JUMAPILI YA 4 YA
KWARESMA-A
Somo I: 1 Sam 16:1b, 6-7, 10-13a
Zab: 23:1-3a, 3b-4, 5, 6
Somo II: Efe 5:8-14
Injili: Yoh 9:1-41
Nukuu:
“Lakini Bwana akamwambia Samweli,
Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa. Bwana
haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali
Bwana huutazama moyo,”
“Yesu
akajibu, Huyu hakutenda dhambi, wala wazazi wake; bali kazi za Mungu
zidhihirishwe ndani yake,” Yoh 9:3
“Muda
nilipo ulimwenguni, mimi ni nuru ya ulimwengu,” Yoh 9:5
“Alipokwisha
kusema hayo, alitema mate chini, akafanya tope kwa yale mate. Akampaka kipofu
tope za macho,” Yoh 9:6
“Basi
yule mtu akajibu, Kwamba yeye ni mwenye dhambi sijui. Najua neno moja, kuwa
mimi nalikuwa kipofu na sasa naona,”Yoh 9:25
“Yesu
akasikia kwamba wamemtoa nje; naye alipomwona alisema, Wewe wamwamini Mwana wa
Mungu?” Yoh 9:35
“Akasema,
Naamini, Bwana. Akamsujudia,” Yoh 9:38
“Yesu
akasema, Mimi nimekuja ulimwenguni humu kwa hukumu, ili wao wasioona waone, nao
wanaoona wawe vipofu,” Yoh 9:39
“Yesu akawaambia, Kama mngekuwa vipofu,
msingekuwa na dhambi; lakini sasa mwasema, Twaona; basi dhambi yenu inakaa,”
Yoh 9:41
“Enendeni
kama watoto wa nuru,” Efe 5:8c
“kwa
kuwa tunda la nuru ni katika wema wote na haki na kweli,” Efe 5:9
“Lakini
yote yaliyokemewa hudhihirishwa na nuru maana kila kilichodhihirika ni nuru,”
Efe 5:13
TAFAKARI:
“Enendeni kama watoto wa nuru,” Efe 5:8c
Wapendwa
wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya nne ya Kwaresma ya mwaka “A” wa
Kanisa. Mwaliko wa Dominika ya leo watutaka sote tuenende katika nuru na kama
watoto wa nuru. Nuru ni alama na uwepo wa Mungu kati yetu, na kwa namna hiyo
hiyo ni vita dhidi ya giza, yaani, uovu. Hivyo kuenenda katika nuru ni kuvipiga
vita vya giza, yaani, aina zote zile za uovu.
Katika
kweli hii, vita dhidi ya uovu vinaushindi katika mpango mathubuti wa Mungu
kupitia watu wake aliowachagua na kupendezwa nao. Kunapotokea udhaifu katika
vita hivi, Mungu umwinua mwingine katika kundi shindwa lile na kufanikisha
hadhma yake.
Ni katika mantiki hiyo
kwamba, baada ya Sauli kukosa sifa mbele za macho ya Mungu, Mungu anafanya
zaidi kwa manufaa ya watu wake. Hivyo Mungu anawachagulia tena Mfalme wana wa
Israeli. Samweli mtumishi wa Mungu anapewa maelekezo na Mungu na anafanya
kadiri ya maelekezo hayo. Yese alikuwa na wana wazuri na wenye uwezo. Pamoja na
hayo yote, Mungu anamchagua yule amtakaye kwa makusudi yake na watu wake.
Baada ya kukosekana
yule amtakaye Mungu, Samweli mtumishi mwaminifu
wa Mungu anamuuliza Yese, “Watoto wako wote wapo hapa? Naye akasema,
Amesalia mdogo wao, na tazama, anawachunga kondoo. Basi Samweli akamwambia
Yese, Tuma watu, wamlete; kwa sababu hatutaketi hata atakapokuja huku,” 1Sam
16:11.
Mtazamo wa leo na
msukumo wa kijamii na kisiasa ni vigumu sana kusikia sauti ya Mungu ndani ya
mioyo yetu. Tunaishi sana katika ushabiki na wakati mwingine tunaingiwa upofu
na kutokuona vitu sawasawa. Leo si jambo la ajabu kuona mtu asiyependwa na watu
ndiye anayetangazwa kuwa mshindi na aliyechakuliwa na watu kwa kishindo.
Demokrasia (iliyovikwa kama koti la dharura) kwa nchi zenye mfumo wa kimla ni
kwamba wengi usema ila baadhi na wacheche sana ndio wanaoamua. Udhalimu huu
hauna nafasi mbele ya Mungu. Kilicho cheupe
na kiwe cheupe na kilicho giza na kitambulike kuwa giza. Kwa nini tunatanguliza
nafsi zetu mbele zaidi ya kile atakacho Mungu kupitia watu wake?
Mungu wetu hatazami kama sisi
tutazamavyo katika hulka na ushabiki wetu. Mungu hufanya kadiri ya ukamilifu
wake. Nasi kama wanadamu tunaalikwa kila siku kuwa wakamilifu kama Yeye Mungu
alivyo. “Basi ninyi mtakuwa
wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mk 5:48. Ni vyema
ufahamu uwepo wako hapa duniani. Ndugu yangu unanye safiri nami katika tafakari
hii elewa kwamba upo hapa nduniani kupigana kufa na kupona juu ya cheo chako
ambacho ni utakatifu wako. Mengine yote na fahari zake ni mbwembe tu. Huwezi
kumwona Mungu kama si mtakatifu. Je, unajua hilo? Msema kweli ni mpenzi wa
Mungu hakumaanishi “mbainisho wa hiki kizuri na hiki kibaya, bali kusimama
katika kweli na haki pale ulipo, ukitambua dhamana uliyopewa na umma wa watu.”
Bila hili kufanyika hayo yote utakayoyaainisha hubaki kuwa mbwembwe tu kama
ulivyo upepo wa kisulisuli.
Hivyo,
Daudi anapata sifa mbele za Mungu ingawa hakuwa matarajio ya familia ya Yese. “Lakini
Bwana akamwambia Samweli, Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa
maana mimi nimemkataa. Bwana haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana
wanadamu huitazama sura ya nje, bali Bwana huutazama moyo,” 1Sam 16:7. Mungu
utazama moyo ule unaomwelekea na kufanya mapenzi yake. Na katika jambo hili,
kutenda lililo jema hakuwezi kugubikwa na mila na desturi zetu, bali katika
kweli na haki.
Injili
ya leo inachanganua taswira tatu katika vita hivi vya mwanga dhidi ya uovu.
Moja; -Kristo Yesu ndiye mwanga halisi, Yoh 1:9, na kielelezo halisi cha
upendo, huruma, kweli, na haki ya Mungu, Yoh 13:1. Na kwa kinywa chake Yesu
anasema, “Muda nilipo ulimwenguni, mimi ni nuru ya ulimwengu,” Yoh 9:5.
Pili;
-ni taswira ya wakumbatia uovu kulikotokana na kufa kwa dhamiri zao. Kwa
nyakati zile za Yesu kundi hili lilibeba Mafarisayo, Waandishi, Masadukayo, na
wale wote kwa namna moja au nyingine waliupinga mwanga ambao ndiye Kristo
mwenyewe. Na leo kama ilivyokuwa nyakati zile za Yesu, watu hawa ni wale wote wanaojihesabia
haki pasipo haki na kweli yenyewe. Ni wale wote wasiona upendo na huruma ya
Mungu, na kutaka kuwa wasemaji wa Mungu kwa kujihesabia urafiki na Mungu. Ni
wale wenye uhakika pasipo uhakika kwani hata wao wenyewe hawajijui sawasawa. Na
hivi ndivyo wanavyojiinua, na kusema, “Twajua ya kuwa Mungu hawasikii wenye
dhambi; bali mtu akiwa ni mcha Mungu, na kuyafanya mapenzi yake, humsikia
huyo,” Yoh 9:31. Je, mwenye dhambi hana sura na mfano wake Mungu? Na kwa maana
hiyo Mungu hana upendo na huruma tena kwa huyu aliyedondoka katika tope la
dhambi? Ndugu yangu, Mungu mwenyewe anakuambia wewe na mimi tulio wadhambi
kwamba, “Haya, njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu
sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa
kama sufu,” Isa 1:18.
Tatu;
-ni taswira ya uovu wenyewe ikiwa ndilo giza lenyewe. Katika Injili ya leo
Ndugu yetu kipofu ndiyo giza lenyewe ambalo Kristo aliye Mwanga analiondoa
ingawa wakumbatia uovu hawapenda tendo hilo. Na sababu kubwa ya kutokupenda ni
kwamba kile kilicho katika giza hufurahia kuwa katika hali hiyo hiyo isiyo
kinzani. Ila kwa Mungu hali hii siyo ya kawaida na isiyovumilika. Naye Yesu
anasema, “Mimi nimekuja ulimwenguni humu kwa hukumu, ili wao wasioona waone,
nao wanaoona wawe vipofu,” Yoh 9:39. ‘Wanaoona wawe vipofu’ kwa maanisha wale
wote wanaojiaminisha kuwa wanajua ilhali hawajui hubaki katika hali hiyo hiyo.
Ni ulemavu katika ufahamu.
Maneno
haya ya Yesu ‘Wanaoona wawe vipofu’ yanamtofautisha mtu ‘mjinga’ na ‘mpumbavu.’
Mjinga hujifunza kutoka katika hali yake ya kutokujua na kufika katika
hali/hatua ya kujua asichokijua. Mpumbavu hana muda wa kujifunza kwa sababu
anajiaminisha katika upumbavu wake kwamba anajua ilhali hajui chochote. Na hili
ndilo jibu la Yesu kwa Mafarisayo waliotaka kujua kama na wao ni vipofu, Yoh
9:40. “Yesu akawaambia, Kama mngekuwa vipofu, msingekuwa na dhambi; lakini sasa
mwasema, Twaona; basi dhambi yenu inakaa,” Yoh 9:41. ‘Kama mngekuwa vipofu
msingkuwa na dhambi,’ kwa maneno mengine Yesu anawakumbusha kwamba, ‘kama
mngekubali ujinga wenu wa kutokujua isingelikuwa kosa kwa sababu mngeukubali
mwanga/kweli nanyi mngekuwa huru, Yoh 8:32.
Tukija
kwenye taswira ya tatu, yaani, giza lenyewe ambalo katika Injili ya leo linawakilishwa
na Ndugu yetu mwenye upofu halisi, Yesu anaweka wazi uhalisia wa tatizo lenyewe
na kusema, “Huyu hakutenda dhambi, wala wazazi wake; bali kazi za Mungu
zidhihirishwe ndani yake,” Yoh 9:3. ‘Kazi za Mungu zidhihirishwe ndani yake’
kwa maanisha kwa upande mmoja hakuna lisilowezekana kwa Mungu hata kama kwa
upeo na uwezo wetu wanadamu jambo hilo lishafika mwisho wake. Na kwa upande
mwingine maneno haya ya Yesu yalibeba ujumbe mzito kwa kile alicho Kristo
mwenyewe (Asili, Nguvu, na Mamlaka), yaani, Njia, kweli, na uzima, Yoh 14:6.
Ndani na katika Kristo Yesu yote hayo matatu (Njia, Kweli, na Uzima) yawezekana
pasipo shaka yo yote. Na hivi ndivyo ilivyokuwa kwa ndugu yetu yule Kipofu:
“Alipokwisha kusema hayo, alitema mate chini, akafanya tope kwa yale mate.
Akampaka kipofu tope za macho,” Yoh 9:6, naye akapata kuona.
Pamoja
na kuzongwa sana na kundi lile la wakumbatia uovu na vipofu wa kujinadi kama
alivyo wathibitisha Yesu mwenyewe kuwa ni vipofu wanaoona, Ndugu yetu aliyepata
kuona anatoa ushuhuda juu ya Kristo Yesu na kusema, “Kwamba yeye ni mwenye
dhambi sijui. Najua neno moja, kuwa mimi nalikuwa kipofu na sasa naona,”Yoh
9:25. Huu ni ujumbe mzito sana kwa Mafarisayo na kwa wakati mwingine wewe na
mimi tunaishi hali hii ya kifarisayo kwa nyakati tofauti tofauti. Je, tunaona
sawasawa? Ndugu yetu aliyekuwa kipofu katika uhasili wake sasa anaona. Je,
ndugu yangu unaona sawasawa? Yesu aliposikia wanamsonga sana kwa sababu la kile
alichomtendea, alitaka kujua msimamo wa Ndugu yetu aliyeponywa kama kweli
anaamini tendo lile. Yesu akamuuliza, “Wewe wamwamini Mwana wa Mungu?” Yoh
9:35. Naye akamjibu, “Naamini, Bwana. Akamsujudia,” Yoh 9:38. ‘Bwana
akamsujudia,’ ni tendo la heshima kubwa sana mtu kupewa na hasa kutoka kwa
Kristo mwenyewe.
Ndugu
yangu, unaposimama katika kweli na haki ni tendo la furaha kubwa sana kwa Mungu
ingawa katika ulimwengu wa giza yakupasa kulipa gharama yake. Tendo hili ni
kuishi kweli ile na chapa ile ya Mungu ndani yako, Mwa 1:27. Ni kuwa kielelezo
halisi cha upendo na furaha ya Mungu kama kiumbe chake. Chapa hii ya Mungu na
uhasili wake ndani yetu tunaipoteza au kuififisha kwa kutenda dhambi.
Wito
kwako na kwangu leo ni kwamba, ili tuwe salama mwili na roho yatupasa kuenenda
“kama watoto wa nuru,” Efe 5:8c. Hapa ndipo tunadhihirisha kweli tu wanafunzi
wa Kristo katika kweli na haki. Tuepuka bla bla nyingi zenye kumpamba Mungu kwa
uzuri wa maneno yetu majukwani ili hali twatembea na upofu ulio tukuka kimwili
na kiroho. Ndugu yangu tuliye safiri wote katika tafakari hii, “…tunda la nuru
ni katika wema wote na haki na kweli,” Efe 5:9. Kwa kuwa “…yote yaliyokemewa
hudhihirishwa na nuru maana kila kilichodhihirika ni nuru,” Efe 5:13. Kristo
Yesu ndiye Nuru yetu halisi, na kielelezo halisi cha hofu ya Mungu ndani mwetu.
Tumwogope Mungu kwa kusimama katika kweli na haki.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Yesu
akawaambia, Kama mngekuwa vipofu, msingekuwa na dhambi; lakini sasa mwasema,
Twaona; basi dhambi yenu inakaa,” Yoh 9:41
Tusali:-Ee Yesu,
tuondolee upofu wetu kama tunda la upumbavu wetu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario