JUMATANO WIKI YA 10 YA MWAKA-C
Somo: 1Fal 18:20-39
Zab: 16:1-2a, 4, 5, 8, 11
Injili: Mt 5:17-19
Nukuu:
“Msidhani
ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali
kutimiliza,” Mt 5:17
“Kwa
maana, amin, nawaambia, Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala
nukta moja ya torati haitaoondoka, hata yote yatimie,” Mt 5:18
“Naye Eliya akawakaribia watu wote, akanena, Mtasita-sita
katikati ya mawazo mawili hata lini? Bwana akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali
ikiwa Baali ni Mungu, haya! Mfuateni yeye. Wale watu hawakumjibu neno,” 1Fal
18:21
“Unisikie, Ee Bwana, unisikie, ili watu hawa wajue ya kuwa
wewe, Bwana, ndiwe Mungu, na ya kuwa wewe umewageuza moyo wakurudie,” 1Fal
18:37
TAFAKARI: “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la,
sikuja kutangua, bali kutimiliza.”
Wapendwa wana wa Mungu,
Sheria ya Bwana ni utaratibu wa kuyaishi yale yampendezayo Mungu, na kuwa na
mahusiano mazuri naye kwani Yeye ndiye uhai na uzima wetu. Wana wa Israeli
walipewa sheria kama mwongozo wa kutenda na kuwa na mahusiano mazuri na Mungu.
“Bwana akamwambia Musa, Njoo huku juu kwangu mlimani, uwe huku; nami nitakupa
mbao za mawe na ile sheria na hiyo amri niliyoiandika ili uwafundishe,” Kut
24:12. Sheria hizi zilipaswa kufuatwa kiaminifu na bila kuzichakachua. “Mioyo
yenu na iwe kamili kwa Bwana, Mungu wetu, kuenenda katika sheria zake, na
kuzishika amri zake, kama ilivyo leo.” 1Fal 8:61.
Ukamilifu na uaminifu
wa mtu ulipatikana katika kuzishika sheria za Bwana. Kwa sababu, “sheria ya
Bwana ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa Bwana ni amini, Humtia
mjinga hekima.” Zab 19:7. Hivi ndivyo ilivyopaswa kuzishika sheria za Bwana. Na
hilo ndilo lililokuwa kusudi la sheria. Jambo la kushangaza wakati wa Yesu,
Wayahudi hawakuwa wanafuata Torati kama iliyokuwa mwanzo, yaani, nyakati za
Musa. Wayahudi walikuwa wanafuata tafsiri ya Torati ambayo iliendana na
matamanio yao na siyo ya Mungu. Huu ndio ugomvi uliokuwepo kati ya Yesu na
Waandishi na Mafarisayo.
Matamanio haya ya
Mafarisayo na Waandishi katika ubinadamu wao ambayo yalienda kinyume na tamanio
la Mungu juu ya sheria nyakati zile za
Yesu, ndiyo hayo yaliyojitokeza pia nyakati zile za Nabii Eliya na wale wafuasi
wa miungu ya Baali. Kuwarudisha kwenye mstari wa kweli na haki, ikiwa ni
kumfuata na Mungu wa kweli na wakuabudiwa, Nabii Eliya anawaasi na kusema, “Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini?
Bwana akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! Mfuateni
yeye. Wale watu hawakumjibu neno,” 1Fal 18:21.
Kwa
kuwafundisha ni Mungu yupi aliye hai na anayepaswa kuabudiwa, Nabii Eliya
anatoa ushauri wa kumtolea Mungu huyo sadaka ya kuteketezwa kama ishara iliyo
hai. Kadiri ya somo letu la leo tumesikia jinsi wafuasi wale 450 wa miungu ya
Baali walivyotoa sadaka yao, na kuliita jina hilo la Baali bila mafanikio licha
ya kujichanja na kutokwa damu. Na ndipo Eliya alipomjeukia Mungu wake aliye hai
na kufanya ishara zilizobeba kumbukumbu
ya safari ya ukombozi ya wana wa Israeli. “Eliya
akatwaa mawe kumi na mawili, kwa hesabu ya kabila za wana wa Yakobo,
aliyejiliwa na neno la Bwana na kuambiwa, Jina lako litakuwa Israeli. Naye akaijenga madhabahu kwa mawe hayo
katika jina la Bwana; akafanya mfereji, kama wa vipimo viwili vya mbegu,
ukiizunguka madhabahu,” 1Fal 18:31-32. Eliya anatambua kuwa Mungu
aliyewafikisha hapo walipo hawezi kamwe kuwakana kwa sababu wanamwamini na wana
matumaini makubwa juu yake.
Baada
ya watesi wake Nabii Eliya kushindwa na kuikubali aibu yao na mungu wao wa
uongo, na “ikawa, wakati wa kutoa dhabihu
ya jioni, Eliya nabii akakaribia, akasema, Ee Bwana, Mungu wa Ibrahimu, na wa
Isaka, na wa Israeli, na ijulikane leo ya kuwa wewe ndiwe Mungu katika Israeli,
na ya kuwa mimi ni mtumishi wako, na ya kuwa nimefanya mambo haya yote kwa neno
lako,” 1Fal 18:36. Kwa jambo hili ambalo Nabii Eliya anataka kulifanya siyo kwa
kujiinua yeye mwenyewe wala kujitukuza, bali huyu Mungu wa Ibrahimu, na wa
Isaka, na wa Israeli ajulikane na kuabudiwa milele. Eliya anafahamu nafasi yake
katika jambo hili, yaani, yeye ni mpelekwa tu wa kuwapa watu ujumbe ule maalumu
wa Mungu. Na kwa namna hiyo, Eliya anajikabidhi
hivi mbele ya Mungu na kusema, “Unisikie,
Ee Bwana, unisikie, ili watu hawa wajue ya kuwa wewe, Bwana, ndiwe Mungu, na ya
kuwa wewe umewageuza moyo wakurudie,” 1Fal 18:37. Eliya hatangulizi maslahi
yake mbele wala kujulikana kwa lolote lile.
Maandalizi yalipo
kamilika, na kuwahakikishia watu wote kuwa Mungu amuombaye ni mwaminifu na
mwenye nguvu kwa kuimwagia sadaka ile ya kuteketezwa maji mapipa manne mara
tatu, “Ndipo moto wa Bwana ukashuka, ukaiteketeza sadaka ya
kuteketezwa, na kuni, na mawe, na mavumbi, ukayaramba yale maji yaliyokuwamo
katika mfereji,” 1Fal 18:38. Huyu ndiye Mungu aliye hai na anayepaswa
kuabudiwa. “Na
watu wote walipoona, wakaanguka kifudifudi; wakasema, Bwana ndiye Mungu, Bwana
ndiye Mungu,” 1Fal 18:39. Ndugu yangu tunayesafiri
sote katika tafakari hii, kwa hiki kilichotokea, Wayahudi hawakupaswa
kukengeuka katika imani yao. Ila kadiri tusomapo historia ya Taifa hili la
Israeli na kutafakari, tunaona mambo hayakuwa kama yalivyopaswa kuwa.
Hali ya uvuguvugu wa imani ya kweli ilikuwa hivyo hata nyakati za Yesu hata
pamoja na kupewa torati kama mwongozo wa kufuata na kuwa karibu na mapenzi ya
Mungu.
Jambo muhimu sana la
kujua ni kwamba kipindi cha Yesu, Wayahudi na hasa mafarisayo na waandishi
hawakuwa wanaifuata Torati kama iliyokuwa, ila tafsiri yake (maisha ya dini na
matendo yake kupitia masimulizi), iliyojulikana kwa ujumla kama TALMUD. Talmud
ilibeba mambo mawili: MIDRASH (tafsiri ya mambo mbalimbali toka Torati), na
MISHNAH (marudio/waliyorudia au mafundisho)
Kwa mantiki hiyo hapo
juu ya TALMUD, vitabu vile vitano vya Torati vingewezwa kuandikwa kwa kurasa
350 tu; wakati TALMUD ilichukuwa hadi vitabu 523; vilivyo rudufiwa (printed)
katika mabando (volumes) 22. Haya ndiyo yanayonukuliwa na mafarisayo na
waandishi kama mapokeo ya wazee. Sehemu nyingi za mafundisho ya Yesu anapinga
jambo hili la kufuata mapokeo ambayo ni tafsiri kutoka Torati, (Mt 15:2-3, 6;
Mk 7:3, 5, 8, 9, 13). Naye Yesu anawaambia, “Ninyi
mwaiacha amri ya Mungu, na kuyashika mapokeo ya wanadamu,” Mk 7:8. Mapokea haya
ni ukweli wa Mungu uliopotoshwa. Mtume Paulo baada ya kuongoka na kuujua
ukweli kuhusu sheria ya Bwana anawaambia Wakolosai, “Angalieni
mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya
mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu, wala si kwa
jinsi ya Kristo,” Kol 2:8. Ukweli ni kwamba, Mtume Paulo kama Mfarisayo kabla
ya kuongoka kwake aliyafuata mapokeo haya ya wazee ambayo yalikuwa ni ‘ukweli
wa Mungu uliopotoshwa.’ Paulo anakiri jambo hili na kusema, “Nami
naliendelea katika dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika
kabila yangu, nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu,” Gal
1:14.
Kwenye jambo hili,
yaani kweli ya Sheria ya Bwana, Yesu anawakemea Mafarisayo na Waandishi na
kusema, “Msidhani ya kuwa nilikuja kuitangua Torati au Manabii; la, sikuja
kutangua, bali kutimiza,” Mt 5:17. Hapa Yesu akubaliani nao kwa swala la
kuichakachua Torati kama walivyokwisha kufanya. Yesu anarudisha mpango mzima wa
Mungu katika safari nzima ya ukombozi wa mwanadamu. Yesu anatoa zaidi maana ya
sheria na ushikaji wa sheria hiyo. Yesu anawakosoa Mafarisayo kwa unafiki wao
katika sheria na kusema, “Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa
mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria,
yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine
msiyaache,” Mt 23:23
Utimilifu wa sheria
kadiri ya mpango mzima na mtazamo wa Yesu umebebwa katika upendo. Hii ndiyo
amri mpya. “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi
mpendane vivyo hivyo,” Yoh 13:34. Mtakatifu Agustino anatuambia kwamba,
“ukipenda utafanya yote.” Ni katika mantiki hii kwamba, “mkipenda, mtazishika
amri zangu,” Yoh 14:15. Je, leo hatushangai kuona baadhi ya viongozi
wakiichakachua Katiba ya nchi zao kwa ajili ya matamanio yao na uchu wao wa
madaraka? Jambo hili limekuwa chanzo kikubwa cha machafuko mengi duniani na
hasa kwenye bara letu la Afrika. Ni ukweli usiopingika kwamba, vikundi vingi
vya kigaidi vimejitokeza pale sauti ya wengi katika mkondo sahihi, yaani,
demokrasia ilipoganyagwa, kubezwa, na hata kubakwa kwa manufaa wa watu wachache
tu katika kundi zima la walio wengi. Ni vyema tukasoma alama za nyakati.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Mtasita-sita
katikati ya mawazo mawili hata lini? Bwana akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali
ikiwa Baali ni Mungu, haya! Mfuateni yeye. Wale watu hawakumjibu neno,” 1Fal
18:21
Tusali:-Ee Mungu
Mwenyezi, na Baba yetu upasaye kuabudiwa, waongoze viongozi wetu waliopewa
dhamana na umma, mara zote wayaone maslahi mapana ya watu wao, na siyo ubinafsi
wao. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario