domingo, 5 de junio de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 10 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 10 YA MWAKA-C
Somo: 1Fal 17:7-16
Zab:5:2-3, 4-5, 7-8
Injili: Mt 5:13-16
Nukuu:
Eliya akamwambia, Usiogope; enenda ukafanye kama ulivyosema; lakini unifanyie kwanza mkate mdogo ukaniletee; kisha ujifanyie nafsi yako na mwanao,” 1Fal 17:13 

Kwa kuwa Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Lile pipa la unga halitapunguka, wala ile chupa ya mafuta haitaisha, hata siku ile Bwana atakapoleta mvua juu ya nchi,” 1Fal 17:14 

 “Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu,” Mt 5:13 

Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 5:16 

TAFAKARI: “Bwana Mungu huwaifadhi na kuwasitiri wote wamwaminio.”

Wapendwa wana wa Mungu, Mungu hudumu katika uaminifu wake katika umilele wote. Hii ni moja ya sifa ya Mungu, kwamba uaminifu wake ni wa milele. Kama sisi hatuamini, yeye hudumu wa kuaminiwa. Kwa maana hawezi kujikana mwenyewe,” 2Tim 2:13. Na huu ndio wito wa Bwana wetu Yesu Kristo anaotutaka tuwe, yaani, wakamilifu kama Baba yetu wa Mbinguni alivyo mkamilifu, Mt 5:48. Hivyo uaminifu kwa Mungu ni jambo muhimu sana katika imani na yale yote tuyafanyao kila siku ya maisha yetu.

 Nabii Eliya ni mfano wa kuigwa wa wale waliomwamini Bwana bila kujibakiza, na  mwisho wa siku Mungu aliwasitiri katika shida zao. Eliya akiwa mgeni na asiyefahamika vizuri kwa mjane yule wa Sarepta. Hata hivyo, Eliya anamwaminisha mjane huyu kuliweka tumaini lake lote kwa Mungu licha ya uhaba ule wa chakula. Eliya akamwambia, Usiogope; enenda ukafanye kama ulivyosema; lakini unifanyie kwanza mkate mdogo ukaniletee; kisha ujifanyie nafsi yako na mwanao,” 1Fal 17:13. Hakika kwa kiasi cha unga na mafuta kilichobaki kiliwatosha tu kwa siku moja. Hata hivyo Eliya Nabii anatumaini kubwa sana kwa Mungu aliye hai. Kwa kuwa Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Lile pipa la unga halitapunguka, wala ile chupa ya mafuta haitaisha, hata siku ile Bwana atakapoleta mvua juu ya nchi,” 1Fal 17:14. Hii ni imani ya kweli na iliyo hai. Mungu wetu siyo Mungu aliyebaki tu kwenye historia na matukio mazuri yaliyokwisha tokea, bali yu hai hata sasa, na tunapomtafuta katika kweli na haki anapatikana, Isa 55:6. Matokeo yake, Lile pipa la unga halikupunguka, wala ile chupa ya mafuta haikuisha, sawasawa na neno la Bwana alilolinena kwa kinywa cha Eliya,” 1Fal 17:16. Mungu kamwe hachoki kuwasitiri wale wote wanaoweka tumaini lao kwake. Nabii Eliya kwa upande mwingine anatufundisha tuwe vielelezo hai vya Mungu kwa wale wasioamini na kusadiki uwepo wa Mungu katika maisha yao.

Wapendwa wana wa Mungu, Injili ya leo inatupa mifano miwili ya kuwa vielelezo vya Mungu aliye hai, na wakati huo huo kutoa ushuhuda wa kweli wa maisha yetu ya kila siku. Vielelezo hivyo ni kuwa chumvi na nuru. Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu,” Mt 5:13. Chumvi kwa matumizi ya kawaida  mbali na kuwa kikolezo cha kuleta ladha nzuri ya chakula, ilitumika kuvihifadhi vyakula ili vitumike kwa muda mrefu. Ili kidumu kwa muda mrefu, chakula kama nyama na samaki vilisowekwa chumvi, na hivyo havikuweza kuharibika. Chumvi katika mantiki hii na hasa katika somo hili la Injili imetumika kama mfano halisi katika maisha ya kijamii. Mimi na wewe ili tuwe kikolezo katika kujenga ushawishi wa maisha yenye malengo yatupasa kuchanganyika na watu. Tunaweza tu kuyajua maisha ya watu pale tunapochanganyika nao na kuwa sehemu ya maisha yao, kwa lengo la kuwasaidia kutoka katika hali zao duni na huzuni zao. Lengo hili lisipofikiwa chumvi kama chumvi haina faida yoyote, zaidi ya kutupwa nje na kukanyagwa na watu, Mt 5:13b

Kielelezo cha pili katika kutoa ushuhuda wa kweli wa maisha yetu ya kila siku ni kuwa nuru ya ulimwengu. Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima,” Mt 5:14. Kimaadili yatupasa kuwa nuru. Nguvu ya kimaadili ni ushawishi mkubwa sana wa watu kutii na kufuata yale tunayowaongoza wayafanye. Nuru ni ushindi katika giza. Na nuru ni kinyume cha giza. Maendeleo ya watu kwa namna yoyote ili ni tokeo la ustaarabu wao. Haya ndiyo maadili ya watu katika kuona na kutenda. Pasipo ustaarabu, maadili pia huwa ovyo. Kwa maana nyingine, palipo na utaratibu pana akili. Nuru ambayo ndiyo maadili, ustaarabu, na kielelezo cha ufahamu wa watu, yaani, akili, ni kitu cha kupewa kipaumbele. Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani,” Mt 5:15. Watu wengi hupatwa na mshangaa pale kunapokuwepo na msuguano kati ya kile akisemacho mtu, na ustaarabu wake yaani, maadili aliyokuwa nayo. Mwenye maadili mazuri, husukumwa na kutawala namna ya sema yake. Mtu wa mtindo huu uchagua maneno la kusema kadiri ya hadhira yake, na somo kusudiwa kwa watu husika. Kwa maana nyingine, mtu huwa na uchaguzi wa maneno ya kusema. Ni kwa maana hiyo kwamba, Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 5:16. Nuru ya mtu ni nguvu ya maadili ya mtu, ambayo ni kama nijamu. Ni vigumu kummiliki farasi katika mwendo kama hauna nijamu.

Tumsifu Yesu Kristo!
Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu,” Mt 5:13

Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 5:16


Tusali:-Ee Bwana Yesu Kristo, nifanye kikolezo halisi pale nitakapo kuwa, na kuwa mfano halisi wa nuru yako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario