SIKUKUU YA MTAKATIFU BARNABA MTUME
11/6
Somo:
Mdo 11:21b-26; 13:1-3
Zab:
98:1, 2-3ab, 3cd-4, 5-6
Injili:
Mt 10:7-13
Nukuu:
“Na huko Antiokia
katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na
Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya
wa mfalme Herode, na Sauli,” Mdo 13:1
“Basi
hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema,
Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia,” Mdo 13:2
“Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa
mbinguni umekaribia,” Mt 10:7
“Pozeni
wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, toeni pepo; mmepata bure, toeni
bure,” Mt 10:8
“Msichukue
dhahabu, wala fedha, wala mapesa mishipini mwenu; wala mkoba wa safari, wala kanzu
mbili, wala viatu, wala fimbo; maana mtenda kazi astahili posho lake,” Mt
10:9-10
TAFAKARI:
“Watu wengi wakaamini, wakamwelekea Bwana.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha kumbumbuku ya Mtakatifu Barnaba Mtume. Mtakatifu
Barnaba anajulikana pia kama ‘Nabii wa wakati wake,’ ‘Mwanafunzi wa karibu wa
njia ile ya Yesu,’ na ‘Mmisionari.’ Barnaba ni kati ya wale Wakristo wa kwanza
kabisa wa jumuiya ya kwanza ya Wakristo ya pale Yerusalemu. Barnaba ambaye hapo
awali alijulikana kama Yusufu, alitoa mali zake zote na kuziweka chini ya
Mitume. “Na Yusufu, aliyeitwa na mitume Barnaba, (maana yake,
Mwana wa faraja), Mlawi, asili yake ni mtu wa Kipro, alikuwa na shamba akaliuza, akaileta fedha,
akaiweka miguuni pa mitume,” Mdo 4:36-37. Barnaba anatambulika pia kama binamu
wa Marko, Kol 4:10. Barnaba na Paulo wanafanikisha vizuri sana Mtaguso ule wa
Yerusalemu kama waleta taarifu juu ya uinjilishaji wao na mikwamo wanayokumbana
nayo. Vile vile walitumika vizuri kama wapeleka taarifa- vyombo vya kupeleka
habari za maamuzi yale ya Mtaguso wa Yerusalemu, Mdo 15:25, 35-37. Licha ya
kutokuwa na uthibitisho wa wazi kwa jambo hili, Mtakatifu Tertulian katika
maandishi yake anamtaja Mtume Barnaba kuwa ndiye mwandishi wa waraka ule kwa
Waebrania. Hata hivyo Maandiko Matakatifu yanatueleza kutokea shida
“mashindano” baina ya Barnaba na Paulo wakajitenga, Mdo 15:39. Kutokuelewa kwa
Barnaba na Paulo kulitokana na Paulo kutopendezwa na kitendo cha Barnaba kumchukua
Yohana alijulikana kama Marko, Mdo 15:38, kwa sababu ndugu huyu aliwaacha huko
Pamfilia asiende nao kazini na kurejea Yerusalemu, Mdo 13:13. Na baada ya kazi
ngumu ya uinjilishaji wa kina, kadiri ya mapokeo, mauti ya kifo dini kama
shahidi wa Kristo yalimkuta Mtume Barnada huko Salamis-Cyprus mwaka 61 BK.
Baada ya historia hiyo
fupi kuhusu Mtume Barnaba na mahusiano yake na Mtume Paulo, kwa namna ya pekee
leo Mama Kanisa anatutaka tutafakari mambo makuu matatu; moja, Msingi wa Kanisa
la wana wa Mungu ulivyojengwa. Pili, wasifu wa Mitume na hasa Barnaba. Na tatu,
maadili yahusuyo kazi hii ya kutumika kwa ajili ya wengine, maisha ya utume
Wapendwa katika Kristo,
Msingi wa Kanisa la wana wa Mungu ulijengwa na Kristo Mwenyewe tunapoliangalia
fumbo zima la mateso, kifo na ufufuko wake. Tukio la Ufufuko, na baadaye tukio
lile la Pentekoste liliwapa nguvu ya ajabu Wakristo wa kwanza. Hawakuwa tena na
woga wa kuhubiri habari njema za Ufufuko na uzima wa milele. Wakristo hawa
walikuwa tayari muda wowote kwa lolote. Kadiri ya Maandiko Matakatifu na
mapokeo ya Kanisa la mwanzo, kutawanyika kwa jumuiya ya kwanza ya Wakristo,
kulitokana na kuhujumiwa kwa jumuiya hiyo, na hasa kile kifo cha Shahidi
Stefano. Kwa upande mwingine, kupitia mateso haya, habari njema zinafika kila
kona na wengi wanamwamini Mungu. “Basi wale
waliotawanyika kwa sababu ya ile dhiki iliyotukia kwa habari ya Stefano,
wakasafiri hata Foinike na Kipro na Antiokia, wasilihubiri lile neno ila kwa
Wayahudi peke yao,” Mdo 11:19. Kutawanyika huku kwa jumuiya hizi za Wakristo
tukienda mbali zaidi ni kutokana na sadaka ile ya pekee aliyoitoa Yesu pale
msalabani. Hakika Damu ya Mwana-kondoo wa Mungu haikupotea bure. Damu hii
imekuwa ‘ufunguo mkuu wa kufungua kila mahali kwa kulifukuza giza na kuuleta mwanga
wa milele. Ni kwa kupitia sadaka hiyo hiyo nasi kwa kila mmoja wetu, Kanisa
linakua na kuenea popote duniani.
Ni kwa namna hiyo
tunapokuwa na Kristo katika nia na matendo yetu tunabarikiwa kwa sababu
tuyafanyayo ni mwendelezo wa kazi yake ya kuikomboa dunia. “Mkono
wa Bwana ukawa pamoja nao, watu wengi wakaamini, wakamwelekea Bwana,” Mdo 11:21.
Hapa tunaona safari ya uinjilishaji ndiyo inaanza, na Kanisa katika maana ya
kila Mbatizwa linakuwa Kanisa la Kimisionari. “Habari
hizo za watu hao zikafika masikioni mwa kanisa lililokuwako katika Yerusalemu;
wakamtuma Barnaba, aende hata Antiokia,” Mdo 11:22. Kazi hizi za kimisionari
ndizo zinazolifanya Kanisa likue na kuenea kila mahali. Kazi hizi pia ndizo
zinazo watambulisha wale wazifanyazo. Ni hapa Antiokia kwa mara ya kwanza
wanafunzi wa Yesu wanaitwa Wakristo. “Na wanafunzi waliitwa Wakristo kwanza
hapo Antiokia,” Mdo 11:26b. Kuitwa kwao huku ni kutokana na matendo yao
kuendana na kile walichokuwa wakikiamini na kukihubiri.
Wapendwa wana wa Mungu,
mtindo huu wa kimisionari unaitajika sana nyakati zetu hata leo. Matendo mema
ndani ya Kristo na katika Kristo, umtambulisha Kristo pale ulipo; na kwa namna
hiyo kwa ubatizo wetu wote tumeitwa kuwa wamisionari. Umisionari wa kutembea na
vipasa sauti kwa sasa hauna nafasi sana. Tunaitaji umisionari wa matendo mema
kwa watu wote. Kristo alishaanza kulifanya hili pale ambapo Wayahudi walitaka
kupata uhakika kama kweli yeye ndiye Kristo mwenyewe. “Yesu
akawajibu, Naliwaambia, lakini ninyi hamsadiki. Kazi hizi ninazozifanya kwa
jina la Baba yangu ndizo zinazonishuhudia,” Yoh 10:25. Kazi azifanyazo Yesu
ndizo zinazomthibitisha na kumtambulisha kuwa yeye ni nani. Ni kwa namna hiyo
hiyo kwamba kazi tuzifanyazo kama wabatizwa na Kanisa kwa ujumla wake
zitamtambulisha Kristo pale tulipo.
Jambo la pili katika
tafakari yetu ya leo ni kuona wasifu wa Mitume na kwa upekee Mtume Barnaba.
Mitume kwa ujumla wao walifanya uinjilishaji wa kina ikiwa ni pamoja na
kuilinda imani ya kweli. Walikuwa tayari na kwa busara ya hali ya juu
wakiongozwa na Roho Mtakatifu walitoa majibu sahihi kwa kile walichoulizwa au
kutuhumiwa. Hivi ndivyo Mtume Petro alivyowasihi wenzake na leo kwa upande wetu,
“Mwe tayari siku zote kumjibu kila mtu
awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu,”
1Pet 3:15. Ni kwa mwono huo, Barnaba na Paulo wanakuwa mstari wa mbele kuhubiri
habari njema ya ufufuko na uzima wa milele.
Barnaba na Paulo
walifanya uinjilishaji wa kina popote pale walipokuwa au kwenda. Safari yao ya
umisionari haikuwa rahisi kwani nyakati nyingine walipata upinzani mkubwa
kutoka kwa Wayahudi na wale wasiomwamini Kristo. Pamoja na kutokukubalika kwa Mtume Barnaba,
Paulo, na wenzake kutokana na ujumbe waliokuwa wakiutoa ikiwa ni mwendelezo wa
kazi ya Kristo, wanakimbilia Listra na Derbe kupata hifadhi. Mtume Barnaba na
Paulo wanafanya mambo makuu kwa mkono wa Mungu, na kuleta tafrani kubwa. Tendo
hili la uponyaji wa mtu mwenye udhaifu wa miguu, kiwete tangu tumboni mwa
mamaye, linaibua hisia za watu hawa wa Likaonia na kuwaona Paulo na Barnaba
kama miungu ya kuabudiwa. “Na makutano
walipoona aliyoyafanya Paulo wakapaza sauti zao, wakisema kwa Kilikaonia,
Miungu wametushukia kwa mifano ya wanadamu. Wakamwita
Barnaba, Zeu, na Paulo, Herme, kwa sababu ndiye aliyekuwa mnenaji,” Mdo
14:11-12. Hakika, tendo hili ni moja ya mambo hatari sana katika utume wetu.
Ukiona hali hii ndani mwa watu inajitokeza na kuacha kumwabudu Mungu na kuanza
kukuabudu wewe kama mchungaji wao, ujue wazi ufanyacho si matakwa ya Mungu bali
shetani amechukua mkondo wake. Ni ukweli usiopingika kwamba, tunastahili
pongezi kwa yale tuyafanyayo na hata wakati mwingine kuthaminiwa hasa kwa
kuitambua kazi tunayoifanya. Ila mtazamo na mwelekeo huu wa kuthaminishwa na
kutambulika kwa yale tuyafanyayo usichukue kamwe nafasi ya Kristo na Mungu.
Ufahamu huu ndiyo unaotupeleka sasa tuangalie sehemu ya tatu, yaani, maadili
yahusuyo kazi hii ya kutumika kwa ajili ya Kristo na wengine.
Hivyo kwa kutambua
kasoro ya kutaka kufanywa miungu watu, Mtume Barnaba na Paulo wanatoa angalizo
kwa Walikaonia na kusema, “Akina bwana, mbona mnafanya haya? Sisi nasi tu
wanadamu hali moja na ninyi; twawahubiri habari njema, ili mgeuke na kuyaacha
mambo haya ya ubatili na kumwelekea Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na nchi
na bahari na vitu vyote vilivyomo; ambaye
zamani zilizopita aliwaacha mataifa yote waende katika njia zao wenyewe,” Mdo
14:14-16. Hatari kubwa katika jambo hili ni kwamba, binadamu anapoukataa
ubinadamu wake, anajeuka kuwa mbaya kuliko shetani, kwani shatani alishaukubali
ushetani wake pale alipomwasi Mungu.
Ndugu yangu, usipompa
Mungu nafasi ya kwanza katika maisha yako chochote kile chaweza kuyaongoza
maisha yako, na mwisho wake ukawa mbaya kwa sababu kitu hicho kama kilivyo
hakina umilele. Maadili ya Mbatizwa yeyote yule ni kuwahubiria watu habari
njema ya wokovu na ufalme wa Mungu. Yesu anasisitiza jambo hili na kusema, “Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme
wa mbinguni umekaribia,” Mt 10:7. Tumeumbwa tuishi milele, na duniani hapa siyo
makao yetu ya kudumu. Tupa hapa kwa maandalizi tu huku tukijua maisha ya hapa
duniani ni jukumu la muda mfupi. Kila mmoja kadiri ya wito na karama zake,
yampasa kutumia vyema karama hizo. Kwa namna hiyo Yesu anatoa wito na kusema, “Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye
ukoma, toeni pepo; mmepata bure, toeni bure,” Mt 10:8. Pamoja na wajibu huu,
Yesu anatoa angalizo pia kuhusu tatizo la kushikamana na mali za dunia hii. “Msichukue
dhahabu, wala fedha, wala mapesa mishipini mwenu; wala mkoba wa safari, wala kanzu
mbili, wala viatu, wala fimbo; maana mtenda kazi astahili posho lake,” Mt
10:9-10. Kuambatana na mambo haya na kuyapa nafasi ya kwanza upunguza hari na
kasi ya kuyatimiza yale tupasayo kufanya.
Ni
vyema pia tukawa waangalifu kwa wale watukaribishao na kutupatia ukarimu wao na
hifadhi. Maisha ya kutangatanga pasipo mwelekeo sahihi ni hatari sana kwa
uchungaji na umisionari kwa ujumla wake. Hivyo “Na
mji wo wote au kijiji cho chote mtakachoingia, tafuteni ni nani humo aliye mtu
mwaminifu; mkae kwake hata mtakapotoka,” Mt 10:11. Ni vyema kufanya kile
kilichokupeleka pale, na fanya hicho tu. “Nanyi mkiingia katika nyumba isalimuni. Na nyumba ile ikistahili, amani yenu
na iifikilie; la, kwamba haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi,” Mt
10:12-13. Tatizo kubwa hutokea pale tunapobadili nia na sababu ya kuwa pale
tulipopaswa kuwa. Tatizo hili ni sawa na “kubadili gia angani ilihali hujui
utaangukia wapi kwa maamuzi hayo.”
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Msichukue
dhahabu, wala fedha, wala mapesa mishipini mwenu; wala mkoba wa safari, wala kanzu
mbili, wala viatu, wala fimbo; maana mtenda kazi astahili posho lake,” Mt
10:9-10
Tusali:-Ee Yesu,
tujalie moyo wa kimisionari pale tulipo. Amina.
Mtakatifu
Barnaba Mtume, utuombee.
No hay comentarios:
Publicar un comentario