. Popote pale kinapokuwepo kimoja, ni kwa namna hiyo hiyo kwamba kingine kipo vitani kukipindua kile kinachoonekana. Hata kama hakionekani haimaanishi kwamba hakipo.

Na sasa tuanze kwa kumtazama Nabii Yeremia kwa kile alichokisimamia katika kweli na haki, na madhara anayokumbana nayo. Utabiri ule wa Yeremia ambao ni ujumbe kutoka kwa Mungu, Yer 26:4-6, unazua taharuki na kufikia hatua ya makuhani na manabii kuitoa roho yake. Ukitaka urafiki na ulimwengu huu, waambie watu kile wanachopenda kusikia. Hapa utapigiwa magoti na makofi kuanzia walevi hadi wafalme wa ulimwengu huu. Kwa vile Yeremia alisimama katika kweli na haki ya Mungu, mambo yalimwendea ndivyo sivyo katika mizania ya kibinadamu. Ndipo hapo makuhani, na manabii, wakawaambia wakuu na watu wote, wakisema, Mtu huyu amestahili kufa, kwa sababu ametabiri juu ya mji huu, kama mlivyosikia kwa masikio yenu,” Yer 26:11. Kutokana na mtafaruku huu, Yeremia haachi kuwaeleza chanzo na sababu ya ujumbe ule wa Mungu. Ndipo Yeremia akawaambia wakuu wote na watu wote, akisema, Bwana ndiye aliyenituma kutabiri juu ya nyumba hii, na juu ya mji huu, maneno hayo yote mliyoyasikia,” Yer 26:12. Mara nyingi hata baada ya kuujua ukweli kwa vile twapenda kuendelea katika uovu, hutumia nguvu kubwa kuushikilia uovu, badala ya kubadilika na kuwa mikono salama zaidi.

Ndugu yangu, katika hali na mazingira kama haya, yakupasa kujiandaa vizuri kwani vitisho huwa vingi sana ili tu kukukatisha tamaa na kurudi nyuma. Je, katika hali na mazingira haya tujisalimishe na kuifunga midomo yetu? La hasha! Pamoja na vitisho hivyo, Yeremia anasimamia maneno yake, na kuwaambia, tengenezeni njia zenu, na matendo yenu, mkaisikilize sauti ya Bwana, Mungu wenu; naye Bwana atayaghairi mabaya aliyoyanena juu yenu,” Yer 26:13. Licha ya kuyasimamia maneno yake, Yeremia anataka waone ukweli kama ulivyo kwa sababu yote hayo ni kwa faida yao wenyewe. Lakini kwangu mimi, tazama, mimi nipo hapa mikononi mwenu; nitendeni myaonayo kuwa mema na haki mbele ya macho yenu,” Yer 26:12. Penye ukweli uongo hujitenga. Na hivi ndiyo asemavyo Yeremia, kwamba, Lakini jueni yakini ya kuwa, mkiniua, mtajiletea juu yenu damu isiyo na hatia itakuwa juu yenu, na juu ya mji huu, na juu ya wenyeji wake; kwa maana ni kweli Bwana amenituma kwenu, kuwaambieni yote mliyoyasikia,” Yer 26:15. Huu ni ujumbe mzito sana kwa wale watesi wake Yeremia. Na walioguswa na neno lile waliuona ukweli na kusema, Mtu huyu hastahili kuuawa; kwa maana amesema nasi katika jina la Bwana Mungu wetu,” Yer 26:16b. Na pona ya Yeremia ilikuwa hivi, mkono wa Ahikamu, mwana wa Shafani, alikuwa pamoja na Yeremia, wasimtie katika mikono ya watu auawe,” Yer 26:24.

Mpendwa, katika Injili ya leo tunaona hathari za matumizi mabaya ya madaraka yanayosababisha maafa makubwa kwa wale watetezi wa haki katika jamii inayowazunguka. Ni jambo la hatari sana kuwa na kiongozi anayeongozwa na mihehuko ya hisia zake, huku akitegemea sifa kutoka kwa watu. Kiongozi mwenye misukumo hii ya kihisia ni rahisi sana kuzikanyaga haki za wale anaowaongoza. Hii ni pamoja na kuwa kutokuwa makini katika ahadi azitoazo kiongozi mbele za watu. Herode anamwahidia binti yake chochote apendacho baada ya kucheza vizuri na kuufurahisha umati wa watu siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwake. Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba,” Mt 14:7. Mfalme Herode anajifunga kwa kauli yake mwenyewe. Mfalme Herode hakuwa na lakusema binti yake alipokitaka kichwa na Yohane Mbatizaji zaidi ya kutimiza ahadi yake na kulinda heshima yake kama kiongozi. Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe,” Mt 14:9. Je, ni watu wangapi huwa kafara kunakotokana na utafutaji wa sifa na umaarufu wa baadhi ya viongozi wetu?

Ni mbaya sana kutafuta umaarufu kwa kukanyaka haki za watu, na hasa wale ambao wapo kinyume chetu kutokana na matendo yetu yasiyo haki na hofu ya Mungu. Yohane Mbatizaji ni mhanga wa viongozi wale wenye kupenda sifa na umaarufu. Kosa la Yohane Mbatizaji ni kusimama katika kweli. Umauti unamfika Yohone Mbatizaji kwa sababu alimwambi Mfalme Herode Si halali kwako kuwa naye,” Mt 14:4. Wapo wahanga wengi wa mtindo wa Yohane Mbatizaji katika familia zetu, Jumuiya zetu ndogondogo za Kikristo, Jumuiya zetu za kitawa, Makanisani mwetu, sehemu zetu za kazi, na mbaya zaidi leo katika mfumo mzima wa utawala.

Herodia ameitumia nafasi hii ipasavyo kumwangamiza mtesi wake ambaye alikuwa kero kubwa hasa pale alipomsaliti mumewe na kuishi na Herode. Kamwe hatuwezi kuhalalisha kosa kwa kutenda kosa. Tunachofanya ni kupata haueni ya muda mfupi tu, ila dhambi na kusutwa kwa ndani hubaki na hata kuongezeka kwa sababu hapa tunacheza na haki ya mtu katika kweli, na kilio kisichokoma cha damu ya mwenye haki. Ni vyema tukayatafakari kwa kina matendo yetu katika kupima faida na hasara zake. Hakika hutobaki salama kwa kufanya dhuluma kwa mtu mwenye haki. Yohana Mbatizaji anawawakilisha wengi leo katika jamii yetu. Wapo wengi leo wamenyamazishwa hata kuuwawa kwa sababu tu za kisiasa na hasa pale waliposema ‘hii halili jambo hili kuwa kama lilivyo.’ Wapo pia wengi walionyamazishwa na hata kuuwawa kwa vile tu walijaribu kuufichua uovu katika maana ya kugusa maslahi ya watu fulani.

Wapendwa tuutafute kwanza ufalme wa Mbinguni na mengine yote tutapewa kwa ziada.

Tumsifu Yesu Kristo!

Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe; akatuma mtu, akamkata kichwa Yohana mle gerezani,” Mt 14:9-10


Tusali:-Ee Mungu, tujalie hekima na busara katika uongozi. AminaT

miércoles, 27 de julio de 2016

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 17 YA MWAKA-C

IJUMAA WIKI  YA 17 YA MWAKA-C
Somo: Yer 26:1-9
Zab: 69:5, 8-10, 14
Injili: Mt 13:54-58
Nukuu:
 “Bwana asema hivi, Simama katika uwanja wa nyumba ya Bwana, useme na miji yote ya Yuda, wajao ili kuabudu katika nyumba ya Bwana; sema nao maneno yote ninayokuamuru kuwaambia, usizuie hata neno moja,” Yer 26:2

 “Nawe utawaambia, Bwana asema hivi, Kama hamtaki kunisikia, kwenda katika sheria yangu, niliyoiweka mbele yenu, kuyasikiliza maneno ya watumishi wangu, manabii, ninaowatuma kwenu, naam, nikiondoka mapema na kuwatuma; lakini ninyi hamkuwasikiliza; basi, nitafanya nyumba hii kuwa kama Shilo, na mji huu nitaufanya kuwa laana kwa taifa zote za dunia,” Yer 26:4-6 

 “Na alipofika nchi yake, akawafundisha katika sinagogi lao, hata wakashangaa, wakasema, Huyu amepata wapi hekima hii na miujiza hii?” Mt 13:54 

Huyu si mwana wa seremala? Mamaye si yeye aitwaye Mariamu? Na nduguze si Yakobo, na Yusufu, na Simoni, na Yuda?” Mt 13:55 

Na maumbu yake wote hawapo hapa petu? Basi huyu amepata wapi haya yote?” Mt 13:56 

Wakachukizwa naye. Yesu akawaambia, Nabii hakosi kupata heshima, isipokuwa katika nchi yake, na nyumbani mwake mwenyewe,” Mt 13:57 

TAFAKARI: “Je, tuache kutenda mema? Tutende mema kwa sababu wema ni uhasilia wa Mungu mwenyewe.”

            Wapendwa wana wa Mungu, vile vyote vilivyotumika kuwakilisha Ukuu na Umungu wa Mungu havikuwa vya ajabu sana wala kustaajabisha sana. Mungu hupenda kutumia watu na mazingira ya kawaida kuufikisha ujumbe wake. Jambo la maana na muhimu lipo katika ‘ufahamu na umaana’ wa kile kisemwacho na chenye uhusino na Mungu. Mfano; Mama Bikira Maria alikuwa Binti na Bikira kama walivyokuwa mabinti wengine katika jamii ile ya Kiyahudi. Ila, Mungu alipenda na ilimpendeza kumchagua Mama Bikira Maria kumshirikisha katika ukombozi wa mwanadamu na kuinua kile kilichoanguka kutoka kwa wazazi wetu wa mwanzo, yaani, Hawa na Adamu. Ni kwa namna hiyo hiyo, Mungu aliweza kuwachagua watu wa kawaida kutoka jamii husika ili kuufikisha ujumbe wake. Na ndivyo ilivyokuwa kwa Nabii Yeremia. Na mambo yalikuwa kama hivi; Mwanzo wa kumiliki kwake Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili lilitoka kwa Bwana, kusema, Simama katika uwanja wa nyumba ya Bwana, useme na miji yote ya Yuda, wajao ili kuabudu katika nyumba ya Bwana; sema nao maneno yote ninayokuamuru kuwaambia, usizuie hata neno moja,” Yer 26:1-2. Bila shaka wapo wakupuuza na wapo wa kutilia maanani. Mara nyingi katika ubinadamu wetu tunatazama yule atoaye ujumbe, na sio uzito wa ujumbe ule utolewao.

Ukitaka kujua ukweli huu, chunguza jumuiya zetu za Kikristo. Wakati mwingine wale wenye nazo, yaani, ushawishi wa pesa na mali, usikilizwa zaidi kuliko akina kapuku kama mimi. Tunaporuhusu hali hii, Mungu ujitenga nasi hadi pale tutakapojirudi. Akiijua hali hiyo, Mungu anamsihi Nabii Yeremia na kusema, Labda watasikia, na kughairi na kuacha kila mtu njia yake mbaya; ili niyaghairi mabaya niliyokusudia kuwatenda, kwa sababu ya uovu wa matendo yao,” Yer 26:3. Ndugu yangu, chochote kile ukisikiacho chenye kubeba uzima wako na umilele wako, tafakari ujumbe ule katika ‘ufahamu wake na umaana’ wake, na siyo mtoa ujumbe, ingawa kufanya hivyo siyo mbaya. Na ujumbe wa Mungu ni huu; Nawe utawaambia, Bwana asema hivi, Kama hamtaki kunisikia, kwenda katika sheria yangu, niliyoiweka mbele yenu, kuyasikiliza maneno ya watumishi wangu, manabii, ninaowatuma kwenu, naam, nikiondoka mapema na kuwatuma; lakini ninyi hamkuwasikiliza; basi, nitafanya nyumba hii kuwa kama Shilo, na mji huu nitaufanya kuwa laana kwa taifa zote za dunia,” Yer 26:4-6. Ndugu yangu, ujumbe wa Mungu waweza kuwa wa kutia moyo, kuonya, kufundisha, na kufurahisha. Kinachotakiwa ni kuufanyia kazi ujumbe huo. Ila mara nyingi mambo hayawi hivyo.

Kwa ujumbe huu Nabii Yeremia anakuwa hatiani. Ikawa, Yeremia alipokuwa amekwisha kusema maneno yote Bwana aliyomwamuru kuwaambia watu wote, ndipo hao makuhani, na manabii, na watu wote, wakamkamata, wakisema, Bila shaka utakufa,” Yer 26:8. Hili lililomkuta Yeremia silo geni katika mazingira yetu tata ya siasa zetu zisizo na mwelekeo na zilizojaa ubinafsi. Wale wote wasiotaka maslahi yao kuguswa hawatakaa kimya. Watatafuta kila njia kuhalalisha uovu wao na kukutia hatiani. Na hivi ndivyo ilivyokuwa kwa Nabii Yeremia, nao wakamuohoji na kusema, Kwa nini umetabiri kwa jina la Bwana, ukisema, Nyumba hii itakuwa kama Shilo, na mji huu utakuwa ukiwa, hautakaliwa na mtu? Watu wote wakamkusanyikia Yeremia katika nyumba ya Bwana,” Yer 26:9. Ndugu yangu, pamoja na utata huu, lililo kweli na lisemwe katika kweli na haki. Hii njia pekee ya kuushinda uovu, tena ule unao sababishwa na uhuru na utashi wetu kama binadamu. Kama hili linatokea leo kwako kupata upinzani katika kweli na haki, wewe sio mtu wa kwanza, kwani hata Kristo alikumbana na hali hiyo hiyo. Kristo kwa wakati na jamii yake, alikuwa ishara ya utata na changamoto ya Imani. Na hili ndilo linalohusu Injili yetu la leo.

Wapendwa wana wa Mungu, ukaribu wa binadamu na Muumba wake hujidhihirisha katika tendo la kuabudu na kujisalimisha kwa mwanadamu huyu kuliko kwa pekee na kwa namna ya juu kabisa. Tendo hili la kiibada huthibitisha udogo wa mwanadamu na ukuu wa Muumba wake. Kwa ufahamu huu, hakuna njia iliyo bora zaidi ya kujisalimisha yenye kuonyesha ukaribu huu kati ya kiumbe na Muumba nje ya tendo la kuabudu.

Ndugu unayesafiri nami katika tafakari hii, ni vyema tukaona na kuzama katika neno hili: “Yesu Kristo ishara ya utata na changamoto ya Imani yetu.” Hatuwezi kuelewa vizuri historia ya wokovu wetu na sababu ya umilele wetu nje na ndani ya Kristo katika maana ya mwanzo na ukamilifu wa historia hii ya wokovu. Mwanzo wa safari hii, Yesu Kristo anasimama katika mizania ya NENO. Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu,” Yoh 1:1. Kwa maana hii, hakuna jambo lolote lile tulionalo leo kwa namna lilivyo pasipo Kristo katika uhasilia wake. Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3. Na ndivyo ilivyo pia katika ukamilifu wa historia hii ya wokovu, Kristo anasimama kama kielelezo na umilele wa kitu hicho. Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli,” Yoh 1:14.

Ni katika msingi huu Yesu Kristo ni ishara ya utata na changamoto ya Imani yetu. Utata uliopo katika fumbo hili la wokovu ni ukweli ulio wazi juu ya mianzo na miisho ya vitu vyote vinavyoonekana na visivyoonekana. Kwa kuwa katika utimilifu wake sisi sote tulipokea, na neema juu ya neema. Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo,” Yoh 1:16-17.

Pamoja na hayo yote niliyoyaelezea hapo juu, uwepo wa Kristo katika maisha yetu ya kila siku unatutaka kwenda juu zaidi tunapotazama mwanzo wa historia ya wokovu watu, na ukamilisho wake ambao kwa vyote viwili Kristo ndiye msingi wa vyote. Hivyo kwa maana nyingine hapakuwa na sababu kubwa na yaajabu kustaajabia yale aliyokuwa anayafanya Yesu kama Wayahudi wangefikiria fumbo hili la wokovu katika upana wake. Tatizo kubwa walilokuwa nalo Wayahudi na hata sisi pia katika changamoto ya Imani yetu, tunaubeba zaidi ubinadamu wetu na kuufanya miwani ya kutazamia Umungu wa Bwana wetu Yesu Kristo. Tufanyapo tendo hili, hatuwezi kuepuka utata katika Kristo. Nasi tutabakia katika hatua hii ya chini kabisa na kujiuliza kama Wayahudi: Huyu si mwana wa seremala? Mamaye si yeye aitwaye Mariamu? Na nduguze si Yakobo, na Yusufu, na Simoni, na Yuda?” Mt 13:55. Ni kweli kwamba hatuwezi kuepuka ubinadamu wetu, ila yatupasa kuushinda ubinadamu wetu siku kwa siku kadiri tunavyokua kiimani.

Ni ukweli pia usiotia shaka kwamba tusipoushinda ubinadamu wetu lazima tutachukizwa na yale ayatendayo Kristo ndani na katika mazingira yetu. Wayahudi wakachukizwa naye. Yesu akawaambia, Nabii hakosi kupata heshima, isipokuwa katika nchi yake, na nyumbani mwake mwenyewe,” Mt 13:57. Ndugu yangu, yaliyomkuta Yesu hasa katika safari hii ya ukamilifu na umilele wa wokovu wetu, hutupata pia sisi pale tunafuata nyayo zake Kristo kwa ukamilifu. Kwetu nasi tutabakia kuwa “ishara ya Utata na Changamoto katika Imani,” ndani na katika Kristo.

Ndugu yangu, ukweli ni kwamba, ukifanya mema utasemwa vibaya, na ukifanya vibaya utasemwa pia. Je, tuache kutenda mema? Tuendelee kufanya mema na kuyatenda mema hayo si kwa kutazamwa na watu. Tunafanya mema kwa sababu wema ni uhasilia wa Mungu mwenyewe, na kutenda jema ni kutenda linalompendeza Mungu lipendwe au likataliwe machoni mwa Mungu halipotezi uhalali wake.

Tumsifu Yesu Kristo!

Wakachukizwa naye. Yesu akawaambia, Nabii hakosi kupata heshima, isipokuwa katika nchi yake, na nyumbani mwake mwenyewe,” Mt 13:57


Tusali:- Ee Yesu na Mkombozi wetu, tupe ujasiri wa kupambana na ouvu pasipo woga. Amina