JUMAPILI YA 11 YA MWAKA-C
Somo
I: 2Sam 12:7-10, 13
Zab: 31:1-2, 5, 7, 11 (K) 5
Somo
II: Gal 2:16, 19-21
Injili:
Lk 7:36-8:3
Nukuu:
“Kwa
nini umelidharau neno la Bwana, na kufanya yaliyo mabaya machoni pake? Umempiga
Uria, Mhiti, kwa upanga, nawe umemtwaa mkewe awe mke wako, nawe umemwua huyo
kwa upanga wa wana wa Amoni,” 2Sam 12:9
“Basi,
sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako, kwa sababu umenidharau, ukamtwaa mkewe
Uria, Mhiti, kuwa mke wako,” 2Sam 12:10
“Daudi
akamwambia Nathani, Nimemfanyia Bwana dhambi. Nathani akamwambia Daudi, Bwana
naye ameiondoa dhambi yako; hutakufa,” 2Sam 12:13
“hali tukijua ya kuwa
mwanadamu hahesabiwi haki kwa matendo ya sheria, bali kwa imani ya Kristo Yesu;
sisi tulimwamini Kristo Yesu ili tuhesabiwe haki kwa imani ya Kristo, wala si
kwa matendo ya sheria; maana kwa matendo ya sheria hakuna mwenye mwili
atakayehesabiwa haki,” Gal 2:16
“Siibatili neema
ya Mungu; maana, ikiwa haki hupatikana kwa njia ya sheria, basi Kristo alikufa
bure,” Gal 2:21
“Akasimama
nyuma karibu na miguu yake, akilia, akaanza kumdondoshea miguu machozi yake, na
kuipangusa kwa nywele za kichwa chake, akiibusu-busu miguu yake na kuipaka yale
marhamu,” Lk 7:38
“Basi,
yule Farisayo aliyemwalika alipoona vile, alisema moyoni mwake, Mtu huyu kama
angekuwa nabii, angemtambua mwanamke huyu amgusaye, ni nani, naye ni wa namna gani,
ya kwamba ni mwenye dhambi,” Lk 7:39
TAFAKARI:
“Neema na Huruma ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu. Matendo yetu tu kama
yalivyo hayatoshi kutuhesabia haki mbele ya Mungu. Ila kwa Neema ya Mungu yote
mema kwetu yawezekana. Sote twaalikwa kufanya toba ya kweli na majuto.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 11 ya mwaka “C” wa Kanisa. Wazo kuu la
tafakari yetu la leo kadiri ya masomo yake ni hii: ‘Neema na Huruma ya Mungu ni
kubwa kuliko dhambi zetu. Matendo yetu tu kama yalivyo hayatoshi kutuhesabia
haki mbele ya Mungu. Ila kwa Neema ya Mungu yote mema kwetu yawezekana. Sote twaalikwa kufanya
toba ya kweli na majuto.’ Kwa kutambua kosa lake na huitaji wa huruma ya Mungu,
Mfalme Daudi akamwambia Nabii Nathani, “Nimemfanyia
Bwana dhambi. Nathani akamwambia Daudi, Bwana naye ameiondoa dhambi yako;
hutakufa,” 2Sam 12:13
Wapendwa
wana wa Taifa la Mungu, kunatofauti kubwa kuusema ukweli na kuuishi ukweli.
Kuna tofauti kubwa pia ya kuhubiri haki na kutenda haki. Vile vile kunatofauti
kubwa sana ya kusema kuhusu upendo na kuishi upendo. Kuyasema mambo kwa ufasaha
ni taaluma ambayo mtu anaweza kuipa kwa kupitia njia na miongozo inayohusu
jambo hilo. Kuishi jambo fulani ni kugeuzwa na jambo hili na kuwa sehemu ya
jambo hilo. Kumbe kwa namna nyingine kama wasemavyo waswahili, ‘kuna kusoma na
kuelimika.’ Hivi ni vitu viwili tofauti.
Nabii
Nathani anatumwa na Mungu kwenda kwa Mfalme Daudi na kumwambia chukizo
alilomfanyia. Nathani anamweleza Daudi uzito wa tatizo na dhambi aliyoifanya
kwa jamii, kwa yeye mwenyewe na kwa Mungu. Kwa nafasi aliyokuwa nayo Daudi kama
Mfalme ilimpasa awe mtetezi wa kweli, haki, Amani na Upendo. Ufalme wake kama
ulivyo uliwakilishwa na taswira na fadhila hizo. Badala yake, Daudi anakuwa
muhujumu wa hiyo kweli, haki, Amani, na Upendo. Huu ndio ule mfano wa mtu yule
aliyekuwa na kondoo wake mmoja na aliyempenda kupita vitu vyote, 2Sam 12:1-4.
Nathani hapa anamaanisha, mtu yule ni Uria, na kondoo wake ni mkewe Bath-sheba Daudi aliyezini naye, na matokeo yake
kupelekea umauti wa Uria. Kama Kondoo, yaani wanawake, Daudi alikuwa nao wengi
na ofisi yake kama Mfalme iliruhusu kuwa na wake hao wengi.
Mazungumzo ya Nabii Nathani na Mfalme Daudi kwa kupitia mfano
wa Mtu na Kondoo wake aliyekuwa anampenda na hivyo kudhulumiwa, yanaamasisha
sifa kuu na uwepo wa falme yoyote ile iliyo kwa ajili ya watu, yaani: ufalme wa
haki, amani, kweli, na upendo. Hivyo Mfalme Daudi anaguswa na mfano ule na
kumwambia Nabii Nathani, “Aishivyo Bwana, mtu huyo aliyetenda jambo hili,
hakika yake astahili kufa; naye atamrudishia yule mwana-kondoo mara nne,
kwa sababu ametenda neno hili, na kwa sababu hakuwa na huruma,” 2Sam 12:5-6.
Mfalme Daudi anajiweka kitanzi mwenyewe kwa makosa yake. Ndugu yangu, kumbuka maneno
ya Yesu, “Wapeni
watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa
hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile
kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa,” Lk 6:38. Ni kwa mizania hii, Nabii
Nathani anamwambia Daudi bila kupepesa macho, “Wewe ndiwe mtu huyo,” 2Sam 12:7. Hivyo kosa na adhabu
inamstahili yeye mwenyewe.
Mungu anatoa adhabu kwa Mfalme Daudi kwa kosa lile ambayo ni
chukizo kwake mwenyewe kama Mfalme na mtetezi wa haki za watu, chukizo na makwazo
kwa jamii, na chukizo kwa Mungu aliye haki, kweli, amani, na pendo. “Basi, sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako, kwa sababu
umenidharau, ukamtwaa mkewe Uria, Mhiti, kuwa mke wako,” 2Sam 12:10. Kwa
kutambua kosa lake na kulikiri, Mungu anathibitisha kuwa Yeye ni Upendo na
Huruma na kumwondolea adhabu ya kifo Mfalme Daudi. “Daudi akamwambia Nathani, Nimemfanyia Bwana dhambi. Nathani
akamwambia Daudi, Bwana naye ameiondoa dhambi yako; hutakufa,” 2Sam 12:12.
Pamoja na hayo, kiumbe kile kama tokeo la uzinifu wa Daudi hakikuishi.
Wapendwa katika Kristo, wewe na mimi kwa njia moja au
nyingine tumefanya kama Daudi na wakati mwingine zaidi hata ya Daudi. Hakuna
njia nyingine ya kujikwamua katika hali hii zaidi ya kufanya toba ya kweli na
majuto. Mungu aliye mwingi wa rehema, neema na upendo yu tayari kutusamehe. Kwa
maana “Wewe, Bwana, U Mungu wa rehema na neema,
Mvumilivu, mwingi wa fadhili na kweli,” Zab 86:15. Amina
Injili ya
leo tunamwona Yesu anaalikwa nyumbani kwa Mfarisayo mmoja kwa chakula. Tukio
hili kwa kiasi fulani linaakisi tukio lile kubwa la mlo wa mwisho wa Yesu na
wanafunzi wake. Tukio lile la mlo wa mwisho Yesu aliandaa na kuwaalika
wanafunzi wake, na kuonyesha kwa upendo jinsi ilivyowapasa kuishi, na kuwapa
rasmi majukumu yako kama watumika na siyo wanaotumikiwa. Katika tukio hili
lenye kuakisi mlo ule wa mwisho; upendo, huruma, na msamaha wa Mungu
unajidhihirisha. Upendo, huruma, na msamaha wa Mungu hautokani na mila na
desturi zetu wanadamu, bali ni kweli iliyo ndani ya Mungu mwenyewe ambayo ina
uhusiano wa karibu kabisa na wa moja kwa moja kwa namna tulivyoumbwa, yaani,
‘kwa sura na mfano wake,’ Mwa 1:27. Sheria zetu licha ya ukweli unaoufunua
kadiri ya mazingira yetu na wakati mwingine katika mapungufu yake, siyo sababu
ya upendo, huruma, na msamaha wa Mungu kwetu, “kwa sababu hakuna mwenye mwili
atakayehesabiwa haki mbele zake kwa matendo ya sheria; kwa maana kutambua
dhambi huja kwa njia ya sheria,” Rum 3:20.
Karne ile
ya kwanza katika ulimwengu ule wa kiyahudi ulitawaliwa na ‘dini’ ya matendo ya
sheria. Matendo haya ya sheria yalitafsiriwa ndivyo sivyo kama sababu ya
kuhesabiwa mtu haki mbele za Mungu. “Kwa
maana, wakiwa hawaijui haki ya Mungu, na wakitaka kuithibitisha haki yao
wenyewe, hawakujitia chini ya haki ya Mungu,” Rum 10:3. Upofu huu katika
tafsiri halisi ya Sheria ndiyo iliyowapoteza Mafarisayo na mwisho wa siku
hawakuifuata Torati kama ilivyokuwa, bali tafsri yake ambayo ililenga ubinafsi wao na matamanio yao. Hivyo
Yesu anatupa angalizo na kusema, “Haki yenu
isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme
wa mbinguni,” Mt 5:20. Mtume Paulo anayafahamu fika matendo ya sheria ambayo
ndani yake hapakuwa na uzima wowote, bali kupotea na kupotoka kwa kujiridhisha
nafasi na kujisadikisha kama asemavyo, “wakinijua
sana tangu mwanzo, kama wakipenda kushuhudia, ya kwamba nalikuwa Farisayo kwa
kuifuata madhehebu ya dini yetu iliyo sahihi kabisa,” Mdo 26:5. Mtazamo huu na
umbumbumbu huu ndiyo Yesu anausema kama mzigo kwa Mafarisayo. “Wao (Mafarisayo) hufunga mizigo mizito na
kuwatwika watu mabegani mwao; wasitake wenyewe kuigusa kwa kidole chao,” Mt
23:4
Hivyo
ndugu zangu, waraka kwa Wagalatia kama tulivyokwisha usoma leo, Wayahudi
waliwataka Wagalatia kuzishika mila zao (kiyahudi), na desturi za Mafarisayo.
Matendo ya sheria hayakuhusiana kabisa na ‘dini’ ya Musa na Agano la Kale,
ambayo ndiyo Torati. Matendo ya sheria hayakuwa kweli kuhusu Torati, bali tafsiri
ya Torati ambayo ilikuwa ukweli wa Mungu ulipotoshwa kama tutakavyoona baadaye
kidogo. Wakristo wengi na hasa baadhi ya Madhehebu ya Kiprotestanti
hawatofautishi ukweli kati ya matendo ya sheria na sheria yenyewe (Torati).
Wengi
hufikiri matendo ya sheria ni kutokuifuata Torati. Hii si kweli. Mtume Paulo
anaposema matendo ya sheria anamaanisha Talmud, yaani ukweli kuhusu Mungu
uliopotoshwa kutokana na tafsiri ya Torati yenyewe. Kwa ujumla mafundisho ya
Mtume Paulo yalilenga au kukazia juu ya Yesu Kristo, yeye mwenyewe Paulo, yaani
kuongoka kwake, na swala zima la neema ya Mungu. Katika fundisho hili Mtume
Paulo anasema, “Nimesulibiwa
pamoja na Kristo; lakini ni hai; wala si mimi tena, bali Kristo yu hai ndani
yangu; na uhai nilio nao sasa katika mwili, ninao katika imani ya Mwana wa
Mungu, ambaye alinipenda, akajitoa nafsi yake kwa ajili yangu,” Gal 2:20. Kuhusu Neema ya Mungu kwetu ambayo kwayo yote
mema yawezekana, Mtume Paulo anasema, “Siibatili
neema ya Mungu; maana, ikiwa haki hupatikana kwa njia ya sheria, basi Kristo
alikufa bure,” Gal 2:21. Sheria isemwayo hapa siyo Torati, bali matendo yale ya
sheria ambayo kwayo kama yalivyo hayana uzima wowote ndani yake. Ni mbwembwe
tu!
Pamoja na
ukweli wa fundisho hilo, kinyume chake ni kwamba, Mtume Paulo anawafundisha
Wagalatia kutii sheria na amri za Mungu, ‘dini’ ya kweli, ikiwa ndiyo njia ya
maisha-Agano la Kale-Torati, angali wakiishi katika neema ya Mungu
iliyowezeshwa na Kristo mwenyewe kwa sadaka yake pale msalabani. Ndiyo maana
kwa mshangao mkubwa Mtume Paulo anawauliza Wagalatia,
“Enyi Wagalatia msio na akili, ni nani
aliyewaloga, ninyi ambao Yesu Kristo aliwekwa wazi mbele ya macho yenu ya kuwa
amesulibiwa? Nataka kujifunza
neno hili moja kwenu. Je! Mlipokea Roho kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia
kunakotokana na imani?” Gal 3:1-2. Kwa matendo ya Sheria hapa, Mtume Paulo haipingi
Torati bali anazungumzia yale yaliyotafsiriwa na kuchukuliwa kama mapokeo ya
wazee na siyo Torati yenyewe, Mk 7:9. Ukweli ni
kwamba “mwanadamu hahesabiwi haki
kwa matendo ya sheria, bali kwa imani ya Kristo Yesu; sisi tulimwamini Kristo
Yesu ili tuhesabiwe haki kwa imani ya Kristo, wala si kwa matendo ya sheria;
maana kwa matendo ya sheria hakuna mwenye mwili atakayehesabiwa haki,” Gal 2:16
Kuishika sheria ya
Bwana kama ilivyo Torati si laana au kulaaniwa, bali “Sheria
ya Bwana ni kamilifu, Huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa Bwana ni amini, Humtia
mjinga hekima,” Zab 19:7. Lakini kinyume chake ni kwamba, “wale wote walio wa matendo ya sheria, wako chini
ya laana; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu asiyedumu katika yote
yaliyoandikwa katika kitabu cha torati, ayafanye,” Gal 3:10. Bila shaka Mtume
Paulo analisema hili na kusimamia ukweli huu kama ulivyo na ilivyopaswa
kuiishika Torati bila kuichakachua. “Na alaaniwe asiyeyaweka imara maneno ya torati
hii kwa kuyafanya. Na watu wote waseme, Amina,” Kumb 27:26
Ndugu
yangu, kuna usalama na ukamilifu katika kuishika sheria ya Bwana kwani wana, “Heri
walio kamili njia zao, Waendao katika sheria ya Bwana,” Zab 119:1. Ni kwa
ukweli huu kuhusu sheria ya Bwana Mtume Paulo anasema, “torati ni takatifu, na ile amri ni takatifu, na ya haki, na
njema,” Rum 7:12. Naye Yesu kwa msisitizo anatuambia, “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la,
sikuja kutangua, bali kutimiliza,” Mt 5:17. Na zaidi kuhusu amri, Yesu
anamwambia yule Bwana tajiri kwamba, “ukitaka
kuingia katika uzima, zishike amri,” Mt 19:17
Yesu
anautambua udhaifu huu wa sheria za wanadamu, na hasa katika jamii yake ambayo
waliachana na torati na kufuata tafsiri ya torati na masimulizi yake, yaani,
TALMUD. “Basi,
yule Farisayo aliyemwalika alipoona vile, alisema moyoni mwake, Mtu huyu kama
angekuwa nabii, angemtambua mwanamke huyu amgusaye, ni nani, naye ni wa namna
gani, ya kwamba ni mwenye dhambi,” Lk 7:39. Ni kweli kwamba wote ni wadhambi,
yaani, mwanamke yule asiyejulikana, na huyu mfarisayo anayemshangaa Yesu
kuguswa na huyu mwanamke. Huyu mfarisayo anaonyesha upendo mdogo, ana mashaka
na Yesu, ana moyo mzito na mgumu, na hivyo kumfanya aonyeshe upendo kidogo.
Kinyume chake, mwanamke huyu anakuwa karibu na Yesu, anamgusa Bwana Yesu,
anaufungua moyo wake na kujiweka wazi mbele ya Mungu wake aliye Huruma.
Mwanamke huyu anaonyesha upendo mkubwa na kupenda kwa sababu anapenda na
anajisikia kupendwa na Bwana aliye Huruma, Yesu Kristo. Huyu mwanamke mdhambi
hajisikii aibu kwa kulia na kuyatoa machozi yake mbele za watu waliokuwa
wanamwangalia na kumuhukumu ndani ya mioyo yao.
Kristo
amekuja na kujitoa kwa wadhambi kwa urafiki wake na kuwapatia wokovu. Kwake
Yesu ni muhimu sana na furaha kwa mdhambi kuupokea urafiki huu na kutambua
umasikini wake, yaani, dhambi zake. Yesu Kristo anafanya urafiki na mdhambi kwa
huruma ya hali ya juu. Hapa tunagundua ukubwa na upendo wa Mungu usiopimika.
Yesu hawabagui watu. Yesu anawapenda watu na kukaa nao karibu, na kuutwaa
wokovu kwa wote. Yesu anajua vyema nani yule mwanamke aliyekuwa karibu naye.
Yesu anajua mwanamke huyu ni mdhambi na yupo tayari kuanza upya naye kwa sababu
anahitaji kukombolewa. Hata hivyo kinachowakwaza Wayahudi ni kuona kwa nini
Yesu anamwacha mwanamke huyu aendelee kumgusa ili hali wanajua ni mdhambi.
Katika tendo hili Yesu anakuambia wewe na mimi kwamba, “Naye
heri mtu ye yote asiyechukizwa nami,” Lk 7:23. Kwa nini basi tunakwazika tuonapo
upendo wa Mungu kwa watu wake? Yohana Mbatizaji alihubiri ubatizo wa toba na
watu waliongoka. Lakini kwa makusudi Mafarisayo waliupinga ubatizo ule kwa vile
walikwishajihesabia haki. Ndugu yangu, bado hatujamaliza kuamini na kuelewa huu
upendo wa Mungu. “Lakini, Mafarisayo na
wana-sheria walilipinga shauri la Mungu juu yao, kwa kuwa hawakubatizwa naye
(Yohana),” Lk 7:30.
Jambo la kushangaza
zaidi wakati wa Yesu, Torati ile ambayo ndiyo ilikuwa mstakabali wa Taifa la
wana wa Mungu-Waisraeli, ilikwisha chakachuliwa vya kutosha na hivyo Taifa hili
lilikuwa linafuata Tafsiri yake tu kwa sehemu kubwa. Jambo muhimu sana la kujua
ni kwamba kipindi cha Yesu Wayahudi na hasa mafarisayo na waandishi hawakuwa
wanaifuata Torati kama iliyokuwa, ila tafsiri yake (maisha ya dini na matendo
yake kupitia masimulizi) iliyojulikana kwa ujumla kama TALMUD. Talmud ilibeba
mambo mawili: MIDRASH (tafsiri ya mambo mbalimbali toka Torati), na MISHNAH
(marudio/waliyorudia au mafundisho)
Kwa mantiki hiyo hapo
juu ya TALMUD, vitabu vile vitano vya Torati vingewezwa kuandikwa kwa kurasa
350 tu; wakati TALMUD ilichukuwa hadi vitabu 523; vilivyo rudufiwa (printed)
katika mabando (volumes) 22. Haya ndiyo yanayonukuliwa na mafarisayo na
waandishi kama mapokeo ya wazee. Sehemu nyingi za mafundisho ya Yesu anapinga
jambo hili la kufuata mapokeo ambayo ni tafsiri kutoka Torati. Ni ukweli wa
Mungu uliopotoshwa.
Wapendwa wana wa Mungu,
Mungu wetu hana macho tuliyo nayo sisi ambayo yana kikomo na umbali fulani wa
kuona. Macho ya Mungu, au kwa namna nyingine muono wa Mungu uvuka hata uwezo
wetu wa kuona na matokeo yetu ya kufikiri. Hivyo Yesu anaurejesha uhai wa Mungu
kwa maisha ya kweli na sababu ya kuumbwa huyu mwanadamu. Hivyo kwa tukio hili
la mwanamke huyu mwenye dhambi nyumbani mwa Mfarisayo, Yesu anasema bila
kupepesa macho yake, “kwa ajili ya hayo nakuambia, Amesamehewa dhambi zake
ambazo ni nyingi, kwa kuwa amependa sana; lakini asamehewaye kidogo, huyo
hupenda kidogo,” Lk 7:47. Licha ya udhaifu wake kama mwanadamu, mwanamke huyu
akuacha kuonja upendo wa Mungu na kurudisha upendo huo kwa Yesu kadiri ya uwezo
wake. Anafanya tendo hili kwa
kumdondoshea machozi miguu ya Yesu, na kuipangusa kwa nywele za kichwa
chake, hakuacha kumbusu sana miguu ya Yesu, na kumpaka miguu ya Yesu marhamu.
Ni ukweli kwamba, “hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wowote. Tukipenda, Mungu
hukaa ndani yetu, na pendo lake limekamilika ndani yetu,” 1Yoh 4:12. Msukumo
huu wa upendo haumzuii Yesu kumwambia mwanamke huyu kuwa, “Imani yako
imekuokoa, enenda zako kwa amani,” Lk 7:50. Kila mmoja wetu anahesabiwa haki
mbele za Mungu si kwa kile alicho, bali ni upendo, huruma, na msamaha wake Mungu
mwenyewe. “Maana ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya
roho ya binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna
ayafahamuye ila Roho wa Mungu,” IKor 2:11.
Yesu
anaonyesha ugumu wa mioyo ya hao wasiopenda kuongoka na wasiopenda kuwatambua
wadhambi. Ukweli ni kwamba wote walio wana wa Mungu hutambua hekima ya Mungu.
Hekima hii ya Mungu ndiyo Huruma yake. Hivyo wenye mioyo migumu hawawezi
kufurahia kuongoka kwa wengine. Dhambi kubwa ya mtu ni pale anaposhindwa kujua
kuwa yeye ni mdhambi mbele ya Mungu. Mtu wa leo hakubali dhambi zake, na
hajisikii kuwa ni mdhambi. Hali hii utuweka mbali na habari njema ya wokovu. Ni
kweli kwamba kadiri tunavyokuwa katika maisha ya kiroho ndivyo hivyo tunavyojisikia
masikini zaidi na wahitaji wa huruma ya Mungu. Neema ya Mungu utufanya tuishi
katika kweli na utuwezesha kugundua hitaji kubwa la kuwa na Mungu.
Je, ndugu
yangu unalo la kumficha Mungu? Basi kama kweli tunataka kuponywa kama mwanamke huyu
na kama alivyoponywa Mfalme Daudi, yatupasa kujisalimisha kila siku mbele za
Mungu. Tunafanya hivyo tukijua kwamba, “wala hakuna kiumbe kisichokuwa wazi
mbele zake, lakini vitu vyote vi utupu na kufunuliwa machoni pake yeye aliye na
mambo yetu,” Ebr 4:13. Hapo vipi ndugu yangu?
Padre
huruma ya Mungu ni mhamasishaji mzuri sana wa maisha ya Jumuiya Ndogondogo za
Kikristo. Kama tujuavyo jumuiya hizi ndilo taswira ya wazi la Kanisa kama mwili
wa Kristo. Hapa tunajuana vizuri siyo tu katika urefu na ufupi wetu, wembamba
na unene wetu, bali pia tabia zetu na historia zetu nzuri na mbaya. Hivyo,
Padre huruma ya Mungu kwa wiki mara mbili husali na moja ya jumuiya zake katika
Parokia yake ya Bikira Maria Mama wa Mateso.
Dada
Natalia ni mmoja wa wana Jumuiya ya Moyo Mtakatifu wa Yesu ambayo ndiyo zamu
yao kutembelewa na Padre huruma ya Mungu. Dada huyu Natalia ni mwana jumuiya wa
kawaida, ila mwenye furaha, uchangamfu na mwenye kujitoa kwenye jumuiya yake
hasa katika swala la mapambo na maandalizi ya altare pale kunapokuwa na
adhimisho la Misa Takatifu katika jumuiya. Huduma hii kwa baadhi ya wanajumuiya
hawakuwa wanapendezwa nayo kwa sababu historia ya maisha Dada Natali haikuwa
nzuri.
Licha ya
kufanya toba ya kweli na kumrudia Mungu, Natalia hakupenda kuficha hali yake na
afya yake kwa baadhi ya wana Jumuiya, ikiwa ni pamoja na viongozi wake wa
Jumuiya. Na kwa sasa Dada huyu ni mwadhirika. Ukweli huu kwa wana jumuiya
wengine waliuchukulia kwa woga sana kiasi kwamba walitaka pia kumzuia kuendelea
kutoa huduma ile aliyokuwa akiitoa kama nilivyosema hapo juu. Mbaya zaidi
hawakupenda asalimiane na Padre huruma ya Mungu. Mmoja wa kiongozi wa Jumuiya
hii aliwahi hata kumvuta sikio na kumwambia asiwe anasalimiana na Padre kwa
kumshika mkono kabla ya Misa na hata wakati wa kutakiana amani.
Hakina
Dada huyu alikuwa na wakati mgumu sana. Hata hivyo hakukatishwa tamaa kutoshiriki
na wana jumuiya wenzake katika sala. Basi siku ile katika adhimisho la Misa
Takatifu na ulipofika muda wa kutakiana amani, Padre huruma ya Mungu bila kujua
chochote alimwendea moja kwa moja na kumpatia mkono wa amani kwa sababu
alimwona kasimama mwenyewe tu kwa muda mrefu. Dada Natalia kwa tendo lile ya
Padre kumpa mkono wa Amani lilimfanya ashindwe kujizuia na kuanza kububujika
machozi. Padre hakuelewa chochote na aliendelea na adhimisho lile la Misa hadi
mwisho.
Mwisho wa
adhimisho lile la Misa ile Takatifu, Padre huruma ya Mungu alitaka kujua
kulikoni. Natalia alimweleza Padre huruma ya Mungu historia yote ya maisha
yake. Na mwisho Natalia alimwambia Padre; “pamoja na hayo yaliyotokea huko
nyuma katika maisha yangu, leo najisikia furaha kubwa sana kunitakia amani.
Hakika nimeonja upendo wa Mungu na nina furaha kubwa sana moyoni mwangu. Asante
sana Padre,”
Padre
huruma ya Mungu alimwambia Dada Natalia huku akiwa amelishika bega lake, “Mungu
asingekuwa na huruma na kusamehe dhambi, mbinguni kungekuwa wazi kabisa.
Watakatifu tayari wana historia yao ya jana, mimi na wewe tulio wadhambi bado
tuna leo na kesho yetu kama tukijaliwa. Basi tuitumie leo yetu vizuri na kesho
na kesho hiyo kama tukijaliwa, ili nasi siku moja tuwe na historia yetu kama
watakatifu.” Padre huruma ya Mungu alimkubatia, na kisha kuingia naye ndani kwa
ajili ya chakula kile kilichoandaliwa na jumuiya. Baadhi ya wanajumuiya hawakuacha kumkazia
macho Natalia kama mijusi.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“na
wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa;
nao ni Mariamu aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba, na Yoana mkewe Kuza, wakili wake
Herode, na Susana, na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao,” Lk
8:2-3
Tusali:
Ee Yesu, uliyetupenda upeo, nijalie pendo lako hilo la kweli na lisilo na ubaguzi kwa kila mmoja ninayekutana
naye na katika hali yoyote ile. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario