viernes, 3 de marzo de 2017

TAFAKARI: JUMAPILI YA 1 YA KWARESMA MWAKA-A


JUMAPILI YA 1 YA KWARESMA-A

Somo I: Mwa 2:7-9; 3:1-7

Zab: 51:3-4, 5-6a, 12-13, 14, 17

Somo II: Rum 5:12-19

Injili: Mt 4:1-11

Nukuu

“Bwana Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” Mwa. 2:7

“kwa maana ikiwa kwa kukosa kwake yule mmoja wengi walikufa, zaidi sana neema ya Mungu, na kipawa kilicho katika neema yake mwanadamu mmoja Yesu Kristo kimezidi kwa ajili ya wale wengi,” Rum 5:15b

“Kisha Yesu alipandishwa na Roho nyikani, ili ajaribiwe na Ibilisi,” Mt 4:1

“Kisha Ibilisi akamwacha; na tazama, wakaja malaika wakamtumikia,” Mt 4:11

TAFAKARI: “Kisha Ibilisi akamwacha; na tazama, wakaja malaika wakamtumikia.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya kwanza ya Kwaresma mwaka “A.” Masomo yetu yote matatu yanatualika tusimame katika Imani ya kweli, na hasa katika matendo. Pili, yatupasa kuwa imara hata baada ya kuyashinda majaribu katika vita hivi vya Imani, kwa sababu yule mwovu shetani kushindwa kwake siyo mwisho wake wa kutujaribu. “Kisha Ibilisi akamwacha; na tazama, wakaja malaika wakamtumikia,” Mt 4:11. Ibilisi kumwacha Yesu haikumaanisha ndiyo mwisho wa jaribu, (Rejea Lk 4:13). Tatu, Huruma na upendo wa Mungu kwetu ni waajabu.

Wapendwa katika Kristo, Mungu ni Upendo na kwake yote huyafanya kwa sababu ya upendo. Wazazi wetu wa mwanzo wanapewa upendeleo ukiambana na utaratibu wa kuishi kwenye hii bustani. Bustani ina mambo makuu matatu; a) Aina zote za miti ya matunda, b) Matunda ya mti wa uzima, na c) Matunda ya mti wa  ujuzi wa wema na mabaya.

Pamoja na kupewa ruksa ya kula matunda yote, waliwe pia angalizo la kutokula matunda ya mti wa ujuzi wa wema na mabaya, Mwa 2:17. Tendo la kwenda kinyume na agizo hili ni KIFO. Cha kujifunza leo ni kwamba tangu mwanza kifo hakikuwa katika mpango wa Mungu. Mungu anatutakia uzima wa milele.

Madhara ya kutokufuata maangalizo na utaratibu fulani iwe ni kazi au aina yeyote ya stadi za maisha yapo mengi. Tazama milipuko ya magonjwa mengi sugu na yasiyoponyeka! Yote yametokana na kutumia utashi wetu vibaya. Mara nyingi binadamu twapenda kujua kwa bidii sana kile kilicho jificha nyuma ya "pazia." Je, haitoshi kuyajua haya yaliyomahitaji yetu na yale tu yenye uzima ndani yake? Ni vizuri tukatumia udadisi wetu kumjua Mungu, kuboresha maisha yetu kuelekea utakatifu, na kuifanya dunia hii kuwa sehemu nzuri zaidi ya kuishi licha ya kwamba ni sehemu ya kujiandaa kwa maisha ya umilele.

Ndugu yangu tunaye safiri sote katika tafakari hii, ni vyema tukazama ndani kidogo kwenye fumbo hili la mtu kama alivyo, ili tuweze kujua ujumbe wa Injili ya leo. Mtu kamili anakuwa katika sehemu kuu tatu:-Nafsi, Roho, na Mwili. “Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi Nafsi zenu na Roho zenu na Miili yenu mhifadhiwe mwe kamili, bila lawama, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo.” I The 5:23

Katika hili Roho na Nafsi huwa pamoja na ndizo wewe mwenyewe. Mwili ni nyumba ya roho na nafsi. Katika uumbaji Mungu aliumba mwili kwa udongo halafu akapulizia pumzi puani ambayo ni roho yake ndipo mtu huyo akawa nafsi iliyo hai. “Bwana Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” Mwa. 2:7. Miili tuliyonayo ni nyumba ya Nafsi na Roho. Kwa hali hii sisi binadamu ni wawili. Kuna mtu wa ndani na mtu wa nje. Mtu wa ndani ni Nafsi na Roho, na mtu wa nje ni Mwili lakini watu hawa wapo pamoja hatuwezi kuwatenganisha wala kumwona kwa macho ya nyama huyu mtu wa ndani, ila yupo.

Ndugu yangu, pamoja na malengo mengi tuliyonayo kwa kutafuta fahamu mbalimbali (elimu) tuzipatazo toka kwenye familia zetu, shule, vyuo, hadi hapo ulipo, moja na la msingi ni kukusaidia kujijua katika maana ya uwezo wako (capacity), karama zako, na mazingira yako ili mwisho wa siku uipate furaha ile ya kweli ndani yako. Ukichepuka katika kweli hii huwezi epuka kuwa kivuli cha kitu kingine. Hicho kivuli hakitoweza kukupa furaha. Ni sawa na kuvaa kinyago na kuificha sura yako halisi.

Kutojipokea ambapo kunapelekea kuishi maisha linganishi na uvuli wa vitu ndicho kisemwacho hapa. Mungu alipomuumba mwanadamu, wazazi wetu wa mwanzo Adam na Hawa, aliwapa pia sehemu nzuri ya kuishi. Na panapokuwa zaidi ya mmoja kuna kuwa na utaratibu wake wa kuishi, na hiyo ndiyo akili. Penye akili kuna utaratibu, na pasipo na utaratibu hapana akili. Kweli hii anaikiri mwanamke yule (Hawa) kwa nyoka yule anayemrubuni ‘kula matunda yote ya bustani’ katika bustani ile Mungu aliyoiandaa yao na kusema, “Matunda ya miti ya bustanini twaweza kula; lakini matunda ya mti ulio katikati ya bustani Mungu amesema, Msiyale wala msiyaguse, msije mkafa,” Mwa 3:2-3. Nyoka kwa kujua udhaifu wao, yaani, wa kutojipokea kama walivyo, anawapa hakikisho la hofu yao, yaani, kifo, na kuwaambia, “Hakika hamtakufa, kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya,” Mwa 3:4-5. Kutokujua uwezo wako ndani yako, ni rahisi sana kurubuniwa kwa sababu nafasi ya kutokuwa na utoshelevu ni kubwa sana ndani yako. Na matokeo yake, “Mwanamke alipoona ya kuwa ule mti wafaa kwa chakula, wapendeza macho, nao ni mti wa kutamanika kwa maarifa, basi alitwaa katika matunda yake akala, akampa na mumewe, naye akala,” Mwa 3:6. Tendo hili la kwenda kinyume cha utaratibu (kutokutii) ni kujipatia utoshelevu ambao ni tokeo la kutojipokea kama walivyo.

Je, ni mara ngapi tunaona vituko mtaani mwetu watu wanavyojipodoa na mwisho wa siku wanabadilika na kuwa vinyago vya kutisha? Leo binadamu amefika mbali zaidi hata anamkosoa Mungu kwa kubadili maumbile yake. Siku ya ufufuo wa wazima na wafu hakika vitashuhudiwa vituko vingi!!! Tokeo la moja kwa moja kwa kile walichokitaka wazazi wetu wa mwanzo kwa kuuvunja utaratibu ule ni hili la kuwa na soni. “Wakafumbuliwa macho wote wawili wakajijua kuwa wa uchi, wakashona majani ya mtini, wakajifanyia nguo,” Mwa 3:7. Sijui siku hiyo ya ufufuo wa wazima na wafu kama kutakuwa na majani ya mtini kuifunika soni itakayojitokeza.

Ndugu yangu, Yesu angezifuata hisia zake, hakika hasingeweza kuyashinda majaribu kule jangwani. Yesu hakuziruhusu hisia zake zimtawale kwa sababu alimruhusu Roho wa Mungu ayatawale maisha yake. Na Yesu, hali amejaa Roho Mtakatifu, alirudi kutoka Yordani, akaongozwa na Roho muda wa siku arobaini nyikani, akijaribiwa na Ibilisi. Ni Roho huyu aliyeyasukuma yote aliyoyafanya na hasa pale alipotangaza rasmi mapambano ya kweli na haki katika lile lililo ovu na kumkomboa mwanadamu. “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa,” Lk 4:18. Na ni Roho huyu huyu aliyemwezesha kuyaona yote kwa mwelekeo wa Mungu Baba. “Saa ile ile alishangilia kwa Roho Mtakatifu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya umewaficha wenye hekima na akili; umewafunulia watoto wachanga; Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyokupendeza,” Lk 10:2.

Huyu ndiye Roho aliyemwezesha kuyashinda yale majaribu jangwa juu ya Sifa, Umaarufu na Utajiri [Mt 4:4, 5-6, 9]. Baada ya ushindi huu wa Yesu, Ibilisi alimwacha, na malaika wakaja kumtumikia. “Kisha Ibilisi akamwacha; na tazama, wakaja malaika wakamtumikia,” Mt 4:11. Unaposhinda majaribu katika maisha yako usije ukajisahu na kubweteka kana kwamba vita hiyo ishafikia ukomo. Yakupasa kuwa macho muda wote kama asemavyo Mtume Petro, “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze,” 1Pet 5:8.

Kila mmoja wetu anajangwa lake ambalo ukitaka uzima wa milele utaupata na ukitaka ya hapa duniani utayapata pia. Ila ni vigumu sana kuyapata ya milele kama utabobea kwa haya ya leo na kesho, yaani ya hapa duniani. Ukiyachuchumilia ya umilele, kuna uhakika wa kuyapata yote ya duniani kwa amani na furaha. Basi “utafuteni ufalme wa Mungu, na hayo mtaongezewa,” Lk 12:31. Maisha yangu kama Mtawa na Padre ni yanipasa kuyaisha kwa uaminifu huku nikiyashinda majaribu yangu ya kila siku kwa nguvu ya sala na uwezo wa Roho Mtakatifu. Nawe ule mlei na kadiri ya wito wako, ni vyema ukajua yakupasayo kuishi na hasa uaminifu kwa kile ulichoitiwa. Kipindi hiki cha kwaresma tunapata nafasi ya kuzama ndani ya nyoyo zetu kwa lengo la kujitakasa na kumrudia Mungu katika kumwabudu kuliko sahihi, halisi, tafakari, na kwa matendo hai. Ibilisi utuacha tu kwa muda ila hajaghairi nia yake ya kutudondosha. Basi tukeshe tukiomba na kushikamana na Kristo aliyeyashinda majaribu yake jangwani.

Maisha yetu leo yana maana sana “kwa maana ikiwa kwa kukosa kwake yule mmoja wengi walikufa, zaidi sana neema ya Mungu, na kipawa kilicho katika neema yake mwanadamu mmoja Yesu Kristo kimezidi kwa ajili ya wale wengi,” Rum 5:15b. Yesu Kristo katurudishia hadhi ya kuwa tena wana wa Mungu na warithi wa ufalme wake wa mbinguni.

Jambo la ajabu ona tunavyoishi na jirani zetu! Unaweka wigo "fence" kiasi kwamba unamzuiya hata jirani yako kufungua mlango. Ona! tusivyo wajali wengine afya zao! Tunaelekeza maji taka kwenye makazi yao bila huruma. Eti kwa vile unapesa, na unajulikana hadi usalama wa Taifa. Eti kwa vile wewe ni kiongozi wa ngazi za juu kwenye utawala dhalimu. Eti kwa vile wewe ni mfanya biashara maarufu nchini. Je, hili ndilo kusudi la Mungu kwa maisha yako hapa duniani?

Ndugu yangu, usisahau kuwa maisha ya hapa duniani ni sawa na kuwa ugenini. Haya si makazi yako ya kudumu, au hatma yako ya mwisho. Unapita tu!  Unatembea tu duniani. Mfalme Daudi anatukumbusha, "Mimi ni mgeni katika nchi, usinifiche maagizo yako," Zab 119:19, na Mtume Petro anasema,  "na ikiwa mnamwita Baba, yeye ahukumuye kila mtu pasipo upendeleo, kwa kadiri ya kazi yake, enendeni kwa hofu katika wakati wenu wa kukaa hapa kama wageni." 1Pet 1:17. Waamini wa kweli wanafahamu wazi kwamba kuna mambo mengi ya maisha kuliko hii miaka michache tunayoishi hapa duniani. Uhakika huu tunapewa na Kristo mwenyewe baada ya kukishida kifo kwa sadaka yake pale msalabani. Sote tumehesabiwa haki kwa kifo cha Kristo. Basi tena, kama kwa kosa moja watu wote walihukumiwa adhabu, kadhalika kwa tendo moja la haki watu wote walihesabiwa haki yenye uzima,” Rum 5:18

Ndugu, kitambulisho chako kiko katika umilele, na nchi yako ni mbinguni kwa sadaka ya Bwana wetu Yesu Kristo aliyekubali kuutoa uhai wake ili mimi na wewe tuwe huru kutoka utumwa wa dhambi. “Na dhambi ilipozidi, neema ilikuwa nyingi zaidi; ili kwamba, kama vile dhambi ilivyotawala katika mauti, vivyo hivyo kwa njia ya haki neema itawale hata uzima wa milele kwa Yesu Kristo Bwana wetu,” 5:20b-21. Yote haya yawezekana kwako na kwangu kwa neema tu ya Mungu. Unapofahamu ukweli huu, utaacha kuwa na wasiwasi wa "kupata kila kitu" hapa duniani. Mungu yupo wazi kabisa kuhusu habari za kuishi kwa ajili ya "hapa" na "sasa" tu huku ukijifananisha na watu wa dunia hii katika kipaumbele na mtindo wa maisha.

Ndugu yangu hapana shaka wa mfahamu vizuri "inzi!" Mdudu huyu kadiri ya utafiki wa kisayansi huishi siku saba tu. Ni wiki moja kati ya wiki 52 katika mwaka mmoja. Tazama fujo na papara za inzi. Hutua kila mahali kwa siku hizo saba; kwenye vyakula (vilivyo chacha na visivyo chacha), kwenye vinjwaji, kwenye vidonda, kwenye vinyesi, nk. Tulio wengi leo maisha yetu hayana tofauti na haya ya inzi. Hutaka kufanya yote na kujaribu yote katika maisha. Ila “mali bila daftari, huisha bila habari.”

Tumsifu Yesu Kristo!

“Kwa maana ikiwa kwa kukosa kwake yule mmoja wengi walikufa, zaidi sana neema ya Mungu, na kipawa kilicho katika neema yake mwanadamu mmoja Yesu Kristo kimezidi kwa ajili ya wale wengi,” Rum 5:15b

Tusali:-Ee Yesu Mwema, nijalie neema na nguvu ili nivishinde vilema vyangu. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario