miércoles, 29 de junio de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 13 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 13 YA MWAKA-C
Somo: Amo 7:10-17
Zab: 19:8, 9, 10, 11
Injili: Mt 9:1-8
Nukuu:
Ndipo Amazia, kuhani wa Betheli, akapeleka habari kwa Yeroboamu, mfalme wa Israeli, akisema, Amosi amefanya fitina juu yako kati ya nyumba ya Israeli; nchi haiwezi kustahimili maneno yake yote,” Amo 7:10 

Kwa maana Amosi asema hivi, Yeroboamu atakufa kwa upanga, na bila shaka Israeli atachukuliwa mbali, hali ya kufungwa, atoke katika nchi yake,” Amo 7:11 

 “Na tazama, wakamletea mtu mwenye kupooza, amelala kitandani; naye Yesu, alipoiona imani yao, alimwambia yule mwenye kupooza, Jipe moyo mkuu, mwanangu, umesamehewa dhambi zako,” Mt 9:2

Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (amwambia yule mwenye kupooza) Ondoka, ujitwike kitanda chako, uende nyumbani kwako,” Mt 9:6

TAFAKARI:Na kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na matumaini daima,” Isa 32:17 

Wapendwa wana wa Mungu, pasipo haki hapana amani, utulivu, na matumaini. Hata hivyo haki uendana na wajibu. Aliyetimiza wajibu wake anastahili haki yake kwa namna yoyote ile. Mfano: ni wajibu wangu kuwa raia mwema ikiwa ni pamoja na kulipa kodi kadiri ya utaratibu uliowekwa kisheri na kikatiba inayoakisi matakwa ya raia wenyewe. Kama hili limefanyika, basi nastahili kupata haki zangu kwa mujibu wa Katiba ambayo ndiyo dira na sheria mama. Na sheria hiyo Mama au Katiba, ndipo watu huamua namna wanavyotaka waongozwe, kuwajibika, na kuwajibishwa pale inapokuwa ndivyo sivyo. Fujo na machafuko utokea pale ambapo haki haitolewi licha ya wajibu kutimizwa.

Ila Mungu wetu aliye Amani anatutaka tuwe na amani na hili ndilo fumbo la uumbaji wetu, ‘kwa sura na mfano wake,’ Mwa 1:27. Penye fujo na machafuko Utukufu wa Mungu hufifishwa tu ila hatuwezi kuuondoa au kuutokomeza. Naye Mungu asema hivi, watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu,” Isa 32:18. Haki, utulivu, na amani havitolewi na mtu kutoka mfukoni mwake. Ni wajibu wa kila mtu/raia pale alipo kuhakikisha vinakuwepo. Wote waliopewa dhamana na umma yawapasa kusimamia hilo pasipo upendeleo na kwa mujibu wa Katiba husika, na siyo dhania binafsi kwa malengo binafsi au kikundi fulani cha waliojihalalishia haki hiyo. “Wabaya wanafanana na bahari iliyochafuka; maana haiwezi kutulia, na maji yake hutoa tope na takataka. Hapana amani kwa wabaya; asema Mungu wangu,” Isa 57:20-21

Chini ya utawala wa Mfalme Yeroboamu haki za watu zilikanyagwa. Mfalme hakupaswa kuguswa wala kukosolewa. Ilikuwa ni kosa kufanya hivyo. Kuhani Amazia alikuwa mtetezi na mtu wa karibu wa Mfalme Yeroboamu. Watu wote waliotaka kumkosoa mfalme walizimwa midomo au kuamuriwa kuikimbia nchi na kuishi uhamishoni. Ni katika mazingira haya Nabii Amosi anapata misukosuko kutoka kwa kuhani wa Betheli juu ya kumkosoa mfalme na kuonya tabia yake ya ukandamizaji. Ili kumnyamazisha Nabii Amosi, Amazia, kuhani wa Betheli, akapeleka habari kwa Yeroboamu, mfalme wa Israeli, akisema, Amosi amefanya fitina juu yako kati ya nyumba ya Israeli; nchi haiwezi kustahimili maneno yake yote,” Amo 7:10. Yaani, kwa maneno mengine, Amosi anashitakiwa kwa kosa la uchochezi. Ndugu yangu hapa ndipo tunapotakiwa kujua maana ya sauti ya kinabii.

Sauti ya kinabii ni sauti ya Mungu iliyojaa maono. Mungu uwafunulia watu wake na hasa wenye utulivu wa ndani, wenye uwezo wa kuliona jambo au hali kama lilivyo au ilivyo, na siyo kama walivyo. Ni msukumo wa ndani uliojaa hofu ya Mungu na kwa watu wa Mungu. Ni maono yaliyobeba kweli, haki, upendo, na amani. Nabii na unabii si kitu cha mkurupuko kama ilivyo ‘bendera fuata upepo.’ Na siyo utabiri kama ilivyo kwa wapiga ramli wenye kulenga hisia binafsi au za watu, bali ni kweli katika kweli, na haki katika haki.

Wapendwa wana wa Mungu, mwenye sauti hiyo ya unabii ni mwiba wa hatari palipojaa dhuluma na giza la uonevu. Watu wa mtindo huu kama alivyo Amosi Nabii, hawakoswi kusingiziwa yasiyo kweli na hata kuhalalishiwa makosa yasiyo kweli. Lengo ni kuwafunga midomo na kuwaangamiza. Mungu anaujumbe huu kwa wote wasimamao katika kweli na haki: Nyakati zao zitakuwa nyakati za kukaa imara; za wokovu tele na hekima na maarifa; kumcha Bwana ni hazina yake ya akiba. Angalia, mashujaa wao wanalia nje, wajumbe wa amani wanalia kwa uchungu.” Isa 33:6-7. Ni kwa namna hiyo Nabii Amosi anashitakiwa kwa Mfalme na kuhani Amazia, na kusema, Yeroboamu atakufa kwa upanga, na bila shaka Israeli atachukuliwa mbali, hali ya kufungwa, atoke katika nchi yake,” Amo 7:11. Na kama haikutosha,  Amazia akamwambia Amosi, Ewe mwonaji, nenda zako, ikimbilie nchi ya Yuda, ukale mkate huko, ukatabiri huko; lakini usitabiri tena huku Betheli; kwa maana ni mahali patakatifu pa mfalme, nayo ni nyumba ya kifalme,” Amo 7:12-13.

Amazia kuhani anamvika umungu Mfalme Yeroboamu. Jambo hili ni hatari sana machoni mwa Mungu. Mungu ndiye mwenye mastahili ya kuabudiwa na kuogopwa, Zab 15:11; 111:9, na siyo mwanadamu mwenye nyama na mifupa, na kifo kikiwa ndiyo rafiki yake wa karibu kama kilivyo kivuli chake kisichosema chochote bali ufuatana nacho daima. Pamoja na vitisho hivyo vya kuhani Amazia, havikuweza kuufunga mdomo wa Nabii Amosi. Ndipo Amosi akajibu akamwambia Amazia, Mimi sikuwa nabii, wala sikuwa mwana wa nabii; bali nalikuwa mchungaji, na mtunza mikuyu; naye Bwana akanitwaa, katika kufuatana na kundi; Bwana akaniambia, Enenda uwatabirie watu wangu Israeli,” Amo 7:14-15. Nabii Amosi anajua wazi kabisa hayafanyi hayo kwa malengo yake binafsi, bali anawakilisha ujumbe wa Mungu kwa watu wake. Hivyo Amosi asiti kuzitema cheche za moto wa kweli na haki kutoka kwa Mungu. Naye alikuwa na ujumbe huu wa Mungu kwa Amazia kuhani, Basi, sasa lisikie neno la Bwana; Wewe unasema, Usitabiri juu ya Israeli, wala usitoe neno lako juu ya nyumba ya Isaka; kwa hiyo, Bwana asema hivi, Mke wako atakuwa kahaba mjini, na wana wako na binti zako wataanguka kwa upanga, na shamba lako litagawanywa kwa kamba; na wewe mwenyewe utakufa katika nchi iliyo najisi; na bila shaka Israeli atachukuliwa mbali hali ya kufungwa kutoka nchi yake,” Amo 7:16-17. Hayo ndiyo yaliyomkuta Amazia kuhani kwa tendo lake la kutetea uovu na udhalimu.

Ndugu yangu, Mungu hachezewi wala hajaribiwi. Yatupasa mimi na wewe kuchunguza mienendo yetu. Ikiwa sauti ya watu ni sauti ya Mungu, basi wayasemayo watu yaliyomabaya juu yako na yangu, yatusaidie kufanya tafakari ya kina kujisahihisha. Hakuna malaika watakaoshuka kutoka mbinguni na kukuambia kweli hiyo tukijua kila mtu ni hekalu la Roho Mtakatifu, 1Kor 6:19, anayetuongoza katika kweli.

Wapendwa wana wa Mungu, Yesu katika Injili ya leo anadhihirisha amani na utulivu wa kweli anapoletewa mgojwa aliyepooza katika kitanda mzegamzega.  Kwa Yesu, watu waliiona amani, utulivu, upendo, haki, na matumaini ya kweli. Kwa Yesu, watu walikuwa na Imani kwani walipata faraja na utulivu wa kweli. Na kwa Yesu watu waliona huruma na msamaha wa dhambi zao. Yesu kuona imani ya watu wale walivyokuwa wakimtaabikia ndugu yao mgonjwa akamwambia yule aliyepoonza, “Jipe moyo mkuu, mwanangu, umesamehewa dhambi zako,” Mt 9:2. Maneno haya ya Yesu ni maneno yenye kubeba ubaba na umama ndani yake. Maneno haya ya Yesu siyo tu ya uponyaji, bali ya kuumba  na kuleta uzima mpya. Tendo hili linawachukiza baadhi ya waandishi kwani walilitafsiri kama ni kukufuru Mungu. Watu hawa hawaoni Umungu ndani ya Yesu. Kuwakata kimbelembele chao, Yesu analiweka wazi jambo hili machoni mwao na kusema, Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (amwambia yule mwenye kupooza) Ondoka, ujitwike kitanda chako, uende nyumbani kwako,” Mt 9:6. Kwa maneno na msimamo huu wa Yesu mbele ya waandishi hawa anadhihirisha mamlaka yake kamili, kwamba, Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3. Pamoja na mamlaka hayo yaliyotukuka, Yesu alibaki kuwa mfano wa pekee katika ‘unyenyekevu na utii. Na “tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba,” Flp 2:8. Huyu ndiye Yesu, na Huyu ndiye Mungu, Bwana wangu na yote yangu. Amina!

Wapendwa katika Kristo, tendo alilolifanya Yesu la uponyaji linakuwa kikolezo cha Imani, na ule mkutano unafunuliwa juu ya Mambo makuu ya Mungu. Makutano walipomwona, walishikwa na hofu, wakamtukuza Mungu, aliyewapa watu amri ya namna hii,” Mt 9:8. Je, wewe ndugu yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii, umefunuliwa jambo gani ambalo waweza kumsifu Mungu? Ndugu yangu, nikuache na maneno haya mazito ya Mtakatifu Paulo yanayoweza kutusaidia kuzama katika unyenyekevu. Kwanza, ni kukubali kufa kila siku na Kristo na kwa sababu ya Kristo. Naye anasema, “ndugu, kwa huku kujisifu kwangu niliko nako juu yenu katika Kristo Yesu Bwana wetu, ninakufa kila siku,” 1Kor 15:31. Ni kufa kila siku katika ‘kweli, haki, upendo, na amani, kwa watu na kwa ajili ya watu na kwa mapenzi ya Mungu. Pili, kujisifu katika kupambana na udhaifu wako. Kuyatambua madhaifu yako na kujisahihisha kuelekea nuru ile ya kweli, yaani, “mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu,” Kol 3:1. Na kujisahihisha katika hali ya udhaifu Mtume Paulo anasema, Ni nani aliye dhaifu, nisiwe dhaifu nami? Ni nani aliyekwazwa nami nisichukiwe? Ikinibidi kujisifu, nitajisifia mambo ya udhaifu wangu. Mungu, Baba wa Bwana Yesu, aliye mtukufu hata milele, anajua ya kuwa sisemi uongo,” 2Kor 11:29-31. Tulenge kila siku katika ukamilifu hata kama udhaifu upo.

Tumsifu Yesu Kristo! 

Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu,” Kol 1:10


Tusali:-Ee Mungu, ilikupendeza na ukaona inafaa tukuumba kama tulivyo wanadamu kwa sura na mfano wako. Tujalie hofu yako ndani yetu ili tuushinde ubinadamu wetu na kuifikia nuru yako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario