lunes, 13 de junio de 2016

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 11 YA MWAKA-C

JUMATATU WIKI YA 11 YA MWAKA-C
Somo: 1Fal 21:1-16
Zab: 5:2-3, 5-6,-7
Injili: Mt 5:38-42
Nukuu:
Lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili,” Mt 5:39 

 “Nabothi akamwambia Ahabu, Bwana apishe mbali nikupe wewe urithi wa baba zangu,” 1Fal 21:3

 “Basi, akaandika nyaraka kwa jina la Ahabu, akazitia muhuri yake, akazipeleka zile nyaraka kwa wazee, na kwa watu wenye nguvu waliokuwa katika mji wake, waliokaa pamoja na Nabothi,” 1Fal 21:8 

 “Wale wazee wa mji wake, na walio wenye nguvu waliokaa mjini mwake, wakafanya kama Yezebeli alivyowaagiza, kama ilivyoandikwa katika nyaraka alizowapelekea,” 1Fal 21:11 

Na hao watu wawili, watu wasiofaa, wakaingia, wakaketi mbele yake; wale watu wasiofaa wakamshuhudia Nabothi mbele ya watu, wakasema, Nabothi amemtukana Mungu na mfalme. Ndipo wakamchukua nje ya mji, wakampiga kwa mawe hata akafa,” 1Fal 21:13

TAFAKARI:Msishindane na mtu mwovu.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Bwana wetu Yesu Kristo anatushauri kwa msisitizo tusishindane na mtu mwovu. Ukweli ni kwamba kitokacho kwa Mungu ni chema na kama kilivyo kina umilele kwa sababu Mungu wetu ni Mtakatifu, Mkamilifu, na Wamilele. Ni kwa mantiki hii kwamba hakuna mti mzuri uzaao matunda mabaya, wala mti mbaya uzaao matunda mazuri; kwa kuwa kila mti hutambulikana kwa matunda yake; maana, katika miiba hawachumi tini, wala katika michongoma hawachumi zabibu,” Lk 6:43-44. Wito wa Yesu kwetu wa tusishindane na mtu mwovu unalenga katika dhana nzima ya uovu, yaani, uovu kama ulivyo hauna umilele. “Msishindane na Mtu mwovu,” badala yake ni kuliweka tumaini lote kwa Bwana ambaye kwake ndiko kwenye chanzo halisi cha wema na jema, haki, na kweli. Ni kumcha Bwana na kuuchukia uovu. Hivyo kumcha Bwana ni kuchukia uovu; Kiburi na majivuno, na njia mbovu, Na kinywa cha ukaidi pia nakichukia,” Mit 8:13.

Ndugu yangu, uovu kwa wingi wake hauna ‘umilele.’ Kama umilele ni maisha ya Utukufu wa Mungu wetu, uovu ambao kutokuwa na uzuri/mafaa, ni dhahiri kwenye umilele huo (Utukufu wa Mungu) hakuna uovu. Uovu ni swala la muda tu. Kwa maana nyingine haki lazima itawale kuona kwetu, kufanya kwetu, na kuhukumu kwetu. Kwani Hazina za uovu hazifaidii kitu; Bali haki huokoa na mauti,” Mit 10:2. Wapo wengi kati yetu huishi kwa dhuluma au kuwezeshwa kwa dhuluma, au vyote viwili kwa wakati mmoja. Ndugu yangu, tenda haki kwa kila mmoja apitaye katika mikono yako nawe utalipwa mema. Uovu ni andaki la dhambi, na aliye zama katika andaki hili la dhambi ni vigumu kuubaini uovu wake kwa sababu hakuna nuru tena. Uovu huwaandamia wenye dhambi; Bali mwenye haki atalipwa mema,” Mit 13:21. Ni wazi lazima kuuchukia uovu, na kutenda haki.

Kwa nini basi Yesu anatuambia tusishindane na mtu mwovu? Kujua ukweli huu yatupasa kuutafakari wasifu wa mtu mwovu. Ushirika na mtu mwovu au ushindani na mtu mwovu mavuno yake ni udhalimu. Njia salama ni kumwepa mtu mwovu kwa kuchukia tabia yake hiyo ili ajirudi. Na kwa sababu hiyo, usitie mkono wako pamoja na mwovu, kuwa shahidi wa udhalimu,” Kut 23:1b. Tabia hii ya mtu mwovu humtenga na Mungu kama asemavyo, kwa kuwa mimi sitamhesabia haki yeye aliye mwovu,” Kut 23:7c. Hivyo kama wewe ni kiongozi hapo ulipo,  kwa nafasi yako wewe ni msimamizi wa kweli na haki kama Mungu anavyoamuru, “basi, usikie mbinguni, ukatende, ukawahukumu watumwa wako; ukimlipiza mwovu, kumpatilizia njia yake kichwani; ukamfanyie haki mwenye haki, ukimjalia kwa kadiri ya haki yake,” 2Nya 6:23. Kiongozi asiyefanya hili, bali elewa wazi wale waliochini yake utawaliwa na hofu na ugumu wa maisha. Je, kama zipo mamlaka za kuwajenga hofu kwa watu tukae kimya kama makaburi? La hasha!

Kukaa kimya kama kaburi kwa kuogopa kuchukiwa  katika vita dhidi ya uovu na mtu mwovu ni kujivika aibu yako mwenyewe. Ila kuishinda hali hii ni kuushinda uovu na mtu mwovu. Hivyo hao wakuchukiao watavikwa aibu; Nayo hema yake mwovu haitakuwako tena,” Ayu 8:22. Kadiri ya historia ya ulimwengu huu na watu wake, hasa watu waovu, mwisho wao hauna mema. Kwa nafasi wanazokuwa nazo na kuzitumia vibaya hasa kukataa kweli na kuikandamiza haki, kilio cha wanyonge huamsha hasira ya Mungu. Hakuna mwenye hati miliki ya ulimwengu huu, na wengine kubaki kama wasindikizaji tu. Na hii ndiyo sehemu ya mtu mwovu kwa Mungu, Na urithi wa hao waoneao, waupokeao kwa Mwenyezi. Watoto wake wakiongezeka ni kwa upanga; Na wazao wake hawatashiba chakula,” Ayu 27:13-14. Mungu huweza ruhusu kucheleweshwa kwa haki ya watu na yule mwovu kwa nia ya kumpa nafasi mwovu huyo kujirudi na kutenda haki, bali Mungu hawezi kufumbia macho kuchezewa milele upatikanaji wa haki hiyo kwa watu wake. Kila mmoja wetu ndani yake anayo chapa ya Mungu, Mwa 1:27. Je, mtu mwovu hupata wapi kiburi chake?

Tabia ya mtu mwovu huamini utetezi wa nguvu zake na kuiondoa kabisa hofu ya Mungu ndani yake. Ni kuishi kwa kujiamini kuliko pindukia. Huku ni kuiasi ile kweli iliyo ndani yako, yaani, ‘umeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu,’ Mwa 1:27. Na kwa sababu hiyo, Kuasi kwake yule mwovu hunena moyoni mwake, Hakuna hofu ya Mungu mbele ya macho yake,” Zab 36:1. Pamoja na ujasiri huu usiokuwa na mwelekeo wa mtu mwovu, Bwana hataiacha nafsi ya mwenye haki ife na njaa; Bali tamaa ya mtu mwovu huisukumia mbali,” Mit 10:3. Hakika mwisho wa mtu mwovu hauna heri! Mtu mwovu hupata mshahara wa udanganyifu; Apandaye haki ana thawabu ya hakika,” Mit 11:18. Katika hali kama hii ni vigumu kumshauri mtu mwovu lile lililo jema kwa sababu hupenda kusikia yale ayapendayo na yaliyoujaza moyo wake. Mtu mwovu hataki neno ila kuasi tu,” Mit 17:11a. Hali na mazingira haya ya mtu mwovu kutamalaki katika uovu wake, na mtu mwenye haki kukandamizwa na kile kilicho kweli na haki yake, inatupeleka kuelewa vizuri uongozi wa mfalme Ahabu na mkewe Yezebeli kwa upande mmoja, na Nabothi kwa upande mwingine kama mdhulumiwa kwenye haki.

Kosa na sababu ya kuuwa kwa Nabothi ni kuitetea haki yake kama urithi kutoka kwa baba zake, yaani, shamba lile la mizabibu lililokuwa karibu na nyumba ya mfalme Ahabu, 1Fal 21:2.Nabothi akamwambia Ahabu, Bwana apishe mbali nikupe wewe urithi wa baba zangu,” 1Fal 21:3. Nabothi hakuwa na lugha nyingine zaidi ya hiyo kwa sababu kwa Myahudi vitu vitatu ndivyo vilivyo ulinda uhai wake. Navyo ni ardhi, Torati kama neno na amri ya Mungu, ilikwa ni pamoja na Hekalu kama sehemu ya kumsifu Mungu na kumtolea shukrani, na jambo la mwisho ni uongozi bora. Kwa hali hii tunaona wazi mambo mawili muhimu yanatikiswa, yaani, ardhi na kutokuwa na uongozi wa haki. Kwa vile mfalme Ahabu aliiruhusu dhuluma ndani ya moyo wake, neno lile la Nabothi lilimnyima raha na usingizi kabisa, akajilaza kitandani pake, akageuza uso wake, akakataa kula,” 1Fal 21:4b. Je, Ahabu atafikiri zaidi kama kiongozi na kuzuia umwagaji wa damu? La hasha!

Kwa vile mtu mwovu hukataa ushauri wa kweli, na badala yake hupenda kusikia yale yaliyoujaza moyo wake, mke wake anatumia nafasi hiyo kuiondoa huzuni aliyokuwa nayo mume wake, yaani, mfalme Ahabu. Yezebeli mke wa mfalme Ahabu anamwamasisha mumewe kwa kusema, Je! Sasa wewe unaumiliki ufalme wa Israeli? Ondoka, ule chakula, moyo wako ufurahi; mimi nitakupa shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli,” 1Fal 21:7. “Sasa wewe unaumiliki ufalme wa Israeli,” maneno haya ni maneno ya uchokozi na chokonozi. Ni sawa na kusema, “iweje ushindwe katika hili ilihali wewe ni mfalme wa Israeli?” Leo tungeweza kuyaweka maneno hayo katika mazingira yetu na kusema, “Je, wewe siye Rais wa Tanzania?” Na tungeweza kwenda mbele zaidi na kusema  kama alivyotaka kusikia mfalme; “iweje ushindwe katika hili ilihali serikali hii ni yako?” Hakika washauri kama Yezebeli ni hatari katika swala la kusimamia kweli na haki kama ilivyo.

Kwa kumfurahisha mfalme na kuirudisha furaha yake, Yezebeli mke wa Ahabu mfalme akaandika nyaraka kwa jina la Ahabu, akazitia muhuri yake, akazipeleka zile nyaraka kwa wazee, na kwa watu wenye nguvu waliokuwa katika mji wake, waliokaa pamoja na Nabothi,” 1Fal 21:8. Mnyonge anapodhulumiwa, tena kwa wale ambao walitakiwa kumtetea, ni vigumu sana kujinasua katika janga hilo. Kila njia na mbinu usukwa ili hazma mbovu na dhuluma itimizwe. Na ndivyo ilivyokuwa kwa mwenye haki Nabothi. Nyaraka ile iliyogushiwa na Yezebeli kwa wazee iliwataka wazee wale kuwainua watu wawili na kuandaa ushahidi wa uongo dhidi ya Nabothi, ili wamshitaki, na kumshuhudia, kunena, Umemtukana Mungu na mfalme. Kisha mchukueni nje, mkampige kwa mawe, ili afe,” 1Fal 21:10. Je, leo tupo tofauti na mazingira kama haya yaliyomkuta Nabothi? Wapo wengi kati yetu wamehukumiwa kwa kesi ya kugushi kama hizi, na bado zipo keshi nyingi za mtindo huu mitaani mwetu. Nani basi wa kutunasua katika mazingira haya? Wale wazee wenye nguvu katika jamii bila kujua na kuchunguzi kwa kina wito ule, nao wanaingia mkenge na wakafanya kama Yezebeli alivyowaagiza, kama ilivyoandikwa katika nyaraka alizowapelekea,” 1Fal 21:11. Ndugu yangu, penye uovu hata wenye ufahamu siyo wakutegemewa kabisa. Hapa ndipo ule usemi huwa kweli kwamba, “machozi ya samaki huenda na maji.”

Uovu una tabia moja. Unapousukuma huendelea kushirikisha wengi na mengi, na mwisho wa siku ni mauti. Na hao watu wawili, watu wasiofaa, wakaingia, wakaketi mbele yake; wale watu wasiofaa wakamshuhudia Nabothi mbele ya watu, wakasema, Nabothi amemtukana Mungu na mfalme. Ndipo wakamchukua nje ya mji, wakampiga kwa mawe hata akafa,” 1Fal 21:13. Ni kweli kwamba Nabothi hakupigwa mawe na wale watu wawili watoa ushahidi wa uongo juu yake. Ni mara ngapi tunakutana na matukio ya kuchomwa watu barabarani nasi kwa kutokujua kilichojiri tunashiriki moja kwa moja katika uovu huo? Je, tunatoa hata muda kidogo kuhoji kwa nini mambo yamekuwa kama yalivyo? Je, ni kweli wanaopatwa na matukio kama hayo wanastahili kufa katika mtindo kama huo? Hata kama kuna sababu, je ni halali kuutoa uhai wa binadamu mwenzako kwa mtindo huo? USIUE! (Kut 20:13, Kumb 5:17, Mt 5:21; 19:18; Mk 10:19; Lk 18:20; Rum 13:9, na Yak 13:9)

Msukumwa na uovu hana mshipa wa aibu, bali ufurahia uovu wake. Hivyo utekelezaji wa tukio lile linamfikia Yezebeli. Wakampelekea Yezebeli habari, wakasema, Nabothi amepigwa kwa mawe, amekufa,” 1Fal 21:14. Yezebeli bila shaka anafarijika kwa tendo lile kwa sababu limekwenda kama alivyolipanga. Hivi ni vifo vya kimfumo ambavyo si ajabu kuvisikia au kuviona katika jamii yetu leo. Tunachoshuhudia ni hili; ‘Sauti usikika kwa kishindo, watu wanapoteza uhai na mali zao, na mwisho kimya kama hakijatokea kitu.’ Hali na matukio kama haya ni faraja tu kwa mtu mwovu, tena faraji hiyo ni kwa muda mfupi tu. Ni kwa mantiki hiyo, Yezebeli aliposikia ya kwamba Nabothi amepigwa kwa mawe na kufa, Yezebeli akamwambia Ahabu, Inuka, ulitamalaki shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli, alilokataa kukupa kwa fedha, maana Nabothi hako hai, lakini amekufa,” 1Fal 21:15. Kwa vile mtu mwovu hupenda kuyasikia yaliyo ndani ya moyo wake tu, tena yaliyomaovu, Ahabu aliposikia ya kwamba Nabothi amekufa, akaondoka, alitelemkie shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli, ili alitamalaki,” 1Fal 21:16. Je, damu ya Nabothi na haki yake itapotea bure? La hasha! Mungu wetu hayupo usingizini kama asemavyo,  “mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu,” Isa 55:8

Wapendwa katika Kristo ni wito kwako na kwangu kwamba tuwe watu wa kusimama katika kweli na haki mara zote. Tuuchukie uovu kwa sababu hufifisha nuru ya Mungu ndani mwetu. Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote,” Rum 12:17. Tutende haki, na tuanze pale tulipo. Tuwe watetezi katika kweli na haki kwa wanyonge na wale wote wanaominywa haki zao. Hivyo neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema wanaosikia,” Efe 4:29. Huku ndiko kuwa nabii kwa wakati wako.

Tusifu Yesu Kristo!

Nabothi akamwambia Ahabu, Bwana apishe mbali nikupe wewe urithi wa baba zangu,” 1Fal 21:3


Tusali:-Ee Yesu uliye haki na kweli yetu, tutumie vyema kama vyombo vyako vya kweli na haki pale tulipo kama ushuhuda hai kwa wote. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario