JUMAPILI YA 13 YA MWAKA-C
Somo
I: 1Fal 19:16b, 19-21
Zab: 16: 1-2, 5, 7-8, 9-10, 11 (K) 5
Somo
II: Gal 4:31b-5:1, 13-18
Injili:
Lk 9:51-62
Nukuu:
“Eliya akapita karibu naye, akatupa vazi lake juu yake,” 1Fal
19:19b
“Naye akawaacha ng'ombe, akamfuata Eliya mbio, akasema, Nipe ruhusa,
nakuomba, nimbusu baba yangu na mama yangu, kisha mimi nitakufuata. Akamwambia,
Enenda, urudi; ni nini niliyokutendea?” 1Fal 19:20
“wala
msinaswe tena chini ya kongwa la utumwa,” Gal 5:1b
“uhuru
wenu usiwe sababu ya kuufuata mwili, bali tumikianeni kwa upendo,” Gal 5:13b
“Kwa maana Mwana
wa Adamu hakuja kuziangamiza roho za watu, bali kuziokoa. Wakaondoka wakaenda
mpaka kijiji kingine,” Lk 9:56
“Yesu akamwambia,
Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa
Mungu,” Lk 9:62
TAFAKARI:
“Mwana wa Adamu hakuja kuziangamiza roho za watu, bali kuziokoa.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya kumi na tatu ya mwaka “C” wa Kanisa.
Kwa namna ya pekee leo Mama Kanisa anatualika tumtafakari huyu Mwana wa Adamu
‘ni nani kwetu kama wafuasi wake katika mwono wa Kanisa,’ na pili, Mwana wa
Adamu ‘ni nani katika maisha yako kama mfuasi wake.’ Msingi wa haya yote mawili
umejengwa katika imani ya kweli juu ya Kristo Yesu. Imani hii ndiyo kielelezo
na namna tunavyochukulia ufuasi wetu. Mimi na wewe tunayo maswali ya kujibu kwa
kina katika uhalisia huu wa Imani ya kweli, yaani, katika ufahamu wa kutosha,
na wenye maana. Je, yatosha kukiri
na kumfuata Yesu popote atakapo kuwa kama upepo na bendera? Je, katika ufuasi
huo natambua mapaswa yake? Je, nipo imara na nitakuwa imara katika nyakati zote
na hasa zile nyakati za sintofahamu? Ushirika wako hai na Kristo ndiyo salama
na ponya yako. ‘Mwana wa Adamu hakuja kuziangamiza roho za watu, bali
kuziokoa.’ Wokovu huu ambao ni bure kwetu na kusiko kwa mastahili yetu binafsi,
unatagemea utayari wako.
Kadiri ya Injili ya leo, Yesu anampa angalizo mtu yule
aliyekutana naye njiani na kusema yupo tayari kufuatana naye ko kote
atakapokwenda. “Yesu akamwambia, Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana
viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake,” Lk 9:58. Kwa
maneno mengine Yesu anatuambia hakuna maslahi yo yote kibinadamu zaidi ya
maisha ya umilele kutoka kwake. Kama ni swala la utajiri na kuwa na maisha
mazuri siyo kipaumbele cha kwanza katika ufuasi wetu kwake. “Bali utafuteni
kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Mt 6:9. Kazi yetu
ya kwanza ni kuutafuta ‘kwanza ufalme wa mbinguni’ na mengine yote tutapewa kwa
ziada na kadiri ya mahitaji yetu.
Jambo la
pili na la muhimu tunalofundishwa leo kuhusu Imani ya kweli na ufuasi usio na
mawaa ni ‘utambuzi wa kweli na kujua nafasi ya Mungu katika maisha yako.’ Bila
shaka wengi wetu tuna hofu ya kifo. Hata hivyo, kifo kipo pale pale tupende au
tusipende. Na kama umezaliwa basi ipo siku utakufa. Kuzaliwa si lazima, bali
kufa ni lazima kama umezaliwa. Kwa hiyo katika mantiki hii ya kifo na uhalisia
wake, hatupaswi kukiogopa. Yatupasa kuishinda hofu ya kifo ili tuwe tayari
kukipokea kifo kama njia pekee ya maisha yale baada ya kifo hapa duniani,
kuishi umilele. Hakutakuwa na maisha ya umilele baadaye bila kupita katika
fumbo hili la kifo.
Hivyo
Yesu anamtoa hofu ndugu yule aliyetoa hoja ya kwenda kwanza kumzika Baba yake
ndipo amfuate. Naye Yesu anamwambia, “Waache wafu wawazike wafu wao; bali wewe
enenda ukautangaze ufalme wa Mungu,” Lk 9:60. Je, Yesu anatukataza kuwazika
wazazi wetu? La hasha! Kufanya hivyo angekuwa anaenda kinyumbe na ile amri ya
nne ya Mungu, “waheshimu baba yako na mama yako; siku zako zipate kuwa nyingi
katika nchi upewayo na Bwana, Mungu wako,” Kut 20:12. Yesu anachotaka kukuambia
wewe na mimi leo ni kwamba, kifo ni ‘kweli isiyopingika na hivyo shughuli zake
na mazingira ya yake, isiwe sababu ya kutokupokea ujumbe wake wa uzima wa
milele.
Na jambo
la tatu na la mwisho tunalofundishwa leo kuhusu Imani na ufuasi thabiti ni
‘kule kuwa na msimamo thabiti wa wito ulio nao na kutunza kile ulichoitiwa.’
Hii ni pamoja na kutokuwa ndumilakuwili au kigeugeu cha kutaka ‘kutazama au
kurudi nyuma ulikotoka kwa malengo ya kujaribu tena.’ Bali lipaswalo ni kujenga uaminifu na utayari wa kutimiza kile ulichoitwa na
kukubali bila shuruti kwa sifa na utukufu wake Mungu. Na hicho ulichoitwa na
kukubali kwa hiari yake kiwe mwitikio chanya hasa pale linapojitokeza swala ya
huduma kwa watu au umma. Wengi wetu baada ya
kubatizwa tumerudi kuishi maisha ya kipagani kabisa. Na wengi katika kundi hili
wamekuwa washirikina wa kupindukia na kuongozwa na nguvu za giza ili hali
wamejivika visakramenti mwili mzima. Ushirikina ‘ni kuamini nguvu fulani kutoka
kitu fulani kisicho na uhusiano kimantiki.’ Katika hili Yesu anatupa angalizo,
na kusema, “Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa
ufalme wa Mungu,” Lk 9:62. Kwa maneno mengine ni heri kuwa baridi au joto,
kuliko kuwa vuguvugu katika Imani.
Ni
katika mwono huu wa kuipokea habari njema ya wokovu wetu, tunaona mshabiano wa
maneno ya Yesu na kile alichokifanya Elisha. Elisha kuwa Nabii kulikuwa hivi; “Eliya akapita karibu
naye, akatupa vazi lake juu yake,” 1Fal 19:19b. Hizi ndizo ishara au alama
zinazotusogeza kwenye kiapo. ‘Ndiyo’ ya Elisha ilikuwa hivi; “Naye
akawaacha ng'ombe, akamfuata Eliya mbio, akasema, Nipe ruhusa, nakuomba,
nimbusu baba yangu na mama yangu, kisha mimi nitakufuata. Akamwambia, Enenda,
urudi,” 1Fal 19:20ab. Na ‘ndiyo’ ya Elisha inakuwa ‘ndiyo kweli,’ pale
Elisha alipoinuka, akamfuata Eliya, akamhudumia, 1Fal 19:21b. Tendo hili ndilo
nililolisema hapo juu kwamba, ‘kujenga uaminifu
na utayari wetu wa kutimiza kile tulichokubaliana kwa sifa na utukufu wake
Mungu, na hasa pale linapojitokeza swala ya huduma kwa watu au umma.’ Je,
kusema tu na kuwa tayari inatosha? La hasha! Wapo Wakristo kati yetu wao ni
‘imani tu inatosha,’ na wapo wengine wao ni ‘kulihubiri neno tu inatosha.’ Kuwa
mfuasi wa Kristo kwa kufanya moja ya hayo mawili utakuwa bado hujalifikia lengo
na sababu ya ufuasi wako. Kumbe yote mawili yanaitajika na mwisho wa siku yawe
chachu ya wewe kuzaliwa upya katika maana ya kuushinda ubinadamu wako ili
kuuvaa utu upya kila siku, yaani, utakatifu. Na hili ndilo analotuambia Mtume
Paulo leo kwamba, “wala
msinaswe tena chini ya kongwa la utumwa,” Gal 5:1b. Kongwa la utumwa ni kuurudia ubinadamu wako
katika hali ya upofu, hali ya giza, na kukosa nuru halisi ya Kristo Yesu. “Kulikuwako
Nuru halisi, amtiaye nuru kila mtu, akija katika ulimwengu. Na wote
waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio
jina lake; waliozaliwa, si kwa damu, wala si kwa mapenzi ya mwili,
wala si kwa mapenzi ya mtu, bali kwa Mungu,” Yoh 1:9, 12-13.
Kumbe kama asemavyo
Mtume Paulo, “uhuru wenu usiwe sababu ya
kuufuata mwili, bali tumikianeni kwa upendo,” Gal 5:13b. Huwezi kubagua au
kujibagua kama kweli una upendo wa kweli. Upendo wa kweli ni msukomo wa wazi na utayari wa kufanya yote
kwa sifa na utukufu wa Mungu kwa nuru ile ya Kristo iliyoko ndani mwako. Upendo
huu ndiyo tunao uona kwa wale wamisionari wa kwanza waliokuwa tayari kwenda
wasipopajua kuifikisha habari njema ya wokovu kwa watu wote.
Ni katika mantiki hii
ya upendo kwamba sheria hukosa nguvu na wakati mwingine kutohitajika au
kuonekana kama upendo wa kweli unatawala maisha ya watu. Na anaye mjali
mwenzake na kuwa tayari kutenda jema kwa ajili yake, haki utawala ndani ya moyo
wa watu huyo. “Maana
torati yote imetimilika katika neno moja, nalo ni hili, Umpende jirani yako
kama nafsi yako,” Gal 5:14. Huku ndiko kuenenda kwa roho na kuvithibiti vilema
vya miili wako, ikiwa ni pamoja na tamaa zake, Gal 5:16. “Kwa
sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa
maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka,” Gal 5:17. Lakini
dereva wa maisha yako akiwa Roho wa Mungu, utaruhusu ndani yako moyo usio na
ubaguzi na kujitoa kwa upendo bila kujibakiza. Na huu ndio ukweli kwamba,
tukiongozwa na Roho hatupo tena chini ya sheria, Gal 5:18
Devota, Mkatukumeni aliyekuwa anajiandaa
kwa Sakramenti ya ubatizo, wiki tatu kabla ya kuipokea Sakramenti ile, yeye na
wenzake walipata nafasi ya maongezi na Baba Paroko. Kwa vile kundi hili
lilikuwa la watu wazima, Baba Paroko aliwashauri na kusema, “endapo unajua
kwamba unaishi uchumba ni vyema kuliweka jambo hilo wazi na ikiwezekana siku ya
ubatizo huu Mama Kanisa akaadhimisha pia Sakramenti ya ndoa.” Wote wakaangua
kichoko huku wakimtazama Devota.
Baba Paroko alimtazama Devota na
kumuuliza, “kuna uhusiano wowote wa kicheko hiki na nilichosema juu ya maisha
yako?” “Hapana Baba Paroko,” Devota alijibu huku akiangalia chini. “Kama unaishi uchumba ni vyema ukaliweka wazi
jambo hili ili tuweze kukusaidia zaidi.” Baba Paroko alisisitiza. Devota
alikataa katu katu kama anamchumba na wanaishi uchumba. “Baba Paroko hawa
wananisingizia tu na wanacheka kwa wasilolijua,” Devota alisema kwa ukali.
Na mwisho Baba Paroko alimwambia Devota,
“ikiwa kuna ukweli katika jambo hili, Roho wa Bwana atalidhihirisha kabla ya
kuipokea Sakramenti hiyo ya Ubatizo.” Basi baada ya hayo, Paroko alitoa baraka
na wote wakatawanyika kila mtu nyumbani kwake.
Siku tatu kabla ya adhimisho la
Sakramenti hii ya ubatizo, mapema asubuhi, Baba Paroko aliletewa taarifa ya
‘mwanaume mmoja kufia chumbani mwa Devota Mkatukumeni. Na Devota hajulikani
alikokimbilia.’ Ndugu yangu, “Mtu
aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu,”
Lk 9:62
Tumsifu Yesu Kristo!
“Mbweha wana pango, na ndege wa
angani wana viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake,” Lk
9:58
Tusali:-Ee
Yesu uliyekimbilio letu, kwako na itoshe. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario