sábado, 29 de abril de 2017

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 3 YA PASAKA


JUMAMOSI  WIKI YA 3 YA PASAKA

Somo: Mdo 9:31-42

Zab: 116:12-13, 14-15, 16-17

Injili: Yoh 6:60-70

Nukuu:

Basi kanisa likapata raha katika Uyahudi wote na Galilaya na Samaria, likajengwa, likiendelea na kuongezeka katika kicho cha Bwana, na faraja ya Roho Mtakatifu,” Mdo 9:31

Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima,” Yoh 6:63

Akasema, Kwa sababu hiyo nimewaambia ya kwamba hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa na Baba yangu,” Yoh 6:65

“Basi Simoni Petro akamjibu, Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu,” Yoh 6:68-69

TAFAKARI: “Jambo lolote lile lenye kuakisi Utukufu wa Mungu lililo chini ya Kristo na ndani yake linausalama. Kristo ndiye neno la uzima wa milele na Mtakatifu wa Mungu.”

Wapendwa wana wa Mungu, ‘jambo lolote lile lenye kuakisi utukufu wa Mungu na lililo chini ya Kristo na ndani yake linausalama. Kristo ndiye neno la uzima wa milele na Mtakatifu wa Mungu.’ Baada ya Ufufuko wake Yesu Kristo, jumuiya ya kwanza ya Wakristo ilijawa hofu na hawakuwa na usalama wa maisha yao hasa hujuma ya wazi iliyokuwa inafanywa na Wayahudi ambao hawakuamini wala kuifuata njia hii. Hali ilikuwa mbaya zaidi pale Sauli ambaye baada ya kuongoka kwake anajualikana kama Paulo, alivyolitesa Kanisa hili la mwanzo. Pauli sasa akiwa ndani na katika Kristo anakiri na kusema, “mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mitume, kwa sababu naliliudhi Kanisa la Mungu. Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami,” 1Kor 15:9-10

Ndugu yangu, kile ulicho na ukifanyacho ndani na katika Kristo, ni baraka na neema za Mungu. Mungu kamwe hawezi kukutupa unapokiri kwenda kinyume na mpango na mawazo yake. Mpango na mawazo ya Mungu kwa kila mmoja wetu ni ya amani na yenye tumaini siku ya mwisho ya kila mmoja. “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho,” Yer 29:11. Kuishi katika mpango na mawazo ya Mungu ni kujisalimisha kwake, na hii ndiyo njia sahihi ya kuishi.

Wakristo wa mwanzo kwa kutambua ukweli huu-‘kujisalimisa’ na njia sahihi ya kuishi, wanawajibika kikamilifu kwa Mungu Baba, Mungu Mwana na Roho Mtakatifu. Ndani ya Utatu huu Mtakatifu na Umoja huu usiogawanyika, unabii wa Yeremia unajidhihirisha wazi kwamba, Nanyi mtaniita, mtakwenda na kuniomba, nami nitawasikiliza,” Yer 29:12. Baada ya kuongoka kwake Paulo ikiwa ni ishara ya wazi ya Kristo kulisimamia Kanisa lake, amani na utulivu kwa wafuasi wa Kristo vinarejea. “Basi Kanisa likapata raha katika Uyahudi wote na Galilaya na Samaria, likajengwa, likiendelea na kuongezeka katika kicho cha Bwana, na faraja ya Roho Mtakatifu,” Mdo 9:31. Hali hii ya Kanisa ni uthibitisho pia wa maneno ya Kristo mwenyewe kwamba, “Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote,” Yoh 15:5. Hakika bila Kristo hatuwezi kufanya lo lote lile liwe dogo au kubwa!

Ni katika amani hii, utulivu, na matumaini ndani na katika Kristo na Roho Mtakatifu ishara nyingi zinafanyika katika jumuiya hii ya kwanza ya Wakristo. Hapa tukumbuke jambo hili muhimu; Ishara hizi siyo kielelezo cha Imani, bali ni kikoleza cha Imani hasa kwa wale ambao bado hayajakomaa Kiroho. Hivyo tunaona Mtume Petro akiwa Lida anamponya Ainea, mtu aliyekuwa amelala kitandani miaka minane; maana alikuwa amepooza, Mdo 9:33.Petro akamwambia, Ainea, Yesu Kristo akuponya; ondoka, ujitandikie. Mara akaondoka,” Mdo 9: 34. Ni huko Lida pia tunaona ishara nyingine akiifanya Mtume Petro kwa njina la Yesu anaurudishia tena uhai wake mwanamke yule Mjane Tabitha, tafsiri yake ni Dorkasi (yaani paa); mwanamke ambaye alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa, Mdo 9:36. “Petro akawatoa nje wote, akapiga magoti, akaomba, kisha akaelekea yule maiti, akanena, Tabitha, ondoka. Naye akafumbua macho yake, na alipomwona Petro akajiinua, akaketi,” Mdo 9:40.

Matendo haya ya uponyaji yanasadifu na kuitimisha unabii wa Yeremia kwamba, “Nanyi mtanitafuta na kuniona, mtakaponitafuta kwa moyo wenu wote,” Yer 29:13. Kristo anaonekana katika maisha ya kila moja kwenye jumuiya hii ya kwanza ya Wakristo iliyomridhia kwa Imani. Jumuiya inakuwa kitu kimoja katika shida na raha ndani na katika Kristo Yesu. Umoja huu wa kupendana na kutaabikiana unazaa utume na uinjilishaji kwa wale wote wasiolifahamu jina hili yenye nguvu na la ajabu-Yesu wa Nazareti. Mtindo huu wa maisha unakamilisha pia unabii wa Yeremia, “Nami nitaonekana kwenu, asema Bwana, nami nitawarudisha watu wenu waliofungwa, nami nitawakusanya ninyi, nikiwatoa katika mataifa yote, na katika mahali pote, nilikowafukuza, asema Bwana,” Yer 29:14a. Ndani na katika Kristo si watumwa tena wa hali yoyote ile, bali tu huru.

Wapendwa wana wa Mungu, hayo yote tuliyoyatafakari yanauzima yakiwa ndani na katika Kristo. Ni katika roho na siyo mwili yote upata uzima. “Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima,” Yoh 6:63. Ni kwa njia ya Mungu Baba na Mungu Mwana-Kristo, tunapewa Roho huyu wa Mungu kuyaishi yale yote kila mtu kadiri ya hali na wito wake. “Kwa sababu hiyo nimewaambia ya kwamba hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa na Baba yangu,” Yoh 6:65. ‘Kristo ndiye njia, kweli, na uzima,’ Yoh 14:6. Miongoni mwetu na tulio Wakristo, yaani wafuasi wake Kristo kwa Sakramenti ya Ubatizo, wapo ambao maisha yao ya kila siku yametawaliwa na ujanja-ujanja tu. Ndugu yangu, fanya yote ufikiriyo kuyafanya, ila kumbuka maneno haya ya Yesu, “pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote,” Yoh 15:5

Mafundisho haya ya Yesu kuhusu kujiachia kwake kunakoendana na wito wa kila mmoja wetu, yanakuwa mafundisho magumu sana kwani yanatuhitaji kujiachilia kwake kabisa. Asilimia 98% hazitoshi! Yatupasa kuushinda ubinadamu wetu kila siku. “Basi Yesu akawaambia wale Thenashara, Je! Ninyi nanyi mwataka kuondoka? Yoh 6:67. Katika hali hii ya kukata tamaa kwa wanafunzi (kundi lile kubwa lililokuwa likimfuata) juu ya fundisho hili la kujiachia bila kujibakiza, na hivyo kurudi nyuma, Simoni Petro anajibu, “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu,” Yoh 6:68-69. Wapendwa wana wa Mungu, Kristo anayo maneno ya uzima. Je, uzima wako unaupata wapi? Ni kwa hila na ujanja-ujanja wako? Embu itazame vizuri filamu ya maisha yako. Yatazame vizuri matukio yale ambayo hukuwa Ufunuo wa Utukufu na Uzuri wa Mungu. Hata kama matukio hayo yanauzunisha na ukajiona kutokuwa na thamani mbele ya Mungu, kamwe usiyafanye ukuta wa kutokuona neema na huruma ya Mungu. Tambua ukweli huu: ‘Neema na Huruma ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu.’

Tumsifu Yesu Kristo!

Basi Simoni Petro akamjibu, Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu,” Yoh 6:68-69

Tusali:-Ee Yesu Mwema, ni kwako tu kuna usalama na uzima wa milele. Tuongoze kila mmoja wetu kufahamu ukweli huu na kuuishi. Liongoze Kanisa lako ili siku zote liwe kielelezo kamili cha uwepo wako. Amina

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 3 YA PASAKA


IJUMAA WIKI YA 3 YA PASAKA

Somo: Mdo 9:1-20

Zab: 117:1ab, 2

Injili: Yoh 6:53-58

Nukuu:

Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe,” Mdo 9:5

“Lakini Anania akajibu, Bwana, nimesikia habari za mtu huyu kwa watu wengi, mabaya mengi aliyowatenda watakatifu wako Yerusalemu; hata hapa ana amri itokayo kwa wakuu wa makuhani awafunge wote wakuitiao Jina lako,” Mdo 9:13-14

“Lakini Bwana akamwambia, Nenda tu; kwa maana huyu ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli,” Mdo 9:15

“Mara akamhubiri Yesu katika masinagogi, kwamba yeye ni Mwana wa Mungu,” Mdo 9:20

Basi Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu,” Yoh 6:53

“Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi,” Yoh 6:57

TAFAKARI: “Hakuna lisilowezekana kwa Mungu; Sauli afanywa chombo kiteule cha Kristo,”

Wapendwa wana wa Mungu, tukiwa tunazidi kutafakari hujuma dhidi ya jumuiya ya kwanza ya Wakristo huko Yerusalemu, na baada ya kuuwawa Shahidi Stefano, Sauli anaomba barua ili awakamate watu wa njia hii na kuwafunga gerezani. Ni katika mateso haya Kristo mwenyewe analisimamia jambo hili, na kumwongoa mtesaji mkuu wa kundi lake. Tendo hili la Yesu Kristo Mfufuka kulisimamia Kanisa lake na hasa wongofu wa Sauli, linathibitisha kweli ya sala la Yesu kabla ya mateso na kifo chake cha Msalaba. Yesu anasali, “Nilipokuwapo pamoja nao, mimi naliwalinda kwa jina lako ulilonipa, nikawatunza; wala hapana mmojawapo wao aliyepotea, ila yule mwana wa upotevu, ili andiko litimie,” Yoh 17:12. Sauli anapigwa upofu na kuanguka chini. Katika hali hii ya giza na ukimya, Sauli anasema, “U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe,” Mdo 9:5.

Kwa matendo haya ya Sauli, Kanisa la mwanzo halikuwa na amani hata kidogo. Pamoja na hofu hii ya Kanisa la Mwanzo juu ya Sauli na genge lake katika hujuma, anatukumbusha siku ile ya kukamatwa kwake alipowauliza wale Maaskari, ‘Mnamtafuta nani?’ Yoh 18:7. “Yesu akajibu, Nimekwisha kuwaambieni ya kwamba ni mimi; basi ikiwa mnanitafuta mimi, waacheni hawa waende zao. Ili litimizwe lile neno alilolisema, Wale ulionipa sikumpoteza hata mmoja wao,” Yoh 18:8-9. ‘Ili litimizwe lile neno alilolisema-wale ulionipa sikumpoteza hata mmoja wao,’ Mwinjili Yohane anatukumbusha ile sala ya Yesu kabla ya mateso yake, Yoh 17:12, na Yesu Kristo ni nani katika safari hii ya ukombozi wa Mwanadamu, Yoh 1:1-3, 14, 17 (Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu. Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika. Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli. Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo)

Kwa nyakati zetu za leo na hasa Kanisa letu la Tanzania kuna kila aina za dalili kuibuka taswira ya Sauli mwingine wa nyakati zetu. Sauli huyu amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kujenga hofu ndani ya waamini leo. Imani yetu leo inawindwa sana. Tumeanza kusongwa na hofu na mashaka hasa tunapokusanyika kwa wingi kumsifu na kumwabudu Mungu. Leo tunaye Sauli mwingine, ambaye huwalipua wakristo na kuwachinja kama kuku. Je, ni mungu gani anayekubali, kubariki na kutetewa na binadamu anayemtoa binadamu mwenzake sadaka tena kwa ukatili kama huu?

Sauli wa nyakati za jumuiya ya kwanza ya Wakristo aliogopeka sana. Hata katika hatua za kumrudishia kuona kwake, haikuwa rahisi wakristo kusadiki kama mtu huyu amemjeukia Kristo. Anania anapoambiwa na Bwana katika maono kufanya kazi hii, anaingiwa na hofu kubwa na mashaka. Anania anajibu, “Bwana, nimesikia habari za mtu huyu kwa watu wengi, mabaya mengi aliyowatenda watakatifu wako Yerusalemu; hata hapa ana amri itokayo kwa wakuu wa makuhani awafunge wote wakuitiao Jina lako,” Mdo 9:13-14. Jambo hili si rahisi kulifanya. Sauli wa leo, siyo tu anamilipuko, bali amejikoka risasi, visu, mapanga, mashoka, na tindikali. Nani anaweza kumsogelea? Nani anaweza kupeleka ujumbe kwa Sauli wa leo kama Anania? Wapendwa wana wa Mungu, leo tunaishi nyakati tofauti kabisa. Mtume Paulo ambaye kabla ya wongofu wake alijulikana kama Sauli, anatupa njia ya kupambana na Sauli wa nyakati hizi kwa kusema, “Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema,” Rum 12:21.

Ndugu yangu, pasipo njia Bwana hufanya njia, I Kor 10:13. Ninayo imani kubwa sana juu ya vita hivi vya kidini. Ni Kristo mwenyewe atakayempiga upofu Sauli huyu wa sana, na kati yetu Kristo atawainua akina Anania na kufanya kazi yake. Yesu Kristo anaondoa hofu ya Anania kwa kumpa ujumbe huu, “Nenda tu; kwa maana huyu ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli,” Mdo 9:15. Ninaimani katika neno hili kwa Sauli wa leo. Kristo yupo tayari kumtumia Sauli wa leo alichukue Jina lake mbele ya Mataifa, na wakuu wote wa dunia hii. “Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo,” Yoh 1:17. Sauli wa leo ameibuka na ndoto kubwa na yupo mbioni kuunda dola ya Kisauli. Ni kwa neema na kweli ndani na katika Kristo, naamini kwa kupitia njia hii ya kuushinda ubaya kwa wema Kristo atalisimamia Kanisa lake pote duniani na kumshinda Sauli wa nyakati zetu leo. Kristo tunayemwamini na kumfuata ni Kristo hai na siyo wa historia.

Ni Kristo huyu ninayemwamini na kumhubiri atakaye mgeuza Sauli huyu wa sasa, na kwa kinywa chake atasema kama alivyosema mara ile ya kwanza baada ya kupigwa upofu, na “mara akamhubiri Yesu katika masinagogi, kwamba yeye ni Mwana wa Mungu,” Mdo 9:20. Naweza nisieleweke katika hili, ila hakuna lisilowezekana kwa Mungu. Siamini kabisa kwamba Kristo atavumilia mateso ya waja wake wanaochinjwa kama kuku huko Somalia, Ethiopia, Misri, na Irak. Siamini jambo hili hata kidogo. Ni swala la wakati tu.

Ndugu yangu, ni katika kuushiriki mwili na damu yake Kristo, hasa katika hali hii ya mateso tunapata uzima wa milele. Naye anasema, “Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu,” Yoh 6:53. Mwili huu na damu hii twaweza kuula na kunywa katika hali ya mateso kama sasa, na ndipo tunapofunuliwa na kuupata uzima huo wa milele ndani yetu. Uhai wetu u salama ukiwa ndani ya Kristo kama Yeye alivyo ndani ya Baba daima. “Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi,” Yoh 6:57. Je, waliamini neno hili?

Tumsifu Yesu Kristo!

Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe,” Mdo 9:5

Tusali: -Ee Yesu nipe Neema ya kujua maana ya Mateso yangu katika wewe na ndani yako. Nifanye Chombo cha Amani yako, ili niushinde ubaya kwa wema kama ulivyo tupenda upeo na kujitoa sadaka pale Msalabani. Amina

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 3 YA PASAKA


ALHAMISI WIKI YA 3 YA PASAKA

Somo: Mdo 8:26-40

Zab: 66:8-9, 16-17, 20

Injili: Yoh 6:44-52

Nukuu:

“Tazama, maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe?,” Mdo 8:36b

Filipo akasema, Ukiamini kwa moyo wako wote, inawezekana. Akajibu, akanena, Naamini ya kwamba Yesu Kristo ndiye Mwana wa Mungu,” Mdo 8:37 

Kisha, walipopanda kutoka majini, Roho wa Bwana akamnyakua Filipo, yule towashi asimwone tena; basi alikwenda zake akifurahi,” Mdo 8:39

Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka; nami nitamfufua siku ya mwisho,” Yoh 6:44

Mimi ndimi chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni; mtu akila chakula hiki, ataishi milele. Na chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu,” Yoh 6:51

TAFAKARI: “Kwa nini nashindwa kukata shauri kuhusu maisha yangu?”

Wapendwa wana wa Mungu, kuna msemo wa kiswahili usemao, ‘kuvuja kwa pakacha nafuu kwa mchukuzi.’ Msemo huu unaendana na somo letu la leo, na kile kilichotokea Jerusalemu baada ya kifo cha Shahidi Stefano. Jumuiya ya kwanza ilitawanjika sehemu mbalimbali, huku ikimbeba Kristo kwa kila walichokuwa wakikifanya. Hivyo tunaona Mtume Filipo akihubiri na mara hii akikutana na Towashi mmoja aliyekuwa amekwenda Yerusalemu kuabudu. Bila shaka kwa namna alivyokuwa Towashi huyu alikuwa tayari ameandaliwa na Mungu mwenyewe kwa tukio ambalo Filipo atalifanya, kama Yesu anavyosema kwenye Injili ya leo, “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka; nami nitamfufua siku ya mwisho,” Yoh 6:44. Ukweli ni kwamba, Filipo anamkuta Towashi huyu akisoma chuo cha Nabii Isaya.

Baada ya mazungumzano na kuhubiriwa kuhusu Kristo, Towashi anafikia hatua ya kukata shauri na kuachana na maisha ya zamani na kuanza maisha mapya, na kusema, “Tazama, maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe?,” Mdo 8:36b. Mpendwa tunayesafiri wote katika tafakari hii, hakuna mtihani mgumu kwa binadamu kama “kufanya maamuzi” na hasa maamuzi ya maisha mapya na yenye mtazamo mpya. Wengi wetu mtihani huu umetushinda na tumebakia kudhani kwamba maisha yetu yamelaaniwa. Kukata shauri ni hatua ya kwanza ya kukua katika maisha ya kawaida na hasa ya kiroho.

Kukata shauri huku kunanikumbusha rafiki yangu mmoja aliyekuwa mtaratibu sana na mwenye kuipenda familia yake. Ila mambo hubadilika mara anapokunywa pombe. Jambo hili lilikuwa kero sana kwa mke wake, na kila lilipotokea basi nilikuwa msuluhishi. Mara zote jamaa huyu alikiri kuwa alifanya makosa na hivyo kuamua kuacha kunywa pombe.

Baada ya muda kama miezi miwili mitatu hivi, jambo hili lilijirudia tena. Na mara hii nilimwuliza; Rafiki, tatizo lipo wapi mbona unarudia kulekule ulipoamua kutokurudi? “Father, tatizo lipo hapo, ‘naomba unisaidie. Ingewezekana kuyatoa mabango yote huko barabarani yenye tangazo ya “KILI TIME,” ingenisaidia kuacha pombe. Ninapoliona tangazo hili, ujue bar ifuatayo lazima niingia na kusaka kinywaji hicho kwa uvumbi na uvumba,” Rafiki yangu alinijibu kwa upole wa hali ya juu.

Wapendwa wana wa Mungu, mtakubaliana na mimi kwamba mabango yalioko huko barabarani hayana tatizo. Tatizo kubwa lipo pale tunaposhindwa kufanya maamuzi ya kina na kuanza maisha mapya kama kweli tunataka mabadiliko. Towashi baada ya kuyaona maji aliamua kubatizwa. Filipo anamwambia, “ukiamini kwa moyo wako wote, inawezekana. Akajibu, akanena, Naamini ya kwamba Yesu Kristo ndiye Mwana wa Mungu,” Mdo 8:37.

Ndugu yangu kwa nini unashindwa kukata shauri na kuanza maisha mapya kwa kuamini utaweza ndani na katika Kristo Yesu? Yapo mambo mengi ya kujikatalia ili ukue mwili na roho. Hapa hakuna jambo kubwa wala dogo kama kwa kiasi fulani linakwamisha kukua kwako kimwili na kiroho. Yawezekana, unaishi uchumba sugu, na hivyo kutoshiriki masakramenti. Uchumba siyo ndoa! Kata shauri na anza maisha mapya. Siku hizi ukipenda na kuamua kufunga ndoa unaweza hasa zile misa za alfajiri na baada ya tukio hilo ukaendelea na shughuli zako za kila siku. Achana na ndoa za matarumbeta na mbwembwe zisizo na maana. Ndoa nyingi zenye mbwembwe huishia mtindo huo huo wa mbwembwe.

Baada ya kazi hii muhimu aliyoifanya Filipo, Roho wa Bwana anamnyanyua na kumpeleka mahali pengine kwa kazi yake. “Kisha, walipopanda kutoka majini, Roho wa Bwana akamnyakua Filipo, yule towashi asimwone tena; basi alikwenda zake akifurahi,” Mdo 8:39. Nasi tunaotoa huduma za kiroho katika vituo tulivyopangiwa tunakumbushwa hapa kwamba, tukishafanya yale tuliyotakiwa kufanya kama watumishi, tusianze kujenga viota. Tuache viota hivyo na kwenda sehemu nyingine mara tunapoamuriwa kufanya hivyo. Wengi pia wameshindwa mtihani huu kwa kukosa utii kwa Roho Mtakatifu na wale waliotuweka kwenye tume hizo-Wahudumu wetu wakuu wa Mashirika.

Wapendwa katika Kristo, tunapomtumikia Kristo tunauhakika wa maisha yenye uzima wa kweli. Katika maisha hayo na Kristo, wote wahudumu na wahudumiwa hustawi na kufikia hatma yake. Ndani ya maisha haya tunapata furaha ya kweli, kwa sababu tunayemtumikia ndiye ALFA na OMEGA. Naye Yesu Kristo anasema, “Mimi ndimi chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni; mtu akila chakula hiki, ataishi milele. Na chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu,” Yoh 6:51

Ndugu yangu tuliyesafiri pamoja katika tafakari hii, nikuache na neno hili; uzima wako hasa wa hapa ulimwenguni bila Kristo hauna maana kabisa. Shughuli zako hapa duniani bila Kristo ni upepo tu usiojua uvumako na uendako. Usalama wetu kimwili na kiroho bila Kristo ni ndoto ya samaki kusihi jangwani. Hata kama ndoto hiyo itatimia, kifuatacho ni Kifo tu. Wapo watu wengi miongoni mwetu, walitamani ndoto kama hizo, na baada ya kufikia malengo ya ndoto zoa tulipigwa mshangao mkubwa na kusema hivi: “AMEKUFA MAPEMA KWELI BILA KUFURAHIA MATUNDA YAKE!

Tumsifu Yesu Kristo!

“Tazama, maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe?,” Mdo 8:36b

Tusali: Ee Yesu na Mwakozi wangu, niwezeshe kufanya maamuzi sahihi kwa wakati sahihi kuiokoa Roho, Mwili, na Nafsi yangu. Amina

TAFAKARI: SIKUKUU YA WATAKATIFU FILIPO NA YAKOBO MITUME


SIKUKUU YA WATAKATIFU FILIPO NA YAKOBO MITUME

MEI 3

Somo: 1Kor 15:1-8

Zab: 19:2-3, 4-5

Injili: Yoh 14:6-14

Nukuu:

ya kuwa Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, kama yanenavyo maandiko,” 1Kor 15:3b

na ya kuwa alizikwa; na ya kuwa alifufuka siku ya tatu, kama yanenavyo maandiko,” 1Kor 15:4

baadaye akamtokea Yakobo; tena na mitume wote,” 1Kor 15:7

Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6

Filipo akamwambia, Bwana, utuonyeshe Baba, yatutosha,” Yoh 14:8

Husadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu? Hayo maneno niwaambiayo mimi siyasemi kwa shauri langu; lakini Baba akaaye ndani yangu huzifanya kazi zake,” Yoh 14:10

Mnisadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu; la! Hamsadiki hivyo, sadikini kwa sababu ya kazi zenyewe,” Yoh 14:11

Amin, amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba,” Yoh 14:12

Nanyi mkiomba lo lote kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana,” Yoh 14:13

“Mkiniomba neno lo lote kwa jina langu, nitalifanya,” Yoh 14:14

TAFAKARI: Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu. Nanyi mkiomba lo lote kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana. Naam ninaamini.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Sikukuu ya Watakatifu Pilipo na Yakobo Mitume. Kadiri ya mapokeo ya Kanisa, Mtume Filipo alizaliwa Bethaida na alikuwa mwanafunzi wa kwanza wa Yohana Mbatizaji na baadaye alimfuata Yesu Kristo. Yakobo mwana wa Alfayo, mtumwa wa Mungu, na wa Bwana Yesu Kristo Yak 1:1, alichaguliwa na kuliongoza Kanisa la Yerusalemu. Mtume Yakobo aliandika moja ya waraka wa Kanisa kwa watu wote, “Barua ya Yakobo.” Kama kiongozi wa Kanisa la Yerusalemu, Yakobo Mtume aliishi maisha kamili na ya mateso mengi kwa ajili ya Imani, na kwa tendo hilo aliwaongoa Wayahudi wengi katika Imani na kumfuata Kristo. Alikufa kifo shahidi mwaka 62 baada ya Kristo.

Wapendwa wana wa Mungu, kama ilivyokuwa kwa Paulo Mtume na wengine, msingi wa Imani kwa Wakristo upo kwenye kifo na ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo. Kwa kifo cha Kristo ambacho ni tokeo la dhambi zetu, kimetufanya sote tuhesabiwe haki mbele ya Mungu na kupata mastahili ya kuwa watoto wake Mungu na warithi Ufalme wake, 1Kor 14:13. Hapa ndipo ulipo uhai wetu kwa sababu, “alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona,” Isa 53:5. Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo uliamsha hari mpya na maisha mapya katika ufuasi wake. Huu ni wito wa kila mmoja wetu kuishi maisha mapya na Kristo, yaani, maisha ya ufufuko. Maisha haya ya ufufuko yanatudai kila siku kulenga katika ukamilifu licha ya kwamba udhaifu upo. Kwa maana nyingine, kama mfuasi wa Kristo na kama ilivyokuwa kwa Filipo na Yakobo Mitume, tusijiridhishe hata mara moja katika hali ya udhaifu wetu na kumsaliti Yesu kwa matendo yetu maovu na dhambi.

Maisha haya ya ufufuko na mapya kwa kila mfuasi wa Kristo ni maisha ya ushuhuda kwa yale aliyotufundisha Kristo na kuyaona kila siku ya maisha yetu. Hata hivyo hatuwezi kuwa mashahidi wa ushuhuda wa ufufuko wa Kristo kama hatupo tayari kushirikishana habari njema ya wokovu wetu. Pili, hatutaweza kushirikishana habari hii njema ya wokovu kama hatupo tayari kulitafakari neno lake. Tatu, hatutaweza kulitafakari neno lake kama hatupo tayari kulipokea neno hilo na habari njema hiyo ya wokovu. Na nne, hatutaweza kulipokea neno hili la wokovu kama hatupo tayari kulisika. Hivyo, mwito wa kuwa mashahidi wa ushuhuda wa ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo na habari njema ya wokovu wetu, kwatutaka kufanya haya yafuatayo: Kulisikia neno, kulipokea neno, kulitafakari neno, na kulishirikisha neno. Hivi ndivyo walivyofanya Mitume hawa Filipo na Yakobo, na Mitume wote wa Kristo, na wale wote waliomfuata hasa tunapolitazama Kanisa hili la Mwanzo. Kwa ushuhuda wao, na kifo dini chao kwa kumwaga damu zao kwa ajili ya Mwana-Kondoo wa Mungu, Kanisa limekuwa na msingi Imara na Imani hadi leo.

Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, maisha na ufuasi wako kama Mkristo lazima yaongozwe na malengo hayo niliyoyasema kama kweli wataka kuwa ndani na katika Kristo Yesu. Naye Yesu anakuambia wewe na mimi hivi; “Mnisadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu; la! Hamsadiki hivyo, sadikini kwa sababu ya kazi zenyewe,” Yoh 14:11. Ndugu yangu, hapa ni Imani ya kweli katika Kristo Yesu! Na msingi Imara ni kumwona Kristo pasipo shaka yoyote katika mambo haya matatu anayotuambia, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Maana ya maneno haya ni nini? Ndugu yangu kama nilivyokwisha kusema mahali pengine, si vibaya nikakukumbusha na leo pia. Yesu Kristo ni njia kama ulivyo Mlango pekee wa kuufikia uzima wa milele. Na njia aliyoichagua Yesu ni Msalaba. Kwa kuibeba misalaba yetu na kuchukuliana kindugu katika misalaba ya wenzetu kwa uaminifu na hofu ya Mungu, tunakutana naye Kristo katika hali na mazingira hayo. Yesu Kristo ni kweli halisi. Kweli hii tunakutana nayo katika neno lake hasa pale tunapokuwa tayari kulisikia neno, kulipokea neno, kulitafakari neno, kulishirikisha neno, na mwisho kuwa shahidi wa neno.

Na Yesu Kristo ni uzima halisi. Kristo ni uzima halisi tunaposhiriki Ekaristi Takatifu katika mastahili yake. Yesu anatuambia, “Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe” Yoh 6:35. Ni katika kula chakula hiki-mwili na damu yake,  Yesu anahaidi mambo mawili makuu: Moja, ni ufufuko siku ya mwisho. Naye anasema, Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho,” Yoh 6:54. Na katika kula chakula hiki-mwili na damu yake, Kristo hukaa ndani yetu. Naye anasema, Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake,” Yoh 6:56. Hata hivyo Mtume Paulo anatupa angalizo la chakula hiki cha uzima. Naye anasema, Basi kila aulaye mkate huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili, atakuwa amejipatia hatia ya mwili na damu ya Bwana,” 1Kor 11:27. Yatupasa kuijongea Meza ya Bwana tukiwa na mastahili ya kufanya hivyo-usafi wa mwili na roho, yaani, pasipo hatia yoyote. Zaidi ya hapo ni kuikufuru Meza ya Bwana.

Kwa uelewa huo, Yesu Kristo anamtoa mashaka Filipo pale alipomtaka Yesu awaonyeshe kwa Baba nayo inatosha, Yoh 14:8. Kuthibitisha kwamba Yeye, yaani, Kristo ndiye Njia, Kweli, na Uzima, na ndiyo mlango sahihi wa kumfika Baba, na Ufalme wa mbinguni, anasema, “Amin, amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba,” Yoh 14:12. Ndugu yangu, kwa kumwishi Kristo na kumwamini una kitu cha kupoteza? Maneno haya ya Yesu kwamba yeye ni njia, kweli, na uzima si maneno ya kufikirika bali ndio kweli yenyewe na jibu sahihi alilolitaka Mtume Filipo. Je, bado unamashaka? Kama bado upo kwenye mashaka, Yesu anakuambia,  Nanyi mkiomba lo lote kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana,” Yoh 14:13. Hatupaswi kuwa na mashaka kama kweli twataka kuishi maisha mapya, yaani, maisha ya ufufuko.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Mkiniomba neno lo lote kwa jina langu, nitalifanya,” Yoh 14:14

Tusali:-Ee Yesu na Mkombozi wetu, wewe kwetu watosha. Amina

Watakatifu Filipo na Yakobo, Mtuombee.

 

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 3 YA PASAKA


JUMANNE WIKI YA 3 YA PASAKA

Somo: Mdo 7:51-59

Zab: 31:3cd-4, 6, 7b, 8a, 17, 21ab

Injili: Yoh 6:30-35

Nukuu:

Enyi wenye shingo gumu, msiotahiriwa mioyo wala masikio, siku zote mnampinga Roho Mtakatifu; kama baba zenu walivyofanya, na ninyi ni vivyo hivyo,” Mdo 7:51

“Lakini yeye akijaa Roho Mtakatifu, akakaza macho yake, akitazama mbinguni, akauona utukufu wa Mungu, na Yesu akisimama upande wa mkono wa kuume wa Mungu,” Mdo 7:55

“Akasema, Tazama! Naona mbingu zimefunguka, na Mwana wa Adamu amesimama mkono wa kuume wa Mungu,” Mdo 7:56

Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja,” Mdo 7:57

Wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli,” Mdo 7:58

“Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu,” Mdo 7:59

Wakamwambia, Unafanya ishara gani basi, ili tuione tukakuamini? Unatenda kazi gani?” Yoh 6:30

Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Siye Musa aliyewapa chakula kile cha mbinguni, bali Baba yangu anawapa ninyi chakula cha kweli kitokacho mbinguni,” Yoh 6:32

“Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe,” Yoh 6:35

TAFAKARI: “Kifo Chema ni kuishi katika Kristo na ndani ya Kristo, yeye ndiye chakula cha uzima.”

Wapendwa wana wa Mungu, hakuna shaka kabisa wote tuliozaliwa ipo siku wote tutakufa kila mmoja kwa wakati wake. Kifo kwa Mkristo ni daraja ya kuvuka kwenda upande mwingine wenye mazingira tofauti na haya tuliyonayo: wenye uzima na uhai. Kifo kwa anayemwamini Kristo ni mlango ambao watupitisha kwenye maisha mengine ya umilele. Kifo kina maana ndani na katika Kristo kwa sababu kupitia mateso yake, na kifo chake msalabani, laana ya kifo imefutwa. Kwa Mkristo kwenye imani, kifo si kitu cha kuogopa bali ni tukio la kujiandaa.

Maandalizi ya kifo Chema ni kuishi kweli ya Kristo kila siku. Ni kumshuhudia Kristo kwa yale yaliyomema na anayotuwasa kuyafanya kama watoto wa Mungu. Ni kutokumwonea aibu Kristo mbele za watu hata kama yatupasa kufa kwa ajili ya kweli. Ukweli huu ndiyo anaouishi Shahidi Stefano na kuhushuhudia. Stefano Shahidi anawaaambia Wayahudi, “Enyi wenye shingo gumu, msiotahiriwa mioyo wala masikio, siku zote mnampinga Roho Mtakatifu; kama baba zenu walivyofanya, na ninyi ni vivyo hivyo,” Mdo 7:51. Jambo la kuelewa hapa katika maisha yetu ya Kiroho, hatuwezi kupingana na mpango wa Roho Mtakatifu. Sifa na kazi mojawapo wa Roho Mtakatifu ni kuleta umoja wa kweli na wakimungu kwa wote walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, Mwa 1:26.

Palipo na Roho Mtakatifu kuna umoja wa kweli na hapo Roho Mtakatifu utenda mambo yake kwa wale aliwaridhia. Shihidi Stefano, “akijaa Roho Mtakatifu, akakaza macho yake, akitazama mbinguni, akauona utukufu wa Mungu, na Yesu akisimama upande wa mkono wa kuume wa Mungu,” Mdo 7:55. Stefano Shahidi anapewa hakikisho la kile anachokisimamia na kukishuhudia. Pamoja na ukweli huu, watesi wake “wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja,” Mdo 7:57.

Ndugu yangu, ni mara ngapi katika mazingira yetu tunakutana na hali kama hii na wala hatufanyi chochote? Yawezekana hali isiwe kama ya Shahidi Stefano ya kupondwa mawe. Ila wote ni mashahidi na labda tumeshaona jinsi watoto wadogo wanavyotendwa kwenye usafiri wetu wa daladala. Mzazi ambaye naye anamtoto kama huyo anayeteswa na kunyanyapaliwa na kondakta, asemi wala akemei chochote. Je, tunatofauti gani na waliomrarua Shahidi Stefano? “Wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli,” Mdo 7:58. Sauli, ambaye leo anajulikana sana kama Mtume Paulo, anashiriki katika kosa hili. Mtume Paulo analifanya kosa hili kwa kutetea mila na desturi za mababu zake, ambaye baada ya kuongoka kwake anakuwa mtetezi mashuhuri wa Kristo na mkosoaji wa mila na desturi hizo. Huku ndiko maana halisi ya kuongoka.

Katika kipigo hiki cha kikatili, Stefano anaikabidhi roho yake kwa Mungu, kama Bwana wetu Yesu Kristo alivyofanya. “Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu,” Mdo 7:59. Hata katika hali hii ya kutisha, Stefano Shahidi habadili msimamo wake, wala hakatishwi tamaa kwa kujitoa kwake muhanga. Mungu anabakia kuwa tumaini lake hadi mwisho. Wengi wetu katika hali kama hii na mara nyingine tunapo ugua kwa muda mrefu bila kujua sawasawa sababu ya magonjwa yetu, hukata tamaa na kusaliti Imani yetu na Mungu wetu. Ni mara ngapi tunawaona Wakristo waliokuwa mstari wa mbele wanakwenda kupiga ramli na hata wengine wanakutwa na umauti kwa waganga wa kienyeji?

Mpendwa, haijalishi wewe ni nani ila kuwa Mkristo bila kuwa na imani thabiti ni hatari sana. Ni sawa na mkate usioiva vizuri kwani ni hatari kwa tumbo. Yesu Kristo katika Injili ya leo anawashangaa wale wasio mwamini pamoja na yote anayoyaishi na kuyatenda. Nao wanataka kuona ishara ili wamsadiki kwamba yeye ndiye kweli wanayemtumainia. “Wakamwambia, Unafanya ishara gani basi, ili tuione tukakuamini? Unatenda kazi gani?” Yoh 6:30. Kwa Wayahudi, Musa alikuwa na nafasi ya pekee sana hata kuweza kuvuka uelewa wa Mungu. Kwa mantiki hiyo, yeyote aliyekwenda kinyume na kile alichosema au fanya Musa alionekana kama mhaini hivi. Yesu kabla ya yote anawapa uelewa wa Mungu ni nani na Musa ni nani. “Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Siye Musa aliyewapa chakula kile cha mbinguni, bali Baba yangu anawapa ninyi chakula cha kweli kitokacho mbinguni,” Yoh 6:32. Musa aliweza kuyafanya hayo yote kwa mkono wa Mungu, ila Kristo ni zaidi ya Musa kwani kwake upo uzima. Kiu na mahangaiko yetu yote yanamajibu tunapoishi katika yeye na ndani yake. “Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe,” Yoh 6:35. Je, unamwamini Kristo? Hakuna sababu ya kutafuta ulizi kwa njia ya giza kama tunaye Kristo. Hakuna sababu ya kuzindika majumba yetu na kutembea na mahirizi kama tunaye Kristo.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe,” Yoh 6:35

Tusali:-Ee Yesu wangu, nami nasadiki wewe ndiye chakula na uzima wangu. Amina

 

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 3 YA PASAKA


JUMATATU WIKI YA 3 YA PASAKA

Somo: Mdo 6:8-15

Zab: 119:23-24, 26-27, 29-30

Injili: Yoh 6:22-29

Nukuu:

Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati;  maana tumemsikia akisema kwamba Yesu huyo Mnazareti atapaharibu mahali hapa, na kuzibadili desturi tulizopewa na Musa,” Mdo 6:13-14

“Watu wote walioketi katika ile baraza wakamkazia macho yao, wakamwona uso wake kuwa kama uso wa malaika,” Mdo 6:15

“Yesu akawajibu, akasema, Amin, amin, nawaambieni, Ninyi mnanitafuta, si kwa sababu mliona ishara, bali kwa sababu mlikula ile mikate mkashiba,” Yoh 6:26

“Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele; ambacho Mwana wa Adamu atawapa, kwa sababu huyo ndiye aliyetiwa muhuri na Baba, yaani, Mungu,” Yoh 6:27

“Yesu akajibu, akawaambia, Hii ndiyo kazi ya Mungu, mmwamini yeye aliyetumwa na yeye,” Yoh 6:29

TAFAKARI: “Mwenye haki ataishi Milele, kazi ya Mungu, ni kumwamini Kristo mwana wa Mungu.”

Wapendwa wana wa Mungu, masomo yetu la leo yanatualika kutafakari neno hili, “mwenye haki ataishi Milele, kazi ya Mungu, ni kumwamini Kristo mwana wa Mungu.” Stefano anakuwa shahidi wa kwanza anaposimama katika kweli na kuiishi. Akiwa mtu aliyenena na kuongozwa na Roho Mtakatifu, Shahidi Stefano anajikuta katika mzozo mkubwa na Wayahudi ambao hawakupenda, kusikia, wala kusadiki mambo yote aliyoyafanya Yesu Kristo. Stefano anaundiwa genge na zogo na mwisho kutungiwa uongo ili kumwangamiza. “Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati; maana tumemsikia akisema kwamba Yesu huyo Mnazareti atapaharibu mahali hapa, na kuzibadili desturi tulizopewa na Musa,” Mdo 6:13-14

Stefano shahidi anakuwa mbegu ya kwanza ya Imani kuoteshwa katika jumuiya ya kwanza ya Wakristo. Watu wenye mtazamo wa Stefano katika jumuiya ya Wakristo hata sasa wapo. Unapojaribu kusimama katika kweli, na kuishi kweli hiyo, jiandae kusongwa na mambo mengi. Kwanza utatungiwa majina ya ajabu ili tu ukatishwe tamaa. Utatungiwa uongo mwingi tu, ili uchafuliwe na Kristo achafuliwe. Unapomkiri Kristo katika kweli na haki, unatangaza vita dhidi ya giza. Je, katika hali hii nini cha kufanya? Kamwe usiache kusimama katika kweli na kunena lililo kweli hata ikikubidi kufa. Stefano shahidi hakuacha kulisema lililo kweli na hata kulisimamia. Jibu katika kweli hii linaonekana hata kabla hajakijongea kifo kile cha kupigwa mawe hadi kufa. “Watu wote walioketi katika ile baraza wakamkazia macho yao, wakamwona uso wake kuwa kama uso wa malaika,” Mdo 6:15.

Ndugu yangu, Kristo pekee ndiye mwenye kutuhesabia haki katika vita hivi vya mwanga dhidi ya giza. Ni katika Kristo, na ndani ya Kristo tunaweza kushinda vita hivi kwa sababu yeye kesha vishinda. Je, unamwamini Kristo? Wapo wengi waliokuwa wanamfuata Kristo ila kwa malengo ya hapa na sasa tu, wala siyo imani ya kweli. Wengi walipenda kumfuata Kristo kutokana na miujiza aliyokuwa akiifanya. Hivyo walikuwa watu wa mshangao tu, na matukio. Wengi walimfuata wakijua kwa uwepo wake utawahakikishia shibe. Mtazamo wa Kristo na watu hawa wa shibe, hauna tofauti ma mahusiano ya fisi na Simba. Fisi anamatumaini makuwa kuwa akiwa na Simba hawezi kukosa masalia ya mzoga.

Yesu Kristo analiona hili mapema na kuwakemea wale waliokuwa wanamtafuta na kumwulizia kwa shahuku. “Yesu akawajibu, akasema, Amin, amin, nawaambieni, Ninyi mnanitafuta, si kwa sababu mliona ishara, bali kwa sababu mlikula ile mikate mkashiba,” Yoh 6:26. Swali ni kwamba, je, ukipata mahitaji yako yote ya kila siku, Kristo bado ana nafasi tena katika maisha yako? “Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele; ambacho Mwana wa Adamu atawapa, kwa sababu huyo ndiye aliyetiwa muhuri na Baba, yaani, Mungu,” Yoh 6:27

Wapendwa, tunaye Mtu mmoja tu anayeweza kutufunulia siri za mbinguni na uzima wa milele. Mtu huyu ni Kristo. Kujua siri za ufalme wa mbingini hatunabudi kumjua Kristo na kufuata matafundisho yake. Kristo ndiye mwenye mamlaka yote ya ufalme wa mbinguni. Ndiye aliyetiwa muhuri na Baba. Je, ni nini cha kufanya? Jambo la msingi kupita yote ni kumwamini Kristo. “Yesu akajibu, akawaambia, Hii ndiyo kazi ya Mungu, mmwamini yeye aliyetumwa na yeye,” Yoh 6:29. Ulimengu tunaoishi sasa, baadhi yetu siyo kwamba tu kwamba hawamwamini Kristo, bali hawapendi kusikua habari zake.

Ni jukumu la kila Mbatizwa na hasa wale waliopewa mamlaka hayo kutoa katekesi ya kina kuhusu uhusiano nadharia kati ya maisha ya kila siku ya Mkristo na kile anachoamini. Mara nyingi, wanachohubiriwa watu hakigusi maisha yao. Kristo anabaki kuwa ni ukweli fulani unaoelea katika urefu fulani ambao hatuwezi kufika kwa urahisi. Kristo anakuwa si tena yule Emmanuel, yaani Mungu pamoja nasi. Mfanye Kristo kuwa Rafiki yako wa karibu, na anza kumuishi kuanzia hapo ulipo na hao wakuzungukao. Kulifanya jambo hili kwa ukweli na kumwamini Kristo, ni kielelezo tosha cha uinjilishaji wako mpya hapo ulipo. Leo tunaitaji sana ushuhuda huu wa ukimya.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele; ambacho Mwana wa Adamu atawapa, kwa sababu huyo ndiye aliyetiwa muhuri na Baba, yaani, Mungu,” Yoh 6:27

Tusali:-Ee Yesu Kristo, tujalie neema ya kuijua kweli yako na kuishi kweli hiyo katika maisha yetu ya kila siku. Amina

TAFAKARI: JUMAPILI YA 3 YA PASAKA-A


JUMAPILI YA 3 YA PASAKA-A

Somo I: Mdo 2:14, 22-33

Zab: 16:1-2, 5, 7-8, 9-10, 11

Somo II: 1Pet 1:17-21

Injili: Lk 24:13-35

Nukuu:

“Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake,” Mdo 2:32

“Kisha Yesu akawaambia, Msiogope; enendeni, mkawaambie ndugu zangu waende Galilaya, ndiko watakakoniona,” Mt 28:10

“Na ikiwa mnamwita Baba, yeye ahukumuye kila mtu pasipo upendeleo, kwa kadiri ya kazi yake, enendeni kwa hofu katika wakati wenu wa kukaa hapa kama wageni,” 1Pet 1:17

Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo,” 1Pet 1:18-19

Ikawa katika kuzungumza na kuulizana kwao, Yesu mwenyewe alikaribia, akaandamana nao,” Lk 24:15.

“Macho yao yakafumbwa wasimtambue,” Lk 24:16.

“Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote; tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha. Nasi tulikuwa tukitumaini ya kuwa yeye ndiye atakayewakomboa Israeli,” Lk 24:19-21.

“Akawaambia, Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake?” Lk 24:25-26.

Wakamshawishi wakisema, Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha,” Lk 24:29.

TAFAKARI: “Kaa pamoja nasi Bwana.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya tatu ya Pasaka ya Mwaka “A” wa Kanisa. Masomo yetu ya leo yanatutafakarisha namna ya kukaa na Bwana wetu Yesu Kristo. Huu ni mkao wa Kipasaka. Ni mkao wa ufufuko. Ni mkao wa kuyatafuta yale ya juu Kristo aliko, Kol 3:1.

Wapendwa wana wa Mungu, moja ya kweli kwamba Kristo amefufuka na yu hai, ni ujasiri wa jumuiya ya kwanza ya Wakristo kuishi kwa matendo na kumuhubiri Kristo mfufuka bila shaka na wasiwasi wowote. Jumuiya hii ya kwanza wapo tayari kwa lolote limuhusuyo Kristo Mfufuka. “Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake,” Mdo 2:32. Ushupavu huu ni kutokana na kuguswa na kuishi uhasilia wa Ufufuko wa Kristo. Hapana shaka kwamba Kristo amefufuka na yu hai katika maisha yetu na hali zetu kila siku.

Injili yetu ya leo inatupa umuhimu wa kukaa muda wote na Kristo Mfufuka. Maisha yetu yanapita kwa kasi sana kama moshi, na wakati mwingine tunaishi tukiwa wakavu sana kiroho. Yesu Kristo kwa walio wengi ni Yesu wa Historia. Kwa walio wengi Yesu huyu hana nguvu tena. Tatizo kubwa tunalokutana nalo katika maisha ni kuyaweka matamanio yetu mbele zaidi ya mafundisho na kweli anayotufundisha Kristo. Sintofahamu hii inawakuta wanafunzi wale ambao wanaona Kifo cha Kristo kama tukio la kudanganywa hivi, na hakuna maana kabisa kwa yule ambaye walimtegemea sana na leo anawaangusha. Kifo hiki cha aibu cha msalaba kwa wanafunzi hawa kimewatoa matumaini yote.

Yesu Kristo hata katika sintofahamu hizi, bado yupo tayari kutusikiliza na kuzidi kutufundisha, licha ya kwamba hatumuoni kwa kuificha taswira yake, ili mradi tu tumpe nafasi. “Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote; tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha. Nasi tulikuwa tukitumaini ya kuwa yeye ndiye atakayewakomboa Israeli,” Lk 24:19-21.

Yesu hachoki kutukumbusha yaliyompasa kufanya na yaliyotabiriwa juu yake. Haya yote yapo katika Maandiko Matakatifu. Mt. Jerome anasema hivi kuhusu Yesu Kristo, “tunapokuwa wajinga wa maandiko matakatifu, ni kwa namna hiyo hiyo tu wajinga kuhusu Yesu Kristo.” Kuhusu jambo hili Yesu anatupa sababu ya yale yote yaliyojiri kuhusu Kifo na Ufufuko wake. “Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake?” Lk 24:25-26. Ndugu yangu hapa tunakumbushwa pia, kwamba hakuna Utukufu pasipo Msalaba. Penye Msalaba pana Utukufu, na sasa ni rahisi kuupata Utukufu kwa sababa Kristo kesha ushinda Msalaba.

Wapendwa, Kristo anajifunua kwetu leo katika kuumega mkate. “Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa. Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao,” Lk 24:30-31. Kuumega mkate kunatanguliwa na kulishwa neno lake na kulielewa. Tukio la wanafunzi wa Yesu kukutana naye njiani kuelekea Kijiji cha Emau, ni mtiririko mzima wa adhimisho la Misa Takatifu. Adhimisho hili lina sehemu kuu mbili; Liturjia ya neno na liturjia ya Ekaristi Takatifu. Kwa mantiki hii, uwezekano wa Kristo kujifunua kwetu wakati wa Ekaristi Takatifu, unabebwa kwanza na ufahamu wetu wa kulisikiliza neno lake, kulipokea, kulitafakari, kulishirikisha, na kuliishi. Wanafunzi hawa wa Yesu wanakuwa na hamu ya kukaa naye zaidi baada ya kulishwa neno na Kristo ingawa hawakumfahamu.

Ndugu zangu, wale ambao wamezoea kuchelewa na mara nyingine kushiriki tu liturjia ya Ekaristi Takatifu, ni wavamizi wa Mlo Mtakatifu wasioujua vizuri. Ni sawa na kukishambulia chakula kitamu na kizuri wakati ukiwa na mikono michafu. Ni vizuri kuhudhuria sehemu zote mbili za kiliturjia na ndivyo inavyotakiwa kwa Mkristo na hasa kwetu, ambao Ekaristi Takatifu kicho kiini cha yote. Wapo kati yetu ambao huingia Kanisani na moja kwa moja kujongea Meza ya Bwana. Huu ni uhuni wa hali ya juu kufanywa na Mkristo. Mwisho na muhimu tusichoke kuudhuria mara kwa mara maadhimisho ya Maabudu ya Yesu wa Ekaristi-Sakramenti Kuu. Hapa anakaa kwetu na kujifunua kwetu.

Kukaa na Kristu kunatuwajibisha kubadili mitazamo yetu ikiwa ni pamoja na kuyaacha mazoea yetu yasiyokuwa na mwelekeo. Kukaa na Kristo ni kuishi maisha yanayoongozwa na malengo. Jambo hili si rahisi sana kwa sababu linakufanya uishi maisha ya kisadaka. Na sadaka nzuri na yenye kumpendeza Mungu ni ili inayouma. Ni sadaka ili inayasema zaidi kile ulicho, na ukitoe chote bila kujibakiza. Hili ndilo fumbo zima la Msalaba.

Pamoja na ugumu huo, Yesu anatutaka tutofautishe namna yetu ya kutenda na kuishi ili tulenge fumbo lile la kifo chake cha Msalaba ambapo ndipo ulipotundikwa wokovu wetu na kumpatia Kristo Utukufu wake, nasi kuhesabiwa haki ya kuwa wana wa Mungu bila ya mastahili yetu binafsi. Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo,” 1Pet 1:18-19.

Damu hii yenye thamani kubwa iwe chachu na kielelezo cha imani yetu na kumwamini Mungu. Ni kwa Damu hii ya Mwana-kondoo huyu aliye na hila, Yesu Kristo, “ambao kwa yeye mmekuwa wenye kumwamini Mungu, aliyemfufua katika wafu akampa utukufu; hata imani yenu na tumaini lenu liwe kwa Mungu,” 1Pet 1:21. Hivyo tenda na ishi yetu isukumwe kwa kuthamini kukombolewa kwetu huku kuliko kwa thamani kubwa ajabu.

Kristo Yesu hali akijua hulka yetu wanadamu anatukumbusha kuepuka kutawala wengine kwa mabavu kama asemavyo, “Mwajua ya kuwa wale wanaohesabiwa kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha,” Mk 10:42. Kristo hataki hilo litokee kwa Mitume na wafuasi wake. Kinyume chake tutangulize mbele ‘kutumika vyema’ na siyo ‘kutumikiwa wala kuogopwa.’ “Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Mk 10:45. Maana yake nini?

Wapendwa wana wa Mungu, Kristo anatutaka tuelewa kuwa utumishi ni kujitoa kwa watu kwa upendo na kuwapenda. Huwezi kuwatumikia watu vizuri kama huwapendi. Na ukifanya hivyo (kuwatumikia ukiwa huwapendi) basi nyuma yake kuna ubinafsi mkubwa na kujitazama wewe tu, familia yako, ndugu zako, marafiki zako, na mwisho kupoteza dhima nzima ya kutumika na umma. Hapa tunahitaji nidhamu ya hali ya juu na yenye kusukumwa na utii wa kweli. Hivyo, “Mkiisha kujitakasa roho zenu kwa kuitii kweli, hata kuufikilia upendano wa ndugu usio na unafiki, basi jitahidini kupendana kwa moyo,” 1Pet 1:22. Kupendana kwa moyo ni kumwona Kristo Yesu kwa wote unaotumika kwao. Hapa ndipo kule kutoa nafsi yako iwe fidia ya wengi, Mk 10:45b.

Pili, kuwa tayari kutumika kunatutaka kusahu uzamani wetu na mazoea yetu. Ni kuzaliwa mara ya pili kwa kuliishi neno la Mungu lenye uzima. Kuliishi neno la Mungu lenye uzima kwanza kabisa ni kuwa tayari kuhusu neno hilo. Pili, ni kuwa na uwezo wa kusikia neno, kulipokea neno, kulitafakari neno, kulishirikisha neno, na kuwa shahidi wa neno hilo likiakisi maisha yako. Kwa kuwa mmezaliwa mara ya pili; si kwa mbegu iharibikayo, bali kwa ile isiyoharibika; kwa neno la Mungu lenye uzima, lidumulo hata milele,” 1Pet 1:23. Ndugu yangu, neno hili tunahubiriwa kila siku. Lifanye kuwa sehemu ya maisha yako kwa sababu, Neno la Bwana hudumu hata milele. Na neno hilo ni neno lile jema lililohubiriwa kwenu,” 1Pet 1:25.

Tatu, kuwa tayari kutumika ni kuukubali utumishi kwanza ambao mwisho wa siku ndio utakao sadifu ukubwa ule kama kweli ndio unaoutamani. Hivyo, “bali mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu,” Mk 10:43b. Pili, kuikubali hali ya utumwa kwa ajili ya wote. Hali hii ya utumwa ndiyo itakayotuweka kuwa wa kwanza au wa mwisho. Hivyo, “na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote,” Mk 10:44.

Ndugu yangu, huu ndio utumishi na kutumika kwa yeyote yule mwenye hofu ya Mungu. Na kama upo tayari kutumika na unamatamanio haya, omba hivyo  ukifahamu wajibu wa kile ukiombacho. La sivyo hutotumika vyema na mwisho wa siku ni kupoteza vyote: Utakatifu wako, na uzima ule wa milele.

Mama Vituka aliye na Kilabu cha pombe ya kienyeji kwa jina la ‘Kilimani’ ni marufu sana kijijini Mtakuja. Jumapili iliyopita kwa jambo la kushangaza hakupata na wateja wa pombe yake ya kienje hadi ilipofika saa kumi na mbili jioni alipoinga mlevi mmoja maarufu kijijini hapa ajulikanaye kwa jina la Matumaini.

Matumaini alipofika kwenye Kilabu kile, Mama vituka alimpatia bohora la pombe la ulanzi. Matumaini alilifyonza kwa hisia kali huku akiimba wimbo wa mwanamzika Bob Marley, “Afrika Unity” akiwa akidesadesa.

Basi wapita njia walipomwoma Bwana Matumaini akikwa na bohora la ulazi huku akiimba kwa hisia wimbo ule, nao walijongea kwani ilipata kiashirio kwamba sehemu ile pombe ipo.

Baada ya nusu saa Kilabu kile kilijaa watu na pombe iliuzika haswa. Kwa kelele za Bwana Matumaini, Mama Vituka aliamua kumtimua nje ili wateja wake wapate utulivu. Kwa kitendo kile watu wote walisimama na kusema kwa ukali, “asingekuwa Bwana huyu, tusingelijua hapa kama kuna kinywaji hiki. Tunaomba usimbughuzi. Mpe pombe sisi tutamlipia.”

Ndugu zangu, wakati mwingine yawezekana mambo yakakuendea vizuri sana, ila usibweteke. Yawezekana kuna akina Bwana Matumaini wengi sana wamekufanya uwe kama ulivyo.

Hivyo, leo Kanisa letu lipo imara kwa sababu Yesu Kristo Mfufuka na aliye hai yupo nasi. Uwepo wa Ekaristi Takatifu waupa uhai Kanisa letu Takatikafu. Wengi miongoni mwetu na wasio jua fumbo hili wanaweza kubeza sana kwa sababu wanaona maumbo haya ya Mkate na Divai kama yalivyo kwa mwono wake wa nje, ila hawajui kile kibebacho fumbo hilo. Amina!

“Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa. Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao,” Lk 24:30-31.

Tusali:- Ee Yesu, kamwe usituache katika sintofahamu zetu. Kaa nasi daima. Amina.