JUMAMOSI WIKI YA 4 YA KWARESMA
Somo:
Yer 11:18-20
Zab:
7:1-2, 8bc-9, 10-11
Injili:
Yoh 7:40-53
Nukuu:
TAFAKARI:
“Haki ya mnyonge ni haki ya Mungu; dhuluma dhidi ya mnyonge ni dhuluma dhidi ya
Mungu, binadamu hawezi kushinda kesi hii.”
“Lakini mimi nalikuwa
kama mwanakondoo mpole, achukuliwaye kwenda kuchinjwa, wala sikujua ya kuwa
wamefanya mashauri kinyume changu, wakisema, “Na tuuharibu mti pamoja na
matunda yake, na tumkatilie mbali atoke katika nchi ya walio hai, ili jina lake
lisikumbukwe tena.”” Yer 11:19
“Je, torati yetu
humhukumu mtu kabla ya kumsikia kwanza, na kujua atendavyo?” Yoh 7:51
Wapendwa wana wa Taifa
ya Mungu, leo kadiri ya masomo yetu, yanatualika tutafakari juu ya “haki ya
mnyonge ni haki ya Mungu; dhuluma dhidi ya mnyonge ni dhuluma dhidi ya Mungu,
binadamu hawezi kushinda kesi hii.” Katika mazingira ya Nabii Yeremia na hata
mazingira na nyakati za Yesu Kristo, wanyonge walidhulumiwa na haki zao kuporwa
au kukanyagwa. Hawakuwa na watetezi, na hata kwenye ukweli juu ya wanyonge,
ulipindishwa kwa visingizio mbalimbali kama tutakavyoona kwa Yeremia na Yesu
Kristo. Je, nyakati zetu hali imebadilika na kuwa bora zaidi, licha kwamba Yesu
Kristo kuwa mtetezi wa wanyonge na hata kuutoa uhai kwake kwa ajili ya kweli?
Ndugu yangu, Nabii
Yeremia anasema ni kwa namna gani mtu mnyonge anavyoonewa kutokana na hali na
upole wake. Katika jamii yoyote ile ya watu, licha ya historia yao na utamaduni
wao, wale waliojaliwa ufahamu wa kuelewa mambo, hutumika sana katika kutafuta
ukweli, usawa, haki, amani, na kuzisimamia. Ni watu hawa hawa kwa kukosa hofu
ya Mungu hutumia upole na hali za wanyonge kuwadhulimu haki zao. Katika uovu
huu, Nabii Yeremia anasema, “Lakini mimi nalikuwa kama mwanakondoo mpole,
achukuliwaye kwenda kuchinjwa, wala sikujua ya kuwa wamefanya mashauri kinyume
changu, wakisema, “Na tuuharibu mti pamoja na matunda yake, na tumkatilie mbali
atoke katika nchi ya walio hai, ili jina lake lisikumbukwe tena.”” Yer 11:19
Mnyonge huyu hanyimwi
tu haki zake, bali huondolewa hata haki za kizazi chake kijacho na kufutwa
kabisa. Lengo ni kuuharibi mti pamoja na matunda yake. Wapendwa wana wa Mungu,
dhuluma kama hii afanyiwayo mnyonge, binadamu mwenye kufanya hayo kamwe hataweza
kushinda katika dhuluma hii. Mungu mara zote hulia na wanyonge. “Bwana huua,
naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha
mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu. Humwinua mnyonge kutoka
mavumbini, Humpandisha mhitaji kutoka jaani, Ili awaketishe pamoja na wakuu,
Wakakirithi kiti cha enzi cha utukufu; Kwa maana nguzo za dunia zina Bwana,
Naye ameuweka ulimwengu juu yake,” I Sam 2:6-8.
Ndugu yangu, dhuluma
dhidi ya mnyonge ni dhuluma dhidi ya Mungu mwenyewe. Tenda haki kwa kila mmoja
kadiri ya mahitaji yake. “Usimnyang’anye maskini; wala usimdhulumu mtu mnyonge
langoni; Kwa sababu Bwana atawatetea; Naye atawateka uhai wao waliowateka,” Mit
22:22-23. Kuna heri na baraka kubwa kutoka kwa Mungu unapotenda mema na
kuwatetea wanyonge. “Heri amkumbukaye mnyonge; Bwana atamwokoa siku ya taabu,”
Zab 41:1. Tuwe watu wa kutenda mema kwa wote na tuanze pale tulipo. Lifanye
jambo hilo kuwa tabia yako nyumbani kwako, kazini kwako na hata kwenye utume
wako, iwe jumuiyani na hata Kanisani. Tuwe watetezi wa wanyonge na hasa wale
wasiokuwa na sauti na mahali pa kupeleka malalamiko na vilio vyao.
Watendao maovu na hasa
kuwanyanyasa wanyonge kwa kunyonga haki zao, kamwe hawataishi kwa amani.
Ninapolitazama taifa letu leo, na harakati zake hasa kwa swala zima la Katiba,
napata mashaka sana. Wasomi wetu na wale tuliowapa dhamana ya kutetea na
kusimamia haki kwa wote na hasa kwa wanyonge, wamekuwa watu wa kwanza kupora
haki za wanyonge na kufanya Katiba pendekezwa kuwa na taswira yenye mwelekeo wa
kulinda maslahi yao na familiza zao, kulinda utajiri waliokwisha pora kwa
wanyonge, kuweka uwezekano wa familia zao na marafiki zao kuwa madarakani
daima, na hata kuzuia mnyonge kupata haki yake pale atakapoidai kwa haki.
Katika hili na mazingira
kama haya, Mungu anasema, “hukumu hii imekuja kwa agizo la walinzi, na amri hii
kwa neno la watakatifu; kusudi walio hai wapate kujua ya kuwa Aliye juu
anatawala katika ufalme wa wanadamu, naye humpa amtakaye, tena humtawaza juu
yake aliye mnyonge,” Dan 4:17. Dhuluma yeyote juu ya wanyonge, Bwana ataijibu
mara moja. Tuwe na hamu na matumaini ya kutenda mema siku zote, na tuendelee
kutenda haki. Kwa kuwa, “Maana mkono wangu ndio uliofanya hivi vyote, vitu hivi
vyote vikapata kutokea, asema Bwana; lakini mtu huyu ndiye nitakayemwangalia,
mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu,”
Isa 66:2. Kumdhulumu mnyonge ni kugusa mboni ya jicho la Mungu.
Injili letu ya leo
yaonyesha ni kwa namna gani mnyonge anavyodhumiliwa haki zake na hasa swala
zima la kutoa hukumu. Yesu Kristo anahukumiwa hata bila kusikilizwa. Wanapanga
njama za kuutoa uhai wake kwa vile tu ananena iliyo kweli na kutenda mema. Hata
licha ya kusutwa na dhamiri zao, Mafarisayo bado wanasukumwa na dhamiri zao mbaya
kutenda uovu. “Je, torati yetu humhukumu mtu kabla ya kumsikia kwanza, na kujua
atendavyo?” Yoh 7:51. Nikodemu, aliyekuwa mfuasi wa siri wa Kristo, na
aliyekuwa anamwendea usiku kupata habari za ufalme wa Mungu, anajaribu kutoa
ushauri ili kuunusuru uhai wa Yesu. Ushauri huu haukubaliki machoni mwa
Mafarisayo kwa sababu binadamu
akishachagua kumtumikia shetani, uwepo wa Mungu unatoweka. Dhamiri iliyo
mbovu na ufu, husahau hata yale mazuri tuliyojiwekea kwa ajili ya kutenda haki.
Ndugu yangu, Taifa letu
linautaratibu mzuri tu wa kutoa haki licha ya kwamba yapo maeneo fulani
yanaitaji marekebisho. Hata hivyo, bado haki za wanyonge zinakanyagwa kiasi
kwamba hata aibu hatuna tena. Kujilimbikizia mali za wizi uliotokana na kodi za
wanyonge, ni dhambi ambayo ukiifanya itakutafuna wewe na hata kizazi chako hadi
kizazi cha nne baada ya wewe. Fedha na mali zisizo halali ni kujiwekea sanamu
na kuanza kuziabudu. Tukianza kuambudu mali na vitu, Mungu hana tena nafasi
ndani yetu. “Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi Bwana wako, ni Mungu
mwenye wivu, nawapatiliza wana wa uovu wa baba zao; hata kizazi cha tatu na cha
nne cha wanichukiao,” Kumb 5:9. Hii ni laana kubwa sana. Ufisadi kwenye Taifa
letu la Tanzania, umekuwa moja ya sifa,
na tunaaminishwa kupokea jambo hilo kama la kawaida. Uovu huu dhidi ya masikini
na wanyonge binadamu hawezi kushinda kamwe kwani ni uovu dhidi ya Mungu
mwenyewe. Leo tupo kwenye mkakati na harakati wa kutumbua
‘majipu.’ Je, tutafikia malengo kweli ikiwa hata watumbuaji wa majibu kikanuni
nao wanamajipu hadi mikononi? It
is just a play within a play!
Bwana wetu Yesu Kristo
ni neno aliyefanyika mwili. Hivyo ni Mungu mwenyewe. Kutokumpatia haki stahili
Yesu Kristo, ni kutokumpatia Mungu mastahili yake. Je, vita hii binadamu
mwenzangu tutashinda, au ndiyo tunazidi kujichumia laana tu kila kukichwa.
Ndugu yangu kilio cha wanyonge katika Taifa letu leo kwa ujumla wake ni kilio
cha Mungu.
Mpendwa, mara zote kuwa
na hofu ya Mungu na tenda wema kwa wote bila kujali historia ya mtu na hata
hali yake kijamii. Sote mbele ya Mungu tunamizania na mastahili sawa. Wayahudi
wanatafuta histori ya neno aliyefanyika mwili-Yesu Kristo, kwenye kumbukumbu
zao. Wanampa Yesu Kristo nafasi ya Nabii. Yesu Kristo siyo nabii, bali ni nafsi
ya Pili ya Mungu. Bado Wayahudi wanawaza kibinadamu. Tusimsaidie mtu au
kumsikiliza mtu shida zake kwa kuanza kutazama historia yake. Hili ni kosa
kubwa sana kufanya. Tumtazame mtu kadiri ya kile anachohitaji kwetu na tufanye
kwa haki na stahili zote.
Tumsifu Yesu Kristo
“Hajanena kamwe
mtu ye yote kama huyu anavyonena,” Yoh 7:46
Tusali:-Ee
Yesu, nipe neema ya kukuona mara zote kwa wale ninao wahudumia. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario