domingo, 19 de junio de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 12 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 12 YA MWAKA-C
Somo: 2Fal 19:9b-11, 14-21, 31-35a, 36
Zab: 48:2-3a, 3b-4, 10-11
Injili: Mt 7:6, 12-14
Nukuu:
 “Alituma wajumbe kwa Hezekia mara ya pili, kusema, Mwambieni Hezekia, mfalme wa Yuda, maneno haya, mkisema, Asikudanganye Mungu wako unayemtumaini, akisema, Yerusalemu hautatiwa katika mikono ya mfalme wa Ashuru,” 2Fal 19:9-10 

 “Naye Hezekia akaomba mbele za Bwana, akasema, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, ukaaye juu ya makerubi, wewe, naam, wewe peke yako, ndiwe Mungu wa falme zote za dunia; wewe ndiwe uliyeziumba mbingu na nchi,” 2Fal 19:15 

 “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii,” Mt 7:12

 “Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache,” Mt 7:14

TAFAKARI: “Huruma na Neema ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu. Moyo wa toba na majuto ya kweli huyajenga upya mahusiano yetu na Mungu.

Wapendwa wana wa Mungu, tulitafakaripo neno la uzima wetu tunagundua kwamba, ‘Huruma na Neema ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu.’ Na hata pamoja na ukweli huu, ‘moyo wa toba na majuto ya kweli huyajenga tena upya mahusiano yetu na Mungu.’ Mungu wetu ni hai na hutujalia uhai kila siku bila kujali njia zetu nzuri au mbaya. Je, hujiulizi pamoja na maovu yako bado anakupa pumzi ya kupumua? Je, tungeitajika kulipa kodi ya hewa tunayopumua, ni nani kati yetu angelipa kwa wakati na muda wote? Je, hili lisingekuwa jambo la kukufanya ujirudi na kumrudia Mungu ambaye anao uwezo wa kusimamisha mtiririko wa pumzi unayovuta bure? Kama nakuambia uongo, basi niambie ni siku gani utakufa hata kama kufa ni kweli isiyopinga.

Ndugu yangu, unapojaribu kupata maana ya maisha yako hapa duniani, na bila kuchoka kudadisi kesho itakuaje, lazima utakiri tu kwamba kuna sehemu kubwa ya maisha yako bado haijulikani sawasawa, na inabaki kuwa fumbo kwako kama mwanadamu mwenye ukomo fulani wa asiyeyajua yote katika ukamilifu wake. Hili tusilolijua sawasawa na hatuchoki kutaka kujua ukweli wake, uwazi huo unatusukuma kadiri ya ufahamu wetu kujua lazima kuna kitu zaidi yetu na chenye ukamilifu wote kwa sababu cha fanya na kusema kile tusichokijua. Uwazi huu unazibwa na Mungu mwenyewe anayejifunua kwetu kupitia Maandiko Matakatifu, na yale yote tunayokutana nayo kila siku katika maisha yetu. Kwa ufahamu wetu hatuupi maana yoyote kwa ulimwengu huu tunaishi kama jukumu la muda mfupi, bali kadiri tuutafakaripo ulimwengu huu tunaoishi kwa muda mfupi unatupa maana ya maisha yetu. Hatua hii ya kutokuona yote sawa na yapo kama yalivyo, ndiyo itusogezayo katika uwepo wa Mungu kama nguvu na uwezo wa yote kama yalivyo kwa utaratibu na ujumla wake pasipo ugonganishi wowote ule. Nguvu hii ya ndani na yenye kuyafanya yote kila moja katika upekee wake, na yote katika mwelekeo wa utulivu na wenye kuufunua umilele katika kila kimoja wapo, ndiye Mungu Mwenyewe.

 Wapendwa wana wa Mungu, tuutazamapo ukweli huu ambao hujionyesha wazi katika maisha yetu ya kila siku, kwa hofu ya Mungu tunatambua kwamba pamoja na udhaifu wetu wa kibinadamu, ‘Neema na huruama ya Mungu ni kubwa kuliko udhaifu wetu, yaani, dhambi zetu.’ Pamoja na Mamlaka na nguvu za kifalme walizokuwa nazo Taifa la Israeli, walijikuta mateka pale walipoukataa uwepo wa Mungu katika maisha yao na kutegemea nguvu na akili zao. Kejeli kama hizi ndizo hata mataifa yaliyowazunguka walizifanya pale walipowanyanyapaa. Mfalme Ashuru anatuma ujumbe kwa mfalme wa Yuda-Hezekia kumkejeli kuhusu Mungu waliyekuwa wana mwamini. Maneno ya ujimbe huo yalisema hivi; Asikudanganye Mungu wako unayemtumaini, akisema, Yerusalemu hautatiwa katika mikono ya mfalme wa Ashuru,” 2Fal 19:9-10. Hata hivyo, Mfalme Hezekia hakushtushwa na ujumbe ule, 2Fal 19:14, licha ya kwamba alionja udhaifu wao kama Taifa mbele ya Mungu. Bado walimtegemea Mungu atafanya tu chochote wanapomwelekea kwa majuto ya kweli. Naye Hezekia akaomba mbele za Bwana, akasema, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, ukaaye juu ya makerubi, wewe, naam, wewe peke yako, ndiwe Mungu wa falme zote za dunia; wewe ndiwe uliyeziumba mbingu na nchi,” 2Fal 19:15. Toba yao kama Taifa inautambua uwepo wa Mungu, tena aliye hai. Wanatambua pia si haki Mungu wao aliye hai kuziakiwa, 2Fal 19:16. Wito wao ni mwamba Mungu atege sikio lake tena na kuwatoa katika mtego na mkono wa adui wao. Basi sasa, Ee Bwana, Mungu wetu, utuokoe na mkono wake, nakusihi, ili kwamba falme zote za dunia zipate kujua ya kuwa wewe ndiwe Bwana Mungu, wewe peke yako,” 2Fal 19:19. Sala hii ya Mfalme Hezekia ni sala ya kujiachia pasipo kujibakiza. Kama ni silaha ya vita bali katumia risasi ya mwisho na yenye matumaini yote. Ndipo Isaya, mwana wa Amozi, akapeleka ujumbe kwa Hezekia, akisema, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kwa kuwa umeniomba juu ya Senakeribu, mfalme wa Ashuru, mimi nimekusikia,” 2Fal 19:20. Tunapojiachi kwa Mungu bila kujibakiza katika toba na majuto ya kweli kama Taifa au mmoja mmoja ya chukizo lake mbele ya Mungu, neema na huruma ya Mungu ni dhahiri kwetu. Mungu kamuumba kila mmoja wetu aishi milele na asipotee. Raha ya Mungu ni kutupata tena na tena.

Ndugu yangu, ufanyapo toba na majuto ya kweli, Mungu haishi kukupa neema na huruma yake tu, bali uyapanga upya maisha yako katika mwelekeo ulio sahihi na wenye umilele. Na hivi ndiyo alivyofanya kwa wana wa Israeli chini ya Mfalme Hezekia kupitia mjumbe wake Nabii Isaya; Basi Bwana asema hivi katika habari za mfalme wa Ashuru, Yeye hatauingia mji huu, wala hatapiga mshale hapa, wala hatakuja mbele yake kwa ngao, wala hatajenga boma juu yake,” 2Fal 19:32. Je, tunapoteza nini tunapojisalimisha mikoni mwa Mungu, ambaye yupo tayari kuanza yote katika maisha yetu? Tatizo ni kiburu na kutokushindwa kwetu. Mwisho wa siku tunakupali kufa na tai zetu shingoni, na siyo kuukubali udhaifu wetu kama wanadamu. Mungu yupo tayari kuyafanya yote sasa na baadaye pale tu tunapoukiri kwa utashi wetu uwepo wake. Kwa kufanya toba na majuto ya kweli, Mungu haturudishii tu imani tuliyoipoteza, bali ufikiria pia mambo yajayo kuhusu maisha yetu. Na hivi ndivyo alivyofanya kwa Mfalme Hezekia na watu wake, kwamba, nitaulinda mji huu, niuokoe, kwa ajili yangu mwenyewe, na kwa ajili ya Daudi, mtumishi wangu,” 2Fal 19:34. Na ndiyo alivyotekeleza ahadi yake, “Ikawa usiku uo huo malaika wa Bwana alitoka, akakiingia kituo cha Waashuri, akawapiga watu mia na themanini na tano elfu,” 2Fal 19:36b. Basi Mungu anavyotutendea mambo makuu kama haya ni wito kwetu pia kutenda wema kwa kila mmoja wetu. Huku ni kusadhifu neema na huruma ya Mungu kwetu.

Wapendwa wana wa Mungu, kwa neema na huruma yake Mungu, katika Injili ya leo, Bwana wetu Yesu Kristo anatupatia suluhu lenye upana uliozidi mipaka ya kifamilia. Suluhu hilo ni kuwa macho muda wote katika kujali na kuwajibika tukifanya jambo hili la msingi, yaani, “yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii,” Mt 7:12. Maana yake ni kwamba, jambo lililo jema ni jema tu siyo kwako ila na hata kwa mwenzako. Basi litende kama lililovyo na vizuri zaidi litende kama lako. Hufanyavyo hivyo, jua ndiyo Mungu apendavyo liwe hivyo kwani hiyo ndiyo hamu ya moyo wake, ambayo kwetu ni sheria. Sheria hii ya  “upendo,” twaifanya si kwakushurutishwa, bali ndicho kiini cha maisha yetu, na hofu yetu kwa Mungu.

Ndugu yangu tunayesafiri wote katika tafakari hii, jambo hilo hapo juu tusipolifanya, na hasa kwa ndugu na wale wote wanaotuzunguka, bado hatujajua thamani ya utu wetu, na upendo wa Mungu Baba kwetu. Hapa tunapewa angalizo: Msiwape mbwa kilicho kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe, wasije wakazikanyaga chini ya miguu yao, wakageuka na kuwararua,” Mt 7:6. Mara nyingi tunavipa vitu heshima kuliko utu wa mtu. Leo na hasa ulaya, mbwa au paka anaweza kugaramiwa na kupewa upendo wa hali ya juu kuliko ombaomba aliye mlangoni mwa Kanisa siku nzima. Mbwa huvalishwa nguo za joto wakati wa baridi, ila masikini huyu hana hata koti kuufunika mwili wake. Binadamu na utu wake atabakia kuwa hivyo hata kama mfumo wa maisha yake utakuwa mbovu au kutokuridhisha. Mbwa au Nguruwe atabakia kuwa nguruwe hata kama tutajaribu kumpandisha na kuwa na hali kama sisi. Sababu ni kwamba yale tuwafanyiayo yenye mastahili ya kibinadamu kwao hayana maana na hayana thamani yoyote kwao. Wanyama wapewe stahiki za wanyama, na binadamu apewe heshima yake kama binadamu licha ya umaskini wake. Ujumbe hapa ni kwamba tuwe na busara kadiri ya stahiki yatu kama wanadamu. Kutokufanya hivyo ni kukosa busara na kupoteza hadhi yetu na utu wetu. Tendo hili ni sawa na pete ya dhahabu katika pua ya nguruwe ambayo ulinganishwa na mwanamke asiye na busara/akili. Kwa nguruwe pete hiyo haina thamani. Nguruwe uweza kuiburuza atakavyo. Na hii ndiyo maana ya maneno haya, kama pete ya dhahabu katika pua ya nguruwe, Kadhalika mwanamke mzuri asiye na akili,” Mit 11:22.

Hapa ndipo penye mtihani mkubwa wa maisha, na tafsiri nzima ya maisha ya umilele ikiwa ni pamoja na hukumu yake. Yesu Kristo anatupatia njia ya kufuata tusijepigwa na mshangao siku ya mwisho. Ingieni kwa kupitia mlango ulio mwembamba; maana mlango ni mpana, na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo,” Mt 7:13. Uzuri wa njia pana ni kwamba kunauwezekano mkubwa wa kubeba kila kitu, yaani ponda mali kadiri ya uwezo wako, ila usisahau kifo kwani huja kwa mtindo huo huo. Na hapo ndipo penye ubaya wa njia pana. Njia nyembamba hutukataza baadhi ya mambo kutokuchukuliana nayo. Wembamba wa njia hutunyenyekesha namna ya kutembea katika njia ile ili tufike kwa usalama mwisho wa safari. Hatuwezi kujiendea kama tutakavyo. Yatupasa kufuata mwelekeo wa njia kama ulivyo. Njia nyembamba inatuadhabisha namna ya kuenenda kwa faida yetu wenyewe. Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache,” Mt 7:14. Waionao njia hii ni wachache kwa sababu hulka ya binadamu si kupata mateso. Hulka ya binadamu ni kuitafuta furaha. Ndugu yangu, elewa hakuna utukufu pasipo msalaba. Hivyo njia nyembamba ndiyo njia sahihi kuelekea uzima wa milele, licha ya machungu na mapaswa yake.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii,” Mt 7:12


Tusali:-Ee Yesu, tujulishe njia yako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario