JUMANNE WIKI YA 13 YA MWAKA-C
Somo: Amo 3:1-8; 4:11-12
Zab: 6:5-6, 7, 8
Injili: Mt 8:23-27
Nukuu:
“Hakika
Bwana MUNGU hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii
siri yake,” Amo 3:7
“Simba amekwisha
kunguruma, ni nani asiyeogopa? Bwana MUNGU amenena, ni nani awezaye neno ila
kutabiri?” Amo 3:8
“Baadhi
yenu nimewaangamiza, kama hapo Mungu alipoiangamiza Sodoma na Gomora, nanyi
mkawa kama kinga kilichonyakuliwa motoni; lakini hamkunirudia mimi, asema
Bwana,” Amo 4:11
“Wanafunzi
wake wakamwendea, wakamwamsha, wakisema, Bwana, tuokoe, tunaangamia,” Mt 8:25
“Akawaambia,
Mbona mmekuwa waoga, enyi wa imani haba? Mara akaondoka, akazikemea pepo na
bahari; kukawa shwari kuu,” Mt 8:26
“Wale
watu wakamaka wakisema, Huyu ni mtu wa namna gani hata pepo na bahari zamtii?” Mt 8:27
TAFAKARI: “Kila jambo lina sababu yake. Simba
amekwisha kunguruma, ni nani asiyeogopa? Bwana MUNGU amenena, ni nani awezaye
neno ila kutabiri? Simama imara katika imani ya kweli.”
Wapendwa wana wa Mungu, ‘kila jambo lina sababu yake. Simba amekwisha kunguruma, ni nani asiyeogopa? Bwana MUNGU
amenena, ni nani awezaye neno ila kutabiri? Simama imara katika imani ya
kweli.’ Bila shaka katika maisha yako yapo mambo mengi mazuri na mengine
yaliyojaa sintofahamu nyingi ambazo hadi sasa hujui sababu yake. Mambo haya
yawe mema au mabaya kwetu kadiri ya mazingira na mitazamo yetu, jambo hilo au
mambo hayo yana sababu yake. Hivyo chochote kile kitokeacho katika maisha yako
au mazingira yako usikipuuze au kukipotezea hivi hivi. Mungu hutumia njia
nyingi na tofauti kutufundisha, kufikisha ujumbe wake, na kuufunua Utukufu wake
kwetu. Yale yote yanayotokea katika maisha yetu tuyajuayo na tusiyoyajua hubeba
siri nzito ya Mungu kama mweza wa yote. “Hakika Bwana MUNGU hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia
watumishi wake manabii siri yake,” Amo 3:7. Jambo lolote litokealo katika
maisha yako usiwe mwepesi wa kulaumu, bali kuwa na mazungumzo rafiki na Mungu,
na muulize kama rafiki yako hivi, ‘Ee Mungu, wataka kunifundisha nini katika
hili lililonitokea?’
Hakika
alifanyalo Mungu na lolote lile litokalo kwa Mungu lina sababu katika maisha
yako. Katika mazingira kama hayo wahitaji imani thabiti katika ufahamu, na
maana kwa kile ukihojicho kuelekea ufahamu halisi. Ndugu yangu, alifanyalo
Mungu ni sawa na “Simba aliyekwisha
kunguruma, ni nani asiyeogopa? Bwana MUNGU amenena, ni nani awezaye neno ila
kutabiri?” Amo 3:8. Jambo la muhimu katika
mazingira kama haya ni kuona kile alichokufunulia Mungu kama kilivyo na siyo
kama ulivyo kadiri ya historia yako, mazigira yako, tamaduni yako, na mitazamo
yako. Lolote lile lenye kubeba Umungu ndani yake ni Tatakatifu. Hivyo yakupasa
kabla ya kulisogelea uvivue viatu vyako kama alivyofanya Musa katika kijiti
kile kilichokuwa kikiwaka moto. “Malaika
wa Bwana akamtokea, katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti, akamwita kutoka katikati ya kile
kijiti, akasema, Musa! Musa! Akasema, Usikaribie
hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi
takatifu,” Kut 3:2b, 4b-c, 5.” Kuvua viatu ni
kuvua ‘kinyago tafsiri cha uhalisia wa mambo kama ulivyo.’ Kila mtu ana kinyago
chake, ‘mask’ kuona uhalisia wa kitu au mambo. Ni kama nilivyosema, yawezekana
watumia uzoefu wako kuukabili ukweli ambao wakati mwingine hukudanganya.
Watumia mila na desturi zenu kuutazama uhalisia ambao wakati mwingine
hukudanganya.
Tunaposukumwa na kinyago hiki, ‘mask’ ni
rahisi kuanguka kusiko kweli na halisi. Tunaporuhusu hali hii licha ya kupewa
maangalizo mbalimbali, kifuatacho ni maanguko makubwa kwa sababu hakuna njia
nyingine. Na hivyo ndivyo ilivyo kama asemavyo Mungu kwamba, “Baadhi yenu nimewaangamiza, kama nilipoiangamiza Sodoma na
Gomora, nanyi mkawa kama kinga kilichonyakuliwa motoni; lakini hamkunirudia
mimi,” Amo 4:11. Mungu hupenda tuwe kama alivyotuumba, yaani, kwa sura na mfano
wake, Mwa 1:27.
Ni kwa
namna hiyo, Injili ya leo inatutaka tuwe watu wa Imani ya kweli. Hatuwezi
kumkiri Yesu kuwa ni njia, kweli na uzima, na wakati huo huo kukosa Imani naye.
Imani hii thabiti ni kwa vipindi vyote; wakati wa mambo yakiwa shwari na wakati
wa migogoro katika jamii. Leo swala la uzazi, familia, na mahusiano ni
changamoto kubwa sana. Yatupasa kusimama katika kweli, na kulisema jambo hilo
kwa Imani iliyo kweli. Haitoshi kupiga kelele tu kuwa tunaangamia, bali
tunapopiga kelele tunaangamia tuwe tumesimama imara katika Imani.
Ni
kweli yatupasa kumwendea Yesu muda wote, na hasa katika mikwamo iliyozidi akili
na maarifa yetu. Mitume wanalifanya jambo hilo wanapoona chombo chao cha
kusafiria kikiwa matatani. “Wanafunzi
wake wakamwendea, wakamwamsha, wakisema, Bwana, tuokoe, tunaangamia,” Mt 8:25.
Kanisa kama chombo kielekeacho uzima wa milele, na sakramenti ya wokovu wetu
kwa wabatizwa wote, mara zote hukaa kama familia na kupeleka maombi mbele ya
Kristo ambaye Kanisa ni mwili wake. Tufanyapo jambo hilo kama mwili wa Kristo
ulioingiliwa na udhaifu (dhambi), twapaswa kusimama katika Imani ya kweli. Yesu
anatoa karipio kwa wanafunzi wake nasi pia katika nyakati zetu na kusema, “Mbona
mmekuwa waoga, enyi wa imani haba? Mara akaondoka, akazikemea pepo na bahari;
kukawa shwari kuu,” Mt 8:26. Je, ndugu yangu,
una imani kweli kwa kile umwombacho Mungu? Au waenda kwake ukiwa na mashaka?
TUZIOMBEE FAMILIA ZETU ILI ZIBAKI SALAMA!
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Huyu
ni mtu wa namna gani hata pepo na bahari zamtii?” Mt 8:27
Tusali:-Ee Yesu na Bwana wangu, niondolee
mashaka juu yako pale napokumbana na sintofahamu katika maisha yangu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario