JUMAMOSI WIKI YA 12 YA MWAKA-C
Somo: Omb 2:2, 10-14, 18-19
Zab: 74:1-2, 3-5a, 5b-7, 20-21
Injili: Mt 8:5-17
Nukuu:
“Wazee
wa binti Sayuni huketi chini, Hunyamaza kimya; Wametupa mavumbi juu ya vichwa
vyao, Wamejivika viunoni nguo za magunia; Wanawali wa Yerusalemu huinama vichwa
vyao Kuielekea nchi,” Omb 2:10
“Manabii
wako wameona maono kwa ajili yako Ya ubatili na upumbavu Wala hawakufunua uovu
wako, Wapate kurudisha kufungwa kwako; Bali wameona mabashiri ya ubatili kwa
ajili yako Na sababu za kuhamishwa,” Omb 2:14
“Yesu akamwambia,
Nitakuja, nimponye,” Mt 8:7
“Yesu aliposikia
hayo, alistaajabu, akawaambia wale waliomfuata, Amin, nawaambieni, Sijaona
imani kubwa namna hii, kwa ye yote katika Israeli,” Mt 8:10
TAFAKARI: “Nitakuja niwaponye.”
Wapendwa
wana wa Mungu, Injili ya leo ni uthibitisho na mwendelezo wa Mungu wetu aliye
hai na mweza wa vyote. Kumbe hatuna sababu ya kubaki na majonzi yoyote yale
tunapokutana na sintofahamu katika maisha kama wanavyokabiliana na hali hiyo
wana wa Israeli. Ndani na katika Kristo hatupaswi kuishi katika ukiwa, hata
kama hatuna jibu la moja kwa moja, ‘tumaini katika maisha’ liwe jibu la
sintofahamu yako. Wana wa Israeli wanaliweka tumaini kwa lao kwa Mungu kwa njia
ya kufanya toba kweli na majuto. “Wazee wa
binti Sayuni huketi chini, Hunyamaza kimya; Wametupa mavumbi juu ya vichwa
vyao, Wamejivika viunoni nguo za magunia; Wanawali wa Yerusalemu huinama vichwa
vyao Kuielekea nchi,” Omb 2:10. Toba ya
kweli na majuto huwa jibu na matumaini ya kweli pale tunapoona kweli kwa
kupotoka kwetu bila kutafuta sababu zozote zile za utetezi au kuhalalisha
dondoko letu.
Hata hivyo, nyakati
kama hizi katika maisha tunahitaji manabii wa kweli, na wasioyumbishwa na
mivumo yoyote ile katika jamii. Tunahitaji watu wa kuuona ukweli kama ulivyo
hata kama utawagharibu maisha yao. Leo na hasa katika jamii yetu ya Tanzania,
tunahitaji nabii wa kweli ‘wa sauti ya wasio na sauti’ ambao ndio wengi. Ni
katika mazingira kama haya ndipo ‘tunapoliona Kanisa la Kristo’ aliye hai na
aliyekufa kwa ajili ya wewe na mimi ili tuwe huru na hai. Na hii ndiyo maana ya
maneno haya tuyasomayo katika somo letu la leo, kwamba; “Manabii wako wameona maono kwa ajili yako Ya ubatili na
upumbavu Wala hawakufunua uovu wako, Wapate kurudisha kufungwa kwako; Bali
wameona mabashiri ya ubatili kwa ajili yako Na sababu za kuhamishwa,” Omb 2:14.
Kanisa ambalo ndilo Mwili wa Kristo na Sakramenti ya Wokovu wetu, linapoufumbia
macho uovu wa namna yoyote ile kwa sababu zozote zile, historia itakuwa hakimu wa kweli na haki kwa wakati wake.
Hivyo kwa mantiki
hii, Kanisa kama Sakramenti ya Wokovu, “Inuka,
ulalamike usiku, Mwanzo wa makesha yake; Mimina moyo wako kama maji usoni pa
Bwana; Umwinulie mikono yako; Kwa uhai wa watoto wako wachanga wazimiao kwa
njaa, Mwanzo wa kila njia kuu,” Omb 2:19. Kanisa, yaani, Mwili wa Kristo, na
kila mbatizwa kama sehemu ya mwili huo, lisipo simama kama ‘sauti ya wasio na
sauti’ katika kweli na haki, litakuwa limekwishapoteza jukumu msingi katika
safari nzima ya ‘kuumba ulimwengu,’ ‘kuukomboa ulimwengu,’ na ‘kuutakasa
ulimwengu.’ Kanisa katika maana ya wabatizwa wote, ni viungo shirikishi katika
uumbaji wa pili wa Mungu, ambao mimi na wewe twaushiriki kadiri ya vipaji
vyetu, wito wetu, na nafasi zetu katika jamii inayotuzunguka.
Wapendwa
katika Kristo, tukiirejea Injili ya leo, Mungu hutujibu mara tunapomwelekea
bila shaka yoyote. Imani ndiyo msingi wa yote tuyaombayo kwa Mungu.
Tunapomwelekea Kristo katika mahangaiko yetu, na kuwa imara katika imani, jibu
lake ni moja tu. “Nitakuja,
nimponye,” Mt 8:7, na kwa maana pana ni kwamba, ‘nitakuja niwaponye.’ Tunakosa
neema hii pale tunapoanza kubabaika katika imani. Mara nyingi twapenda kupata
majibu mepesi ya haraka kwa maswali magumu kwa kile kinachotusumbua bila la
kujua hathari zake, na hasa hatma ya mahangaiko yetu. Hatma ya mahangaiko yetu
ni uponyaji wa kweli. Tunaposukumwa na majibu tu mepesi ya yale yanayotusumbua,
tunaishia kwanye ufahamu wa haraka na usio na uweledi wa kiimani. Hapa ndipo
Wakristo wengi hudondoka. Rejea ‘kikombe cha Babu wa Loliondo.’ Tupo kati yetu
tunaoamini kwanza majibu ya waganga wa kienyeji kabla ya kupeleka kesi hiyo
mbele ya ufahamu wetu wa kibinadamu, yaani tafiti za kisayansi, na mwisho
tukikosa jibu, kwa hakimu mwenye haki na mamlaka yote, yaani, Yesu Kristo,
ambaye ndiye tumaini letu. Pamoja na utayari wa yule akida juu ya Imani
aliyokuwa nayo kuhusu Yesu, haoni sababu ya Yesu kufanya safari na kuleta
uponyaji huo ili hali uzima upo ndani na katika Kristo. Hivyo anaonyesha imani
yake isiyo na shaka kwa Yesu na kusema, “Bwana, mimi sistahili wewe uingie
chini ya dari yangu; lakini sema neno tu, na mtumishi wangu atapona,” Mt 8:8.
Ndugu yangu, hiki ni kikomo cha hali ya juu kwa kile tukiaminicho.
Kwa upande mwingine, Yesu alifumbii jambo hili macho
bila kulisemelea. Hapa ndipo mahali Yesu anapotuonyesha
nini maana ya Imani ya kweli. Pamoja na mamlaka aliyokuwa nayo yule Akida,
alitambua mamlaka aliyokuwa nayo Kristo Yesu. Kujishusha kwa Akida huyu ndipo
kunapo muhesabia haki. Hivyo “Yesu
aliposikia hayo, alistaajabu, akawaambia wale waliomfuata, Amin, nawaambieni,
Sijaona imani kubwa namna hii, kwa ye yote katika Israeli,” Mt 8:10. Je, ni
wangapi kati yetu tulio tayari kuuvua ubwana wetu na kuuvaa utwana?
Ndugu yangu, katika
Imani ya kweli ndipo penye uponyaji wa kweli. Uponyaji wa kweli ndani yetu
tunatembea nao ila hatujua ni wapi pa kushika. Jambo hili linajidhihirisha wazi
kwa maneno ya Yesu mwenyewe. Naye anamwambia yule Akida, “Nenda
zako; na iwe kwako kama ulivyoamini,” Mt 8:13. Ndugu yangu, bila shaka unafanya
maombi kwa nia mbalimbali. Leo ngoja nikumegee siri ya kufanikiwa katika maombi
yako. Kwanza, kuwa na imani kwa kile unachokiomba kana kwamba umeshakipata
tayari. Pili, kila neno ulitamkalo kwa imani hiyo, nena maneno hayo hivi; “nani
nasimama katika neno hili nililolitamka bila shaka.” Hapa ndipo Mungu ulitimiza
lile tuliombalo na ulitamkalo kadiri tulivyoliamini.
Kristo mara zote
anatutakia uhai, tena uhai wa kweli. Ni kwa namna hii, “ili
litimie lile neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Mwenyewe aliutwaa udhaifu
wetu, Na kuyachukua magonjwa yetu,” Mt 8:17. Yesu anamponya mama mkwe wa Petro
na mama huyu anawahudumia. Kristo mara zote anatwaa udhaifu wetu na kuyachukua
magonjwa yetu, na madhaifu yetu. Ndugu yangu, magonjwa yako wayapeleka wapi?
Achana na ‘Kalimanzila!’
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nenda zako; na iwe kwako kama
ulivyoamini,” Mt 8:13b
Tusali:-
Ee Yesu, nakuamini. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario