ALHAMISI WIKI YA 3 YA KWARESMA
Somo:
Yer 7:23-28
Zab:
95:1-2, 6-7, 8-9
Injili:
Lk 11:14-23
Nukuu:
“Taifa hili ndilo
lisilosikiliza sauti ya Bwana, Mungu wao, wala kupokea mafundisho; uaminifu
umepotea, umekatiliwa mbali na vinywa vyao,” Yer 7:28
“Lakini, ikiwa mimi
natoa pepo kwa kidole cha Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia,” Lk
11:20
TAFAKARI:
“Huwezi
shindi vita na Mungu. Ushindi ni kuishi kwa ajili yake na katika yeye tu,
yaani, kujisalimisha kwake.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo tutafakari kwa undani juu ya neno hili, “Huwezi shindi vita na Mungu.
Ushindi ni kuishi kwa ajili yake na katika yeye tu, yaani, kujisalimisha
kwake.” Wengi wetu kwa kufahamu au kutokufahamu, tunaishi kwa kupingana na
Mungu. Mfumo huo kimaisha hautaweza kuleta mafanikio yo yote hata kama tukiweka
bidii zetu zote, yaani, nguvu, akili, na moyo katika mpango huo. Tendo hilo
kiimani ni kuwekeza pasipo na usalama. Huu ndio wito wa masomo yetu yote ya
leo.
Somo la kwanza
linatueleza hasara ya kutosikiliza sauti ya Mungu kupitia watumishi wake
manabii. Waisraeli wanasahau kwamba hakuna kushinda bila uwepo wa Mungu.
Kinyume chake wanakosa baraka na msaada wa Mungu kwa kila wafanyacho. Hii ni
laana ya wazi kabisa. Mungu anasema kupitia kinywa cha Nabii Yeremia, “Taifa
hili ndilo lisilosikiliza sauti ya Bwana, Mungu wao, wala kupokea mafundisho;
uaminifu umepotea, umekatiliwa mbali na vinywa vyao,” Yer 7:28.
Ndugu yangu, unapokosa
uaminifu mbele ya Mungu, hakuna mafanikio yo yote uwezayo kupata kwa sababu
huamini nguvu ya Mungu, nafasi ya Mungu, na msaada wa wake katika maisha yako.
Huku ni kujihesabia haki mbele ya Mungu pasipo mastahili. Uaminifu mbele ya
Mungu hujengwa kwa kujisalimisha kwako. Kujisalimisha mbele ya Mungu ni tendo
zima la KUABUDU.
Tendo
hili la kujisalimisha kwa maana nyingine ni kujiweka kwa ajili ya Mungu tu. Ni
kujiweka wakfu kwa ajili yake, Kumfanya Yesu Bwana wako, Kuchukuwa msalaba
wako, Kuifisha nafsi, na Kujitoa kwa Roho Mtakatifu. Ni kitu ambacho kibinadamu
ni vigumu kufanya kwa sababu hakuna anayetaka kupoteza kwa ajili ya kupoteza,
hasa kwa ulimwengu wetu huu wa ushindani. Tupo kwenye ulimwengu wa kushinda tu,
na mashindano muda wote. Lakini Yesu anatupa angalizo na kusema, “Kwa kuwa
itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake? Ama mtu atoe nini badala ya nafsi yake?” Mk
8:36-37. Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, njia sahihi ya
maisha yako ni kujisalimisha katika mikono salama ya Mungu.
Nini
maana ya kujisalimisha?
Kujisalimisha
kwa Mungu si kujiuzulu na kukaa tu kusubiri, au kuamini kuwa yote yameandikwa
binadamu hana hiari, au kuwa na udhuru na wivu. Siyo kukubali hali hiyo hiyo
uliyo nayo. Inaweza kumaanisha kinyume cha haya; kujitoa sadaka maisha yako au
kuteseka ili kubadilisha yanahitajika kubadilishwa. Mara nyingi Mungu huwaita
watu waliojisalimisha kwake kupiga vita kwa jina lake. Kujisalimisha sio kwa
uoga au mazulia. Mungu asingependa kupoteza akili alizokupa! Mungu hapendi watu
wawe kama mitambo (robots) ili kumtumikia. Kujisalimisha siyo kukomesha utu
wako. Badala ya kukomesha utu wako, kujisalimisha hukutia nguvu. C. S Lewis
alisema, “kadiri tunavyomruhusu Mungu atutawale ndivyo tunavyozidi kuwa sisi
wenyewe, kwa sababu yeye ndiye aliyetuumba. Alibuni namna mbalimbali za watu
wote tofauti ambao mimi na wewe tulikusudiwa kuwa… Ni pale ninapomgeukia
Kristo, ninapojikabidhi nafsi yangu kwake, ndipo ninapokuwa na ule utu wangu
halisi.”
Kujisalimisha
kunadhihirika vyema katika KUTII. Unasema ‘ndivyo, Bwana’ kwa chochote
anachokueleza. Kusema “hapana, Bwana” ni kutamka vinyume. Hatuwezi kumwita Yesu
Bwana na wakati huo huo hatutaki kumtii. Baada ya usiku kucha bila kupata
samaki, Simioni alionyesha kujisalimisha pale Yesu alipomwambia kujaribu tena”
“Bwana tumefanya kazi kwa bidii usiku wote na hatujakamata samaki yeyote.
Lakini kwa sababu umesema, nitatia nyavu majini,” Lk.5:5. Watu waliojisalimisha
hutii neno la Mungu hata kama linaonekana kutokuwa na maana.
Jambo
lingine katika kujisalimisha ni IMANI. Ibrahimu alifuata maelekezo ya Mungu
bila kujua alikokuwa akienda. Hana alisubiri wakati wa Mungu bila kujua ni
lini. Mariamu alitarajia muujiza bila kufahamu utatendekaje. Yusufu aliamini
lengo la Mungu bila kujua kwa nini mazingira yalikuwa hivyo. Kila mmoja wa watu
hawa alikuwa amejisalimisha kwa Mungu alipomtegemea.
Utafahamu
umejisalimisha kwa Mungu unapomtegemea Mungu akutengenezee mambo yako badala ya
kujaribu kuwafanyia hila wengine, ukapitisha jambo lako, na mwisho ukatawala
mazingira hayo. Unamwachia Mungu afanye, Huhitaji wakati wote kuwa,
“mwangalizi.” Mzaburi anasema, “Jisalimishe nafsi yako kwa Bwana, na umsubiri
kwa uvumilivu.” Zab. 37:7a. Baada ya
kujaribu sana, umwamini zaidi. Pia unafahamu kwamba unajisalimisha unapokuwa
huchukizwi na lawama na kukimbilia kujitetea. Mioyo iliyojisalimisha huonyesha
mahusiano mazuri na wengine. Huwatupilii mbali wengine, hudai haki zako, na
hutumikii nafsi yako kama umejisalimisha.
Eneo
gumu sana kwa watu wengi kujisalimisha ni PESA zao. Wengi wamefikiri, “Nataka
kuishi kwa ajili ya Mungu lakini pia nataka kupata pesa nyingi ili niishi kwa
raha baadaye nipumzike.” Kupumzika siyo lengo la maisha ya kujisalimisha, kwa
sababu huku ni kushindana na Mungu kwa sababu ya kuweka mkazo kwanza kwa maisha
yako. Yesu anasema, “Huwezi kutumikia Mungu na pesa,” Mt. 6:24 na kwamba
“popote hazina yako ilipo ndipo na moyo wako upo,” Mt. 6:21. Yesu anatupa
angalizo la shamba la mtu yule mmoja tajiri lililo kuwa limezaa sana. Mtu huyu
alipanga kujibohofisha; kupumzika, kula, kunywa na kufurahi. Naye Yesu anasema,
“Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe,
usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya
nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye
nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu,” Lk 12:20-21.
Wapendwa
wana wa Mungu, kielelezo kikubwa cha kujisalimisha ni Yesu. Usiku ule kabla ya
mateso Yesu alijisalimisha kwa mpango wa Mungu. Alisali, “Baba kila kitu
kinawezekana kwako. Tafadhali niondolee kikombe hiki cha mateso. Lakini nataka
mapenzi yako, siyo yangu,” Mk.14:36
Yesu
hakuomba, “Baba, kama unaweza kuniondolea maumivu haya,
tafadhali fanya hivyo.” Alikuwa tayari amethibitisha kuwa Mungu ana uwezo wa
kufanya lolote! Badala yake aliomba, “Mungu, kama inapendeza kwako kuniondolea mateso haya, tafadhali
fanya hivyo. Lakini kama yanatimiza kusudi lako, ndivyo ninavyotaka
pia.
Kujisalimisha
halisi husema, “Baba, kama tatizo hili, maumivu, ugonjwa, au hali yoyote
inahitajika kutimiza lengo lako na utukufu kwako katika maisha yangu au ya
mwingine, tafadhali usiliondoe.” Kiwango hiki cha ukomavu hakiji kwa urahisi. Kwa
upande wa Yesu, aliugua sana kuhusu mpango wa Mungu kiasi cha kutoa jasho la
damu. Kwa upande wetu, ni vita kali dhidi ya asili yetu ya ubinafsi.
Kujisalimisha
ndiyo njia bora ya kuishi:
Kila
mtu hatimaye hujisalimisha kwa mtu au kitu fulani. Kama sio kwa Mungu,
utajisalimisha kwa matarajio au maoni ya watu wengine, au pesa, chuki, hofu, au
kwa kiburi chako au tamaa mbaya, au ubinafsi. Ulibuniwa kumwabudu Mungu-na kama
utashindwa kumwabudu, utatengeneza vitu vingine (sanamu) ili uvipe maisha yako.
Unao uhuru wa kuchagua usalimishe maisha yako, lakini huko huru na matokeo ya
uchaguzi huo. E. Stanly Jones alisema, “kama hutajisalimisha kwa Kristo,
utajisalimisha kwa machafuko.” Kujisalimisha si njia bora ya kuishi; ni njia
pekee ya kuishi. Hakuna kitu kingine cha kukufanikisha.
Njia nyingine zote hukuongoza kwenye
kukukatisha tamaa, na kuziangamiza nafsi. Tafsiri ya King James huita
kujisalimisha “huduma yenu yenye maana.” Rum 12:1. Tafsiri nyingine inasema,
“njia yenye maana zaidi ya kumtumikia.” Rum 12:1 Kusalimisha maisha yako si
hisia za kipumbavu lakini ni tendo la akili na busara ambalo unaweza kulifanya
kwa ajili ya maisha yako. Ndiyo maana Paulo alisema, “Ni lengo letu kwamba
tumpendeze yeye,” 2Kor 5:9. Nyakati zako za busara zitakuwa zile ambazo unasema
NDIYO kwa Mungu.
Wakati
mwingine huchukua miaka, lakini hatimaye unagundua kwamba kizuizi kikubwa kwa
Baraka za Mungu maishani mwako sio watu wengine, ni wewe mwenyewe, yaani,
matakwa yako binafsi, kiburi cha hali ya juu, na matarajio yako. Huwezi
kutimiza lengo la Mungu kwa maisha yako
huku ukikazania malengo yako binafsi.
Kama
Mungu ataenda kufanya kazi ya kina ndani yako, itaanza hivyo. Kwa hiyo mpe yote
Mungu: kushindwa kwako hapo nyuma, matatizo yako ya sasa, matarajio yako ya
mbele, hofu zako, ndoto, udhaifu, tabia, maumivu, na madhara yoyote uliyo nayo.
Mweke Yesu katika kiti cha dereva wa maisha yako na uondoe mikono yako toka
kwenye usukani. Usiogope; hakuna chochote katika uongozi wake kinaweza kupoteza
dira. Chini ya uongozi wa Kristo kunaweza kudumu chochote. Utakuwa kama Paulo,
“Niko tayari kwa lolote na kuwa sawa na chochote kwa njia ya yeye anayetia
nguvu ndani yangu, yaani, ninajitosheleza katika utoshelvu wa Kristo.”Flp 4:13
Kujisalimisha
kwa Paulo kulitokea katika njia ya Dameski alipoangushwa chini na mwanga mkali
uliompofusha. Kwa watu wengine, Mungu anapata mwitikio wao bila kutumia njia ya
ajabu sana. Pamoja na hayo, kujisalimisha siyo tukio la wakati mmoja tu. Paulo anasema,
“Nakufa kila siku.” I Kor 15:3 Kuna wakati wa kujisalimisha, na kuna tendo la
kujisalimisha, ambalo ni la muda-hadi-muda na maisha yote. Tatizo la sadaka iliyo hai ni kwamba inaweza kutambaa na
kutoa madhabahuni, hivyo unaweza kutakiwa kujisalimisha hata mara hamsini kwa
siku. Ni lazima ufanye jambo hili kuwa tabia yako ya kila siku. Yesu anasema,”
kama watu wanapenda kunifuata ni lazima waache mambo wanayoyapenda. Lazima wawe
tayari kuacha maisha yao kila siku na kunifuata,” Lk 9:23
Ngoja
nikuonye: unapoamua kuishi maisha ya kujisalimisha kikamilifu, uamuzi huo
utapimwa. Wakati mwingine itamaanisha kufanya mambo yasiyostahili, ya gharama,
au yanayoonekana hayawezekani. Mara nyingi itamaanisha kufanya kinyume cha
unavyojisikia kufanya.
Lakini tukijipima nguvu
zetu na Mungu, kamwe vita hii hatuwezi kushinda. Ni kupiga ngumu kwenye upepo
au ukuta. Ni kujaza maji kwenye gunia la katani, kamwe halitajaa. Tujisalimishe
kwake, kwa kuwa, “Mungu wako, ni Mungu wa rehema; hatakukosa wala kukuangamiza,
wala hatalisahau agano la baba zako alilowaapia,” Kumb 4:31. Katika historia ya
wokovu wetu, mara zote binadamu ameshindwa kwa kosa la kutojisalimisha kwa
Mungu.
Injili yetu ya leo
inafafanua kwa undani zaidi namna ya kujisalimisha, na hasa kujisalimisha kwa
ufalme wa Mungu. Ndugu yangu, katika miaka ile mitatu ya mwisho ya Bwana watu
Yesu Krisito, alisisitiza mambo makuu matatu; kwanza, kufanya toba ya kweli kwa
kuwa ufalme wa Mungu u karibu (Mk 1:15), Pili, kuwachagua na kuwaandaa wafuasi
wake kwa kazi hii ya kuhubiri habari njema (Mk 1:16-20, Mt 28:19-20), na tatu,
kulitakasa Hekalu (kama jengo na nyumba ya sala, na mwili ambao ni hekalu la
Roho Mtakatifu; Yoh 2:14-21, 1Kor 6:19)
Injili ya leo Yesu
Kristo analifanya jambo hilo la tatu; kulitakasa Hekalu-Mwili ambalo ni makazi
ya Roho Mtakatifu. “Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu
aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe; maana
mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu.” 1Kor
6:19-20.
Ndugu yangu, kwa vile
tusivyojisalimisha kwa Mungu, hujisalimisha kwa vitu au watu. Watu waliokuwepo
katika uponyaji wa bubu aliyekuwa na pepo bubu, wanamuhukumu Yesu kuwa
anayafanya hayo kwa nguvu za Beelzebuli. Mara nyingi huwa tunawahukumu watu kwa
namna tunavyofikiri na kutenda. Kwa vile wao huamini juu ya nguvu hizo za
Beelzebuli, wanafikiri na Yesu Kristo anayafanya hayo kwa nguvu hizo. La hasha!
Yesu anawaambia, “Lakini, ikiwa mimi natoa pepo kwa kidole cha Mungu, basi
ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia,” Lk 11:20. Yesu anayafanya hayo kwa mkono
wa Mungu.
Ndugu yangu, leo wapo
watu ambao hawaamini nguvu ya Mungu, na uwepo wa Kristo katika maisha yao. Watu
wa mtindo huu, wapatwapo na majaribu kidogo tu, hukimbilia kupata ishara nje ya
Kristo. Kristo kwetu anatosha. Hatuitaji ishara zaidi yake. Mateso, kifo na
ufufuko wake ni Ushindi mkubwa wetu na Ishara ya kutosha kabisa. Ndugu yangu,
kiguru na njia kila siku kwa waganga utaacha lini? Kama wewe ni Mkristo na
waamini uwepo wa Kristo katika maisha yako, mganga wa kienyeji ana nafasi gani
kwako? Kwa nini wajisalimisha kwa mwanadamu na wakati mwingine kwa shetani?
Ndugu yangu, elewa
jambo hili, “Bwana asema hivi, Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu,
Amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake Na moyoni mwake amemwacha Bwana,” Yer 17:5
Tumsifu Yesu Kristo!
“Taifa hili ndilo lisilosikiliza
sauti ya Bwana, Mungu wao, wala kupokea mafundisho; uaminifu umepotea,
umekatiliwa mbali na vinywa vyao,” Yer 7:28
Tusali:-Ee
Yesu Kristo, hakuna usalama na hata ushindi nisipojisalimisha kwako. Nisaidie
mara zote kuelewa kuwa Wewe ndiye Njia,
Uzima, na Ukweli. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario