ALHAMISI WIKI YA 13 YA MWAKA-C
Somo: Amo 7:10-17
Zab: 19:8, 9, 10, 11
Injili: Mt 9:1-8
Nukuu:
“Ndipo
Amazia, kuhani wa Betheli, akapeleka habari kwa Yeroboamu, mfalme wa Israeli,
akisema, Amosi amefanya fitina juu yako kati ya nyumba ya Israeli; nchi haiwezi
kustahimili maneno yake yote,” Amo 7:10
“Kwa
maana Amosi asema hivi, Yeroboamu atakufa kwa upanga, na bila shaka Israeli
atachukuliwa mbali, hali ya kufungwa, atoke katika nchi yake,” Amo 7:11
“Na tazama, wakamletea mtu mwenye kupooza,
amelala kitandani; naye Yesu, alipoiona imani yao, alimwambia yule mwenye
kupooza, Jipe moyo mkuu, mwanangu, umesamehewa dhambi zako,” Mt 9:2
“Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri
duniani ya kusamehe dhambi, (amwambia yule mwenye kupooza) Ondoka, ujitwike
kitanda chako, uende nyumbani kwako,” Mt 9:6
TAFAKARI: “Na kazi ya haki itakuwa amani; na
mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na matumaini daima,” Isa 32:17
Wapendwa wana wa Mungu, pasipo haki hapana amani, utulivu, na
matumaini. Hata hivyo haki uendana na wajibu. Aliyetimiza wajibu wake
anastahili haki yake kwa namna yoyote ile. Mfano: ni wajibu wangu kuwa raia
mwema ikiwa ni pamoja na kulipa kodi kadiri ya utaratibu uliowekwa kisheri na
kikatiba inayoakisi matakwa ya raia wenyewe. Kama hili limefanyika, basi
nastahili kupata haki zangu kwa mujibu wa Katiba ambayo ndiyo dira na sheria
mama. Na sheria hiyo Mama au Katiba, ndipo watu huamua namna wanavyotaka
waongozwe, kuwajibika, na kuwajibishwa pale inapokuwa ndivyo sivyo. Fujo na
machafuko utokea pale ambapo haki haitolewi licha ya wajibu kutimizwa.
Ila Mungu wetu aliye Amani anatutaka tuwe na amani na hili ndilo fumbo
la uumbaji wetu, ‘kwa sura na mfano wake,’ Mwa 1:27. Penye fujo na machafuko
Utukufu wa Mungu hufifishwa tu ila hatuwezi kuuondoa au kuutokomeza. Naye Mungu
asema hivi, “watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani
zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu,” Isa 32:18. Haki,
utulivu, na amani havitolewi na mtu kutoka mfukoni mwake. Ni wajibu wa kila
mtu/raia pale alipo kuhakikisha vinakuwepo. Wote waliopewa dhamana na umma
yawapasa kusimamia hilo pasipo upendeleo na kwa mujibu wa Katiba husika, na
siyo dhania binafsi kwa malengo binafsi au kikundi fulani cha waliojihalalishia
haki hiyo. “Wabaya wanafanana na bahari iliyochafuka; maana haiwezi kutulia, na
maji yake hutoa tope na takataka. Hapana
amani kwa wabaya; asema Mungu wangu,” Isa 57:20-21
Chini ya utawala wa Mfalme Yeroboamu haki za watu zilikanyagwa. Mfalme
hakupaswa kuguswa wala kukosolewa. Ilikuwa ni kosa kufanya hivyo. Kuhani Amazia
alikuwa mtetezi na mtu wa karibu wa Mfalme Yeroboamu. Watu wote waliotaka
kumkosoa mfalme walizimwa midomo au kuamuriwa kuikimbia nchi na kuishi
uhamishoni. Ni katika mazingira haya Nabii Amosi anapata misukosuko kutoka kwa
kuhani wa Betheli juu ya kumkosoa mfalme na kuonya tabia yake ya ukandamizaji.
Ili kumnyamazisha Nabii Amosi, “Amazia,
kuhani wa Betheli, akapeleka habari kwa Yeroboamu, mfalme wa Israeli, akisema,
Amosi amefanya fitina juu yako kati ya nyumba ya Israeli; nchi haiwezi
kustahimili maneno yake yote,” Amo 7:10.
Yaani, kwa maneno mengine, Amosi anashitakiwa kwa kosa la uchochezi. Ndugu
yangu hapa ndipo tunapotakiwa kujua maana ya sauti ya kinabii.
Sauti ya kinabii ni
sauti ya Mungu iliyojaa maono. Mungu uwafunulia watu wake na hasa wenye utulivu
wa ndani, wenye uwezo wa kuliona jambo au hali kama lilivyo au ilivyo, na siyo
kama walivyo. Ni msukumo wa ndani uliojaa hofu ya Mungu na kwa watu wa Mungu.
Ni maono yaliyobeba kweli, haki, upendo, na amani. Nabii na unabii si kitu cha
mkurupuko kama ilivyo ‘bendera fuata upepo.’ Na siyo utabiri kama ilivyo kwa
wapiga ramli wenye kulenga hisia binafsi au za watu, bali ni kweli katika
kweli, na haki katika haki.
Wapendwa wana wa Mungu,
mwenye sauti hiyo ya unabii ni mwiba wa hatari palipojaa dhuluma na giza la
uonevu. Watu wa mtindo huu kama alivyo Amosi Nabii, hawakoswi kusingiziwa
yasiyo kweli na hata kuhalalishiwa makosa yasiyo kweli. Lengo ni kuwafunga
midomo na kuwaangamiza. Mungu anaujumbe huu kwa wote wasimamao katika kweli na
haki: “Nyakati zao zitakuwa nyakati za kukaa imara; za wokovu tele
na hekima na maarifa; kumcha Bwana ni hazina yake ya akiba. Angalia, mashujaa wao wanalia nje,
wajumbe wa amani wanalia kwa uchungu.” Isa 33:6-7. Ni kwa namna hiyo Nabii
Amosi anashitakiwa kwa Mfalme na kuhani Amazia, na kusema, “Yeroboamu
atakufa kwa upanga, na bila shaka Israeli atachukuliwa mbali, hali ya kufungwa,
atoke katika nchi yake,” Amo 7:11. Na kama haikutosha, “Amazia
akamwambia Amosi, Ewe mwonaji, nenda zako, ikimbilie nchi ya Yuda, ukale mkate
huko, ukatabiri huko; lakini
usitabiri tena huku Betheli; kwa maana ni mahali patakatifu pa mfalme, nayo ni
nyumba ya kifalme,” Amo 7:12-13.
Amazia
kuhani anamvika umungu Mfalme Yeroboamu. Jambo hili ni hatari sana machoni mwa
Mungu. Mungu ndiye mwenye mastahili ya kuabudiwa na kuogopwa, Zab 15:11; 111:9,
na siyo mwanadamu mwenye nyama na mifupa, na kifo kikiwa ndiyo rafiki yake wa
karibu kama kilivyo kivuli chake kisichosema chochote bali ufuatana nacho
daima. Pamoja na vitisho hivyo vya
kuhani Amazia, havikuweza kuufunga mdomo wa Nabii Amosi. “Ndipo
Amosi akajibu akamwambia Amazia, Mimi sikuwa nabii, wala sikuwa mwana wa nabii;
bali nalikuwa mchungaji, na mtunza mikuyu; naye
Bwana akanitwaa, katika kufuatana na kundi; Bwana akaniambia, Enenda uwatabirie
watu wangu Israeli,” Amo 7:14-15. Nabii Amosi anajua wazi kabisa hayafanyi hayo
kwa malengo yake binafsi, bali anawakilisha ujumbe wa Mungu kwa watu wake. Hivyo Amosi asiti kuzitema cheche za moto wa
kweli na haki kutoka kwa Mungu. Naye alikuwa na ujumbe huu wa Mungu kwa Amazia kuhani, “Basi, sasa lisikie neno la Bwana; Wewe unasema, Usitabiri juu
ya Israeli, wala usitoe neno lako juu ya nyumba ya Isaka; kwa hiyo, Bwana asema hivi, Mke wako
atakuwa kahaba mjini, na wana wako na binti zako wataanguka kwa upanga, na
shamba lako litagawanywa kwa kamba; na wewe mwenyewe utakufa katika nchi iliyo
najisi; na bila shaka Israeli atachukuliwa mbali hali ya kufungwa kutoka nchi
yake,” Amo 7:16-17. Hayo ndiyo yaliyomkuta Amazia kuhani kwa tendo lake la
kutetea uovu na udhalimu.
Ndugu
yangu, Mungu hachezewi wala hajaribiwi. Yatupasa mimi na wewe kuchunguza
mienendo yetu. Ikiwa sauti ya watu ni sauti ya Mungu, basi wayasemayo watu
yaliyomabaya juu yako na yangu, yatusaidie kufanya tafakari ya kina
kujisahihisha. Hakuna malaika watakaoshuka kutoka mbinguni na kukuambia kweli
hiyo tukijua kila mtu ni hekalu la Roho Mtakatifu, 1Kor 6:19, anayetuongoza
katika kweli.
Wapendwa wana wa Mungu, Yesu katika Injili ya leo
anadhihirisha amani na utulivu wa kweli anapoletewa mgojwa aliyepooza katika
kitanda mzegamzega. Kwa Yesu, watu
waliiona amani, utulivu, upendo, haki, na matumaini ya kweli. Kwa Yesu, watu
walikuwa na Imani kwani walipata faraja na utulivu wa kweli. Na kwa Yesu watu
waliona huruma na msamaha wa dhambi zao. Yesu kuona imani ya watu wale
walivyokuwa wakimtaabikia ndugu yao mgonjwa akamwambia yule aliyepoonza, “Jipe
moyo mkuu, mwanangu, umesamehewa dhambi zako,” Mt 9:2. Maneno haya ya Yesu ni
maneno yenye kubeba ubaba na umama ndani yake. Maneno haya ya Yesu siyo tu ya
uponyaji, bali ya kuumba na kuleta uzima
mpya. Tendo hili linawachukiza baadhi ya waandishi kwani walilitafsiri kama ni
kukufuru Mungu. Watu hawa hawaoni Umungu ndani ya Yesu. Kuwakata kimbelembele
chao, Yesu analiweka wazi jambo hili machoni mwao na kusema, “Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu
anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (amwambia yule mwenye kupooza) Ondoka,
ujitwike kitanda chako, uende nyumbani kwako,” Mt 9:6. Kwa maneno na msimamo
huu wa Yesu mbele ya waandishi hawa anadhihirisha mamlaka yake kamili, kwamba, “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika
cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3. Pamoja na mamlaka hayo yaliyotukuka, Yesu
alibaki kuwa mfano wa pekee katika ‘unyenyekevu na utii. Na “tena, alipoonekana
ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya
msalaba,” Flp 2:8. Huyu ndiye Yesu, na Huyu ndiye Mungu, Bwana wangu na yote
yangu. Amina!
Wapendwa katika Kristo, tendo alilolifanya Yesu la uponyaji
linakuwa kikolezo cha Imani, na ule mkutano unafunuliwa juu ya Mambo makuu ya
Mungu. “Makutano walipomwona, walishikwa na hofu,
wakamtukuza Mungu, aliyewapa watu amri ya namna hii,” Mt 9:8. Je, wewe ndugu
yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii, umefunuliwa jambo gani ambalo
waweza kumsifu Mungu? Ndugu yangu, nikuache na maneno haya mazito ya Mtakatifu
Paulo yanayoweza kutusaidia kuzama katika unyenyekevu. Kwanza, ni kukubali kufa
kila siku na Kristo na kwa sababu ya Kristo. Naye anasema, “ndugu, kwa huku kujisifu kwangu niliko nako juu yenu katika
Kristo Yesu Bwana wetu, ninakufa kila siku,” 1Kor 15:31. Ni kufa kila siku
katika ‘kweli, haki, upendo, na amani, kwa watu na kwa ajili ya watu na kwa
mapenzi ya Mungu. Pili, kujisifu katika kupambana na udhaifu wako. Kuyatambua
madhaifu yako na kujisahihisha kuelekea nuru ile ya kweli, yaani, “mkiwa
mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono
wa kuume wa Mungu,” Kol 3:1. Na kujisahihisha katika hali ya udhaifu Mtume
Paulo anasema, “Ni
nani aliye dhaifu, nisiwe dhaifu nami? Ni nani aliyekwazwa nami nisichukiwe? Ikinibidi kujisifu, nitajisifia mambo
ya udhaifu wangu. Mungu, Baba wa
Bwana Yesu, aliye mtukufu hata milele, anajua ya kuwa sisemi uongo,” 2Kor
11:29-31. Tulenge kila siku katika ukamilifu hata kama udhaifu upo.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Mwenende
kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila
kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu,” Kol 1:10
Tusali:-Ee
Mungu, ilikupendeza na ukaona inafaa tukuumba kama tulivyo wanadamu kwa sura na
mfano wako. Tujalie hofu yako ndani yetu ili tuushinde ubinadamu wetu na
kuifikia nuru yako. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario