ALHAMISI WIKI YA 10 YA MWAKA-C
Somo: 1Fal 18:41-46
Zab: 65:10, 11, 12-13
Injili: Mt 5:20-26
Nukuu:
“Ikawa, muda si muda, mbingu zikawa nyeusi kwa mawingu na
upepo, ikanyesha mvua nyingi. Ahabu akapanda garini, akaenda zake Yezreeli,”
1Fal 18:45
“Mkono
wa Bwana ulikuwa juu ya Eliya; akajikaza viuno, akapiga mbio mbele ya Ahabu mpaka
kuiingia Yezreeli,” 1Fal 18:46
“Maana
nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo,
hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni,” Mt 5:20
“Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya
kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu
yako, kisha urudi uitoe sadaka yako,” Mt 5:23-24
“Patana
na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije
akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani,” Mt
5:25
TAFAKARI: “Haki yenu isipozidi hiyo haki ya
waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.”
Wapendwa katika Kristo,
Injili yetu ya leo yatutaka tuyapime matendo yetu vyema hasa katika mizania ya
kusamehe na kusamehewa. Yesu katika hili anatoa angalizo kubwa na kusema,
"haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia
kamwe katika ufalme wa mbinguni," Mt 5:20. Mafarisayo na waandishi
walijihesabia haki kuwa ni watu wema, na ndiyo kipimo cha kweli. Ndugu yangu,
Mungu pekee ndiye hutuhesabia haki, tena si kwa matakwa yetu, bali kwa matakwa
yake kwa sababu Yeye tu ndiye HAKI. Sisi binadamu tunashiriki tu ukamilifu wa
Mungu kwa kuwezeshwa naye. Mafarisayo na waandishi walijihesabia haki na kuwa
miungu watu. Huu ni upofu uliopitiliza. Kuwajua vizuri Mafarisayo na Waandishi
nakualika usome sura yote ya 23 ya mwinjili Mathayo. Ni kwa sababu hiyo Yesu
anatoa angalizo kwanza kama kweli tunataka uponyaji, lazima kusamehe kama hatua
muhimu na mizania ya kusamehewa.
Kusamehe ni amri kama
kweli na sisi tunataka kusamehewa. Sala ya ‘Baba yetu’ imeliweka jambo hili
wazi kama sharti la upatanisho na Mungu. Cha ajabu sala hii tunaisali wengine
kila siku na kila mara kwa siku, ila bado kusamehe ni shiiida! Je, utaponywaje
kama tatizo lako ni kuvunjika mguu, ila "P.O.P" umefunga shingoni?
Mbona kila siku unatibu ugonjwa usioumwa kwa dawa tofauti? Kwa nini inakuwiya
vigumu kusamehe na kupatana na ndugu yako? Je, wewe ni mkamilifu sana? Unatofauti
gani na mafarisayo na waandishi wanachukuwa nafasi ya Mungu kwa kujihesabia
haki?
Wapendwa
wana wa Mungu, ukitaka sala yako, na maombi yako yapate kibali mbele ya Mungu,
jipatanishe wewe mwenyewe, wewe na uliyekosana naye, na pia wewe na Mungu. Hivyo
“basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na
huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako,
iache sadaka yako mbele ya
madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako,”
Mt 5:23. Wengi na hasa wale tuliokosewa hupenda kuyarefusha mambo sana, na
wakati mwingine tungependa tunyunyuziwe ubani kwa cheteso cha dhahabu ili tuwe
tayari kwa kuyaongelea yale yaliyotutatiza.
Ila
baraka na neema hutujia pale tunapokuwa na uhusiano mzuri na wenzetu,
mazingira, na Mungu Muumba wetu. Nabii
Eliya ni mfano wa kweli hii kama tulivyosikia somo letu la leo. Pamoja na ukame
ulioikumba nchi, Mungu anawarudishia tena uhai kwa kuinyeshea nchi mvua, “Naye
Eliya akamwambia Ahabu, Haya! Inuka, ule, unywe; kwani pana sauti ya mvua
tele,” 1Fal 18:41. Alisemalo Eliya ni uthibitisha wa ukaribu wake, na urafiki
wake na Mungu. Hana shaka lolote juu ya Mungu kwani hakuwahi kuuvunja uhusiano
wake na Mungu. Hivyo “Ikawa, muda si muda,
mbingu zikawa nyeusi kwa mawingu na upepo, ikanyesha mvua nyingi. Ahabu
akapanda garini, akaenda zake Yezreeli,” 1Fal 18:45. Furaha ya Mungu kwetu ni
kuuishi upendo wa kweli na kuwa na mahusiano mazuri kati yetu na viumbe vyake
vingine. Mahusiano haya mazuri huufunua utukufu wake Mungu. Nabii Eliya ni
uthibitisho huo wa mahusiano mazuri na Mungu. “Mkono wa Bwana ulikuwa juu ya Eliya; akajikaza
viuno, akapiga mbio mbele ya Ahabu mpaka kuiingia Yezreeli,” 1Fal 18:46. Maisha
kama safari, yatupasa yatupasa kuulinda uhusiano huo na ndugu zetu, mazingira
na Mungu kadiri tunavyosafiri hadi mwisho wa safari yetu hapa duniani.
Ni kwa mantiki hiyo
agizo la Yesu lakutaka wewe na mimi, "patana na ndugu yako uwapo naye
njiani," Mt 5:25. Maana yake ni nini? Kupatana
na ndugu yako mngali njiani ni kufanya juu chini kupatana na ndugu yako angali
yu hai. Msivute muda pasipo sababu. Kengele ikishagongwa hakuna tena pa
kujitetea. Maapizo na laana hazikusaidii chochote. Unazidi jizibia riziki zako
bure na baraka kutoka kwake mwenyezi Mungu. Unaposamehe unajiponya na kumponya
mwenzako pia. "Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi
wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi," Yoh 13:35.
Wapendwa wana wa Mungu,
ibada na sadaka zetu kwa Mungu huwa safi na za kumpendeza Mungu pale tunapokuwa
na amani ya kweli ndani mwetu, na ndugu zetu, mazingira yetu, na Muumba wetu. “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku
ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya
madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka
yako,” Mt 5:23-24. Amani hii ni pale unapokuwa tayari kupatana na kusamehe bila
kipimo.
Wapendwa
wana wa Mungu, ukitaka sala yako, na maombi yako yapate kibali mbele ya Mungu,
jipatanishe wewe mwenyewe, wewe na uliyekosana naye, na pia wewe na Mungu. Wengi
na hasa wale tuliokosewa hupenda kuyarefusha mambo sana, na wakati mwingine
tungependa tunyunyuziwe ubani na kupigiwa cheteso cha dhahabu ili tuwe tayari
kwa kuyaongelea yale yaliyotutatiza.
Wengi
tumeshuhudia watu hawapendi kupatana na kuishia kuapizana pasipo sababu. Wapo
wengine hata baada ya kuzidiwa wakiwa kitandani karibu ya kufa wanapoomba
upatanisho na ndugu yake kunakuwa na mkwamo bila mwitikio wowote na mwisho mtu
huyo hufariki katika hali ya majonzi
makubwa. Hivi unajisikiaje ndugu yako kufa akikuomba upatane naye nawe kwa
kiburi chako hukusikia na hatimaye ndugu yako anafariki? Ndugu yangu, “Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja
naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka
kwa askari, ukatupwa gerezani,” Mt 5:25. Je, kwa kutokupatana na ndugu yako
angali hai, utajibu nini mbele ya Kadhi-Mungu mwisho wa siku?
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Patana
na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije
akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani,” Mt
5:25
Tusali:-Ee
Yesu Mwema na Mungu uliye Huruma, Msamaha na Upendo; tujalie Moyo wa kusamehe
muda wote tusafiripo hapa duniani. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario