JUMATATU WIKI YA 10 YA MWAKA-C
Somo: 1Fal 17:1-6
Zab: 121:1bc-2, 3-4, 5-6, 7-8
Injili: Mt 5:1-12
Nukuu:
“Basi Eliya
Mtishbi, wa wageni wa Gileadi, akamwambia Ahabu, Kama Bwana, Mungu wa Israeli,
aishivyo, ambaye ninasimama mbele zake, hakutakuwa na umande wala mvua miaka
hii, ila kwa neno langu,” 1Fal 17:1
“Neno
la Bwana likamjia, kusema, Ondoka
hapa, geuka, uende upande wa mashariki, ujifiche karibu na kijito cha Kerithi
kinachokabili Yordani,” 1Fal 17:2-3
“Kunguru
wakamletea mkate na nyama asubuhi, na mkate na nyama jioni, akanywa maji ya
kile kijito,” 1Fal 17:6
“Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila
neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu,” Mt 5:11
“Furahini,
na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo
walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu,” Mt 5:12
TAFAKARI: “Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa
mbinguni.”
Wapendwa wana wa Mungu, sehemu kubwa ya maisha ya mwanadamu hapa
duniani ni kutafuta maana ya maisha yake, na kuipata ile furaha ya kweli.
Binadamu huyu ulifanya jambo hili anapoitazama historia yake kama somo kwa
lengo ya kuyarekebisha yale ambayo hayakwenda vyema kwa wakati huu aishipo
sasa, ili kule aendapo asipokujua vizuri kuwe na tumaini. Hivyo, somo la Injili
ya leo kwa upana wake linaelezea hali halisi katika mahangaiko ya mwanadamu, na
ulimwengu juu tunaoishi. Na kwa kulisema hilo, Yesu leo anatutaka tuzitafakari
kwa kina heri hizo alizozisema, Mt 5:3-12.
Lakini ili tuifikie furaha ile ya kweli ambayo hiyo ndiyo lengo
halisi, hatuna budi kuufahamu ulimwengu huu tunaoishi leo. Bila kuujua
ulimwengu huu ambapo ndipo tunapoishi, ni vigumu pia kuiona furaha ile ya kweli
inayoendana na malengo ya kuumbwa kwetu. Mimi na wewe tumeumbwa ili tuishi
milele. Kwa ufupi na kwa kina, Yesu anatupa siri ya hali halisi ya ulimwengu
huu tunaoishi leo. Naye anasema, “Amin,
amin, nawaambia, Ninyi mtalia na kuomboleza, bali ulimwengu utafurahi; ninyi
mtahuzunishwa, lakini huzuni yenu itageuka kuwa furaha,” Yoh 16:20. Pamoja na
mazingira kama haya, na tunaposimama kwa lile lililo kweli na haki, Kristo
hatotuacha kamwe. Ni katika kweli hii Mungu anamwahidia Nabii Eliya uhai mbele
ya safari ambao kwa akili ya kibinadamu ni vigumu kuamini. Naye Mungu anasema, “Kunguru wakamletea mkate na nyama asubuhi, na mkate na
nyama jioni, akanywa maji ya kile kijito,” 1Fal 17:6. Ni kwa sababu hiyo
Yesu aliyatoa maisha yake, ili mimi na wewe leo tuwe huru kutoka utumwa wa
dhambi na uovu wake wote. “Basi ninyi hivi
sasa mna huzuni; lakini mimi nitawaona tena; na mioyo yenu itafurahi, na furaha
yenu hakuna awaondoleaye,” Yoh 16:22. Hivyo tuitafutapo furaha hiyo ya kweli hatuna
budu kujua hali ya ulimwengu wetu tunaoishi kama alivyotufunulia Bwana wetu
Yesu Kristo. Je, tunafanye nini sasa?
Jambo la kufanya ni
kuziishi heri alizotuambia Bwana wetu Yesu Kristo katika Injili ya leo. Katika
tafakari hii sintozipitia heri hizo moja baada ya nyingine, bali niwatake
tutafakari heri hizo kwa kuyatazama mambo makuu manne ambayo kwa kiasi fulani
yanasema juu ya maisha yetu ya leo. Mambo hayo ni kama yafuatayo: Kwanza, kuwa
na nafasi ndani ya moyo wako. Pili, hapo ulipo fanya zaidi na achana na mazoea.
Tatu, hapo ulipo kuwa mzalendo kwa kujipokea, kuwapokea wengine, na kuipigania
jamii yako-Taifa lako. Na nne, kuwa alama na kielelezo hai cha amani ya kweli
hapo ulipo.
Wapendwa wana wa Mungu,
tuanze na hili la ‘kuwa na nafasi ndani ya moyo wako.’ Huwezi kuwa na furaha ya
kweli kama hakuna nafasi ya Mungu ndani ya maisha yako. Hofu ya Mungu ndani
yetu ni mizania ya kujipokea kama tulivyo, na kutufanya tujitahidi kufika pale
ambapo tunapatamani. Itakuaje basi kufanya hivyo kama huna nafasi ya Mungu
ndani yako? Kuwa na nafasi ndani ya moyo wako, Yesu ameizungumzia katika Injili
ya leo kwa mtindo huu, “Heri walio maskini wa roho; Maana ufalme wa mbinguni
ni wao,” Mt 5:3. Ni umaskini huu wa roho, yaani, kuwa na nafasi ya Mungu ndani
yako, kutakao kupeleka katika furaha ile ya kweli, yaani, ufalme ule wa
Mbinguni baada ya kuvishinda vita hivi hapa duniani. Haya ndiyo maisha yale ya
umilele kama lengo halisi la kuumbwa kwetu, yaani, tumeumbwa tuishi milele.
Pili,
‘fanya zaidi na achana na mazoea.’ Hakuna saratani mbaya katika maisha ya
mtindo wowote ule, pale unapofikia hatua ya kuridhika na kila kitu, na kuacha
mambo yaende tu kama yalivyo, kwa vigezo kwamba kama juzi na jana ilikuwa
hivyo, basi hata leo na kesho itakuwa hivyo hivyo. Mwenendo huu wa maisha ni
mwendo wa ‘kufa pole pole’ huku ukiona. Kumbe kuishi maisha yenye malengo ni
kufanya zaidi ukijua siyo kwa sababu ya ubinafsi wako, bali kwa ajili ya
wengine kwa sasa na hata vizazi vijavyo. Mtume Paulo anatufafanulia vizuri
kuhusu kweli hii na kusema, “Mtu
asitafute faida yake mwenyewe, bali ya mwenzake,” 1Kor 10:24. Na tutakuwa
tunafanya hivyo siyo kwa kuutafuta utukufu binafsi, bali kuifikia tumaini lile
ambalo kila mmoja wetu bila kujali historia yake, itikadi zake, familia au
kabila, anatamani kuipata. Kwa Mkristo na mfuasi wa Kristo aliye hai hufanya
hivyo akijua ukweli huu kwamba, “hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi
yake, wala hakuna afaye kwa nafsi yake. Kwa
maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi
kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana,” Rum 14:7-8. Hivyo ndugu yangu,
kulifikia tumaini hili yakupasa wewe na mimi kuwa na njaa ya tumaini hilo. Ni
katika mazingira haya Yesu anasema, “Heri
wenye njaa na kiu ya haki; Maana hao watashibishwa,” Mt 5:6. Je, hali ipo vipi
hapo ulipo? Jamii inayokuzunguka inatenda haki nawe ukiwa mmoja wapo? Kama hilo
halipo itakuwaje basi uwe na furaha ya kweli? Changamoto hii ni yangu na yako
pia. Tuwe na njaa na kiu ya haki. La sivyo hatutaweza kushibishwa, yaani kuwa
na furaha ya kweli.
Tatu, hapo ulipo ‘kuwa
mzalendo’ kwa kujipokea, kuwapokea wengine, na kuipigania jamii yako-Taifa
lako. Ndugu yangu, mizania ya haki na kweli, ipo ndani ya usafi wa moyo wa mtu.
Kuna msemo wa kifalsafa usemao kwamba, “mtu hutoa kile alichokuwa nacho.” Hivyo
huwezi kutoa kile usichokuwa nacho. Lakini naweza kuifikia mizania hii ya usafi
wa moyo kwa kufanya hatua hii muhimu sana katika maisha yangu, yaani, kujipokea
kama nilivyo. Hapa simaanishi tu kuyaona mazuri yako na mabaya yako ukaridhika
nayo na kutokufanya chochote. Wito wa kila mmoja wetu ni kuwa wakamilifu kama
Baba yetu wa Mbinguni alivyo makamilifu, Mt 5:48. Kama hili ndilo lengo msingi
la maisha na malengo yangu, sinabudi kuurekebisha udhaifu wangu ili kuufikia
usafi ule wa moyo kila siku ya maisha yangu. Hii siyo kazi ya siku moja.
Jambo hili, yaani,
‘kujipokea’ likichukua mkondo wake sawa sawa, mengine hufuata, yaani, kuwapokea
wengine, na kuwa tayari kwa maslahi mapana ya jamii inayokuninguka, na Taifa
zima. Huu ndio uzalendo tunaouzungumzia hapa, yaani, fanya yote kwa ajili ya
wengine kwa kulitazama tumaini lililo mbele yako na kwa wote. Katika kweli hii,
jambo hili litawezekana kama Yesu anasemavyo, “Heri
wenye moyo safi; Maana hao watamwona Mungu,” Mt 5:8. Ni katika moyo ulio safi
utofautisha namna ya kufikiri kwetu, kuamua kwetu, na kutenda kwetu. Mlolongo
huu ndiyo ule unaotupatia cheo chetu halisi, yaani, utakatifu wako. Hivyo
tutamwona Mungu tu tukiwa na cheo hiki, yaani, Utakatifu kwa sababu Mungu wetu
ni Mtakatifu.
Na nne, ‘kuwa alama na
kielelezo hai cha amani ya kweli hapo ulipo.’ Ni moyo safi huo ambao utuwezesha
kuona kitu kama kilivyo, na kusema kama kilivyo, ili kibaki kama kilivyo katika
hali yake daima. Tatizo kubwa hapa mara nyingi mimi na wewe huvaa miwani ya
‘tulivyo,’ na kupoteza uhalisi wa jambo au kitu kama kilivyo. Miwani hii ya
‘tulivyo,’ yaweza kuwa itikadi zetu kisiasa na kidini. Miwani hii ya ‘tulivyo
inaweza kuwa pia familia zetu, koo zetu, na makabila yetu. Kwa mtindo huo,
tutawezaje kuwa wapatanishi wa kweli? Ndugu yangu, tunapoambatana na mambo hayo
kwa kushikamanana nayo ou kung’ang’ania nayo kama yalivyo, twajisababishia
upofu wa kudumu. Ni vyema mimi na wewe tukatoka katika boksi hilo na kupata
mwanga halisi wa kuona vizuri ukweli wa kile tukitazamacho. Huku ndiko kuwa
‘wapatanishi’ kama asemavyo Yesu, “Heri
wapatanishi; Maana hao wataitwa wana wa Mungu,” Mt 5:9. Mungu yu mpatanishi
wetu katika maana nzima ya Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, Yoh 1:14. Ni
upananisho huu ambao kilele chake kilikuwa kifo cha Mwanaye Mpenzi pale
msalabani, ambacho kifo hicho kilituhesabia haki kuwa wana na warithi wa ufalme
wa Mungu. Hivyo leo mimi na wewe tunapokuwa wapatanishi tunamwakilisha Mungu
kama watoto wake. Na huu ndio uwana wa Mungu, yaani, kuwa mpatanishi pale
ulipo.
Mambo
yote manne tuliyoyaona hapa juu yanahitaji sadaka. Sadaka ya kwanza ni
kujikatalia nafsi yako mwenyewe ili uwe na mizania ya kweli na haki katika yale
yote utakayokutana nayo kwa kufikia malengo ya mambo hayo manne. Somo la kwanza
leo linatupa kweli hiyo kwa mfano wa nabii Eliya. Aliyaona mambo kama yalivyo
na kuyasema kama yalivyo. “Basi Eliya Mtishbi, wa wageni wa Gileadi, akamwambia Ahabu,
Kama Bwana, Mungu wa Israeli, aishivyo, ambaye ninasimama mbele zake,
hakutakuwa na umande wala mvua miaka hii, ila kwa neno langu,” 1Fal 17:1. Sadaka
uitoayo ina maana kwa sababu mbele kuna heri na tumaini. Kielelezo cha heri
hiyo na tumaini ni Kristo mwenyewe. Mateso na majaribu lazima tutakutana nayo
katika safari hii. Kwa msisitizo mkubwa Yesu anasema, “Heri
ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa
ajili yangu. Furahini, na
kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo
walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu,” Mt 5:11-12. Kuna furaha kubwa sana
moyoni kuhukumiwa kwa sababu tu umetenda haki na kuishuhudia kweli. Haya ndiyo
maisha ya ushuda hasa katika nyakati zetu hizi tunapoona na kushuhudia
ubabaishaji kila kona.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Heri
ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa
ajili yangu,” Mt 5:11
Tusali:-Ee Yesu, furaha ya
kweli ni pale ninapokufia katika kweli na haki. Nipo ujasiri ya kukijongea kifo
hicho. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario