JUMATANO WIKI YA 12 YA MWAKA-C
Somo: 2Fal 22:8-13; 23:1-3
Zab: 119:33, 34, 36, 37, 40
Injili: Mt 7:15-20
Nukuu:
“Jihadharini na manabii
wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni
mbwa-mwitu wakali,” Mt 7:15
“Vivyo hivyo kila mti
mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya,” Mt 7:17
“Mti mwema hauwezi
kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri,” Mt 7:18
“Mfalme akamwamuru Hilkia kuhani, na Ahikamu, mwana wa Shafani,
na Akbori, mwana wa Mikaya, na Shafani mwandishi, na Asaya, mtumishi wa mfalme
akasema, Enendeni, mkamwulize
Bwana kwa ajili yangu, na kwa ajili ya watu hawa, na kwa ajili ya Yuda yote,
katika habari za maneno ya kitabu hiki kilichoonekana; kwa kuwa hasira ya Bwana
ni kubwa aliyotukasirikia, kwa sababu baba zetu hawakuyaangalia maneno ya
kitabu hiki, kufanya kama hayo yote tuliyoandikiwa,” 2Fal 22:12-13
“Mfalme
akasimama karibu na nguzo, akafanya agano mbele za Bwana, kumfuata Bwana, na
kuyashika maagizo yake, na shuhuda zake, na amri zake, kwa moyo wake wote, na
kwa roho yake yote, na kuyathibitisha maneno ya agano hilo yaliyoandikwa katika
kitabu hicho; nao watu wote wakalikubali agano lile,” 2Fal 23:3
TAFAKARI: “Maisha yako ni dhamana.”
Wapendwa wana wa Mungu, ‘maisha yako hapa duniani ni dhamana.’ Maisha
ni dhamana tunapo utafakari mfano ule wa talanta, Mt 25:14-28. Ni kwa mtazamo
huo masomo ya leo yanatutaka tuyaone maisha yetu kuwa ni dhamana hapa duniani.
Hapo ulipo yakupasa “kuwa zaidi” ya kile ulicho katika kweli, haki, na wema. Ni
kwa mizania hiyo “kila mwenye kitu
atapewa, na kuongezewa tele; lakini asiye na kitu, hata kile alicho nacho
atanyang'anywa,” Mt 25:29. Kuyaona maisha kuwa dhamana ni kukubali
kutojihesabia haki kwa chochote kile ufanyacho hata kama ni sababu ya furaha
yako na wale wanaokuzunguka. Kwa maana nyingine ni kutokukubali kujilinganisha
na vitu. Wewe kama mwanadamu, uliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, na ndivyo niaminivyo, umeumbwa ili uishi milele.
Kuyaona maisha katika mtazamo huu ni hatua muhimu sana ya kuyaishi maisha huru
katika unyenyekevu wa kweli.
Maisha
huru na ya unyenyekevu wa kweli kamwe hayasukumwi na kile tulicho katika maana
ya nafasi na madaraka tuliyonayo katika jamii. Ila ni maisha yenye utayari wa kusikia
yasemwayo juu yako, na kusikia zaidi ya kusema. Ni maisha yanayosukumwa zaidi
na tafakari ya ndani kwani kile tusichotaka kusikia mara nyingi ndicho tulicho.
Huwezi kufika kule usipotaka kupasikia kama huna maisha ya tafakari ya ndani.
La sivyo mambo yako na maamuzi yako yataongozwa na vionjo vyako na wale
wanaokuzunguka ili mradi tu kuujenga uhusiano bandia na usiodumu.
Mfalme
Yosia aliyetawazwa kuwa Mfalme akiwa na umri wa miaka minane, na kutawala kwa muda
wa miaka thalathini na moja, 2Fal 22:1, hakuwa kama mtangulizi wake, yaani Baba
yake. Mfalme Yosia alijaliwa masikio ya kusikia na kuyatafakari yale
aliyoambiwa na wale waliomshauri ambao kwa hakika walikuwa na hofu ya Mungu
kama kuhani mkuu wa wakati wake, yaani Hilkia. Mfalme licha ya mamlaka yake na
nafasi yake hakuacha kuomba ushauri ili asimame daima katika kweli na haki
katika utawala wake. Licha ya kuzirarua nguo zake za kifalme kama ishara ya
kukiri udhaifu wake alipoambiwa ukweli juu ya hali yake, 2Fal 22:11, hakuishia
hapo. “Mfalme akamwamuru Hilkia kuhani, na Ahikamu, mwana wa
Shafani, na Akbori, mwana wa Mikaya, na Shafani mwandishi, na Asaya, mtumishi
wa mfalme akasema, Enendeni,
mkamwulize Bwana kwa ajili yangu, na kwa ajili ya watu hawa, na kwa ajili ya
Yuda yote, katika habari za maneno ya kitabu hiki kilichoonekana; kwa kuwa
hasira ya Bwana ni kubwa aliyotukasirikia, kwa sababu baba zetu hawakuyaangalia
maneno ya kitabu hiki, kufanya kama hayo yote tuliyoandikiwa,” 2Fal 22:12-13
Licha
ya nafasi aliyokuwa nayo mfalme alifahamu fiki mipaka yake kama mwanadamu
kwamba hawezi kufanya yote kwa wakati wote. Na pale aliposhauriwa kwenda
kinyume na matakwa ya Mungu hakuacha kufanya agano jipya tena na Mungu.
Kiongozi asiyekuwa na hofu ya Mungu ni hatari sana. Mfalme Yosia hakuwa hivyo.
Daima aliona uwezo na mipaka yake kama mwanadamu, na alitambua nafasi ya Mungu
katika maisha yake, na wale aliopewa dhamana kuwaongoza. Na hivi ndiyo
ilivyokuwa pale mambo yalipokwenda ndivyo sivyo, “Mfalme
akasimama karibu na nguzo, akafanya agano mbele za Bwana, kumfuata Bwana, na
kuyashika maagizo yake, na shuhuda zake, na amri zake, kwa moyo wake wote, na
kwa roho yake yote, na kuyathibitisha maneno ya agano hilo yaliyoandikwa katika
kitabu hicho; nao watu wote wakalikubali agano lile,” 2Fal 23:3. Wengi wa
watawala wetu leo ni sawa na miungu watu. Kumgusa mfalme (viongozi wetu) leo
katika kweli na haki katika mazingira yetu ni sawa na kuigusa mboni ya jicho la
mamba. Hakika hutakuwa salama!
Katika
injili, Yesu anatufundisha hali ya uhusiano wetu na Mungu ipasavyo kuwa. Kitu
cha kwanza kabisa katika nyakati zetu, Yesu anatuwasa, kwa kusema, “Jihadharini
na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa
ndani ni mbwa-mwitu wakali,” Mt 7:15. Watu hawa waongo si kwenye nyanja tu za
Imani/kidini, bali hata kwenye nyanja za kijamii. Maneno haya ya Yesu
yanaujumbe mahususi hasa kwetu hasa pale tunapoona utofauti mkubwa kati ya kile
asemacho mtu (aliyepewa dhamana na umma) na baada ya kukupiga mgongo kufanya
tofauti kabisa. Watu hawa wameupata umaarufu wa haraka sana kwa kuihubiri amani
midomoni mwao, ila ndani ya mioyo yao wamejaa chuki, visasi, na vita
inayosubiri muda tu kulipuka. Tuwapima watu hawa kwa matendo yao kwa sababu,
“kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya,” Mt
7:17. Kama historia yake imetawaliwa na wema na hofu ya Mungu, basi kile
atuambiacho kitakuwa na mashiko. La sivyo ni sawa na kutegemea ndizi mbuvu
kutoka kwenye mti wa limao. “Mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti
mwovu kuzaa matunda mazuri,” Mt 7:18. Mara
zote mtu hutoa kile alichokuwa nacho. Huwezi kutoa kile usichokuwa nacho.
Ni kwa mantiki hii ya kutoa kile
ulichonacho ndivyo kila mmoja wetu kaitwa kwa namna ya pekee kuishi wito wake hapa
duniani. Ni katika kuishi hiki ulicho kwa ukamilifu na uaminifu wake
kutakakompendeza Mungu. Tendo hilo litakuwa sababu ya neema zake kwako ili
ufikie taji lile alilokuandalia yaani utakatifu wako. Kama wewe ni mlei,
hulazimiki kuishi maisha ya kitawa au ukleri ili ufikie taji hili. Kaa pale
ulipo kwa uaminifu, na hapo ndipo utakapo kutana naye. Hiyo ndiyo Galilaya yako
(Mk 16:7). Kila mmoja wetu akae nafasi yake kwa uaminifu na hapo ndipo
tutakapokutana naye. Maneno haya ya Yesu ‘mti mwema hauwezi kuzaa matunda
mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri,’ yanatuashiria hukumu yetu ya
mwisho. Kwa kuishi kwetu hapa duniani kila mmoja wetu lazima “awe zaidi.” Haupo
hapa duniani kwa bahati mbaya. Yakupasa kuwa zaidi pale ulipo kadiri ya wito
wako. Usipokuwa zaidi katika mema ujue kifuatacho ni kuhukumiwa milele. “Kila
mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni,” Mt 7:19. Je, wasubiri hali
hiyo ikufike?
“Mti mwema hauwezi kuzaa matunda
mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri,” Mt 7:18
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, yakamilishe yote mema yaliyo ndani ya moyo na nafsi zetu kwa sifa
na utukufu wako, na watu wako. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario