lunes, 13 de junio de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 11 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 11 YA MWAKA-C
Somo: 1Fal 21:17-29
Zab: 51:3-4, 5-6a, 11, 16
Injili: Mt 5:43-48
Nukuu:
Neno la Bwana likamjia Eliya Mtishbi, kusema, Ondoka, ushuke, ukutane na Ahabu mfalme wa Israeli, akaaye katika Samaria; yuko katika shamba la mizabibu la Nabothi, ndiko alikoshukia ili alitamalaki,” 1Fal 21:17-18 

 “Ukamwambie, ukisema, Bwana asema hivi, Je! Umeua, ukatamalaki? Nawe utamwambia, kusema, Bwana asema hivi, Mahali pale mbwa walipoiramba damu ya Nabothi, mbwa watairamba na damu yako, naam, damu yako,” 1Fal 21:19

 “Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo?” Mt 5:46 

Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48

TAFAKARI:Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.”

Wapendwa wana wa Mungu, pasipo shaka yoyote ile, mwisho wa maisha yetu na mbele ya kiti kile cha hukumu tutahukumiwa katika mizania ya upendo. Bila shaka msoma mashtaka yetu, yaani, Yesu Kristo akiwa mbele ya Mungu Baba atakuuliza wewe, na mimi kila mmoja kwa nafasi yake hivi; “Je, ulipenda kwa kiasi gani? Nikiwa kielelezo chako nilikupenda upeo, Yoh 13:1, na kuyatoa maisha yangu na kufa kifo cha aibu kwa ajili yako. Swali la pili nafikiri litatoka kwa Mungu Baba. Nalo ni hili; Mwanangu, niambie umetumia vipi vipaji nilivyokupa? Kumbe kujibu vizuri maswali haya mbele ya safari yakupasa wewe na mimi kuishi vyema katika hofu ya Mungu, na wale wote wanaotuzunguka bila kujali hali zao na historia zao.

Somo letu la leo, linafafanua vizuri namna tupasavyo kuishi, yaani kuwa na hofu ya Mungu, na mahusiano yetu na jirani. Jana tuliona kile kilichojiri kwa Mfalme Ahabu na Mkewe Yezebeli. Kwa uovu wao na kutokuisimamia haki wanakuwa sababu ya kifo cha Nabothi mtu mwenye haki. Mungu wetu yu hai na huona yote tuyafanyayo. Mungu huchukizwa sana pale tunapoipoteza nuru yake ndani yetu kwa kujipenda zaidi. Na kwa sababu hiyo, Mungu anavunja ukimya ili haki itendeke. Na Neno la Bwana likamjia Eliya Mtishbi, kusema, Ondoka, ushuke, ukutane na Ahabu mfalme wa Israeli, akaaye katika Samaria; yuko katika shamba la mizabibu la Nabothi, ndiko alikoshukia ili alitamalaki,” 1Fal 21:17-18. Nabii Eliya Mtishbi anakuwa mjumbe halali wa ujumbe maalum wa Mungu. Hii ndiyo maana halisi ya kuwa Nabii. Mungu hutumia watu wake aliowateua kwa kazi maalum ili ujumbe wake uwafikie walengwa, na hawa ndio manabii kama Nabii Eliya. Ujumbe wa Mungu kwa mfalme Ahabu kupitia Nabii wake Eliya wasema hivi; Ukamwambie, ukisema, Bwana asema hivi, Je! Umeua, ukatamalaki? Nawe utamwambia, kusema, Bwana asema hivi, Mahali pale mbwa walipoiramba damu ya Nabothi, mbwa watairamba na damu yako, naam, damu yako,” 1Fal 21:19. Mungu anatangaza kiama kwa mfalme Ahabu kwa uovu wake. Ni ujumbe kwetu pia kuyatumia vizuri mamlaka ya Mungu tuliyopewa kupitia watu wake kwa njia halali ya kupiga kura, yaani, demokrasia huru na ya haki.

Mungu huitangaza na hata kuionyesha wazi hasira yake pale tunapokengeuka na kukataa wazi upendo wake. Na hii ndiyo maana ya dhambi, yaani, kuukataa upendo Mungu tukiwa na ufahamu wa kutosha kuhusu kile tukitendacho. Kwa kuukataa upendo huu wa Mungu (mfalme Ahabu), Mungu kwa kupitia Nabii Eliya anasema, Angalia, nitaleta mabaya juu yako; nami nitakuangamiza kabisa, nitamkatia Ahabu kila mume, aliyefungwa na aliyeachwa katika Israeli,” 1Fal 21:21. Ndugu yangu, Mungu amekuumba kwa malengo, yaani, umjue, umpende, umtumikie, na mwisho urudi kwake. Kwa kutokutambua wajibu huu na kutenda kinyume chake, Mungu uchukizwa sana, na huweza pia kuzidisha adhabu yake pale tunapomkasirisha kwa kutokuwa kusudi la kuumbwa kwetu. Hivyo katika ukweli huu Mungu anasema zaidi kuhusu Ahabu, Kisha nitaifanya nyumba yako iwe kama nyumba ya Yeroboamu mwana wa Nebati, na kama nyumba ya Baasha mwana wa Ahiya, kwa ajili ya chukizo ulilonichukiza, hata kunighadhibisha, ukawakosesha Israeli,” 1Fal 21:22 

Wapendwa katika Kristo, Mungu uchukizwa zaidi na yule asababishaye makwazo na hata kudongokwa kwa mtu katika hali ya dhambi. Na hii ndiyo adhabu ya mke wa mfalme Ahabu aliye gushi nyaraka za mfalme na kusababisha mauti ya Nabothi mtu mwanye haki. Naye Mungu anasema kupitia kinywa cha Nabii Eliya juu ya Yezebeli mke wa mfalme, Mbwa watamla Yezebeli katika kiwanja cha Yezreeli,” 1Fal 21:23. Dhambi hii ya makwazo Yesu anaisema kwa msisitizo mkubwa, kwamba, “Na ye yote atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, afadhali afungiwe jiwe la kusagia shingoni mwake, na kutupwa baharini,” Mk 9:42. Ni wito kwetu pia kutokuwa vikwazo kwa wengine. Adhabu yake ni kubwa. Katika hili, yeyote yule kwa njia moja au nyingine, kwa kujua na kushiriki kosa la wengine au mwingine hatokuwa salama. Kama ni kichapo ni kile kile! Naye Mungu anasema, Mtu wa nyumba ya Ahabu afaye mjini, mbwa watamla, na yeye afaye mashambani ndege wa angani watamla,” IFal 21:24. Unapoujua ukweli wa jambo na kukaa kimya bila kufanya chochote katika kweli na haki, washiriki uovu ule ule. Tendo hili ni sawa kabisa na yule aliyejua na kushiriki moja kwa moja katika uovu ule ule.

Wapendwa wana wa Mungu, haki ya Mungu huyafanya tena upya agano jipya na watu wake. Mungu husahau historia ya mabaya yetu na kutupa tena nafasi ya kuwa wapya katika yote. Naye anasema, Lakini hapakuwa na mtu kama Ahabu, aliyejiuza atende maovu machoni pa Bwana ambaye Yezebeli mkewe alimchochea,” 1Fal 21:25. Mimi na wewe hulivunja agano na Mungu kwa kuasi kwetu na kwenda kinyume na upendo wa Mungu. Na kumwasi Mungu ni kutokuwa na nafasi naye. Na ndiyo ilivyokuwa kwa watu wa utawala ule wa mfalme Ahabu. Mungu akachukiza mno, kwa kuzifuata sanamu sawasawa na yote waliyoyafanya Waamori, Bwana aliowafukuza mbele ya wana wa Israeli,” 1Fal 21:26. Unapokosa nafasi ya Mungu ndani ya moyo wako, nafasi hiyo hupata mpangaji mwingine ambaye huyabomoa maisha yako.

Tunapomkosea Mungu ni vyema kukajirudi na kufanya toba ya kweli. Hivyo ndivyo Mfalme Ahabu alivyoupokea ujumbe ule wa Mungu kupitia mtumishi wake Nabii Eliya na kufanya toba ya kweli. Ahabu alipoyasikia maneno hayo, akayararua mavazi yake, akavaa magunia mwilini mwake, akafunga, akajilaza juu ya magunia, akaenda kwa upole,” 1Fal 21:27. Neema na Huruma ya Mungu kwa mfanya toba ya kweli na majuto ni kubwa kuliko dhambi zake. Naye Mungu anasema, kwa sababu amejidhili mbele yangu, sitayaleta yale mabaya katika siku zake,” 1Fal 21:29a.

Ndugu yangu, maisha ya ufufuko ni ushindi dhidi ya uovu. Na upendo ndio kielelezo chake. Naye Yesu katika upendo wa kweli anasema, wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki,” Mt 5:44-45. Kumbe kupenda siyo tu kwa wale wanaotupenda. Yatupasa kufanya zaidi na kupenda zaidi. Tumwone Kristo kwa kila mmoja bila kujali historia yake iwe nzuri au mbaya. Kristo anatupa nafasi tena na tena ya kuwa wapya. Wakati fulani Mtume Petro alitaka kujua kipimo cha kusamehe, naye Yesu akamjibu, “sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini,” Mt 18:22. Kwa maneno mengine, ‘mpe uliyechukuzwa nawe muda wa kutosha.’

Upendo wa Mkristo anayeishi maisha ya ufufuko hana kipimo cha kuutoa upendo wake zaidi ya kupenda bila kipimo akiitafakari thamani ya kuokolewa kwake kwa sadaka ile ya mwenye haki pale Msalabani, yaani, Yesu Kristo. Na hii ndiyo maana ya maneno haya ya Yesu kwetu; Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo?” Mt 5:46. Upendo wa kweli na maisha mapya ya ufufuko hayafungamanishwi na uhasili wetu wa kuzaliwa, bali kila siku ni vita ya kuushinda ubinadamu wetu na kuelekea nuru ile ya milele, yaani maisha ya milele. Na hii ndiyo maana ya maneno haya; Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! Nao hawafanyi kama hayo?” Mt 5:47. Kuushinda ubinadamu wetu ndiyo dira na kuishi maisha ya malengo hapa duniani. Tunaishi kwa malengo, na malengo yetu ni kuufikia uzima ule aliyotuhaidia Yesu Kristo, “Kwa kuwa mapenzi yake Baba yangu ni haya, ya kwamba kila amtazamaye Mwana na kumwamini yeye, awe na uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho,” Yoh 6:40. Kusudi la kila mmoja wetu ni kuwa kama aliyetuumba, yaani, kuupata ule ukamilifu. Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48. Ukamilifu huu, ambao ndio Utakatifu, ndicho kigezo cha kuishi maisha hayo ya umilele na Baba yetu wa Mbinguni huko Mbinguni.

Tumsifu Yesu Kristo!
Ikawa, Ahabu alipoyasikia maneno hayo, akayararua mavazi yake, akavaa magunia mwilini mwake, akafunga, akajilaza juu ya magunia, akaenda kwa upole,” 1Fal 21:27


Tusali:-Ee Yesu Mwema, tuhurumie kwa kuwa tumetenda dhambi na tujalie neema na huruma yako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario