miércoles, 8 de junio de 2016

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 10 YA MWAKA-C

IJUMAA WIKI YA 10 YA MWAKA-C
Somo: 1Fal 19:9a, 11-16
Zab: 27:7.8a, 8b-9abc, 13-14
Injili: Mt 5:27-32
Nukuu:
 “Na tazama, Bwana akapita; upepo mwingi wa nguvu ukaipasua milima, ukaivunja-vunja miamba mbele za Bwana; lakini Bwana hakuwamo katika upepo ule,” 1Fal 19:11b

“na baada ya upepo, tetemeko la nchi; lakini Bwana hakuwamo katika lile tetemeko la nchi,” 1Fal 19:11c 

na baada ya tetemeko la nchi kukawa na moto; lakini Bwana hakuwamo katika moto ule; na baada ya moto sauti ndogo, ya utulivu,” 1Fal 19:12 

Ikawa, Eliya alipoisikia, alijifunika uso wake katika mavazi yake, akatoka, akasimama mlangoni mwa pango. Na tazama, sauti ikamjia, kusema, Unafanya nini hapa, Eliya?” 1Fal 19:13

 “Imenenwa pia, Mtu akimwacha mkewe, na ampe hati ya talaka; lakini mimi nawaambia, Kila mtu amwachaye mkewe, isipokuwa kwa habari ya uasherati, amfanya kuwa mzinzi; na mtu akimwoa yule aliyeachwa, azini,” Mt 5:31-32 

TAFAKARI:Toka, usimame mlimani mbele za Bwana.”

Wapendwa wana wa Mungu, ‘kutoka na kusimama mlimani mbele za Bwana’ ni uthibitisho wa maisha bila hatia, na kielelezo cha kuisimamia hukumu ya Bwana iliyo haki na kweli. Mlima kama kitu kilicho juu, chochote kilicho juu yake uonekana vizuri kwa wale walio chini yake. Hivyo hiki kilicho juu ili kionekane na wote chapaswa kuonekana bila kuzongwa na uvuli, yaani kitabia kisiwe na hatia. Ni kusimama katika kweli bila kuwa na ‘dhania’-“bias” katika hukumu ya haki na kweli. Hali na tabia hii humpa mtu ‘nguvu ya maadili’ katika kusema, kuonya, na hata kuamrisha pale mambo yanapokwenda ndivyo sivyo. Hali na nguvu hii ya kimaadili haijalishi maumbile ya mtu katika udogo wake, au ukubwa wake.

Kwa kuwa Bwana alipendezwa na Nabii Eliya, anamkubusha nguvu aliyonayo na aache woga katika kutenda kwake hata kama mazingira yanayomzunguka yamejawa hofu, 1Fal 19:11a, 14. Katika mazingira kama hayo yatupasa kwenda kwa utulivu wa ndani, na siyo kukurupuka. Mungu kamwe hapatikani katika ghasia au machafuko yanayotuzunguka. Hivyo ni wito kwetu kuwa na busara na utulivu wa ndani ‘palipo machafuko na sintofahamu’ kuona uhalisia wa mambo, na kutoa suluhu lenye heri. Hapa ndipo tunapoona busara ya kiongozi anavyokabiliana na sintofahamu katika maisha ya wale anaowaongoza. Lengo siyo wepesi wa kutoa majibu ‘mepesi kwa maswali magumu’ bila kufikiri kwa kina, bali kuwa na uelewa mpana wa kile kisichojulikana vizuri kwako na kwa wengi. Na usemapo iwe mara moja na kueleweka kwa wote.

Kwa upande wetu binadamu kuelewa mafumbo mazito kama haya twaitaji utulivu wa ndani. Ni katika utulivu Mungu hujidhihirisha. Mfano, Mungu anajidhihirisha kwa Nabii Isaya kwa namna hii: Na tazama, Bwana akapita; upepo mwingi wa nguvu ukaipasua milima, ukaivunja-vunja miamba mbele za Bwana; lakini Bwana hakuwamo katika upepo ule; na baada ya upepo, tetemeko la nchi; lakini Bwana hakuwamo katika lile tetemeko la nchi; na baada ya tetemeko la nchi kukawa na moto; lakini Bwana hakuwamo katika moto ule; na baada ya moto sauti ndogo, ya utulivu,” 1Fal 19:11-12. Tunapopatwa na jambo la kutuhuzunisha au tusilolifahamu, moyo wetu hupitia hatua mbalimbali kama upepo wa nguvu, tetemeko la nchi, na moto. Katika hali hizi zote za uchungu na hasira Mungu hawezi kamwe kujidhihirisha ndani yetu. Hivyo katika hali kama hiyo yakupasa kutulia na kutokufanya chochote zaidi ya kutafakari hali ile. Kwa maana nyingine usifanye maamuzi yoyote ukiwa katika hali ya hasira. Mwisho wa hasira yako, maamuzi uliyoyafanya yatakugharimu maisha yako, na hali yako. Mtu yeyote yule mwenye kutoa maamuzi katika hali isiyo ya utulivu, madhara yake ni makubwa sana, na mbaya zaidi akiwa yeye ndiye kiongozi au mzazi. Ni wanyenyekevu tu uweza kurudi nyuma na kusawazisha mambo kwa kukiri kudondoka kwao na kuomba msamaha kwa maamuzi yao mabaya na yasiyokuwa na tija. Mwenye kiburu uzidi kujitetea na kuhalalisha alichokifanya, na hapo ndipo huaribu kabisa.

Wapendwa wana wa Mungu, hapa ndipo tunapoweza kuona udogo wa kitu unavyokuwa na kufikia ukubwa wake ambao unatuwia vigumu kujinasua. Huu ndio mtazamo wa dhambi kadiri ya Injili ya leo. Kumbe kadiri ya Injili ya leo dhambi haihesabiki tu kwa kufanya tendo halisi, bali hata kwa kuwaza na kuvutwa kwa hisia ya kufanya dhambi hiyo. Mizania ya dhambi ipo sawa kwa kufanya au kutokufanya ili hali tu tamaa ile ya kufanya jambo hilo ipo ndani yako. Kilichokosekana hapo ni mazingira halisi ya kulitenda jambo hilo, ila uzito wa dhambi ni ule ule. Tafsiri hii ya dhambi inatupeleka mbali zaidi na kututoa katika mtazamo wa kizamani wa kusema kuna dhambi ndogo na kubwa. Yesu anatupa angalizo katika jambo hili: Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini; lakini mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake,” Mt 5:27-28. Je, si yale yamtokayo mtu moyoni mwake ndiyo yamtiayo unajisi? Je, si ndani ya moyo wa mtu ndipo kwenye vyanzo vya yale yote yamjazayo mtu na kumfanya kile alicho? Pasipo utulivu wa ndani viongoza matamanio yako ya nje (jicho, au mkono, Mt 5:29-30) hukosa mwelekeo. Nuru ile ya ndani inapofifishwa yote ya nje huenda mrama.

Wapendwa wana wa Mungu, “Hamjafahamu bado ya kuwa kila kiingiacho kinywani hupita tumboni, kikatupwa chooni? Bali vitokavyo kinywani vyatoka moyoni; navyo ndivyo vimtiavyo mtu unajisi,” Mt 15:17-18. Utulivu wa ndani ndiyo taswira halisi ya mtu.

Tumsifu Yesu Kristo!

lakini mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake,” Mt 5:28


Tusali: Ee Yesu Mwema, tujalie utulivu wa ndani katika kuona, kuamua na kutenda. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario