martes, 14 de junio de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 11 YA MWAKA-C

JUMATANO WIKI YA 11 YA MWAKA-C
Somo: 2Fal 2:1, 6-14
Zab: 31:20, 21, 24
Injili: Mt 6:1-6, 16-18
Nukuu:
 “Hata ikawa, walipokwisha kuvuka, Eliya akamwambia Elisha, Omba kwangu lo lote utakalo nikutendee, kabla sijaondolewa kwako. Elisha akasema, Nakuomba, sehemu maradufu ya roho yako na iwe juu yangu,” 2Fal 2:9 

Akalitwaa lile vazi la Eliya lililomwangukia, akayapiga maji, akasema, Yuko wapi Bwana, Mungu wa Eliya? Naye alipoyapiga maji, yakagawanyika huku na huku, Elisha akavuka,” 2Fal 2:14

Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 6:1

 “Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso; ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi,” Mt 6:17-18

TAFAKARI: “Baba yako aonaye sirini atakujazi.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo natulitafakari neno hili “Baba yako aonaye sirini atakujazi.” Hatuna sababu ya kuwa na hofu tunapojisalimisha kwa Mungu bila kujibakiza, na hasa pale tunapofunga kwa ajili ya kujitakatifuza, na tunapoomba kwa ajili yetu na wengine. Hatuna chochote cha kumficha Mungu, wala kujinyambulisha na kuwa kile tusicho. Mungu anatujua vizuri kuliko tujijuavyo kwa sababu Yeye ndiye aliyetuumba, tena kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Naye Mungu, yaani, Neno aliyemwilishwa na kukaa kwetu, Yoh 1:14, anatuambia, Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi, bora ninyi kuliko mashomoro wengi,” Lk 12:7. Hakiti tu kito chenye samani mbele ya Mungu licha ya udogo wetu. Hivyo ni vyema tukaacha maigizo katika maisha.

Somo letu la leo linaelezea “maisha ya ukaribu.” Na kama ilivyo hada, linatupa ukaribu wa Eliya na Elisha kama ilivyokuwa ukaribu Yesu Kristo na wanafunzi wake. Nabii Eliya yupo wazi kwa Elisha, na kabla ya kuondoka kwake anamtaka Elisha aombe chochote naye atatenda. Hata ikawa, walipokwisha kuvuka, Eliya akamwambia Elisha, Omba kwangu lo lote utakalo nikutendee, kabla sijaondolewa kwako. Elisha akasema, Nakuomba, sehemu maradufu ya roho yako na iwe juu yangu,” 2Fal 2:9. Kwa upande wa Yesu, sharti la kupata kile tuombacho yatupasa kukaa ndani ya Kristo, na kuachana na  michanganyo katika imani. Naye Yesu anasema, Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa,” Yoh 15:7. Yesu anaenda mbali zaidi na kusema, kama imani tunayao bila  michanganyo tuombalo hata sasa tutalipata, Hata sasa hamkuomba neno kwa jina langu; ombeni, nanyi mtapata; furaha yenu iwe timilifu,” Yoh 16:24. Furaha ya kweli katika maisha na hasa ya kiroho hukamilishwa na Kristo mwenyewe.

Uwezo wa mwanadamu wa kujenga mawazo (taswira) ya kufikirika ni moja ya njia azitumiazo mwanadamu kugundua vitu na hata kuviboresha vile vinavyomzunguka. Lakini ubaya wa mawazo fikirika ni pale mwegemeo wake unapoelekea kwenye ubinafsi wa mtu husika. Hii ni hatari kwa sababu uwezekano huo waweza kuwa hatari kwa mtu binafsi na hata watu na mazingira yanayomzunguka. Jibu la Nabii Eliya kwa kile alichokiomba Elisha kwamba “umeomba neno gumu,” 2Fal 2:10, linaonyesha mwegemeo huo wa ubinafsi. Jibu hili halina tofauti na jibu la Yesu kwa kile walichokiomba (mmoja wao aketi upande wa kuume wa Yesu na mwingine upande wa kushoto) wana wa Zebedayo, “Hamjui mnaloliomba. Mwaweza kunywea kikombe ninyweacho mimi, au kubatizwa ubatizo nibatizwao mimi?Mk 10:38. Hata baada ya kujidhihirisha kwamba wapo tayari kubatizwa ubatizo huo, Mt 10:39, bado Yesu anawataka wafikiri vizuri zaidi kwa sababu hicho wakiombacho kinavigezo vyake. Naye Yesu anawaambia, lakini habari ya kuketi mkono wangu wa kuume au mkono wangu wa kushoto si langu kuwapa, ila wao watapewa waliowekewa tayari,” Mk 10:40

Kuondoka kwa Nabii Eliya kulikuwa kwa namna ya pekee sana. Nabii Eliya nachukuliwa na gala la moto, na farasi wa moto. Na  walipokuwa wakiendelea mbele na kuongea, tazama! Kukatokea gari la moto, na farasi wa moto, likawatenga wale wawili; naye Eliya akapanda mbinguni kwa upepo wa kisulisuli,” 2Fal 2:11. Moto ni ishara ya uwepo wa Mungu na Utakatifu wake. “Pumzi zake huwasha makaa, Na miali ya moto hutoka kinywani mwake,” Ayu 41:21. Moto licha ya kuwa ishara na uwepo wa Mungu, ni ishara ya kutakatifuzwa, kufundishwa na hata onyo kutoka kwa Mungu. Na hili ndilo neno la faraja kutoka kwa Mungu kupitia Nabii Isaya, “na mkono wa Bwana utajulikana, uwaelekeao watumishi wake, naye atawaonea adui zake ghadhabu. Maana Bwana atakuja na moto, na magari yake ya vita kama upepo wa kisulisuli; ili atoe malipo ya ghadhabu yake kwa moto uwakao, na maonyo yake kwa miali ya moto,” Isa 66:14b-15

 Namna hii ya kuondoka Nabii Eliya kunafanana na kupaa kwake Bwana wetu Yesu Kristo Mbinguni ingawa Yeye haikuwa kwa gari na farasi wa moto. Hata hivyo kitu cha kutazama hapa ni ujumbe ule ulioachwa na namna ulivyopokelewa na wale walioachiwa ujumbe husika. Kwa upande wa Elisha ilikuwa hivi; Naye Elisha akaona, akalia, Baba yangu, baba yangu, gari la Israeli na wapanda farasi wake! Asimwone tena kabisa; akashika mavazi yake mwenyewe, akayararua vipande viwili,” 2Fal 2:12. Kuondoka kwa Eliya ni huzuni kubwa kwa Elisha. Ni hali na ujumbe wa huzuni. Yesu alivyopaa alituhaidi kutupatia Roho Mtakatifu, na kutotuacha mayatima kwani atatujia, Yoh 14:18. Na zaidi ya hilo, alituachia kazi ya kufanya, yaani, kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi wake kwa kuwahubiria habari njema na kuwabatiza, Mt 28:19-20.

Kanisa linaachiwa kazi ya kufanya hadi mwisho wa nyakati. Huu ndio uwezo uliopewa Kanisa, yaani, kwa kila  aliyebatizwa na mwenye kuziishi ahadi zake za ubatizo vyema. Hili ni sawa na vazi lile la Eliya lililomwangukia Elisha, na kumwezesha kufanya aliyofanya mtanzulizi wake. Elisha Akalitwaa lile vazi la Eliya lililomwangukia, akayapiga maji, akasema, Yuko wapi Bwana, Mungu wa Eliya? Naye alipoyapiga maji, yakagawanyika huku na huku, Elisha akavuka,” 2Fal 2:14. Vazi na ishara aliyoifanya Elisha ina  mfanano wa fimbo ya Musa aliyopewa na Mungu kwa kuzifanya ishara. Naye Mungu ananena juu ya fimbo ile, Nawe utatwaa fimbo hii mkononi mwako, na kwa hiyo utazifanya zile ishara,” Kut 4:17, ikiwa ni  pamoja na kuyagawa maji ya baharí, watapita kati ya bahari katika nchi kavu,14:16. Ndugu yangu, uwezo aliokupa Mungu yaani karama na vipaji ulivyonavyo ndiyo ni sawa na fipo ile ya Musa na vazi hili la Eliya ambao sasa ameachiwa Elisha. Leo kama wewe ni mzazi unayejali na kuwajibika, urithi mkubwa kwa mwanao ni elimu. Mpe mwanao ufahamu huo kwa sababu, "Mwelimishe mwenye hekima, naye atazidi kuwa na hekima; Mfundishe mwenye haki, naye atazidi kuwa na elimu,” Mit 9:9. Hata pamoja na elimu hiyo kuwa muhimu, usisahu pia kumjengea mwanao hofu ya Mungu kwa sababu, “Kumcha Bwana ni mwanzo wa hekima; Na kumjua Mtakatifu ni ufahamu,” Mit 9:10
Njili yetu leo inatupa kinagaubaga namna ya kufanya na inavyompendeza Mungu. Na hii ndiyo maana halisi ya kumacha Bwana na kumjua, Mit 9:10. Leo tulio wengi tunapowasaidia wahitaji na hasa; wazee, mayatima na wajane, tunatenda tendo hili kwanza kwa kuwakusanya watu ili waone tunachokitoa. Pili, tuna viita vyombo vya habari ili wautangazie ulimwengu jinsi tunavyotoa na tulivyo wema. Tufanyapo tendo hili kwa mfumo na mtazamo huu twajisikia raha nafsini mwetu, na kujipongeza kwa kufanya kazi nzuri ya kijamii na hata kichunguji. Je, kuwa Baba au Mama mwema na mkarimu na karibu kwa familia yako unaitaji kuvaa au kubeba bango lenye maandishi kama haya; “Baba mwema na mkarimu,” ili familia ijue ukweli huo? Nafikiri hapa kwa kiasi kikubwa tunakosea sana tunavyofanya hivyo. Yesu anatoa onyo na angalizo kwa kusema, Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 6:1. Tendo kama hili halina dhawabu yo yote machoni mwa Mungu.

Ni kweli watu watatusifia na kutuandika kwenye magazetu yao, ambayo kesho yake magazeti hayo hayo yaliyopambwa jana kwa utoaji wetu yatafungia vitumbua na historia yote inaishia hapo. Je, imani na matumaini yako ipo kwa watu? Bwana asema hivi, “Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake Na moyoni mwake amemwacha Bwana,” Yer 17:5. Bali, Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea Bwana, Ambaye Bwana ni tumaini lake. Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, Uenezao mizizi yake karibu na mto; Hautaona hofu wakati wa hari ujapo, Bali jani lake litakuwa bichi; Wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, Wala hautaacha kuzaa matunda,” Yer 17:7-8. Tunapowategemea wanadamu hasa kwa matendo yetu ili yawapendezeshe hatuna tofauti na Mafarisayo nyakati zile za Yesu.

Leo Yesu anatupeleza mbali zaidi na hasa matendo yale tuyafanyayo ilikwa ni kumrudishia Mungu sifa na shukrani, hatupaswi kuyafanya kama maonyesho mbele za watu ili watuone. Jamii yetu leo kwa kiasi kikubwa imetawaliwa na maigizo na habar iza kufikirika tu kila kukicha. Yesu anatutaka leo tuyaone matendo yetu ya huruma tuyafanyayo kwa watu ni sehemu ya sadaka, sala, na kufunga. Anayetukirimia neema na baraka katika matendo hayo ya kiroho ni Mungu mwenyewe. Hakuna maana yo yote ya kuomba huruma kwa watu mara tuyafanyapo mambo haya. “Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; sadaka yako iwe kwa siri; na Baba yako aonaye sirini atakujazi,” Mt 6:3b-4. Ni kweli utoapo kwa siri, ndivyo hivyo Baba yako aonaye sirini atakujazi. Ila tusimwibie Mungu au kumdanganya Mungu kwa kumpa kile kisicho halali. Mfano mdogo ni huu; ukiangalia shilingi hamsini hadi mia mbili huwezi kukuta maneno haya, “Fedha halali kwa malipo ya shilingi, mia tano, elfu moja au elfu kumi,” ambayo yapo pia kwenye noti ya shilingi elfu mbili, na elfu tano. Je, unapotoa sadaka yako jumapili shilingi hamsini, mia moja, au mia mbili, unatoa fedha halali ukilinganisha kwa kipato chako cha mwezi? Kama kuna uwiyano hautakuwa umetenda kosa, na hautakuwa umejifungia baraka na neema za Mungu. Kama unacho kingi na unasema kwa matendo yako unacho kidogo, Mungu atakipunguza kadiri ya matendo yako. “Wakamkasirisha kwa matendo yao; tauni ikawashambulia,” Zab 106:29. Mungu aweza kukufanya chochote kadiri ya uchoyo wako.

Na tusalipo yatupasa kuunganika na Mungu katika undani wetu na siyo kupayukapayuka ili watu wajue tunasali. Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi,” Mt 6:6. Hatumpendezeshi yeyote tunaposali, bali Mungu ambaye ni yote katika yote, na tunauonja ukaribu wetu na Mungu, kwa njia ya kumshukuru, kumtukuza, kumwomba na kumsifu.

Na mwisho tunapofanya tendo la kufunga kuwe na malengo. Licha ya kuwa ni tendo la kiroho, kufungu ni tendo la kiafya pia. Je, ninavyojinyima nafanya hivyo kwa sababu gani hasa? Na kwa kufunga kwangu kumelenga maisha yangu ya kiroho? Je, ninalenga hasa utakaso ndani mwangu, au nalifanya tendo hilo kwa vile imekuwa mazoe kila kipindi fulani cha mwaka watu hufanya hivyo nami nafanya? Pili, tendo hilo mwisho wa siku linawalenga watu gani kama shukrani kwa Mungu? Haya ni maswali muhimu sana ya kujiuliza kabla ya kufanya zoezi hili la kiroho, mfungo. Maswali hayo yakipata majibu yake fanya hivi, wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso; ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi,” Mt 6:17-18. Kujipaka mafuta ni kutokuwavuta watu kujua unachokifanya kwa sababu tendo hili ni la kiroho zaidi.

Tumsifu Yesu Kristo!

Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso; ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi,” Mt 6:17-18


Tusali:-Ee Yesu, ujuaye undani wetu, tuongoze katika kweli na haki ili tuwe kweli tunda la upendo wako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario