martes, 21 de junio de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 12 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 12 YA MWAKA-C
Somo: 2Fal 24:8-17
Zab: 79:1-2, 3-4a, 4b-5
Injili: Mt 7:21-29
Nukuu:
Yekonia alikuwa na umri wa miaka kumi na minane alipoanza kutawala; akatawala miezi mitatu katika Yerusalemu; na jina la mama yake aliitwa Nehushta binti Elnathani wa Yerusalemu,” 2Fal 24:8 

Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, mfano wa yote aliyoyafanya baba yake,” 2Fal 24:9 

 “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 7:21 

Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?” Mt 7:22

Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu,” Mt 7:23

TAFAKARI:Alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi wao.”

Wapendwa wana wa Mungu, masomo ya leo na hasa somo la Injili, linatutafakarisha mambo makuu mawili. Moja, ‘onja moyoni yale utamkayo mdomoni.’ Na pili, ‘tambua kile kisukumacho maisha yako.’ Tukianza na hili la kwanza, ‘onja moyoni yale utakayo mdomoni,’ Yesu anasema, Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 7:21. Maneno maneno tu hayatoshi. Yatupasa kuyaishi maneno hayo na kuyafanya kuwa sehemu ya maisha yetu. Hapo ndipo penye ufalme wa mbinguni. Kati yetu wapo mabingwa wa kuapa na wakati mwingine kulitaja jina la Mungu kama ndege yule kasuku. Kumbe yatupasa kulisikia neno na kulitenda. Kwa kufanya hivyo twaonyesha tu watu wenye ufahamu wa Mungu, na yale yote tuyafanyayo msingi wake utakuwa imara daima. La sivyo tuwe tayari kwa karipio hili ya Yesu siku ile ya mwisho, “Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu,” Mt 7:23. Kumbe tuonje moyoni yale tutamkayo mdomoni.

Hakuna kitu chochote kitakacho weza kutuyumbisha kutoka kwenye imani hiyo kama kabla ya kutamka kitu tunakipa tafakari ya pekee. Kwa maana hiyo Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba,” Mt 7:24-25. Twaweza kulifanya jambo hili kama tutaonja moyoni yale tuyatamkayo mdomoni. Fikiri kwa kina na sawa sawa kabla ya kutamka lolote mbele za watu, na zaidi kama una dhamana juu yao.

Watu wengi wanamshangaa Yesu mafundisho yake kwa sababu mamlaka yake yamebebwa na maadili yake. Nguvu ya kimaadili ina kina kirefu kuliko nguvu itokanayo na mamlaka nyingine, mfano; kisiasa. Nguvu ya kimaadili huja yenyewe kwa kujionyesha nje kadiri ya tabia ya mtu ilivyo jengwa, njema, na yenye kulenga mara zote katika ukamilifu licha kwamba udhaifu upo. Waliomzunguka Yesu wanapigwa na butwaa kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi wao,” Mt 7:29. Je, huyapima maneno yako kabla ya kuyatamka?

Ndugu zangu katika Kristo, jambo la pili katika masomo yetu ya leo, ‘tambua kile kisukumacho maisha yako.’ Kitu hicho ndicho kinachotakiwa kuwa na mamlaka juu ya maisha yako. Kwa maneno haya ya Yesu, Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni,” Mt 7:21a, ni mizania tosha ya kupima kile kisukumacho yale tuyafanyayo au utamkayo. Kwa maana nyingine unaweza kuwa mbwekaji mzuri sana kwa kuwapendezesha watu wanaokuzunguka kwa kuwaaminisha pasipo kumaanisha, ukawa kama mbwa anayebweka usiku kucha kumwaminisha tajiri yake kwamba ulinzi upo imara kumbe ni woga wa miluzi ya upepo.

Mfalme Yekonia aliyeanza kutawala akiwa na umri wa miaka kumi na nane, 2Fal 24:8a, hakujifunza kutoka makosa ya Baba yake, na hivyo naye akawa chukizo machoni pa Bwana kama alivyofanya Baba yake, 2Fal 24:9. Mfalme Yekonia aliendeleza yale yale ya Baba yake bila kujali hitaji la wale aliokuwa anawaongoza. Huu ndiyo udhaifu wa kuridhishana utawala na mamlaka kama ilivyo kitu cha mila na desturi tena zisizo badilika. Ni kukosa picha pana ya ukweli wa jambo kwa kukubali na kuendelea kujifungamanisha na mtindo ule ule hata kama hauna tija na maono chanya kadiri ya hitaji na wakati. Ni kutazama maslahi makubwa kwa kundi dogo la watu wanao neemeka mfumo huo wa utawala, ingawa wetu wanateketea. Kwa upande mwingine ni kutokuwa tayari kujifunza kutoka historia ambayo maisha ya watu leo na sasa ni tokeo lake. Mtazamo na mazingira ya mtindo huu ndivyo ilivyokuwa rahisi kwa Taifa hili ya Israeli kudondoka mara kwa mara katika mikono ya maadui zao. Mataifa yaliyowazunguka yaliufahamu udhaifu wao kwa sababu waliijua historia vizuri. Mfalme Yekonia baada ya kuzidiwa hakuwa na ujanja zaidi ya kujisalimisha mwenyewe chini ya utawala wa mfalme Nebukadreza wa Babeli kama mateka katika mwaka wa nane wa utawala wake, 2Fal 24:12b

Tawala nyingi zisizopenda kubadilika kutokana na hitaji la wakati ikiwa ni pamoja maono pevu kuelekea kule wasipokujua ila wanapatamani, huwa mwanzo wa anguko lao. Taifa linaweza kuwa huru, yaani, uhuru wa bendera ila halina nguvu licha ya rasilimali lilizo nazo. Mali na utajiri wake uchukuliwa kwa mlango wa nyuma na mataifa majanja yanayoenda na mabadiliko na hitaji la wakati, ikiwa ni pamoja na maono pevu, yaani, sera sahihi za uchumi wa wakati husika. Na hivi ndivyo ilivyokuwa katika Taifa la Waisraeli (ambao kwa sasa ni mateka-Babeli) chini ya utawala wa mfalme Yekonia,Akatoa huko hazina zote za nyumba ya Bwana, na hazina za nyumba ya mfalme, akavikata-kata vyombo vyote vya dhahabu ambavyo Sulemani, mfalme wa Israeli, alivifanya katika hekalu la Bwana, kama Bwana alivyosema,” 2Fal 24:13. Mfalme huyu akupoteza tu rasilimali vitu, bali pia rasilimali watu ambayo ndiyo iliyokuwa  nguzo ya taifa na msingi  wa vyote.  Mfalme wa Babeli, Nebukadreza, Akawachukua mateka watu wa Yerusalemu wote pia, na wakuu wote, na mashujaa wote, watu elfu kumi; na mafundi wote, na wafua chuma wote; hapana mtu aliyebaki, ila waliokuwa wanyonge wa watu wa nchi,” 2Fal 24:14. Hili lilikuwa pigo kubwa sana kwa Taifa hili la Israeli. Tukiacha haya ya kijamii, kisiasa na utamaduni, embe kwa sasa tuzame ndani zaidi kwa haya ya kiroho. Kwa upande huu wa maisha ya kiroho, Yesu anatupa angalizo kwamba, ni yule tu “afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni (Mungu) ndiye atakayeingia katika ufalme wa mbinguni.” Mt 7:21b.  Je, kufanya mapenzi ya Mungu kunamaanisha nini?

Wapendwa wana wa Mungu, kufanya mapenzi ya Mungu ni “kukaa katika pendo” la Mungu. Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini. Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake,” 1Yoh 4:16. Ni kuwa tayari kuongozwa na mamlaka ya Mungu katika mfumo wa Upendo. Tunakaa katika upendo wa Mungu kwa kuyatimiza mapenzi yake pale tu tunapolipokea neno lake, tunapolisoma neno lake, tunapolifanyia tafiti neno lake, tunapolikumbuka neno lake, na tunapolitafakari neno lake. Haya mambo matano ni muhimu sana kama tunataka kweli kukaa naye na kuyafanya mapenzi yake. Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba,” Mt 7:24-25. Hakuna awezaye kutung’oa kwenye mwamba huu wa imani hata kikija kimbunga cha tsunami. 

 Tusipo lishika neno la Mungu vizuri tutakuwa tayari kuongozwa na mamlaka hizi; mila zetu (kwa kufanya yale yanayotutia hofu bila kuhoji sababu yake), desturi zetu (kwa kufanya kadiri ya mapokea ya wazee wetu katika hali ya upofu), hisia zetu (kwa kufanya kadiri ya miyeuko yetu na siyo utashi wetu). Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa,” Mt 7:26-27. Hakika kwa hali hii tunabaki kuwa kama bendera fuata upepo. Na kwa sababu hiyo, kila ajitokezaye na kutushawishi hatutakuwa na nguvu ya kuimili vishindo vya imani kwani tu wepesi kama pamba.

Tumsifu Yesu Kristo!

Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, mfano wa yote aliyoyafanya baba yake,”
2Fal 24:9


Tusali:- Ee Yesu Mwema, tuongoze kwa lililo jema tukitambua kwamba maisha yetu hapa duniani ni jukumu la muda mfupi, hivyo tutumie vyema wakati na nafasi tuliyo nayo. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario