domingo, 26 de junio de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 13 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 13 YA MWAKA-C
Somo: Amo 3:1-8; 4:11-12
Zab: 6:5-6, 7, 8
Injili: Mt 8:23-27
Nukuu:
Hakika Bwana MUNGU hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake,” Amo 3:7

Simba amekwisha kunguruma, ni nani asiyeogopa? Bwana MUNGU amenena, ni nani awezaye neno ila kutabiri?” Amo 3:8 

Baadhi yenu nimewaangamiza, kama hapo Mungu alipoiangamiza Sodoma na Gomora, nanyi mkawa kama kinga kilichonyakuliwa motoni; lakini hamkunirudia mimi, asema Bwana,” Amo 4:11 

Wanafunzi wake wakamwendea, wakamwamsha, wakisema, Bwana, tuokoe, tunaangamia,” Mt 8:25

Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga, enyi wa imani haba? Mara akaondoka, akazikemea pepo na bahari; kukawa shwari kuu,” Mt 8:26 

Wale watu wakamaka wakisema, Huyu ni mtu wa namna gani hata pepo na bahari zamtii?” Mt 8:27

TAFAKARI: “Kila jambo lina sababu yake. Simba amekwisha kunguruma, ni nani asiyeogopa? Bwana MUNGU amenena, ni nani awezaye neno ila kutabiri? Simama imara katika imani ya kweli.”

Wapendwa wana wa Mungu, ‘kila jambo lina sababu yake. Simba amekwisha kunguruma, ni nani asiyeogopa? Bwana MUNGU amenena, ni nani awezaye neno ila kutabiri? Simama imara katika imani ya kweli.’ Bila shaka katika maisha yako yapo mambo mengi mazuri na mengine yaliyojaa sintofahamu nyingi ambazo hadi sasa hujui sababu yake. Mambo haya yawe mema au mabaya kwetu kadiri ya mazingira na mitazamo yetu, jambo hilo au mambo hayo yana sababu yake. Hivyo chochote kile kitokeacho katika maisha yako au mazingira yako usikipuuze au kukipotezea hivi hivi. Mungu hutumia njia nyingi na tofauti kutufundisha, kufikisha ujumbe wake, na kuufunua Utukufu wake kwetu. Yale yote yanayotokea katika maisha yetu tuyajuayo na tusiyoyajua hubeba siri nzito ya Mungu kama mweza wa yote. Hakika Bwana MUNGU hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake,” Amo 3:7. Jambo lolote litokealo katika maisha yako usiwe mwepesi wa kulaumu, bali kuwa na mazungumzo rafiki na Mungu, na muulize kama rafiki yako hivi, ‘Ee Mungu, wataka kunifundisha nini katika hili lililonitokea?’

Hakika alifanyalo Mungu na lolote lile litokalo kwa Mungu lina sababu katika maisha yako. Katika mazingira kama hayo wahitaji imani thabiti katika ufahamu, na maana kwa kile ukihojicho kuelekea ufahamu halisi. Ndugu yangu, alifanyalo Mungu ni sawa na Simba aliyekwisha kunguruma, ni nani asiyeogopa? Bwana MUNGU amenena, ni nani awezaye neno ila kutabiri?” Amo 3:8. Jambo la muhimu katika mazingira kama haya ni kuona kile alichokufunulia Mungu kama kilivyo na siyo kama ulivyo kadiri ya historia yako, mazigira yako, tamaduni yako, na mitazamo yako. Lolote lile lenye kubeba Umungu ndani yake ni Tatakatifu. Hivyo yakupasa kabla ya kulisogelea uvivue viatu vyako kama alivyofanya Musa katika kijiti kile kilichokuwa kikiwaka moto. Malaika wa Bwana akamtokea, katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti, akamwita kutoka katikati ya kile kijiti, akasema, Musa! Musa! Akasema, Usikaribie hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi takatifu,” Kut 3:2b, 4b-c, 5.” Kuvua viatu ni kuvua ‘kinyago tafsiri cha uhalisia wa mambo kama ulivyo.’ Kila mtu ana kinyago chake, ‘mask’ kuona uhalisia wa kitu au mambo. Ni kama nilivyosema, yawezekana watumia uzoefu wako kuukabili ukweli ambao wakati mwingine hukudanganya. Watumia mila na desturi zenu kuutazama uhalisia ambao wakati mwingine hukudanganya.

Tunaposukumwa na kinyago hiki, ‘mask’ ni rahisi kuanguka kusiko kweli na halisi. Tunaporuhusu hali hii licha ya kupewa maangalizo mbalimbali, kifuatacho ni maanguko makubwa kwa sababu hakuna njia nyingine. Na hivyo ndivyo ilivyo kama asemavyo Mungu kwamba, Baadhi yenu nimewaangamiza, kama nilipoiangamiza Sodoma na Gomora, nanyi mkawa kama kinga kilichonyakuliwa motoni; lakini hamkunirudia mimi,” Amo 4:11. Mungu hupenda tuwe kama alivyotuumba, yaani, kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. 

Ni kwa namna hiyo, Injili ya leo inatutaka tuwe watu wa Imani ya kweli. Hatuwezi kumkiri Yesu kuwa ni njia, kweli na uzima, na wakati huo huo kukosa Imani naye. Imani hii thabiti ni kwa vipindi vyote; wakati wa mambo yakiwa shwari na wakati wa migogoro katika jamii. Leo swala la uzazi, familia, na mahusiano ni changamoto kubwa sana. Yatupasa kusimama katika kweli, na kulisema jambo hilo kwa Imani iliyo kweli. Haitoshi kupiga kelele tu kuwa tunaangamia, bali tunapopiga kelele tunaangamia tuwe tumesimama imara katika Imani.

Ni kweli yatupasa kumwendea Yesu muda wote, na hasa katika mikwamo iliyozidi akili na maarifa yetu. Mitume wanalifanya jambo hilo wanapoona chombo chao cha kusafiria kikiwa matatani. Wanafunzi wake wakamwendea, wakamwamsha, wakisema, Bwana, tuokoe, tunaangamia,” Mt 8:25. Kanisa kama chombo kielekeacho uzima wa milele, na sakramenti ya wokovu wetu kwa wabatizwa wote, mara zote hukaa kama familia na kupeleka maombi mbele ya Kristo ambaye Kanisa ni mwili wake. Tufanyapo jambo hilo kama mwili wa Kristo ulioingiliwa na udhaifu (dhambi), twapaswa kusimama katika Imani ya kweli. Yesu anatoa karipio kwa wanafunzi wake nasi pia katika nyakati zetu na kusema, “Mbona mmekuwa waoga, enyi wa imani haba? Mara akaondoka, akazikemea pepo na bahari; kukawa shwari kuu,” Mt 8:26. Je, ndugu yangu, una imani kweli kwa kile umwombacho Mungu? Au waenda kwake ukiwa na mashaka? TUZIOMBEE FAMILIA ZETU ILI ZIBAKI SALAMA!

Tumsifu Yesu Kristo!

Huyu ni mtu wa namna gani hata pepo na bahari zamtii?” Mt 8:27


Tusali:-Ee Yesu na Bwana wangu, niondolee mashaka juu yako pale napokumbana na sintofahamu katika maisha yangu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario