jueves, 2 de junio de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 9 YA MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI YA 9 YA MWAKA-C
Somo: 2Tim 4:1-8
Zab: 71:8-9, 14-15ab, 16-17, 22
Injili: Mk 12:38-44
Nukuu:
 “lihubiri neno, uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho,” 2Tim 4:2 

Maana utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe watajipatia waalimu makundi makundi, kwa kuwa wana masikio ya utafiti; nao watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo,” 2Tim 4:3-4 

 “Akaja mwanamke mmoja, mjane, maskini, akatia senti mbili, kiasi cha nusu pesa,” Mk 12:42 

Akawaita wanafunzi wake, akawaambia, Amin, nawaambia, Huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote wanaotia katika sanduku la hazina; maana hao wote walitia baadhi ya mali iliyowazidi; bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo, ndiyo riziki yake yote pia,” Mk 12:43-44

TAFAKARI: Maana utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima.”

Wapendwa wana wa Mungu, baadhi ya sehemu ya Kanisa la Magharibu limekumbwa ukavu mkubwa wa Imani. Baadhi ya maeneo hayo ni vigumu wakuwakuta vijana na watu wa umri wa kati makanisani. Na kama utawakuta basi elewa wapo tu kwa matukio au maadhimisho ya masakramenti ambayo kwa kiasi kikubwa hufanywa  tu kutimiza utaratibu fulani, na kwa kuwa imekuwa mtindo fulani wa maisha. Leo maeneo haya utawakuta vikongwe tu makanisani.

Pamoja na sababu nyingi zitolewazo kwa mujibu wa historia ya Kanisa hili la Magharibu, hii ni dhahiri; kutokuwepo kwa Katekesi ya kina. Kwa kiasi kikubwa Kanisa lilijisahau. Watu/Waamini walilishwa mafundisho ya Kanisa bila kuyacheua. Mafundisho ya mtindo huu yalimzunguka mtu kila kona. Mtu alikutana na mafundisho ya mtino huo Kanisani, na kwenye mfumo mzima wa kijamii na siasa. Matokeo yake ni kwamba mtu alijiona kama mfungwa katika mtindo fulani wa maisha uliokuwa vigumu kuuhoji na kujinasua. Kwa mtindo huu, uasi wa dini na imani uliza kujitokeza taratibu, kwani binadamu anapobanwa sana utafuta pa kutokea. Kulianza pia taratibu kujengeka chuki kwa baadhi ya watu juu ya Kanisa. Kanisa lilionekana kuuchukua kabisa uhuru wa mtu.

Ni vyema mtu ajue vizuri kile akiaminicho, na siyo kukimeza tu bila kucheua. Usipo kijua vizuri kile ukiaminicho ni vigumu pia kukitetea au kuwa sehemu ya maisha yako. Mtume Paulo anampa angalizo Timotheo, ambalo leo tungelihusiha na utoaji wa Katekesi ya kina. Naye anasema,lihubiri neno, uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho,” 2Tim 4:2. Tusipo jali leo kuwapa waamini katekesi ya kina juu ya imani ya kweli, muda si mrefu nasi tutakumbana na hiki kinachoendelea katika Kanisa la Magharibi. Maana utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe watajipatia waalimu makundi makundi, kwa kuwa wana masikio ya utafiti; nao watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo,” 2Tim 4:3-4. Sambamba na kutoa katekesi ya kina, tuliopewa dhamana hiyo na Kanisa yatupasa kujifunza kwa kina juu ya ‘teología ya mawasiliano.’ Pasipo mawasiliano katika uinjilishaji vyote uvurugika. Ni sawa na kuujenga mnara wa babeli. Waamini wanapaswa kushirikishwa vizuri maswala ya uinjilishaji kadiri ya nafasi zao. Makleri hawawezi kufanya mambo yote. Tujifunze historia ya Kanisa la mwanzo na changamoto zake. “Wale Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani,” Mdo 6:2. Hii ni faida ya kujifunza Teología ya mawasiliano. Kielelezo cha Teología hii ni uwepo wa Utatu Mtakatifu, Mungu mmoja nafasi tatu.

Teología hii ya mawasiliano katika utekelezaji wa katekesi ya kina inatutaka tuwe na kiasi, na kila mmoja katika familia ya wana wa Mungu awajibike kadiri ya nafasi yake. Hivyo Mtume Paulo anamwambia Timotheo, mimi na wewe leo kwamba, Bali wewe, uwe na kiasi katika mambo yote, vumilia mabaya, fanya kazi ya mhubiri wa Injili, timiliza huduma yako,” 2Tim 4:5. Mtume Paulo analiona hili na umuhimu wake kwa sababu umri wake unakwenda, na nguvu pia zinapungua. Hawezi tena kuyanya kwa nguvu kama zamani, na kufanya yote mwenyewe. Kwa maana, mimi sasa namiminwa, na wakati wa kufariki kwangu umefika,” 2Tim 4:6. Haya ni mang’amuzi binafsi kutoka kwa Mtume Paulo. Mang’amuzi katika maisha ni mwalimu mzuri wa kutusaidia kuzisoma alama za nyakati. Kanisa katika historia yake, limepata mang’amuzi makubwa sana. Ni vyema tukaitumia elimu hii, kuzisoma alama za nyakati zetu.

Hii ndiyo vita ya kiimani aisemayo Mtume Paulo kwamba, Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda,” 2Tim 4:7. Kila mmoja kadiri ya nafasi yake katika Kanisa lazima ailinde imani yake licha ya changamoto tunazokumbana nazo kila siku. Leo tunaishi katika ulimwengu wa umimi na vitu. Ni vigumu kwa mtazamo huo kuwa na Teología ya mawasiliano kama kila mtu atakuwa amejifungia katika kiota chake. Kumbe leo kwa namna ya pekee twahitaji kuziimarisha jumaiya zetu ndogondogo za Kikristo. Hapa ndipo tunapoweza kutoa katekesi ya kina na kuumega mkate kwa kina. Mtindo huu wa maisha ya Jumuiya Ndogondogo za Wakristo, ndiyo ulivyokuwa kwa Kanisa lile la mwanzo.  Ni mahali hapa tunapoambiwa kwamba, “wakawa wakidumu katika fundisho la Mitume, na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika kusali,” Mdo 2:42. Je, waijua Jumuiya yako? Kama waijua huwa unajumuika nao katika ushirika, kuumega mkate, na katika kusali?

Wapendwa wana wa Mungu, ni katika kutimiza wajibu huu muhimu juu ya imani yetu ndipo tunapoweza kusema kama Mtume Paulo, kwamba, baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake,” 2Tim 4:8. Umoja na mshikamano katika Kanisa, yaani, wabatizwa wote, ni muhimu kufanikisha hazma hii ya uinjilishaji wa kina. Kwa namna hiyo, sote ni ndugu na tumehesabiwa haki na kuwa wana na warithi wa Mungu kwa sadaka ile ya Yesu pale Msalabani. Kwa kutambua upendeleo huo yatupasa kuwa waangalifu na matendo yale yote yatakayo dhuru afya ya kuwa wana wa Mungu.

Katika Injili ya leo, Yesu katika mafundisho yake anatupa maangalizo hayo na kusema, Jihadharini na waandishi, wapendao kutembea wamevaa mavazi marefu, na kusalimiwa masokoni,” Mk 12:38. Hakuna sababu ya kupoteza muda mwingi kwa kufanya maigizo badala ya kuwajibika kila mmoja kadiri ya nafasi yake, na wito wake. Huu ndio ule unafiki alioukemea Yesu tuisomapo sura yote ya 23 ya Injili kama ilivyoandikwa na Mwinjili Mathayo. Maigizo haya yasiyo na tija ni ya wale ambao hupenda kuketi mbele katika masinagogi, na viti vya mbele katika karamu; ambao hula nyumba za wajane, na kwa unafiki husali sala ndefu; hawa watapata hukumu iliyo kubwa,” Mk 12:39-40. Hawa ni wale wanasisasa wa wetu wa leo ambao hupenda kucheza na akili za watu kwa sababu wanaujua udhaifu na mapungufu ya wananchi wao. Wakiwa na masikini hujifanya kuwa nao bega kwa bega na kuwahaidia mbingu isiyofikika. Wakiwa na matajiri hujifanya kuwa nao karibu wakiwahaidi kulinda maslahi yao, na wakiwa Makanisani na Misikitini hujipambanua kupiga vita dhidi ya ufisadi na uovu wa kila aina kumbe ndani mwao wasukumwa na roho hiyo hiyo ya kufisidi.

Ni vyema kila mmoja wetu akawa kile alicho na kujitoa bila kujibakiza. Na huu ni ule mfano wa mwanamke mjane na masikini. Mwanamke huyu alijitoa bila kujibakiza. Akaja mwanamke mmoja, mjane, maskini, akatia senti mbili, kiasi cha nusu pesa,” Mk 12:42. Ni vyema kila wakati maneno yetu yaseme matendo yetu, na matendo yetu yaseme maneno yetu. Hili lisipoonekana kwa kiongozi yeyote yule humuondolea ile nguvu ya kimaadili. Mwanamke huyu mjane na masikini kwa nafasi yake anaonyesha nguvu yake ya kimaadili. Kwa msisitizo juu ya hili Yesu Akawaita wanafunzi wake, akawaambia, Amin, nawaambia, Huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote wanaotia katika sanduku la hazina; maana hao wote walitia baadhi ya mali iliyowazidi; bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo, ndiyo riziki yake yote pia,” Mk 12:43-44. Je, ndugu yangu, kadiri ya nafasi yako na wito wako, umetia yote hapo ulipo; katika imani yako, uinjilishaji wako, na jamii inayokuzunguka?

Tumsifu Yesu Kristo!

“Jihadharini na waandishi, wapendao kutembea wamevaa mavazi marefu, na kusalimiwa masokoni, na kuketi mbele katika masinagogi, na viti vya mbele katika karamu; ambao hula nyumba za wajane, na kwa unafiki husali sala ndefu; hawa watapata hukumu iliyo kubwa,” Mk 12:38-40


Tusali:-Ee Yesu Mwema, tufanye daima vyombo vya Amani yako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario