ALHAMISI WIKI YA 11 YA MWAKA-C
Somo: YbS 48:1-15
Zab: 97:1-2, 3-4, 5-6, 7
Injili: Mt 6:7-15
Nukuu:
“Siku zake zote huyu pia hakushawishwa kwa kumwogopa mwenye kutawala,
wala hakutiishwa na mtu yeyote,” YbS 48:12b
“Lakini kwa ajili ya hayo yote
watu hawakutubu wala hawakuziacha dhambi zao, hata walipochukuliwa mateka
kutoka nchi yao, wakatawanyika juu ya uso wa dunia yote,” YbS 48:15
“Kwa
maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi,”
Mt 6:14
“Bali
msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu,”
Mt 6:15
TAFAKARI: “Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu
hatawasamehe ninyi makosa yenu.”
Wapendwa wana wa Mungu, kusamehe hakumaanishi kusahau ulichotendewa,
bali ukumbukapo ulichotendewa badala ya kubaki katika hali ya uchungu, mateso
na majonzi, unajazwa furaha ndani ya moyo wako kwa sababu unaonja furaha ya
Utukufu ule alioupata Yesu Kristo kupitia kifo kile cha Msalaba. Kusamehe kweli
ni kutambua kweli thamani ya ushindi wa msalaba dhidi ya uovu. Na ndiyo maana
yakupasa kujua, ‘hakuna utukufu pasipo msalaba.’ Na niutazamapo Msalaba
Mtakatifu unikumbushe Mti ule wa ajabu na wenye bahati ambao wokovu wangu
ulitundikwa juu yake. Mahangaiko yetu katika maisha ndani na katika Kristo
hupata bahati kama ya mti huu kwa sababu mwisho wa mateso hayo upo wokovu.
Kumbe siyo vyema kumlaumu Mungu na kukasirika juu ya Yesu pale ninapopatwa
mateso pasipo hatia yoyote. Je, Kristo Yesu alikuwa na hatia alipoukabili
msalaba zaidi ya kuukubali ili tuwe huru kutoka kifungo cha dhambi?
Hata pamoja na hali hiyo ya mateso makubwa, Yesu Kristo hakuacha kutoa
msamaha. Akiwa amewambwa Msalabani aliweza kutamka maneno haya pasipo shaka
yoyote, “Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo,” Lk 23:34a.
Je, ninao ujasiri huo wa kutamka maneno hayo hata pale ninapotambua wazi kuwa
nimeonewa? Hakika ni changamoto kubwa sana leo, hasa kwenye ulimwengu huu wa
‘haki sawa.’ Lakini pamoja na wigo huu mpana wa ‘haki sawa’ Yesu anakuambia
wewe na mimi kwamba, “msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu
hatawasamehe ninyi makosa yenu,” Mt 6:15. Je, kwa maendeleo ya leo twaweza sema
alichokisema Yesu kimepitwa na wakati? La hasha! “Yeye
anikataaye mimi, asiyeyakubali maneno yangu, anaye amhukumuye; neno hilo
nililolinena ndilo litakalomhukumu siku ya mwisho,” Yoh 12:48. Maandiko
Matakatifu yana uzima nyakati zote, na ya hai muda wate.
Yapo mambo mawili
tunayoweza kujifunza katika Injili ya leo. Jambo la kwanza ni kuhusu Sala. Na
jambo la pili ni namna ya kusala. Sala anayo tufundisha Bwana wetu Yesu Kristo
leo, na ili kuyapata yote tuyaombayo kuna sharti moja lazima tulitimize, yaani,
makosa yetu husamehewa na Mungu kwa mizania ile ile tuitumiayo kuwasamehe wale
waliotukosea. “Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo
wadeni wetu,” Mt 6:12. Pili kuzama katika sala ni kusali katika utulivu.
Hivyo Yesu anasema, “Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama
watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao
kuwa mengi,” Mt 6:7. Je, sala hii ya Baba Yetu ina maana yoyote kwa
wabebao mzigo wa visasa, chuki, na kutokusamehe?
Wapendwa katika Kristo,
“mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa
mbinguni atawasamehe ninyi. Bali
msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu,”
Mt 6:14-15. Je, kunafaidha gani kutembea na gunia hili la chuki, visasi, na
kutokusamehe? Kwa nini hutaki kumsamehe huyo uliyembeba muda wote katika kichwa
chako, moyo wako, na maisha yako yote? Kwa nini hutaki kujiweka huru?
Yawezekana aliyekutenda hilo usilotaka kusamehe hana habari na ugomvi wako
nawe. Yeye yupo huru ila wewe bado upo kwenye maabusu hiyo ya kutokusamehe bila
kujua tarehe rasmi ya kusikilizwa kesi yako.
Pamoja na mkwano huo
tunaojijengea wenyewe, Jambo la pili tunalofundishwa leo ni namna ya kusali.
Yesu anatufundisha namna ya kusali na mapaswa yake. Anatoa angalizo katika
sala. Sala ya kweli na yenye utulivu ni kule kusali bila kupayuka. Ni sala ya
kumsikiliza mtu wa ndani. Ni kujisikiliza na kusikiliza matakwa ya Mungu. Ni
utulivu wa ndani ambapo katika utulivu huu tunakutana na Mungu. Hivyo kuabudu
kuliko kwa kweli ni kuabudu katika usahihi, uhalisi, tafakuri, na matendo hai.
Kama haya mambo hayafanyiki, kuabudu kweni ni kupayuka payuka. “Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama
watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao
kuwa mengi. Basi msifanane na hao; maana Baba yenu anajua mnayohitaji kabla
ninyi hamjamwomba,” Mt 6:7-8
Sala hii ya Baba yetu
ni ufupisho kwa yale yote tunayotakiwa kufanya kila dakika tunapopumua.
Mahitaji yetu, utulivu wetu, matakwa yetu, uhusiano wetu na wengine, mahangaiko
na vishawishi vyetu vyote hupata majibu katika sala hii. Je, tunatafakari hayo
tusalipo sala hii ya baba yetu? Mfano swala la MSAMAHA. Kusamehe ni amri na sio
ombi. Yatupasa Kusamehe na hiki kicho kipimo cha sisi kusamehewa. “Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu
wa mbinguni atawasamehe ninyi,” Mt 6:14. Ndugu
yangu, kusamehe siyo kusahau kama nilivyo kwisha kusema. Ukweli ni kwamba
hatuwezi kufuta aliyofanyiwa Yesu na kufa kifo kile cha aibu msalabani. Ila
tunasema msalaba ni ushindi tunapotazama Utukufu wa Msalaba. ‘Huu ndio ule uti
wa msalaba, ambao wokovu wa dunia umetundikwa juu yake.’ Maneno haya ya ushindi
na matumaini husemwa siku ile ya Ijumaa Kuu unapofunuliwa msalaba uliofunikwa.
Unapomsamehe mtu mbele
yako upo Utukufu. Tunapokumbuka uchungu tuliofanyiwa tunapata faraja kwani
katika hilo tumeshinda kwa kusamehe. Ni faraja ya kweli na tumaini jipya.
Tusibaki kwenye uchungu na mateso ila tukumbatie Utukufu ule wa milele. Hili
ndilo fumbo la kusamehe na Utukufu unaopatikana katika tendo hilo. “Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu
hatawasamehe ninyi makosa yenu,” Mt 6:15. Na kwa kufanya hivyo ndugu yangu,
yaani kutokusamehe kwako, mbele huko ya safari hakuna Utukufu wala Mbingu-Uzima
wa milele.
Kudumu
katika mambo haya mawili yaani, sala kwa ujumla wake, na namna ya kusali,
utujengea urafiki wa karibu na Mungu pasipo woga. Tunakuwa tayari kumwendea na
kuzungumza naye siyo nyakati zile tunazomwitaji tu, yaani, nyakati za shida,
bali nyakati zote kama rafiki mwema na wakaribu. Ni kutambua kwa kina kwamba
wakuogopwa licha ya kwamba ni rafiki yetu, ni Mungu tu. Binadamu pamoja na ukuu
na mamlaka yake si wa kuogopwa bali kuheshimiwa kwa kile anachokisimamia katika
kweli na haki. Hivyo katika kweli na haki, mtawala au kiongozi anapaswa
kuulizwa na kufikika kwa sababu nguvu alizokuwa nazo kapewa na umma anaouongoza.
Hivi ndivyo ilivyokuwa kwa Nabii Elisha kwamba, “Siku zake zote huyu pia hakushawishwa kwa kumwogopa mwenye kutawala,
wala hakutiishwa na mtu yeyote,” YbS 48:12b. Kwenye kuisema kweli na kuitetea
haki pale ambapo hapana fursa ya kufanya hivyo, huleta mateso na sintofahamu
nyingi. Hata hivyo kukaa kimya siyo jibu.
Kweli na haki huwezwa kudhoofishwa lakini haiangamizwi bali ujikusanya
na kuwa na nguvu zaidi katika umilele wake. Hii ni kwa sababu kweli na haki ni
asili ya Mungu kwenye umilele. Hii ndiyo iliyokuwa tabia ya Nabii Elisha mbele ya kweli na
haki, yaani “Hakukutokea neno
lililokuwa gumu la kumshinda, hata na alipolala mautini mwili wake ulitoa
unabii,” YbS 48:13. Hapa ndipo pale Yesu anaposema, “Msiwaogope
wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye
kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum,” Mt 10:28. Kilicho haki hudumu
katika umilele wake hata kama kitahujumiwa kwa wakati kwa kukinyamazisha.
Masimulizi
ya maisha ya Nabii Elisha yanathibitisha ukweli huu kwamba, “Kama alivyofanya miujiza katika maisha yake,
kadhalika na katika mauti yake kazi zake zikawa za ajabu,” YbS 48:14. Ni nani
basi mwenye uwezi wa kuinyamazisha Roho ya Mungu ndani ya mtu mwenye haki? Ni
kweli kabisa kwamba kuwa kipofu siyo kwamba huna uwezo wa kuona, bali upofu
mbaya ni ule wa kutokuikubali kweli kwa sababu tu wewe siyo wa upande huo wa
pili wenye kuiona kweli kama ilivyo. Mungu hakosi kutuwajibisha pale
tunapoichezea kweli ambayo ni moja ya sifa yake. Hivyo pamoja na Elisha kuipigania
kweli hadi mauti yake, “watu hawakutubu wala hawakuziacha dhambi zao, hata
walipochukuliwa mateka kutoka nchi yao, wakatawanyika juu ya uso wa dunia
yote,” YbS 48:15. Kwani leo miongoni mwetu hawapo wenye kuutetea uovu ilihali
wakijua madhara yake?
Mpendwa tuliyeongozana
pamoja katika tafakari hii, turudi kwa swala letu kuu la kusamehe na kama
umeguswa na tafakari hii, embu tulia na fikiri uliyembeba kwa muda mrefu bila
kumsamehe. Leo au kesho tafuta njia ya kumsamehe. Ni vizuri akijua pia
umemsamehe. Kwa tendo hilo unaleta pia uponyaji kwako na kwake. Na fanya hivyo
kwa upendo na uhuru. Wakati ndio sasa!
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kwa maana
mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi,” Mt
6:14
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, nikumbushe daima kuwa kipimo cha kusamehe ni kusamehe bila kipimo
kama ulivyojitoa sadaka pale Msalabani kwa upendo mkubwa bila kujibakiza na
kusamehe yote. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario