IJUMAA WIKI YA 13 YA MWAKA-C
Somo: Amo 8:4-6, 9-12
Zab: 119:2, 10, 20, 30, 40, 131
Injili: Mt 9:9-13
Nukuu:
“Angalia, siku zinakuja, asema Bwana MUNGU, ambazo nitaleta
njaa katika nchi; si njaa ya kukosa chakula, wala kiu ya kukosa maji, bali ya
kukosa kuyasikia maneno ya Bwana,” Amo 8:11
“Nao
watatanga-tanga toka bahari hata bahari; na toka upande wa kaskazi hata upande
wa mashariki; watapiga mbio, wakienda huko na huko, kulitafuta neno la Bwana,
wasilione,” Amo 8:12
“Naye aliposikia,
aliwaambia, Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi,” Mt 9:12
“Lakini
nendeni, mkajifunze maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka; kwa
maana sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi,” Mt 9:13
TAFAKARI: “Nataka rehema, wala si sadaka; kwa maana sikuja
kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi.”
Wapendwa wana wa Mungu, maneno haya ya Bwana wetu Yesu Kristo, “Nataka
rehema, wala si sadaka; kwa maana sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye
dhambi,” kwetu ni mwito wa toba na wongofu. Ni maneno yaliyojaa neema na huruma
ya Mungu. Ni maneno yenye uzima na yenye kutoa fursa kwa kila mmoja wetu
kuziacha njia zake mbaya na ovu, na kumrudia Mungu. Ni maneno yasiyobeba hukumu
kwa yeyote yule mwenye kuiona na kuitafakari huruma na neema ya Mungu. Na kwa
maneno hayo ya Yesu, kila mmoja wetu ana nafasi ya pekee mbele ya uso wa Mungu
licha ya mapungufu na udhaifu wake.
Huu ndio ujumbe wa
Mungu anaoutoa Nabii Amosi kwa matajiri
na mwenye mamlaka waliokuwa sababu ya dhuluma kwa masikini. Ujumbe huu
unawataka waziache njia zao mbaya na kumrudia Mungu. Naye anasema: “Lisikieni
hili, ninyi mnaopenda kuwameza wahitaji, na kuwakomesha maskini wa nchi, mkisema, Mwezi mpya utaondoka lini,
tupate kuuza nafaka? Na sabato nayo, tupate kuandika ngano? Mkiipunguza efa na
kuiongeza shekeli, mkidanganya watu kwa mizani ya udanganyifu; tupate kuwanunua maskini kwa fedha, na
wahitaji kwa jozi ya viatu; na kuziuza takataka za ngano,” Amo 8:4-6. Leo Nabii Amosi angalikuwa katika jamii yetu
angeongelea ugumu wa maisha uliosababishwa na unaosababishwa na watu wachache
waliolifisidi taifa letu na wanaoendelea kulifisidi. Hawa ndio wale wajulikanao
kwa ‘umaarufu wao’ kama ‘mafisadi.’ Wito ni kuonja moyoni na kughairi uovu kwa
sababu waovu na uovu ni chukizo mbele ya uso wa Mungu. “Laana ya Bwana i katika
nyumba ya waovu, Bali huibariki maskani ya mwenye haki,” Mit 3:33
Lolote lile lililo ovu halina
umilele ndani yake. Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu (Yesu Krito), sadaka
hii ya Mwana wa Mungu pale Msalabani, na ufufuko wake, ndicho kikomo cha uovu
wote. Hii ndiyo njia aliyoichangu Mungu kuushinda uovu. Na tunaushinda uovu
tukiwa ndani na katika Kristo Yesu. Na hivi ndivyo alivyotabiri Nabii Amosi
kwamba, “Tena itakuwa siku hiyo, asema Bwana MUNGU, nitalifanya jua
litue wakati wa adhuhuri, nami nitaitia nchi giza wakati wa nuru ya mchana,”
Amo 8:9. Tendo hili ndilo fumbo zima la kifo kile cha aibu pale Msalabani
ambacho kwayo ‘wokovu wetu ulitundikwa.’ Hakuna uhai kwa yeyote yule mwenye
kufurahia mateso ya wengine kwa namna yoyote ile, au mwenye kusukumwa na
ghariba ya uovu. Kumbe njia salama ni kuukumbatia Msalaba Mtakatifu wa Bwana
wetu Yesu Kristo ambao ni ishara hai ya huruma na neema ya Mungu. Naye Mtume
Paulo anasema, “Lakini
mimi, hasha, nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu
Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa
ulimwengu,” Gal 6:14. Pamoja na Utukufu uliopo katika Msalaba Mtakatifu,
Msalaba utuvuta kwenye neema na huruma ya Mungu.
Mvuto huu leo wa
Msalaba wenye kutupeleka kwenye neema na huruma ya Mungu, Nabii Amosi
anauzungumzia kwa nyakati zile ambazo zilikuwa bado kufunuliwa kwao kwa maneno
haya; “Nami nitazigeuza sikukuu zenu kuwa maombolezo, na
nyimbo zenu zote kuwa vilio; nami nitatia nguo za magunia katika viuno vyote,
na upaa katika kila kichwa; nami nitayafanya haya kuwa kama maombolezo kwa
ajili ya mwana wa pekee, na mwisho wake kama siku ya uchungu,” Amo 8:10. Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari
hii, mwana huyu wa pekee anayezungumziwa hapa si mwingine bali ‘Neno
aliyefanyika mwili na kukaa kwetu,’ Yoh 1:14. Kwake neno huyu kuna huruma,
uelewa, na kujituma. Tufanyapo toba ya kweli na majuto kwake (Yesu Kristo) kuna
huruma ya kweli. Kristo Yesu ni mwelewa na anaelewa hali yetu na ubinadamu
wetu. Yesu kwa kumwilishwa kwake na kuchukua umbo la mwanadamu, aliishi kama
sisi ila “Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake,” 1Pet
2:22. Na mwisho, Kristo Yesu alijituma bila kujibakiza. Uthibitisho huu wa
kujituma kwake kwa sababu yako na mimi ni kuutoa uhai wake pale msalabani. Huu
ni upendo wa hali ya juu. Hakika, “hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa
mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,” Yoh 15:13. Na hivi ndivyo
tunavyotakiwa kupendana. Kujitoa kwa kutotanguliza kupokea. Ni kwa namna hii ya
kupendana tunakuwa rafiki ya Yesu, Yoh 15:14.
Upendo huu wa ajabu na
urafiki huu wa Yesu pale tunapopendana kwa dhati ndiyo ile kiu na njaa kwa
ujumbe ule wa Mungu kupita Nabii wake Amosi. “Angalia,
siku zinakuja, asema Bwana MUNGU, ambazo nitaleta njaa katika nchi; si njaa ya
kukosa chakula, wala kiu ya kukosa maji, bali ya kukosa kuyasikia maneno ya
Bwana,” Amo 8:11. Neno la Bwana ni uzima kama anavyothibitisha Yesu mwenyewe. “Ninyi
mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya lile neno nililowaambia. Kaeni ndani yangu, nami ndani
yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu; kadhalika
nanyi, msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo
huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote,” Yoh 15:3-5.
Ndugu yangu, bila Kristo Yesu hutoweza kufanya lolote lile, ‘liwe dogo au
kubwa!’ Na hivi ndivyo Mungu alivyoufunua ukweli huu wa ‘maisha bila NENO-Yesu Kristo,’ kupitia Nabii
wake Amosi; “Nao watatanga-tanga toka bahari hata bahari; na toka
upande wa kaskazi hata upande wa mashariki; watapiga mbio, wakienda huko na huko,
kulitafuta neno la Bwana, wasilione,” Amo 8:12. Ndugu yangu, ‘Kristo Yesu ndiye
Njia, Kweli, na Uzima,’ Yoh 14:6.
Wapendwa
wana wa Taifa ya Mungu, kwa mantiki hiyo, kila mmoja wetu kadiri ya wito na
hali yake, anapoishi hapa duniani yampasa kujua sababu ya kuumbwa kwake. Tunapojua
sababu ya kuumbwa kwetu ni kwa namna hiyo twafahamu kuwa maisha ya kila mmoja
wetu ni wito maalumu. Maisha kama wito, yanatudai kujitoa sadaka kwa kile
tulichochagua kuishi kwa kuwezeshwa na Mungu mwenyewe. Leo katika Injili
tunaona namna Mathayo alivyoitwa na Yesu na mara kuacha mpangilia wa maisha
yake ya zamani. Kuujua wito wako ni kuanza mpangilia mpya wa maisha yako. Na
ndivyo ilivyokuwa, “Yesu
alipokuwa akipita kutoka huko aliona mtu ameketi forodhani, aitwaye Mathayo,
akamwambia, Nifuate. Akaondoka, akamfuata,” Mt 9:9. Ukweli ni kwamba tendo hili
la kumfuata Yesu katika mazingira aliyokuwa nayo Mathayo, linamlazimu muhusika
kujimamanua kutoka yale aliyojifungamanisha nayo. Mathayo anaamua kuiacha kazi
yake ya ukarani na kumfuata Yesu ambaye hana chochote katika maisha linganishi
(mali na utajiri) ingawa vyote ni vyake, Zab 24:1, ila uzima wa milele. Yesu
anasema, “Mbweha wana pango, na ndege wa
angani wana viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake,” Lk
9:58. Kumfuata Yesu kwa ukaribu na uthabiti, kunatualika kuitafakari changamoto
hii.
Kitendo cha Yesu kumchagua Mathayo kuwa mmoja wa Mitume wake na kula
pamoja na wenye dhambi kinawakasirisha sana Mafarisayo. Yesu anawajibu
Mafarisayo kwa kulenga sababu ya uwepo wake hapa duniani: “Wenye
afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi,” Mt 9:12. Yesu amekuja kwa sababu
ya wale wenye uhitaji wa mwili na roho. Yesu amekuja kwa ajili ya wadhambi na
wale wote wenye moyo wa hofu ya Mungu. Hili ndilo fumbo tunalotakiwa
kulitafakari kila siku. Pili, kama nilivyokwisha kusema hapa mwanzo wa tafakari
hii, ‘ni Mungu peke yake wenye kutuhesabia haki.’ Hivyo, “Lakini
nendeni, mkajifunze maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka; kwa
maana sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi,” Mt 9:13. Ndugu yangu, embu
ona Yesu anavyokupenda kupita upeo. Kuuthaminisha upendo huu ni kuishi kadiri
ya mpango wa Mungu na yale yote Mwanaye Mpendwa aliyotufundisha.
Tumsifu Yesu Kristo!
Wenye
afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi,” Mt 9:12
Tusali:-Ee
Yesu ninakuhitaji daima. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario