sábado, 4 de junio de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 10 YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 10 YA MWAKA-C
Somo I: 1Fal 17:17-24
Zab: 30:1, 3-5, 10-12 (K) 1
Somo II: Gal 1:11-19
Injili: Lk 7:11-17
Nukuu:
Akamwambia Eliya, Nina nini nawe, Ee mtu wa Mungu? Je! Umenijia ili dhambi yangu ikumbukwe, ukamwue mwanangu?” 1Fal 17:18

Akamwomba Bwana, akanena, Ee Bwana, Mungu wangu, je! Umemtenda mabaya mjane huyu ninayekaa kwake hata kumfisha mwanawe,” 1Fal 17:20 

 “Bwana akaisikia sauti ya Eliya; na roho ya mtoto ikamrudia, akafufuka,” 1Fal 17:22 

 “Kwa maana, ndugu zangu, injili hiyo niliyowahubiri, nawajulisha ya kuwa siyo ya namna ya kibinadamu,” Gal 1:11

Kwa kuwa sikuipokea kwa mwanadamu wala sikufundishwa na mwanadamu, bali kwa ufunuo wa Yesu Kristo,” Gal 1:12

 “Bwana alipomwona alimwonea huruma, akamwambia, Usilie,” Lk 7:13 

Akakaribia, akaligusa jeneza; wale waliokuwa wakilichukua wakasimama. Akasema, Kijana, nakuambia, Inuka,” Lk 7:14

Yule maiti akainuka, akaketi, akaanza kusema. Akampa mama yake,” Lk 7:15 

TAFAKARI: “Kila jambo linakusudi lake, litazame kwa jicho la imani, na wala usiruhusu manung’uniko na kujihukumu. Tazama tumaini lililopo mbele yako.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya kumi ya Mwaka ‘C’ wa Kanisa. Kwa namna ya pekee  tunaalikwa kuwa na mtazamo chanya pale tunapokutana na changamoto za imani. Masomo yetu yote matatu ya leo yanatuelekeza katika fundisho hilo. Ukweli ni kwamba kila jambo lina kusudi lake, litazame kwa jicho la imani, na wala usiruhusu manung’uniko na kujihukumu pale mambo yanapokwenda ndivyo sivyo. Tazama mara zote tumaini lile lililopo mbele yako. Tusomapo masomo ya leo tunapata mifano mitatu ya watu waliotazama tumaini lililopo mbele ya maisha yao. Watu hawa ni Mama Mjane yule wa Sarepta, IFal 17:9, Mtume Paulo wa Tarso, mji wa Kilikia, Mdo 22:3, na mwisho ni Mama yule wa mji wa Naini aliyefiwa na mwanaye wa pekee, Lk 7:11-12. Watu hawa na matukio yao kiimani yanatufundisha kuishi kwa tumaini pale tunapokumbana na sintofahamu katika maisha.

Baada ya mateso na mahangaiko mengi nyikani, ikiwa ni pamoja na kukata tamaa ya kuishi, Nabii Eliya kwa mwongozo wa Mungu, 1Fal 17:9, anapata ufadhili na kukirimiwa na mwanamke yule mjane wa Sarepta. Mama huyu alijaliwa kuwa na mtoto mmoja tu wa pekee. Hata pamoja na ukarimu wa familia hii jambo la ajabu linatokea, yaani, katika mazingira yasiyo ya kawaida mtoto huyu anafariki. Tendo hili ni uchungu na huzuni kubwa kwa mama huyu majane, na fedheha kubwa kwa Eliya. Ni wazi kama binadamu, na akiyatazama mateso yake ya huko nyuma, Eliya alijiuliza ‘kwa nini haya yote yanitokee mimi?’ Kwa upande mwingine mjane huyu alipatwa na mashaka juu ya mgeni wake, yaani, Eliya. Akamwambia Eliya, Nina nini nawe, Ee mtu wa Mungu? Je! Umenijia ili dhambi yangu ikumbukwe, ukamwue mwanangu?” 1Fal 17:18. Ni dhahiri swali hili lilimsononesha sana Eliya aliye kirimiwa kwa upendo mkubwa katika familia hii, ambayo ilikuwa tayari kushikiri kile kidogo walichokuwa nacho, 1Fal 17:12-13. Pamoja na huzuni hii, bado Eliya aliyaweka matumaini yake kwa Mungu. Eliya Akamwomba Bwana, akanena, Ee Bwana, Mungu wangu, je! Umemtenda mabaya mjane huyu ninayekaa kwake hata kumfisha mwanawe,” 1Fal 17:20. Eliya hakuanza kumtafuta mchawa kuhusu kifo kile, ila machozi, huzuni na fedheha ile aliipeleka mbele ya Mungu.

Ndugu yangu, Mungu upatikana pale tunapo mtafuta pasipo shaka na kwa nia na moyo thabiti, Isa 55:6. Hivyo Eliya  “Akajinyosha juu ya mtoto mara tatu, akamwomba Bwana, akanena, Ee Bwana, Mungu wangu, nakusihi, roho ya mtoto huyu imrudie ndani yake tena,” 1Fal 17:21. Kwa tumaini hili alilokuwa nalo Eliya, Mungu hakukawia kujibu ombi lake, na kumwondolea fedheha ile ugenini. Hapa Mungu anadhihirisha uwepo wake na kutowatupa wale wamgemeano na kumwamini pasipo shaka. Na Bwana akaisikia sauti ya Eliya; na roho ya mtoto ikamrudia, akafufuka,” 1Fal 17:22. Ni fundisho kwetu pia kwamba upatwapo na tatizo usiishie kulalama tu, bali mwambie Mungu ‘anataka kukufundisha nini kutokana na tatizo hilo.’ Hivyo omba kwa Mungu nguvu na uwezo wa kutatua tatizo hilo. Hapa ndipo tuwezapo kuliona tatizo katika mwono na jicho la Mungu. 

Wapendwa wana wa Mungu, fudisho kubwa la tukio hili lipo kwa Eliya mwenywe, mwanamke mjane, na kwetu sisi. Kwa mwanamke mjane anaelewa na kuamini nguvu za Mungu kupitia mtumishi wake Eliya. “Mwanamke akamwambia Eliya, Sasa najua ya kuwa wewe ndiwe mtu wa Mungu, na ya kuwa neno la Bwana kinywani mwako ni kweli,” 1Fal 17:24. Kwa uthibitisho huo, Eliya pia anatambua upendo wa Mungu kwake, na kamwe Mungu hawezi kumtupa hata akiwa katika shida za mtindo gani. Tumaini halisi na lenye uhakika ni kwake Mungu tu. Nasi tunafundishwa kumwelekea Mungu hata pale tunapopatwa na hisia mbaya kwa wale tuliojitoa kwao na mara kuona kama ndiyo sababu ya mateso yetu. Swali la kujiuliza katika sintofahamu kama hiyo hi hili: Je, ‘Mungu wataka kunifundisha nini katika hiki nisichokifahamu vizuru?’ Na mwisho yatupasa kuliweka tumaini lote kwake Mungu, kama asemavyo Mtume Paulo; Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili,” 1Kor 10:13. Mungu hawezi kutugeuzia kisogo tunapomtumainia.

Mtu wa pili anayetufundisha tumaini la kweli pale tupatwapo na sintofahamu nyingi katika maisha ni Mtume Paulo. Mtume Paulo hakuwa na historia nzuri katika maisha yake kabla ya kuongoka. Bila shaka nawe pia ukiitazama historia yako na hayo yanayokutokea leo unakata tamaa na kujihukumu kila kukicha. Tazama tumaini lililo mbele yako, na hasa ukitazama historia ya Mtume Paulo na kuongoka kwake. Katika hili, Mtume Paulo mwenyewe anatusimulia kwa ufupi historia ya maisha yake. Naye anasema,  Mimi ni mtu wa Kiyahudi, nalizaliwa Tarso, mji wa Kilikia, ila nililelewa katika mji huu, miguuni pa Gamalieli, nikafundishwa sheria ya baba zetu kwa usahihi, nikawa mtu wa jitihadi kwa Mungu kama ninyi nyote mlivyo leo hivi; nikawaudhi watu wa Njia hii hata kuwaua, nikawafunga, nikiwatia gerezani, wanaume na wanawake,” Mdo 22:3. Historia hii ya Mtume Paulo inasema chochote kuhusu hali na maisha yako? Kama haitoshi, mtazame Yesu pale msalabani, kwani kaubebe ujumbe mzito sana juu ya maisha yako. Kwa kuwambwa kwake Msalabani anakuambia hivi; “ona nilivyo hapa. Nimeyafanya haya yote kwa sababu na kupenda upeo.” Hakika hakuna sababu ya kujiona mnyonge na mtu aliyetengwa ninapoutafakari Msalaba Mtakatifu. Kristo ndilo tumaini la kweli, na Yeye ndiye njia, kweli, na uzima wetu, Yoh 14:6.

Mtume Paulo baada ya kuongoka kwake, ikiwa ni msukumo wa moja kwa moja wa Kristo mwenyewe baada ya kutupwa chini, Mdo 9:4-5, tumaini lake lote alilielekeza kwa Kristo Yesu. Naye kwa kutoa ushuhuda wa kweli hiyo anasema,  “Kwa maana, ndugu zangu, injili hiyo niliyowahubiri, nawajulisha ya kuwa siyo ya namna ya kibinadamu,” Gal 1:11. Kwa maneno mengine ni kwamba kile alicho na anachokihubiri Mtume Paulo  siyo tokeo la nguvu zake au maarifa yake binafsi, bali ni neema ya Kristo iliyo ndani yake. Kwa kuwa sikuipokea kwa mwanadamu (Injili hiyo) wala sikufundishwa na mwanadamu, bali kwa ufunuo wa Yesu Kristo,” Gal 1:12. Mtume Paulo hafichi historia yake mbaya na kuona aibu kuisema mbele za watu. Ila anataka mimi na wewe tuelewe kwamba misimamo yetu iliyojengwa na inayojegwa na mila na desturi zetu potofu, ndani yake hakuna uzima. Naye anasema, Maana mmesikia habari za mwenendo wangu zamani katika dini ya Kiyahudi, kwamba naliliudhi kanisa la Mungu kupita kiasi, nikaliharibu,” Gal 1:13. Ndugu yangu, kama wewe ni mmoja wa kujipambanua kwa ubora wa kabila lako, misimamo ya kabila lako isiyo na mwono wa Kimungu, na hata umaarufu wake, basi elewa haupo njia sahihi kama wataka kuwa mfuasi wa Yesu. Mtume Paulo anakuambia wewe na mimi kwamba, Nami naliendelea katika dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika kabila yangu, nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu,” Gal 1:14. Hata kwa kufanya hayo yote, Mtume Paulo anagundua hapakuwa na tumaini lolote, zaidi ya kupotea kwa misimamo isiyo na mwelekeo wa Kimungu na kuikosa njia ile sahihi.

Wapendwa katika Kristo, usipotambua uwepo wa Mungu katika maisha yake, chochote ujengacho juu yake hukosa msingi imara, na mwisho wake uporomoka. Baada ya kuongoka kwake, Mtume Paulo anagundua nguvu na uwepo wa Mungu katika maisha yake. Mungu aliyenitenga tangu tumboni mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake,” Gal 1:15. Hivyo kile alicho Paulo baada ya kuongoka kwake, yaani, kurudi katika njia iliyo sahihi, Kristo ndiye kila kitu kwake. Ni kwa sababu hiyo Paulo anasema kwamba, Mungu alipoona vema kumdhihirisha Mwanawe ndani yangu, ili niwahubiri Mataifa habari zake; mara sikufanya shauri na watu wenye mwili na damu; wala sikupanda kwenda Yerusalemu kwa hao waliokuwa mitume kabla yangu; bali nalikwenda zangu Arabuni, kisha nikarudi tena Dameski,” Gal 1:16-17. Je, umeyapitia machungu na mahangaiko kama Mtume Paulo?

Na mwisho, mtu wa tatu mwenye kutupa tumaini la kweli katika udogo na mahangaiko yetu ni mwanamke yule wa mji wa Naini aliyefiwa na mwanaye wa pekee, Lk 7:11-12. Injili ya leo inatupa simulizi hili kwa namna ya pekee. Yesu Kristo katika safari zake za kuihubiri habari njema ya wokovu akiwa na wanafunzi wake, wanakutana na msafara uliobeba maiti ya mwana pekee wa mama mjane. Na alipolikaribia lango la mji, hapo palikuwa na maiti anachukuliwa nje, ni mwana pekee wa mamaye ambaye ni mjane, na watu wa mjini wengi walikuwa pamoja naye,” Lk 7:12. Bila shaka msafara ule wa maiti ile na hali za watu kama zilivyokuwa kwa kusikitika juu ya msiba ule, na hasa mama huyu ambaye anaonekama kuwa mwema kwa jirani zake, unamsikitikisha Yesu pia. Bwana alipomwona (mama mfiwa) alimwonea huruma, akamwambia, Usilie,” Lk 7:13. Neno ‘usilie’ katika mazingira haya limebeba ujumbe, ‘ondoa hofu na uwe na matumaini.’ Tumaini lenyewe hapa na katika uhasilia wake ni Kristo Yesu mwenyewe. Kwa upendo wa ajabu na huruma ya Kimungu, ambaye kwa sasa ni Mungu na mwanadamu, Yesu Akakaribia, akaligusa jeneza; wale waliokuwa wakilichukua wakasimama. Akasema, Kijana, nakuambia, Inuka,” Lk 7:14. Baada ya tukio hili la pekee kabisa na ajabu, Yule maiti akainuka, akaketi, akaanza kusema. Akampa mama yake,” Lk 7:15. Bila shaka mimi na wewe tungekuwa katika msafara huo tungetimua mbia kwa hofu! Pamoja na hofu waliokuwa nayo watu wale katika msafara ule, walibaki na tumaini kubwa mbele yao. Hofu ikawashika wote, wakamtukuza Mungu, wakisema, Nabii mkuu ametokea kwetu; na, Mungu amewaangalia watu wake,” Lk 7:16. Hili ni fundisho kwetu pia. Twapaswa daima kumshukuru Mungu na kuliweka tumaini kwake tu aliyetutendea mambo ya ajabu, badala ya kujitafutia utukufu binafsi, na hata kutaka kuabudiwa. Pili, tuwe vyombo vya kusambaza habari njema kwa wengine, badala ya chuki. Habari hii yake ikaenea katika Uyahudi wote, na katika nchi zote za kando kando,” Lk 7:17. Je, ndugu yangu, hapo ulipo watumika kama chombo cha habari njema ya wokovu, au ndiyo upande wa pili, yaani, mzalisha chuki?

Siku moja jioni nikiwa na Babu yangu Mzee Ngilishi, ambaye sasa hupo mbele za haki, alinisimulia hadithi hii kuhusu Jogoo. Nyakati zao Babu waliweza kudamka mapema asubuhi kwa msaada wa vitu viwili. Moja, ilikuwa kuwika kwa Jogoo, na pili, sauti ya Kengele kutoka Parokiani. Pamoja na msaada wa viashiria hivyo viwili vya kuujua muda, Jogoo hakuweza kuwasaliti isipokuwa pale mwezi unapoandama.

Lakini Babu aliendelea kusema, “pamoja na kuwika kwake Jogoo, nasi kujua kumekuchwa, Jogoo alikuwa ana tafsiri yake ambayo ni tofauti kidogo. Jogoo hufikiri kwamba asipowika hakuwezi kukakuchwa.” Baba aliendelea kusimulia, “kwa ukweli wa jambo hili kama wapo jogoo wawili watatu, hukosi kusikia ushindani wao kwa wao katika kuwika. Moja huanza hivi, “mimi ni wa kwanzaaaaaa,” na mwingine huitikia, “umekoseaaaaaa, haaaaa!” Babu na mimi tuliangua kicheko!

Mwisho, Babu akasema, “mara nyingi twaweza kuwa tunafanya mazuri na mwisho tukajifananisha nayo huku tukisahau yule aliyetuwezesha kuyafanya hayo yote. Unapokosa msingi huu, na kujiweka katikati ya yote yale uyafanyayo, mambo yanapoharibika au kutokwenda vizuri kadiri ya mazoea yetu, ni rahisi kukata tamaa kabisa. Na hapa ndipo unapolikosa lile tumaini la kweli la kusonga mbele kwa sababu yote umeyaweka pamoja nawe ukijiaminisha ndiyo yote katika yote. Hivyo huwezi kuona mbele upatwapo na sintofahamu katika maisha. Mjukuu wangu usiwe ukuta wako mwenyewe na kushindwa kuona mazuri zaidi yaliyopo mbele yake. Sasa nenda kalale na uyasikilize vizuri Majogoo,” Baba alimalizie simulizi lile.

Tumsifu Yesu Kristo!  

Bwana alipomwona alimwonea huruma, akamwambia, Usilie,” Lk 7:13


Tusali:-Ee Yesu na Mwokozi wangu, usiniondolee lile tumaini ndani yangu. Nijalie niweze kuyaona yote katika tumaini la kweli. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario