viernes, 17 de junio de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 12 YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 12 YA MWAKA-C
Somo I: Zek 12:10-11
Zab: 63: 1-5, 7-8, (K) 1
Somo II: Gal 3:26-29
Injili: Lk 9:18-24
Nukuu:
Nami nitawamwagia watu wa nyumba ya Daudi, na wenyeji wa Yerusalemu, roho ya neema na kuomba; nao watamtazama yeye ambaye walimchoma; nao watamwombolezea, kama vile mtu amwombolezeavyo mwanawe wa pekee; nao wataona uchungu kwa ajili yake, kama vile mtu aonavyo uchungu kwa ajili ya mzaliwa wake wa kwanza,” Zek 12:10 

Siku hiyo kutakuwa na maombolezo makuu huko Yerusalemu, kama maombolezo ya Hadadrimoni katika bonde la Megido,” Zek 12:11 

Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa Mungu kwa njia ya imani katika Kristo Yesu,” Gal 3:26 

 “Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu,” Gal 3:28 

 “Akawaambia, Nanyi mwasema ya kwamba mimi ni nani? Petro akamjibu akasema, Ndiwe Kristo wa Mungu,” Lk 9:20 

 “Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha,” Lk 9:24 

TAFAKARI: “Nao watamtazama yeye ambaye walimchoma. Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya kumi na mbili ya mwaka “C” wa Kanisa. Tafakari yetu ya leo yatutaka tuzame katika fumbo zima la ‘Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu,’ Yoh 1:14. Neno huyu ndiye kielelezo chetu, matumaini yetu, na ukomo wa ufunuo wa Mungu Baba Mwenyezi kwetu. Hivyo tutamfikia Mungu Baba Mwenyezi kwa kupitia Mwanaye, yaani Yesu Kristo, kama Kristo mwenyewe anavyothibitisha kwetu kwamba, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Kristo kama njia, kweli, na uzima, asili yake katika maana ya lengo lake hapa duniani ni ‘wokovu wa kila kiumbe,’ binadamu akipewa nafasi ya pekee, Mwa 1:27.

Hivyo lengo hili-wokovu, Mungu alianza kulifunua tangu kuumbwa kwa ulimwengu, na hasa kwa manabii wake, na kwa namna ya pekee leo kupitia Nabii Zakaria kama tulivyokwisha kusikia katika somo letu la kwanza, yaani,  Nami nitawamwagia watu wa nyumba ya Daudi, na wenyeji wa Yerusalemu, roho ya neema na kuomba; nao watamtazama yeye ambaye walimchoma; nao watamwombolezea, kama vile mtu amwombolezeavyo mwanawe wa pekee; nao wataona uchungu kwa ajili yake, kama vile mtu aonavyo uchungu kwa ajili ya mzaliwa wake wa kwanza,” Zek 12:10. Ndugu yangu, hiki ndicho kilichotokea siku ile ya Ijumaa Kuu. Tendo hili la Ijumaa Kuu ndiyo utimilifu wa wakati ambapo Mungu alisema sasa inatosha kwa watu wangu. Mtume Paulo anasema, Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana,” Gal 4:4-5. Uwana huu wa Mungu, unatuweka sawa mbele za Mungu kwa kuwa Mungu aliona inafaa na hivyo kutuhesabia haki kwa sadaka ya Mwanaye Mpenzi pale Msalabani. Hivyo, Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu,” Gal 3:28. Umoja wetu huu siyo umoja usiokuwa na malengo. Ni umoja uliojengwa mwa msingi thabiti wa Imani ndani na katika Kristo Yesu kama kielelezo chetu hai, Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa Mungu kwa njia ya imani katika Kristo Yesu,” Gal 3:26. Je, nini maana ya maneno haya; “Nao watamtazama yeye ambaye walimchoma?”

Wapendwa wana wa Mungu, manane haya ya Nabii Zakaria, ‘watamtazama yeye ambaye walimchoma,’ unabii huu ulikamilika tunaposoma Mwinjili Yohane 19:28-37. Hakika ulimwengu ulipata maombolezo na kimya kikuu kama alivyotabiri Nabii Zakaria, kwamba, Siku hiyo kutakuwa na maombolezo makuu huko Yerusalemu, kama maombolezo ya Hadadrimoni katika bonde la Megido,” Zek 12:11. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa kadiri ya tafsiri ya maneno haya ‘watamtazama yeye ambaye walimchoma,’ tunapotafakari sehemu hiyo, Yoh 19:29-37.

Yohani Mtakatifu anaunganisha tukio la kifo cha Yesu na kutukuzwa kwake. Yesu anaonyeshwa akiwa anaiendea saa yake, ndio saa ya kutukuzwa kwake, kwa kifo, ufufuko na kupaa kwake Mbinguni. Anamwonyesha Yesu anatoka kwa Baba na anarudi kwa Baba.
Yesu anapokufa msalabani anatoa roho yake, anatupa roho huyu aliyempokea wakati anaanza kazi yake, aliposema, “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:18-19. Yohani anaunganisha tukio la kifo cha Yesu, tukio la msalaba na Pentekoste. Pale msalabani Yesu anatoa roho wake, nasi tunampokea kutoka ubavuni mwake tunapopokea sakramenti zake, “damu na maji”, katika Kanisa lake. “Lakini askari mmojawapo alimchoma ubavu kwa mkuki; na mara ikatoka damu na maji,” Yoh 19:34

Sisi tunapobatizwa tunampokea roho huyu wa Kristo, Roho Mtakatifu. Anatufanya kuwa wana wa Mungu na wana wa Kanisa. Kwa sakramenti ya Kipaimara, Roho Mtakatifu anatufanya kuwa askari hodari wa Yesu Kristo kwa njia ya mapaji yake saba tunayopokea. Kuwa tayari kutoa ushuhuda juu ya Yesu. Na tunafanya hivyo na kuwa hivyo kwa, Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo,” Gal 3:27. Ni katika Kanisa tunapewa karama ya Roho Mtakatifu. “Na Mungu ameweka wengine katika Kanisa, wa kwanza mitume, wa pili manabii, wa tatu waalimu, kisha miujiza, kisha karama za kuponya wagonjwa, na masaidiano, na maongozi, na aina za lugha,” 1Kor 12:28.  Anatoa karama mbalimbali kwa wafuasi wa Kristo. Karama hizi ni kwa ajili ya manufaa ya Kanisa lote, ingawa zinaweza kuwa na msaada kwa aliyepewa. “Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yeye yule; mwingine imani katika Roho yeye yule; na mwingine karama za kuponya katika Roho yule mmoja; na mwingine matendo ya miujiza; na mwingine unabii; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri za lugha; lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye,” 1Kor 12:7-11.  Kanisa lina wajibu wa kupima kwamba karama inapojitokeza kama kweli ni kutoka kwa Roho Mtakatifu. Kama si kutoka kwa Roho Mtakatifu, hii si karama bali ni kitu kingine. “Basi pana tofauti za karama; bali Roho ni yeye yule,” 1Kor 12:4 

Kama wafuasi wa Yesu, tunapojaliwa karama na Roho Mtakatifu, tunavutwa daima kumtazama yule waliyemchoma, yule tuliyemchoma. Tukifanya hivyo karama na vipaji vyetu havitakosa kuwa vya manufaa kwa Kanisa zima. Tunapomtazama tunatambua kweli tuna karama. Je, tutamtazama namna gani? Katika Kanisa lake hasa anapotufundisha kwa njia ya neno lake alilowakabidhi mitume, viongozi wa Kanisa ambao ndio wenye madaraka ya kututafsiria neno la Mungu na karama mbalimbali katika Kanisa na kuona kama kweli ni karama au ni hisia au maigizo au mahangaiko ya  kisaikolojia n.k.

Karismatiki katoliki ni karama ya Roho Mtakatifu katika Kanisa. Ni tofauti na karismati za kilokole na madhehebu mengine au dini nyingine. Ipo hatari ya kuchanganya Karismatiki Katoliki na hasa karismatiki ya kilokole. Siku hizi katika Karismatiki Katoliki wapo baadhi yetu wanaoiga mambo mengi ya kilokole kama nyimbo, namna ya kucheza, namna ya kuongea na kuhubiri, namna ya kusalimiana na kufurahi, namna ya uponyaji na kukemea uovu n.k. Je, haya hapa kwetu hayapo? Si tu Karismatiki Katoliki wamekumbwa na tamaa hii ya kuiga na kutumia mambo ya wengine, bali hata wakatoliki wengi hutumia nyimbo, muziki, na hisia za kilokole katika tafrija, sherehe, mikutano na semina zao. Kweli sisi wakatoliki tumechuja kiasi hicho kwamba tulivyo navyo, mathalani nyimbo zetu hazigusi nafsi na hisia zetu?  Kuna kila dalili ya kuweka vya kwetu chini, au kuvichimbia na kukumbatia vya wengine na kuwasaidia kuvieneza hata ndani ya Kanisa Katoliki.

Ni vizuri ieleweke kwamba, si dhambi wala kosa kuiga jambo jema na zuri kutoka kwa mwenzako au jirani yako hata kama mnatofautikiana kwa namna moja au nyingine. Hata hivyo tunapoyaiga hayo mazuri kutoka kwa wenzetu, tumeitendea haki ‘teología,’ hasa jumbe za nyimbo tunazoziimba? Pamoja na mambo mengi yanayobeba ‘teología ya kikatoliki,’ hili ni dhahiri, yaani, jumbe za nyimbo hizo ni vyema zikabeba haya; Imani ya kweli, tumaini la kweli, na Upendo wa kweli wa Mungu. Muhimu hapa ni ‘teología ibebayo ujumbe ule unaoimbwa,’ na siyo namna waimbavyo, wachezavyo, na ishara au viashiria wavitoavyo ikiwa vinamwelekea Mungu mwenyewe wanayemwimbia na kumsifu. Zipo njia mbalimbali za kufikisha ujumbe ule ule mahususi kwa Mungu kadiri ya mila, tamaduni, na desturi za watu. Mungu ufurahi tunavyojiachia kwake kama tulivyo katika kumsifu, kumshukuru na kumwabudu. Mungu asingependa tuwe kama ‘maroboti.’ Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana,” Rum 12:1. Ni ibada yenye maana, na siyo tu iliyobeba ufahamu, bali yote mawili, yaani, ufahamu wa kile ukifanyacho, na umaana wake (Rationality and Significativity). Hivyo wale wanaobeza kuwa Karismatiki kusali kwao na kuimba kwao ni kwa kupayuka payuka kusikokuwa na maana yoyote, ni sawa na mtu anayepoteza muda wake kumkemea chura kutoa kwake sauti akiitafsiri kuwa ni kelele. Je, kelele za chura kama unavyozitafsiri haziufunui utukufu wa Mungu aliyemuumba chura huyo? Jiulize! Je, nani kakuambia kusali kwako ndiko kuliko bora kuliko kwa wengine wote?

Tufanyeje basi? Tuanze kumtazama yule waliyemtoboa, tuliyemtoboa, ndio kutumia vile ambavyo kweli ni mapokeo sahihi ya Kanisa na kuyaboresha tuliyonayo, yaani, kuyatamadunisha kwa mwanga wa Injili yale yanayobeba tamaduni, mila na desturi zetu. Tutafanikiwa hili tukiwa na ushirikiano sisi wenye, na viongozi halali wa Kanisa, tukiwatumia wataalamu wetu [kwaya zetu, waalimu wa kwaya, makatekista wetu] na pia tukitumia vipawa tulivyopewa na Mungu. Yapo mengi tunaweza kuiga toka kwa wenzetu yakatusaidia lakini hii inahitaji umakini wa hali ya juu na ruhusa ya Kanisa kama nilivyokwisha kusame hapo awali. Si kila mtu anajiamulia kitu chake na kukileta katika Kanisa Katoliki, kuna utaratibu tangu enzi za mitume ambao unaongozwa na Roho Mtakatifu. Kila mtu akileta utaratibu wake au kitu chake itakuwa ni fujo na hakutakuwa na umoja ambao unaletwa na Roho Mtakatifu. Penye migogoro, ubinafsi na hali ya kupenda kuwa juu ya mamlaka ya Kanisa, ambapo hakuna utii, hakuna karama, bali kiburi na majivuno ndio vinatawala.

Wafuasi wa Yesu, tunapomtaza yule waliyemtoboa, tuliyemtopoa/mchoma pale msalabani, sadaka ya Misa ambayo ni sadaka ya Yesu msalabani, ni kiini, na kilele cha sala na ibada zetu zote. Tuipe Ekaristi takatifu, Ibada ya Misa Takatifu nafasi ya pekee, kwani pekee ndipo tunapokutana na kumtazama yule waliyemchoma, yule tulimchoma. Yesu ambaye anatupa roho wake, ndiye chanzo cha karama na vipaji vyetu vyote. Kazi zetu, ibada zetu, na sala zetu zituandae kuadhimisha Ekaristi takatifu, Misa Takatifu na Misa Takatifu iwe chemchemi ya kutuhuisha, na kuhaisha karama na vipaji vyetu.

Mama Maria ambaye alimleta huyu ambaye tunamtazama, anatupa sisi na ulimwengu. Yeye hachoki kutuombea na kutuletea zawadi za ukombozi. Maria alipata mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, akawa hekalu la Roho Mtakatifu na hekalu la Mwana pekee wa Mungu, Tabernakulo ya kwanza. Kama Mungu amempa heshima hiyo, kuwa mama wa Mungu, sisi hatuoni ugumu kwani ni mama yetu. Anatuombea nasi tuwe mahekalu au Tabernakulo ya Roho Mtakatifu na ya Mwanaye, kwa ubatizo na kipaimara kwa namna ya pekee. Tutakuwaje tabernakulo la Roho Mtakatifu na Yesu, kama hatuna heshima kwa mama yake? Kama hatuithamini Misa takatifu, Ekaristi takatifu ambayo inawezekana na inafanyika kwa uwezo wa Roho Mtakatifu? Tutakuwaje Tarbenakulo ya Roho Mtakatifu na Yesu, kama hatuna heshima na utii kwa Kanisa lake, ambamo ndimo tunaweza kujua, karama za Roho Mtakatifu?

Hata hivyo yatupasa kumjua huyu Yesu ni nani kwetu. Yesu alitaka kujua kutoka kwa watu na hata kwa wanafunzi wake wa karibu kabisa wanamtazamo gani juu yake. Mtume Petro anatoa jibu sahihi kuhusu Yesu, na lile lililo mpasa Kristo katika ulimwengu huu. Akawaambia, Nanyi mwasema ya kwamba mimi ni nani? Petro akamjibu akasema, Ndiwe Kristo wa Mungu,” Lk 9:20.

Mpendwa unayesafiri nami katika tafakari hii nikuulize swali la msingi; pamoja na majibu ya wengine, na hasa jibu alilolitoa Petro kuhusu swali alilouliza Yesu, wewe binafsi Yesu kwako ni nani? Jibu la Petro kwa tafsiri, Kristo yaani Masiha wa Mungu, ndiye yeye tu aliyewekwa katika mpango mzima wa ukombozi wa mwanadamu. Hivyo tutaiona mbingu na kuufurahia uhuru wa kweli endapo tu tutakuwa tayari kushikamana na mwana huyu wa Mungu. “Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina lingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 4:11-12. Hivyo kufikia hatua hii la kuokolewa kwetu kupitia jina hili hatunabudi kushiriki njia ile aliyopitia Bwana wetu Yesu Kristo kama anavyowanong’onozea wanafunzi wake siri hii na kusema, “Imempasa Mwana wa Adamu kupata mateso mengi, na kukataliwa na wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa na siku ya tatu kufufuka,” Lk 9:22. Ndugu yangu hakuna PASAKA PASIPO IJUMAA KUU. Ndivyo hivyo kwetu kama wafuasi wake Kristo tulio hai kwamba hakuna UTUKUFU PASIPO MSALABA.

Padre Tomasi Songambele akiwa ofisini mwake, alipigiwa simu na mmoja wa viongozi wa Jumiya ndogondogo kutoka moja ya kigango cha parokia yake. Ujumbe ule ulikuwa ni taarifa ya mgonjwa aliyezidiwa na alihitaji huduma ya kiroho.

Baada ya ujumbe ule wa simu, Padre Tomasi Songambele alionekana kutoka na kuingia sakristia akiwa anatafuta kitu fulani. Mwisho, katekista aliyekuwa karibu, alijaribu kujua nin hasa, na  hivyo alimuuliza, “Padre kulikoni, mbona wa ingia na kutoka, na unaonekana kuna jambo linakusumbua?” Padre alimjibu, “natafuta chupa ya kubeba maji ya baraka!”

Katekista alitabasamu na kumwambia, “Padre, wewe ni ‘PADRE,’ nenda huko kwa mgonjwa utayafanya yote.” Wote walicheka, na Padre akasema huku akiondoka, “asante sana Katekista, leo upo juu!” Padre akawasha gari na kuondoka. Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo,” Gal 3:27. Hivyo katika Kanisa kila mbatizwa yampasa kujua nafasi yake, na kwa namna hiyo, mwili wa Kristo tukiwa sisi ni viungo vyake, utakuwa na afya.

Tumsifu Yesu Kristo! 

Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha,” Lk 9:24


Tusali: Ee Yesu, nifanye kiungo chako hai katika mwili wako, yaani, Kanisa. Amina 

No hay comentarios:

Publicar un comentario