jueves, 16 de junio de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 11 YA MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI YA 11 YA MWAKA-C
Somo: 2Nya 24:17-25
Zab: 89:4-5, 29-30, 31-32, 33-34
Injili: Mt 6:24-34
Nukuu:
Hata baada ya kufa kwake Yehoyada, wakuu wa Yuda wakamwendea mfalme, wakamsujudia. Naye mfalme akawasikiliza maneno yao,” 2Nya 24:17 

 “Na roho ya Mungu ikamjia Zekaria, mwana wa Yehoyada, kuhani; naye akasimama juu ya watu, akawaambia, Mungu asema hivi, Kwani ninyi kuzihalifu amri za Bwana, hata msiweze kufanikiwa? Kwa kuwa mmemwacha Bwana, yeye naye amewaacha ninyi,” 2Nya 24:20 

 “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali,” Mt 6:24

TAFAKARI:Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu.”

Wapendwa wana wa Mungu, tafakari ya leo inatuzamisha katika dhana nzima ya ‘uaminifu’ katika maisha, na hasa kwa yule mwenye kutuwezesha yote katika yote. Huyu si mwingine bali ni Mungu mwenyewe. Ni kuishi maisha yanayoongozwa na malengo, yaani, maisha ya hofu ya Mungu. Ikiwa ni maisha yenye malengo na yanayoongozwa na hofu ya Mungu, ni wazi maisha hayo ‘yatakuwajibisha.’ Hiki ndicho asemacho Bwana wetu Yesu Kristo kwamba, Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali,” Mt 6:24. Sehemu ya pili ya angalizo ya Yesu limejikita kwenye Mungu na mali. Mara nyingi uwezo wa mtu kwa upande wa mali alizonazo zimekuwa chanzo cha kiburi chake na kuuvaa upofu wa kutokuona nafasi ya Mungu katika maisha yake, na mwisho kujisadikisha kuwa na uwezo wa kufanya kila jambo kwa mali alizonazo. Mali ikiwa ni pamoja fedha alizokuwa nazo mtu, Mtume Paulo analiona jambo hili wazi pale fedha hiyo inapo mtawala mtu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi,” 1Tim 6:10

Tukiachana na fedha, jambo lingine ambalo ni hatari ni matumizi mabaya ya mamlaka aliyonayo mtu. Nguvu ya mamlaka kwa wengine huwatia kiburi hasa pale mamlaka hiyo inapokuwa na mwelekeo ‘neno la mwisho’ dhidi ya mali, maisha, na uhai wa watu, yaani, mamlaka isiyohojiwa wala kukosolewa pale ambapo mambo yanapokwenda ndivyo sivyo. Ni rahisi kwa mwenye nguvu hizi kimamlaka kujisahau na kuchukua nafasi ya Mungu. Mwenye kufanya hivyo ni kuusahau pia ubinadamu wake ikiwa  ni pamoja na mapungufu yake. Hivi ndiyo hali ilivyokuwa kwa mfalme Yoashi aliyesahau historia nzima ya ufalme wake mara baada ya kufa kwake kuhani Yehoyada. Hata baada ya kufa kwake Yehoyada, wakuu wa Yuda wakamwendea mfalme, wakamsujudia. Naye mfalme akawasikiliza maneno yao,” 2Nya 24:17. Sujudio la watu kwa mfalme ni kiashirio cha anguko kimahusiano kati ya Mungu na mamlaka ya kibinadamu. Ndugu yangu, wakusujudiwa ni Mungu tu.  Ni nani asiyekucha, Ee Bwana, na kulitukuza jina lako? Kwa kuwa wewe peke yako u Mtakatifu; kwa maana mataifa yote watakuja na kusujudu mbele zako; kwa kuwa matendo yako ya haki yamekwisha kufunuliwa,” Ufu 15:4. Jaribu la kufanywa Mungu watu liliwakuta pia Mtume Paulo na Barnaba uko Likoania katika safari yao ya kimisionari.  

Tendo la uponyaji wa mtu mwenye udhaifu wa miguu-kiwete tangu tumboni mwa mamaye, linaibua hisia za watu hawa wa Likaonia na kuwaona Paulo na Barnaba kama miungu ya kuabudiwa. Na makutano walipoona aliyoyafanya Paulo wakapaza sauti zao, wakisema kwa Kilikaonia, Miungu wametushukia kwa mifano ya wanadamu. Wakamwita Barnaba, Zeu, na Paulo, Herme, kwa sababu ndiye aliyekuwa mnenaji,” Mdo 14:11-12. Tendo hili ni moja ya mambo hatari sana katika utume au utumishi wa aina na ngazi yoyote ile. Ukiona hali hii ndani mwa watu inajitokeza na kuacha kumwabudu Mungu na kuanza kukuambudu wewe kama mchungaji wao au kiongozi wao, ujue wazi ufanyacho si matakwa ya Mungu bali shetani amechukua nafasi yake. “Tazama, nakupa walio wa sinagogi la Shetani…, nitawafanya waje kusujudu mbele ya miguu yako, na kujua ya kuwa nimekupenda,” Ufu 3:9

Hivyo kwa kutambua kasoro hii, Mtume Paulo na Barnaba wanatoa angalizo kwa Walikaonia na kusema, “Akina bwana, mbona mnafanya haya? Sisi nasi tu wanadamu hali moja na ninyi; twawahubiri habari njema, ili mgeuke na kuyaacha mambo haya ya ubatili na kumwelekea Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo; ambaye zamani zilizopita aliwaacha mataifa yote waende katika njia zao wenyewe,” Mdo 14:14-16. Hatari kubwa katika jambo hili ni kwamba, binadamu anapoukataa ubinadamu wake, anajeuka kuwa mbaya kuliko shetani, kwani shatani alishaukubali ushetani wake pale alipomwasi Mungu. Na ndivyo ilivyokuwa katika utawala ule wa mfalme Yoashi kwamba, Wakaiacha nyumba ya Bwana, Mungu wa baba zao; wakatumikia maashera na sanamu; ghadhabu ikawajia Yuda na Yerusalemu kwa sababu ya hiyo hatia yao,” 2Nya 24:18. 

Katika hali na mazingira kama haya, Mungu haachi kuwainua watumishi wake kutoa maonyo kwa watu wake waliokengeuka katika imani ili wabaki katika kweli. Na roho ya Mungu ikamjia Zekaria, mwana wa Yehoyada, kuhani; naye akasimama juu ya watu, akawaambia, Mungu asema hivi, Kwani ninyi kuzihalifu amri za Bwana, hata msiweze kufanikiwa? Kwa kuwa mmemwacha Bwana, yeye naye amewaacha ninyi,” 2Nya 24:20. Mara nyingi walio kolea katika uovu ni vigumu sana kutazama nyuma na kuanza upya kwani “tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti,” Yak 1:15. Ni kwa namna na ugumu huo hawakumsikia Zekaria mwana wa Yehoyada, na badala yake wakaazimia kumuua, 2Nya 24:21. Mfalme Yoashi anasahau historia yake na namna alivyookolewa kuuwawa akiwa mtoto mdogo na hata kutawazwa kuwa mfalme. Basi hivyo mfalme Yoashi hakuukumbuka wema, ambao Yehoyada, baba yake, alimfanyia, bali alimwua mwanawe. Naye alipokufa, alisema, Bwana na ayaangalie haya, akayatakie kisasi,” 2Nya 24:22. Katika kweli na haki, Mungu kamwe hafumbi macho licha ya kuchelewa kwake kutimiza kweli na haki hiyo. Yeye anatujua ni wakati gani unafaa. Pamoja na kuvamiwa na mataifa ya jirani, mfalme kwa kosa lake la kuruhusu maabudu ya miungu mingine katika utawala wake linayafanya maisha yake kutokuwa na mwisho mzuri. Hata walipoondoka kwake, (nao walimwacha ameshikwa sana na maradhi,) watumishi wake mwenyewe wakamfanyia fitina kwa ajili ya damu ya mwana wa Yehoyada kuhani, wakamwua kitandani pake, akafa; wakamzika mjini mwa Daudi, lakini hawakumzika katika makaburi ya wafalme,” 2Nya 24:25. U ndumilakuwili katika maisha siyo mzuri. Ni heri kuwa joto au baridi, kuliko kuwa vuguvuvu.

Ni kwa mtazamo huo, Yesu katika Injili ya leo anatupa angalizo na kusema, hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali,” Mt 6:24. Hata ukifanikiwa ni kwa muda mfupi tu. Je, kwa nini twapaswa kumtumikia bwana mmoja? Sababu ya wazi na ya moja kwa moja ni kuondoa ile roho iliyojigawa vipande vipande. Mfano; kama umepata mialiko miwili ya harusi inayofanyika muda ule ule na siku ile ile, yakupasa kuchagua moja wapo utakayokwenda hata kama zote zina uzuri au zimetofautiana. Kuchagua huku ndiko Yesu anapotushauri kuutafuta kwanza ufalme wa Mbinguni, na kuondoa roho ya kujigawa vipande vipande. Naye Yesu anasema, Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Mt 6:33. Ndugu yangu, unaloneno zaidi ya ukweli huu wa Bwana wetu Yesu Kristo?

Ni ukweli usiotia shaka kwamba ukishaingia katika mfumo huu, na mtazamo huu wa fundisho hili ya Yesu, kuutafuta ufalme wa mbinguni kwanza, huwezi kupata presha unapowaona watu wakipigana vibega kwa kumwangaikia mfalme tumbo na utajiri wake. Kristo anapokuwa katikati ya yote, yeye atakupatia kadiri ya mahitaji yako na kwa wakati wake. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.” Mt 6:34. Ndugu yangu yatupasa kumuishi Kristo leo na sasa katika yale yote yampendezayo. Ingawa kesho inasikika akilini mwetu, tuelewe kesho hiyo ipo mikono mwa Mungu katika uhalisia wake.

Tumsifu Yesu Kristo!

Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Mt 6:33

Tusali:- Ee Yesu, uwe kitoshelezo chetu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario