miércoles, 1 de marzo de 2017

TAFAKARI: IJUMAA BAADA YA JUMATANO YA MAJIVU


IJUMAA BAADA YA JUMATANO YA MAJIVU

Somo: Isa 58:1-9a

Zab: 51:3-4, 5-6a, 18-19

Injili: Mt 9:14-15

Nukuu:

Je! Kufunga namna hii ni saumu niliyoichagua mimi? Je! Ni siku ya mtu kujitaabisha nafsi yake? Ni kuinama kichwa kama unyasi, na kutanda nguo za magunia na majivu chini yake? Je! Utasema ni siku ya kufunga, na ya kukubaliwa na Bwana?” Isa 58:5

Je! Saumu niliyoichagua, siyo ya namna hii? Kufungua vifungo vya uovu, kuzilegeza kamba za nira, kuwaacha huru walioonewa, na kwamba mvunje kila nira?” Isa 58:6

Je, Siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? Umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche  na mtu mwenye damu moja nawe?" Isa 58:7

Ndipo nuru yako itakapopambazuka kama asubuhi, na afya yako itatokea mara; na haki yako itakutangulia; utukufu wa Bwana utakufuata nyuma ukulinde,” Isa 58:8

“Ndipo utaita, na Bwana ataitika; utalia, naye atasema, Mimi hapa,” Isa 58:9

Yesu akawaambia, Walioalikwa arusini wawezaje kuomboleza, muda bwana arusi akiwapo pamoja nao? Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi; ndipo watakapofunga," Mt 9:15

TAFAKARI: “Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi; ndipo watakapofunga. Na wakati huo ndio sasa. Mfungo na matendo ya huruma.”

Wapendwa wana wa Mungu, masomo yetu ya leo yanatutaka kutafakari kwa kina maneno haya; “lakini siku zitakuja watakapoondolewa Bwana arusi; ndipo watakapofunga. Na wakati huo ndio sasa. Mfungo na matendo ya huruma.” Sehemu ya kwanza katika tafakari ya maneno haya, ni jibu la Yesu kwa wanafunzi wa Yohane Mbatizaji walioshangazwa na tendo la wanafunzi wake Yesu la kutokufunga. Nao walimuuliza Yesu, “kwa nini sisi na Mafarisayo twafunga, bali wanafunzi wako hawafungi?” Mt 9:14. Bila shaka jibu la Yesu lililenga dhana nzima ya uelewa wa kufunga.

Jibu la Yesu linaibua ufahamu huu kwa wanafunzi wa Yohane Mbatizaji kwamba, ‘tusipende kufanya mambo kwa mazoea bila kujua kiini chake na kwa nini tunafanya kama tunavyofanya.’ Kwa mantiki hii, jibu la Yesu linaeleza asichokisema Yesu moja kwa moja kwamba, ‘kwa sasa wanafunzi wake wapo shuleni kujifunza fumbo zima la mfungo.’ Basi nyakati zitakapotimia, yaani kuondolewa kwa Bwana Arusi-[Yeye mwenyewe, kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wake], ndipo watakapo funga na kuelewa vizuri sababu ya kufunga, huku wakiendeleza yale yote aliyowafundisha.

Mafarisayo na hata baadhi yetu leo twafikiri mfungo ni ‘kufanya tu yale yanayoonekana nje kwa faida ya kujitukuza wenyewe, ikiwa ni pamoja na kutokula kwa ratiba ya kawaida, na kujiweka katika hali ya huzuni na kuhurumiwa na watu.’ Mafarisayo walipoteza lengo zima na maana ya mfungo. Kipindi hiki cha siku 40, yaani ‘muda wa kutosha,’ hatufanyi maonyesho kwa lengo la kujiinua nafsi zetu, na wala hatufanyi mazoezi ya mwili kwa lengo la kuuweka mwili vizuri ingawa tuifanyapo saumu yetu vizuri twaweza kufaidika pia kimwili.

Nabii Isaya katika somo la kwanza ameeleza vizuri sana lengo la Saumu, yaani  Mfungo. Mfungo si maonyesho ya namna yoyote ile ya kuziinua nafsi zetu. Naye anasema kwa mtindo wa kuhoji na tafakari; Je! Kufunga namna hii ni saumu niliyoichagua mimi? Je! Ni siku ya mtu kujitaabisha nafsi yake? Ni kuinama kichwa kama unyasi, na kutanda nguo za magunia na majivu chini yake? Je! Utasema ni siku ya kufunga, na ya kukubaliwa na Bwana?” Isa 58:5. Hakika hili silo lengo la mfungo. Lengo la Mfungo au Saumu ni pamoja na haya ayasemayo Nabii Isaya kwa kuihoji nafsi; “Je! Saumu niliyoichagua, siyo ya namna hii? Kufungua vifungo vya uovu, kuzilegeza kamba za nira, kuwaacha huru walioonewa, na kwamba mvunje kila nira?” Isa 58:6. Saumu ya kweli ni pamoja na kupatazama pale ulipokosea kutokana na uovu wako, na kupigania haki za watu ikiwa ni pamoja na wale walioonewa kijamii kutokana na mifumo miovu ambayo nawe ni sehemu ya mfumo huo. Haya ndiyo matendo ya huruma yanayopaswa kuendana na Saumu ya kweli.

Matendo hayo ya huruma ndiyo anayoyahoji Nabii Isaya; "Je, Siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? Umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche na mtu mwenye damu moja nawe?" Isa 58:7. Kama najinyima kwa lengo la kufunga, kile ninachojinyima kiwalenge wahitaji. Kundi hili la wahitaji tunao pande zote na siku zote. Anza hapo ulipo! Naye Yesu anatuambia ukweli huu kama alivyowaambia wale waliomnung’unikia juu ya Marhamu ambayo alimwagiwa kichwani na Mwanamke yule mkosefu, ingeuzwa ili fedha ile wapewe maskini. Naye akawajibu na kusadifu tendo lile la mwanamke yule kwa kusema, “maana sikuzote mnao maskini pamoja nanyi, na kila mpendapo mwaweza kuwatendea mema; lakini mimi hamnami sikuzote,” Mk 14:7

Wapendwa katika Kristo, tunapofanya matendo haya ya huruma tunakutana na Yesu katika sura na maumbo tofauti tofauti. Ni kwa namna hii somo la kwanza kutoka nabii Isaya linalandana kabisa na ayasemayo Yesu katika Injili ya Mathayo 25:31-46. Hapa tunakutana na Yesu mwenye njaa, mgonjwa, mfungwa, aliye uchi, mwenye kiu, aliye kifungoni nk. Huku ni kukutana naye katika maisha yetu ya kawaida na ya kila siku. Mwisho wa siku Yesu anasema, "Amin nawaambia, kadiri msivyomtendea mmoja wapo wa hao walio wadogo, hamkunitendea mimi," Mt 25:45.

Ndugu yangu, hapa ndipo ilipolala hukumu yetu ya mwisho. Wenye haki watakwenda kwenye uzima wa milele, na wasio haki wataingia katika adhabu ya milele, (Mt 25:46). Bwana harusi hatunaye tena. Huu ndio wakati muhafaka wa kufunga na kufanya toba. Zoezi hili kwa Mkristo na kwa yeyote yule mwenye hofu ya Mungu ni zoezi na tendo endelevu maisha yake yote. Yesu kesha tufundisha mengi tulipokuwa naye katika makuzi yetu ya maisha ya kiroho, na sasa yatupasa kuyaishi. "Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi; ndipo watakapofunga," Mt 9:15b. Kuyafanya haya kwa uhakika, uaminifu, na ukamilifu wake ndiyo baraka na neema kwetu. “Ndipo nuru yako itakapopambazuka kama asubuhi, na afya yako itatokea mara; na haki yako itakutangulia; utukufu wa Bwana utakufuata nyuma ukulinde, Ndipo utaita, na Bwana ataitika; utalia, naye atasema, Mimi hapa,” Isa 58:8-9. Amina!

Hivyo ndugu yangu niliye safiri nawe katika tafakari hii, usisahau kamwe kundi la wahitaji katika mfungo wako. Daima uwe mtu wa kutenda haki na kuitetea pia pale haki hiyo inapokosekana au kukandamizwa kadiri ya nafasi yako na wito wako.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Walioalikwa arusini wawezaje kuomboleza, muda bwana arusi akiwapo pamoja nao? Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi; ndipo watakapofunga," Mt 9:15

NA

“Heri amkumbukaye mnyonge; Bwana atamwokoa siku ya taabu. Bwana atamlinda na kumhifadhi hai, Naye atafanikiwa katika nchi; Wala usimtie katika hali wamtakiayo adui zake,” Zab 41:1-2

Tusali:-Ee Yesu na Mwalimu wangu, katika mfungo huu nijalie nikuone kwa kila nitakayekutana naye, na iwe sehemu ya shukrani yangu kwako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario