JUMATATU WIKI YA 13 YA MWAKA-C
Somo: Amo 2:6-10, 13-16
Zab: 50:16bc-17, 18-19, 20.21, 22-23
Injili: Mt 8:18-22
Nukuu:
“kwa
sababu wamewauza wenye haki kwa fedha, na maskini kwa jozi ya viatu; nao hutwetea mavumbi yaliyo juu ya vichwa
vya maskini, na kuipotosha njia ya mwenye upole,” Amo 2:6b-7a
“nao hujilaza karibu na kila madhabahu juu ya nguo zilizowekwa
rehani, na katika nyumba ya Mungu wao hunywa divai ya watu waliotozwa fedha,”
Amo 2:8
“Mwandishi mmoja
akamwendea, akamwambia, Mwalimu, nitakufuata ko kote uendako,” Mt 8:19
“Yesu akamwambia,
Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana viota; lakini Mwana wa Adamu hana pa
kulaza kichwa chake,” Mt 8:20
TAFAKARI: “Uongozi ni wito na dhamana. Ni kutumika na siyo kutumikiwa.”
Wapendwa wana wa Mungu, ni kosa na dhambi ya jamii-‘social sin,’ pale
unapotumia nafasi uliyonayo na cheo ulichonacho kuzikanyaga haki za raia
wenzako kwa manufaa yako binafsi. Mmomonyoko huu wa maadili amboa ndiyo picha
halisi ya nyakati zile za Nabii Amosi, hauna tofauti sana na jamii yetu leo.
Ukijaribu kuitazama jamii yetu leo walio na nafasi ya kutoa huduma katika jamii
kwa na kwa mujibu wa sheria na mamlaka waliopewa, wamekuwa watu wa ‘ujanja
ujanja’ hivi. Kila mwenye nafasi hiyo kwa lugha iliyozoeleka tungesema wamekaa
‘kidili dili.’
Kwa mtizamo huu wa “kidili dili,” wanyonge ambao ndio wengi kwao kilio
hakina ukomo. Uovu na uonevu kwa wanyonge ni kitu ambacho Mungu kamwe
hatokivumilia. Sote tunamastahili sawa mbele ya Mungu licha ya tofauti zetu
kihali. Mungu kwa kupenda kwake yeye mwenyewe aliona inafaa kutuumba kwa sura
na mfano wake, Mwa 1:27. Hata hivyo, wanyonge kwa wingi wao leo wanatumika kama
daraja-“uwezekano” la walionazo (matajiri wachache), wanasiasa, na watu wengine
wenye ushawishi katika jamii, ikiwa ni pamoja na baadhi ya viongozi wa dini ili
kufikia malengo yao binafsi. Mzaburi anatuambia, “heri amkumbukaye mnyonge;
Bwana atamwokoa siku ya taabu,” Zab 41:1. Watu hawa wasio na uchungu na
wanyonge baada ya kuyafikia malengo yao huwasahau wanyonge na huwatumikisha na
hadi tone la mwisho.
Jamii inapofikia hali na mazingira kama haya, kuna hitaji kubwa sana
la ‘sauti ya wasio na sauti,’ yaani, mtu au taasisi yenye uwezo wa kuona uovu
kama ulivyo, kuukemea kwa vitendo, na kuyaponya majeraha kwa kutoa mwanga mpya
na njia mbadala kuelekea tumaini la kweli na hai. Wote wale waliovunjika moyo
na kuumizwa katika hali kandamizi katika jamii, lazima wajengewe tumaini la
kweli na yenye mabadiliko chanya. Nabii Amosi alikuwa ‘sauti ya wasio na sauti’
wa nyakati zake. Naye aliuona uovu na kuusema kama ulivyo. Naye hakusita
kusema, “wamewauza wenye haki kwa fedha, na maskini kwa jozi ya viatu; nao hutwetea mavumbi yaliyo juu ya
vichwa vya maskini, na kuipotosha njia ya mwenye upole,” Amo 2:6b-7a. Ukitaka
kujua ukweli huu katika jamii yetu leo, rejea vipindi vyote vya kampeni na
mazingira yote ya chaguzi uliyokwisha yashuhudia. Je, ni wangapi wananunuliwa?
Wakati mwingine kwa gharama ya sahani ya wali na maharage!
Leo swala la maadili kwa viongozi wa ngazi zote, na kwa namna ya pekee
katika familia zetu limeporomoka sana. Tuelewe kwamba familia zisipokuwa na
msingi imara kimaadili ikiwa ni pamoja na msisitizo wa kuuchukia uovu,
tusitegemee kuwapata viongozi malaika ilihali viongozi hao ni tunda la familia
hizi zisizo na maadili na hofu ya Mungu. Nyakati za Nabii Amosi ‘mtu na baba yake waliweza kumwendea mwanamke mmoja, hata
kulitia unajisi jina la Mungu ambalo ni Takatifu,’ Amo 2:7b. Je, leo hatuna
matukio kama hayo? Ni mara ngapi tunasikia binti akijigamba bila kuwa na mshipa
wa aibu kuwa na mahusiano ya kimapenzi na Baba yake mzazi?
Hali
hii ya maadili mabovu haikuwa tu kwenye maswala ya kijamii, bali ilikwenda hata
kwenye maswala ya kiimani. Waliotegemewa kuwa mfano, yaani, ‘viongozi wa
kidini,’ walitumia nafasi yao vibaya wakiutazama zaidi ubinafsi wao. Watu hawa
waliokosa hofu ya Mungu ‘walijilaza karibu
na kila madhabahu juu ya nguo zilizowekwa rehani, na katika nyumba ya Mungu wao
hunywa divai ya watu waliotozwa fedha,’ Amo 2:8. Je, vituko kama hivyo vimekoma
leo katika jamii yetu? Leo ipo mifumuko mingi ya imani za ajabu ajabu, na
kufanya kuchipuka ‘vikanisa’ vingi katika jamii yetu. Ni vyema tukatafakari
maneno haya ya Mtume Paulo; “Na roho za manabii huwatii manabii. Kwa maana
Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani; vile vile kama ilivyo katika
makanisa yote ya watakatifu,” 1Kor 14:32-33. Hapa ndipo tunapoona uongozi kama
wito na dhamana.
Hili ndilo analolizungumzia Yesu katika Injili
ya leo. Wito na kuitika wito si swala la kumfuata Yesu popote aendapo, bali
kujua nini maana ya kumfuata Yesu, na matakwa yake. Kumfuata Yesu kadiri ya
injili ya leo ni “KUACHA” utaratibu, mitazamo, na matamanio tuliyoyazoea ambayo
ni kinyume na kile tulichoitiwa. Kauli ya kutangaza nia ya kumfuata Yesu ni rahisi
sana kama anavyojinadi mwandishi huyu, na kusema, “Mwalimu, nitakufuata ko kote uendako,” Mt 8:19. Akilijua hilo ni
jambo rahisi kutamka kama nia, Yesu anamjibu mwandishi huyu, “Mbweha wana
pango, na ndege wa angani wana viota; lakini Mwana wa Adamu hana pa kulaza
kichwa chake,” Mt 8:20. Kwa maana nyingine Yesu anataka kumwambia jambo hili:
je, upo tayari kuyaacha mazuri haya ya ulimwengu na ufahari wake wote, na kuwa tayari kutaabika na kudharauliwa kwa
sababu yangu? Hapa ndipo tunaposhindwa wengi. Ni sawa na kusema, “utawa
naupenda, ila ufukara siupendi.” Ni sawa na kusema, “maisha ya ndoa nayapenda,
ila uzazi na malezi sipendi.” Huu ni mchanganyo wa hali ya juu.
Kumfuata
Yesu Kristo inamaanisha kujibadua kutoka katika mnaso wa mazoea, au uhasili. Hapa
yatupasa kujipanga vizuri katika hatua hii. Wengi tumeshindwa kujibandua kutoka
mnaso wa kiasili tuliokuwa nao kutokana na uhasili wa maisha yetu kama tokeo la
historia yetu (mila na desturi zetu). Hakuna kati yetu aliye kisiwa wala
aliyedondoka kama mana jangwani. Sote tumetoka katika familia, na familia hizo
zinaushawishi mkubwa kuhusu hatma ya maisha yetu ya kila siku. Ila leo Yesu
anasema JIBANDUE KUTOKA JELA HIYO. Mnaso
huu utupelekea kujiuliza moja ya maswali haya ya kifamilia tunayoyaishi kila siku.
“Mwingine katika wanafunzi wake akamwambia, Bwana, nipe ruhusa
kwanza, niende nikamzike baba yangu,” Mt 8:21. Ni hekima na busara kwenda
kuwazika wazazi na hata kuwahudumia hadi siku ya mwisho ya maisha yao kadiri ya
amri ya nne, “waheshimu baba yako na mama yako; amri hii ndiyo amri ya kwanza
yenye ahadi, upate heri, ukae siku
nyingi katika dunia,” Efe 6:2-3. Ila Yesu anatupa jibu la uhakika tunapoamua
kumfuata. Yesu anasema, “nifuate; waache wafu wazike wafu wao,” Mt 8:22.”
Hatukatazwi kuwazika wazazi wetu, bali tunaonywa kuwa “mkiongozwa na Roho,
hampo chini ya sheria,” Gal 5:18. Je, ndugu yangu wewe unaongozwa na nini?
Tumsifu
Yesu Kristo!
Mbweha wana pango, na
ndege wa angani wana viota; lakini Mwana wa Adamu hana pa kulaza kichwa chake,”
Mt 8:20
Tusali:-Ee Yesu Mwema na
Mchungaji wetu, tuonyeshe njia ya uzima. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario