domingo, 5 de marzo de 2017

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 1 YA KWARESMA


JUMANNE WIKI YA 1 YA KWARESMA

Somo: Isa 55: 10-11

Zab: 34:4-5, 6-7, 16-17, 18-19

Injili: Mt 6:7-15

Nukuu:

ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma, Isa 55:11

Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi,” Mt 6:7 

Basi msifanane na hao; maana Baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba,” Mt 6:8

“Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi,” Mt 6:14

“Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu,” Mt 6:15: 

TAFAKARI: "Basi msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu."

Wapendwa wana wa Mungu, masomo yetu ya leo yanatualika kutambua wema wa Mungu na nguvu ya msamaha hasa kwa somo letu la Injili. Somo la kwanza, nabii Isaya anatupa wema wa Mungu katika mfano wa mvua. Mvua inyeshapo katika ardhi, vyote vyenye uwezo wa kumea humea bila upendeleo. Iwe michongoma, matunda, maua rozi nk. Wema wa Mungu haubagui walio wema na wabaya. Na “ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma, Isa 55:11. Kila dakika ya uhai wetu Mungu anatupa nafasi ya kuwa wema kama Yeye. Tunapopoteza nafasi hiyo kwa kubeba magunia ya chuki, visasi, lawama, wivu, majungu na kutowatakia mema wengine, ndipo tunapopoteza uhai wa Mungu ndani yetu.

Ni kweli usiotia shaka kwamba wengi wetu tushakufa kiroho licha ya kwamba bado tunatembea. Wema wa Mungu kwetu ni mwelekeo wa kuyaona yote katika Yeye. Ndugu yangu, achia gunia hilo na uwe uru mwili na roho. Kwa nini unawabeba wengine katika roho yako na Mungu kukosa nafasi?

Injili ya leo Yesu anatufundisha namna ya kusali. Anatoa angalizo katika sala. Sala ya kweli na yenye utulivu ni kule kusali bila kupayuka. Ni sala ya kumsikiliza “mtu wa ndani.” Ni kujisikiliza na kusikiliza matakwa ya Mungu. Ni utulivu wa ndani ambapo katika utulivu huo tunakutana na Mungu. Hivyo kuabudu kuliko kwa kweli ni kuabudu katika usahihi, uhalisi, tafakuri, na matendo hai. Kama haya mambo hayafanyiki, kuabudu kwetu huwa kwa kupayuka payuka. “Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi. Basi msifanane na hao; maana Baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba,” Mt 6:7-8

Sala hii ya Baba yetu ni ufupisho wa yale yote tunayotakiwa kufanya kila dakika tunapopumua. Mahitaji yetu, utulivu wetu, matakwa yetu, uhusiano wetu na wengine, mahangaiko na vishawishi vyetu vyote hupata majibu katika sala hii. Je, tunatafakari hayo tusalipo sala hii ya baba yetu? Mfano swala la MSAMAHA. Kusamehe ni amri na sio ombi. Yatupasa Kusamehe na hiki kicho kipimo cha sisi kusamehewa. “Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi,” Mt 6:14. Ndugu yangu, kusamehe siyo kusahau uliotendewa. Ukweli ni kwamba hatuwezi kufuta aliyofanyiwa Yesu na kufa kifo kile cha aibu msalabani. Ila tunasema msalaba ni ushindi tunapotazama Utukufu wa Msalaba. ‘Huu ndio ule uti wa msalaba, ambao wokovu wa dunia umetundikwa uu yake.’ Maneno haya ya ushindi na matumaini husemwa siku ile ya Ijumaa Kuu unapofunuliwa msalaba uliofunikwa.

Unapomsamehe mtu mbele yako upo Utukufu. Tunapokumbuka uchungu tuliofanyiwa tunapata faraja kwani katika hilo tumeshinda kwa kusamehe. Ni faraja ya kweli na matumaini mapya. Tusibaki kwenye uchungu wa mateso ila tukumbatie Utukufu ule wa milele. Hili ndilo fumbo la kusamehe na Utukufu unaopatikana katika tendo hilo. “Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu,” Mt 6:15. Na kwa kufanya hivyo ndugu yangu, yaani, kutokusamehe kwako hakuna Utukufu wala Mbingu-Uzima wa milele.

Mpendwa embu tulia na fikiri uliyembeba kwa muda mrefu bila kumsamehe. Leo au kesho tafuta njia ya kumsamehe. Ni vizuri akijua pia umemsamehe. Kwa tendo hilo unaleta pia uponyaji kwako na kwake. Na fanya hivyo kwa upendo na uhuru. Wakati ndio sasa!

Tumsifu Yesu Kristo!

Kwa maana Wewe, Bwana, U mwema, Umekuwa tayari kusamehe, Na mwingi wa fadhili, Kwa watu wote wakuitao,” Zab 86:5

Tusali:-Ee Yesu Mwema, uliyeteseka na kufa kifo cha aibu kwa ajili yangu, yaponye maumivu yangu yote ya ndani, na nijalie neema ya kusamehe yote pasipo kipimo. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario